Kuhitimu kwa Darasa la Gileadi la 83 Pindi ya Kisikukuu Kweli Kweli
“PENI Yehova asante, Ee ninyi watu, kwa maana yeye ni mwema: kwa maana fadhili-upendo yake ni kwa wakati usiojulikana.” (Zaburi 136:1, NW) Hayo ndiyo yaliyokuwa maoni ya kusisimuka moyoni ya wote 4,391 ambao walihudhuria zile shughuli za kuhitimu za darasa la 83 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa mlinzi katika vuli hii. Zile hotuba, mambo yaliyoonwa, na mwigizo wa Kibiblia, ambazo zilipokezwa wakati wa shughuli zile zilifanya wote waondoke wakiwa na roho zilizochangamsha. Kuhitimu huko kulitukia Septemba 6, 1987, kwenye Jumba la Kusanyiko la Mji wa Jersey lenye sura nzuri, ambalo hapo kwanza lilijulikana kama Stanley Theater.
Baada ya wimbo wa kufungua, na sala ikitolewa na John Booth wa Baraza Linaloongoza, mwenyekiti, Albert Schroeder, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, alikaribisha mmoja na wote kwenye pindi hii ya kisikukuu. Wale wanafunzi 24 walikuwa wamekuja kutoka nchi tano, na sasa wao walikuwa wakitumwa kwenye nchi tofauti nane. Ndugu Schroeder alikazia uhakika ambao watu wa Yehova wanao kwa sababu imani yao iko juu ya msingi wa mathibitisho kamili. Mathalani, wao wanajua kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima na kwamba Neno lake, Biblia Takatifu ni ukweli uliothibitishwa kwa ukamili. Jambo hilo linatofautiana wazi sana na falsafa za kibinadamu zilizo juu ya msingi wa mashaka-mashaka na makisio-makisio.
Msemaji wa kwanza alikuwa Martin Poetzinger, pia mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ambaye alitumia miaka tisa katika kambi za mateso za Nazi. Kichwa cha habari yake kilikuwa “Ni Katika Nani Wewe Unaitibari?” Kikiwa juu ya msingi wa Mithali 3:5, 6. Yeye alikazia kwa wanafunzi hao uhitaji wa kuitibari kwa ukamili katika Yehova na tengenezo lake linaloonekana, na pia kujithibitisha mmoja mmoja kuwa wanaoitibarika. Yale mazoezi ya wanafunzi Gileadi yalikuwa msingi tu; sasa wao walipaswa kujenga juu ya mazoezi hayo kwa kufuata shauri la Paulo kwenye Waefeso 5:15, 16. ‘Msisimame tuli,’ akahimiza msemaji. ‘Ninyi mtakuwa na matatizo yenu katika mgawo wenu wa umisionari kwa habari ya lugha, tabia ya majira ya nchi, chakula, na mambo kama hayo; lakini kwa kuitibari katika Yehova, ninyi mnaweza kutatua matatizo hayo yote. Upendo kwa watu ndio ufunguo wenu kwa fanikio. Kila kitia-moyo ni kutoka kwa Mungu; kila kivunja-moyo ni kutoka kwa Shetani.’
Msemaji aliyefuata alikuwa Eldor Timm, mshiriki wa Halmashauri ya Karakana, ambaye alitegemeza maelezo yake juu ya 2 Wakorintho 13:5, NW: “Endeleeni kujitahini kama mu katika imani.” Wanafunzi walikuwa wamemaliza mitihani ya kuandika, yeye akasema, lakini wao wataendelea kuelekeana na mitihani mingine katika migawo yao ya umisionari. Jinsi ambavyo wao watakabiliana na mitihani hiyo ndilo jambo ambalo litaamua fanikio lao wakiwa wamisionari. Wao wanahitaji kujikinga dhidi ya kuwa na uhakika wa kupita kiasi ndani yao wenyewe kwa kutii shauri hili: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Wakorintho 10:12) Wao watazidi kufanya maendeleo ikiwa wataendeleza mwelekeo mwema wa kiakili.
Mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi, Joel Adams, alifuata. Yeye alisema juu ya habari: “Fikiri Kama Yesu, Onyesha Upendezi wa Kibinafsi Katika Wengine.” Ni kielelezo kizuri kama nini ambacho Yesu aliweka katika jambo hilo! Kielelezo chake cha kutokuwa na ubinafsi na cha unyenyekevu kinakaziwa kwetu kwenye Wafilipi 2:3-5. Ikiwa watu fulani ni jaribu kwetu sisi kwa sababu ya makosa yao ya kupungukiwa au ukosefu wa hadhari, acheni sisi tujiondokee kuwaonyesha fadhili. Wakati wa ule mtaala wa Shule ya Gileadi, wengi walionyesha upendezi katika wanafunzi; sasa ilikuwa juu yao kufanya ivyo hivyo kuelekea wengine. Wamisionari walio na mafanikio zaidi ni wale ambao wanaonyesha upendezi katika desturi, lugha, mahitaji, na mambo kama hayo ya wengine.
Halafu, wanafunzi walitiwa moyo na mmoja ambaye alikuwa misionari kwa miaka mingi, Lloyd Barry, pia mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Yeye alisema juu ya kichwa cha habari “Mwimbieni Yehova,” kikitegemea msingi wa Zaburi 96:1, NW. Watu wa Yehova wanafurahia kuimba. Kuimba kunaambatana na furaha, na kwa hiyo yeye aliwatia moyo wanafunzi wasipoteze kamwe ile furaha ya kuletea wengine ule ukweli. ‘Ikiwa ninyi mtalazimika kujifunza lugha mpya,’ yeye akahimiza, ‘tieni moyo wenu ndani ya jambo hilo kutoka pale mwanzo. Ibilisi atajaribu kuwavunja ninyi moyo, kuwafanya mgonjweke hisia za kutaka kurudi nyumbani, kusababisha ukosefu wa umoja katikati yenu. Msimruhusu kamwe hata inchi moja!’ Ndugu Barry alirejeza kwenye yule “mmisionari wa wamisionari,” Edwin Skinner, ambaye amekuwa katika mgawo wake wa nchi ya kigeni katika India kwa miaka 60, na ambaye sasa kwenye umri wa miaka 93 bado anafanya kazi ya siku nzima. Kulingana na Ndugu Skinner, ufunguo wa kufanikiwa ukiwa misionari umo katika maneno manne: “Unyenyekevu ndio ufunguo mkuu!”
Kufuata maelezo hayo, mwenyekiti alisoma simu-barua kadha zikiwapongeza wanafunzi na kuwatolea ukaribishaji. Ujumbe ulipokewa kutoka Bolivia, Kanada, Ekwedori, Honduras, Hispania, Sweden, na Trinidad.
Jack Redford, mmoja wa walimu wa Shule ya Gileadi, alitoa hotuba juu ya habari “Endelea Kuwa Rafiki ya Yehova.” Yeye alianza kwa kusema kwamba kuna vyama vingi vya kibiashara ambavyo vinatoa mazoezi juu ya mtu kupata fanikio katika kazi kwa kuvutia watu wawe marafiki wanachama. Wanafunzi, wakiwa wamisionari wa wakati ujao, wamefunzwa pia jinsi ya kuvutia watu wawe marafiki, lakini si kwa ajili ya pato la ubinafsi, bali ili kwamba watu hao waweze kuwa rafiki za Mungu. ‘Yenu ni maisha ya kujidhabihu,’ akasema msemaji. ‘Ninyi mlipokea bure, toeni bure. Hakuna uradhi au furaha iliyo kubwa kuliko ile ya kufanikiwa katika kusaidia watu wawe rafiki za Mungu. Urafiki pamoja na Mungu ndio heshima kubwa zaidi ambayo kiumbe ye yote anaweza kuwa nayo. Yakobo 2:23 husema kwamba Abrahamu akawa rafiki ya Yehova kwa sababu ya kujizoeza imani katika Mungu. Yeye alienda kwenye nchi ya kigeni na hakutazama nyuma; wala ninyi wamisionari hampaswi kutazama nyuma, bali mtazame mbele kwenye baraka ambazo zitakuwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.’
