Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Ni nani waliokuwa “wale kumi na wawili” ambao Yesu alijionyesha kwao, kama inavyotajwa katika 1 Wakorintho 15:5, NW?
Ule mwonekano unaotajwa katika 1 Wakorintho 15:5 unaelekea kuwa ni ule ulioandikwa katika Yohana 20:26-29, ambao ulimhusu Tomasi. Hata hivyo, jambo hili linarejezelea kwenye wale mitume wakiwa kikundi na inaelekea kwamba Mathiya alikuwamo.
Katika kuzungumza juu ya ufufuo, Paulo aliandika juu ya mionekano ya Yesu kwa wanadamu baada ya Yeye kuinuliwa. Mtume alisema kwamba Kristo “alijionyesha kwa Kefa, halafu kwa wale kumi na wawili. Baada ya hapo yeye alijionyesha kwa kadiri ya kwenda juu ya ndugu mia tano.”—1 Wakorintho 15:5, 6, NW.
Kutoka miongoni mwa wale ambao walimfuata wakiwa wanafunzi wake, Yesu alichagua mitume 12. (Mathayo 10:2-5) Yuda Iskariote alikuwa mmoja wa wale 12, lakini yeye aligeuka kuwa msaliti, akamsaliti Yesu, halafu akajinyonga mwenyewe. (Mathayo 26:20-25; 27:3-10) Kwa hiyo wakati wa kifo na kufufuliwa kwa Kristo walikuwako mitume 11 tu waaminifu kati ya wale 12 wa asili. Yesu alijionyesha kwa wanafunzi mbalimbali kati ya kufufuliwa na kupaa kwake kwenda mbinguni. Baada ya hapo mitume waling’amua ule uhitaji wa kuweka mwingine mahali pa Yuda. Kwa mwongozo wa kimungu, Mathiya alichaguliwa, “naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na mmoja.”—Matendo 1:6-26.
Hivyo watu fulani wameshangaa wakiuliza ni kwa sababu gani Paulo angeandika kwamba Yesu alijionyesha kwa “wale kumi na wawili,” kwa kuwa wakati huo Yuda alikuwa mfu na Mathiya alikuwa hajachaguliwa bado. Kwa kutaja wazi, wakati huo kulikuwa na “mitume kumi na mmoja” tu ambao ndio waliokuwa hapo asili wametajwa kwa majina na kutumwa na Yesu.—Luka 6:13-16.
Ni jambo la kawaida kusema juu ya kikundi fulani kwa ujumla hata ikiwa mshiriki mmoja hayupo. (“Baraza la wakurugenzi liliamua kwamba . . .” “Baraza la wazee lilikutana . . . ”) Kwa hiyo ule mtajo “wale kumi na wawili” huenda sana ukawa ulitumiwa kurejezelea kwa kile kikundi kizima cha mitume, hata ikiwa mmoja au wawili hawakuwapo katika pindi moja. (Linganisha Matendo 6:1-6.) Wakati Yesu alipojionyesha mara ya. kwanza kwa wanafunzi katika chumba kilichofungwa kwa kufuli, “Tomasi, mmoja wa wale kumi na wawili,... hakuwa pamoja na wao.” Siku nane baadaye yeye alikuwapo na shaka lo lote alilokuwa nalo liliondolewa. (Yohana 20:19-29, NW) Ingawa Mathiya hakuwa ametajwa kwa jina wakati huo kwamba ndiye angechukua mahali pa Yuda, yeye alikuwa mwanafunzi kwa muda mrefu. (Matendo 1:21,22) Kwa kuwa yeye alishiriki, kwa ukaribu pamoja na wale mitume wa asili na muda mfupi baada ya hapo ‘alihesabiwa kuwa pamoja nao, lile elezo lenye kuelekeza nyuma kuhusu kujionyesha kwa Yesu kwa “wale kumi na wawili” inaelekea kwamba lilitia ndani Mathiya.