Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Wanachuo fulani wanakazania kwamba neno“kamba”linapasa lichukue mahali pa “ngamia”kwenye Mathayo 19:24, ambayo inasomwa hivi:“Ni rahisi zaidi ngamia kupenya tundu ya sindano.” Ni neno jipi lililo sahihi?
Wanachuo fulani wa Biblia wanakata shauri kwa njia yenye makosa kwamba maneno ya Yesu hapa yaliandikwa hapo awali katika Kiaramu. Neno la Kiaramu ambalo lilitumiwa katika fasiri kama hizo gam·la’ʹ linaweza kumaanisha “ngamia.” Hata hivyo, kwa kutegemea habari zinazozunguka andiko, neno hilo linaweza kufasiriwa “kamba kubwa na boriti.” Lakini kulingana na Papias wa Hierapolis, ambaye labda ni mtu aliyeishi wakati mmoja na mtume Yohana, Mathayo aliandika usimulizi wake wa Injili hapo awali katika Kiebrania, si Kiaramu, na baada ya hapo akautafsiri katika Kigiriki. Neno la Kiebrania kwa ngamia (ga·malʹ) ni tofauti sana na maneno yaliyotafsiriwa kamba (cheʹvel) au ugwe (‛avothʹ), na ni hakika kwamba lazima Mathayo awe alichagua neno la Kigiriki lililo sahihi.
Hati za mkono zilizo za zamani zaidi na zenye kutegemeka zaidi za Kigiriki (Sinaiticus na Vatican Na. 1209) zina neno kaʹme·los, ambalo linamaanisha ngamia. Neno ilo hilo linatumiwa kwenye Mathayo 23:24, ambapo hapana shaka sana kwamba neno “ngamia” ndilo lililokusudiwa.
Muda wa karne zilizopita wengine wamejaribu kupunguza uzito wa misemo ya Yesu yenye mkazo mwingi mno. Watu fulani hata walijipatia uhuru wa kupita kiasi kuhusiana na andiko takatifu hilo. Kutoka karibu karne ya tano, neno linalofanana nalo kaʹmi·los linapatikana kwenye andiko hilo katika hati fulani za mkono za Kigiriki. Neno hilo linalopatikana mara chache sana linamaanisha “kamba, amari ya merikebu.” Kulingana na A Greek-English Lexicon of the New Testament kilichotungwa na Arndt na Gingrich, neno hilo “halina mahali palo katika lile AJ [Agano Jipya].” Wanachuo wa Kigiriki Westcott na Hort wanalaumu neno-mbadala hilo kuwa lilisababishwa na Mkristo wa kujidai wa karne ya tatu Cyril wa Alexandria, ambaye alishikilia kwamba neno lililotumiwa na Mathayo (kaʹme·los) lingeweza kumaanisha amari (uzi mnene wa chuma) akisema: “Ni desturi ya wale walio na ujuzi mwingi katika ubaharia kuziita amari zilizo nene zaidi ‘ngamia.’” Hata hivyo, juu ya wazo hilo Westcott na Hort wanasema: “Hilo ni kosa kwa uhakika.”
Lile wazo la ngamia mkubwa sana akijaribu kujipenyeza aingie katika tundu la sindano ndogo sana ya kushonea “linasikika kuwa limetiwa chumvi ya Mashariki,” kulingana na kitabu kimoja cha marejezo. Kwa kweli, katika kuzungumza juu ya watu fulani mmoja mmoja waliokuwa na sifa kubwa ya kuwa na uelekevu mwingi sana hata ikaonekana kama kwamba wao walifanya mambo yasiyowezekana, The Babylonian Talmud inasema: “Wao wanavuta ndovu apite katika tundu la sindano.” Kwa hiyo Yesu alikuwa akitumia mfano wa jambo halisi lenye kutendeka nchi za Mashariki kukazia kutowezekana kwa jambo fulani huku akitumia mtofautisho wenye kueleweka wazi sana. Kwa kweli, haingewezekana kupitisha kama uzi kitu cho chote kikubwa katika tundu la sindano—kiwe ni kamba, ngamia au ndovu.
Yesu hakuwa akisema kwamba haikuwezekana kwa mtu tajiri kupata uzima, kwa maana watu fulani mmoja mmoja matajiri walikuja kuwa wafuasi wake. (Mathayo 27:57; Luka 19:2, 9; Yohana 19:38, 39) Lakini kabla tu Yesu hajatoa ‘usemi mgumu’ huo, kijana mwanamume mmoja tajiri alikuwa ameepuka kukubali nafasi kubwa za kiroho kwa sababu ya kupenda sana “miliki nyingi” zake. (Mathayo 19:16-22, NW) Haingewezekana kwa mtu tajiri yo yote mwenye mwelekeo huo kurithi uzima wa milele. Ni kwa msaada mkubwa mno wa Mungu kwamba mtu kama huyo angeweza kubadilika na kupokea wokovu ambao lazima uje kupitia uwezo wa Mungu.—Mathayo 19:25, 26.