Ulysses Glass, mwalimu mmoja wa Gileadi na mwandikishi wa ile shule, sasa alisema juu ya habari “Lile Somo la Hatima.” Yeye alisema kwamba wanafunzi walikuwa wamejifunza jinsi hasa sheria za Yehova zilivyo za mfiko wa mbali na zenye kutaka utii. Kwa njia ya kielelezo, yeye alionyesha mambo mengi madogo-madogo yaliyoshirikishwa na dhabihu zilizotolewa Siku ya Upatanisho na wale wanyama wengine ambao walihusika. (Walawi, sura 16) Yeye alisifu wanafunzi kwa uthamini wao wa moyoni wenye kina kirefu ulioonekana wazi na akasema kwamba Zaburi 145:7, NW, inaeleza vizuri mwelekeo wao wa kiakili: “Kwa mtajo wa ule wingi wa wema wako wao watabubujika, na kwa sababu ya uadilifu wako wao watalia kwa kupaaza sauti kwa furaha.” Katika umalizio wake, yeye alitumia pia maneno ya Mithali 3:5-7, NW akikazia uhitaji wao wa ‘kuitibari katika Yehova kwa moyo wao wote.’
Ndugu F. W. Franz, yule msimamizi wa Shule ya Gileadi mwenye umri wa miaka 94 na pia aliye msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti, aliitoa hotuba ya kumalizia ya asubuhi hiyo. Katika hiyo yeye alisimulia historia ya Sosaiti kutoka ule wakati wa msimamizi wa kwanza, C. T. Russell, mpaka kusimamishwa imara kwa ile Shule ya Gileadi. Utoaji wake wenye sulubu na idili ulithaminiwa sana na wote. Baada ya hotuba yake, wale wanafunzi 24 walipokea diploma zao pamoja na zawadi fulani-fulani, na ndipo mmoja wa wanafunzi akasoma barua nzuri ikionyesha uthamini wa wanafunzi kwa msaada wote ambao wao walikuwa wamepokea kutoka Baraza Linaloongoza na pia kutoka kwa jamaa ya Betheli.
Baada ya kituo cha saa zipatazo mbili hivi, Phil Wilcox, mshiriki wa Halmashauri ya Mashamba ya Mnara wa Mlinzi, aliendesha funzo lililofupishwa la somo la Mnara wa Mlinzi wa karibuni zaidi ambamo maswali ya funzo yalijibiwa na wanafunzi. Hiyo ilifuatwa na programu ya wanafunzi ambamo wao walirudia kuigiza vituko vya mambo yaliyoonwa ambayo wao walifurahia walipokuwa wakitoa ushuhuda nyakati za alasiri za Jumatano katika mji wa New York. Hiyo ilikuwa sehemu ya mazoezi yao ya Gileadi. Walionyesha waziwazi sana pia matatizo mbalimbali ambayo wao wangeweza kutazamia kukutana nayo wakati wangefika kwenye migawo yao ya nchi za kigeni.
Ukiwa umalizio wenye kufaa wa programu nzima ile, wanafunzi walitoa mwigizo wa Kibiblia wenye mavazi-miigizo ukiwa katika sehemu mbili, ukikazia uzito wa nyakati ambamo sisi tunaishi. Mwigizo huo ulifanya hivyo kwa kulinganisha siku zetu na vipindi vya hukumu vya wakati uliopita. Saa 10:15 alasiri, ulipoimbwa wimbo “Ongezeko la Theokrasi” na sala yenye kutolewa na Milton Henschel mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ile programu ya kufurahisha sana ilifikia mwisho.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Darasa lenye kuhitimu la 83 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi
Katika orodha iliyo chini, safu zimehesabiwa kutoka mbele kwenda nyuma na majina yameorodheshwa kutoka kushoto kwenda kuume katika kila safu. (1) Melin, D.; Goode, M.; Ramos, M.; Chow, N.; Hermanson, A.; Dagostini, D. (2) David, E.; DiPaolo, A.; Neiman, D.; Shephard, J.; Foster, M.; Ramos, R. (3) Foster, W.; Melin, D.; Fristad, D.; Fristad, R.: White, L; Dagostini, F. (4) Neiman, D.; Ness, S.; Shephard, D.; Goode, J.; White, K.; Hermanson, L.