Misri ya Kale ya Kwanza ya Zile Serikali Kubwa za Ulimwengu
MISRI—bara la kale la wale Mafarao na ule Mto Naili—ilikuwa moja ya vyanzo vikubwa vya mwerevuko katika ulimwengu. Sanaa ya bara hilo inapamba majumba yenye sifa kubwa ya kuhifadhia vitu vya kihistoria. Historia yalo inasimuliwa katika vitabu vya mafundisho ya shule. Majengo yalo makubwa sana ya ukumbusho yanastaajabisha sana watalii. Zaidi ya hilo, matukio mengi ya Kibiblia ama yalitukia ama yalihusika katika bara hilo. Misri na watu wayo wanafanyiwa marejezo ya kimaandishi zaidi ya mara 700 katika Biblia.
Hata hivyo, wewe unajua nini kwa kweli juu ya Misri ya kale? Kujifunza mengi zaidi juu yayo kutakusaidia wewe ufahamu mambo mengi yanayotajwa katika Biblia.
Katika Misri, wachimbuzi wa vitu vya kale wamepata mengi ambayo yanathibitisha maandishi ya kumbukumbu ya Biblia. Mathalani, fikiria ule usimulizi juu ya Yusufu. Majina, mitajo ya cheo, cheo cha Yusufu akiwa maneja wa nyumba, kile cheo alichopewa yeye kuwa mtawala wa pili katika bara hilo na kuwa msimamizi wa ugawaji chakula, yale mazoea ya maziko ya Kimisri, na hata lile zoea la waokaji kuchukua vikapu vya mkate vikiwa juu ya vichwa vyao—yote hayo yamepatwa kuwa yanapatana na desturi za Kimisri za wakati huo.—Mwanzo sura 39-47; 50:1-3.
Lile Bara na Watu Walo
Misri inategemea ule Mto Naili. Bonde lenye rutuba nyingi la mto huo, ambalo lina wastani wa kilometa zapata 19 katika upana kutoka Aswan mpaka Cairo, linatandaa kuelekea kaskazini kama utepe mwembamba wa nguo wa kijani kibichi kuvuka lile jangwa la Kiafrika lenye ukame. Katika wakati uliopita, mafuriko ya kila mwaka ya bara hilo yalileta mchanga na matope yenye kutia rutuba katika udongo, na vitu hivyo vilifanya Misri iwe nchi yenye kupeleka bidhaa za chakula na kuwa mahali pa kimbilio katika wakati wa ukosefu wa chakula. (Mwanzo 12:10) Mafunjo, ambayo yanapatikana kando-kando ya kingo za mto huo, yalifanywa yakawa karatasi iliyo ya mapema zaidi ya zote.
Ile delta pana, ambapo maji ya Naili yanasambaa kwa umbo la kipepea-hewa kabla ya kumiminika kuingia ndani ya ile Bahari ya Kati ya rangi-bluu, inaitwa Misri ya Chini. Hapa, inaonekana, ndipo lililokuwa “lile bara la Gosheni,” ambapo Waisraeli waliishi wakati wa ugeni wao mrefu katika Misri.—Mwanzo 47:27, NW.
Dini ya Kimisri
Wamisri wa kale waliitikadi kwamba Farao wao alikuwa mungu. Uhakika huo unaongeza maana kwenye swali la madharau yenye kiburi ambalo Farao alimuuliza Musa: “Yehova ni nani, ili kwamba mimi nipaswe kutii sauti yake?” (Kutoka 5:2, NW) Wamisri walikuwa pia na miungu mingine mingi. Majina ya miungu ipatayo 740 kati ya hiyo yalipatwa katika orodha moja iliyogunduliwa katika lile kaburi la Thutmose wa 3. Wamisri waliabudu mafungu matatu-matatu ya miungu, au utatu-utatu, na moja la fungu la miungu hiyo ambalo lilipendwa zaidi na watu wengi lilikuwa lile fungu la Osirisi, Isisi, na Horusi.
Mingi ya miungu iliyo mashuhuri zaidi ya Misri ilifananishwa kwa miili ya kibinadamu na vichwa vya wanyama. Wamisri waliwakilisha Horusi na kichwa cha ndege-kipanga na wakawakilisha Thoth na kichwa cha korongo wa maji au sokwe. Paka, mbwa-mwitu, mamba, nyani-uchi, na ndege wa namna-namna walifikiriwa kuwa watakatifu kwa sababu ya ushirika wao pamoja na miungu fulani. Yule fahali Apisi, ambaye alionwa kuwa umbo lililogeuka upya kutokana na yule mungu Osirisi baada ya maisha ya kwanza, aliwekwa katika hekalu moja kule Memphis, halafu akapewa maziko yenye madoido mengi na hata maiti yake ikagandishwa alipokufa. Vile vijiwe vya Kimisri vyenye sifa kubwa, ambavyo vilivaliwa kama punje za shanga ili ziwe hirizi za kutoa himaya ili kutopatwa na mabaya, vilikuwa viwakilishi vya mdudu-tutua wa samadini (dundu)—ambaye alifikiriwa kuwa udhihirisho wa yule mungu-muumba.
Ijapokuwa walikaa muda mrefu katika Misri na walikaribiana na watu wa bara hilo, Waisraeli walikuwa na Mungu mmoja tu, Yehova, na walipaswa kumtumikia yeye peke yake. Wao walionywa wasifanye mfano wo wote wa kidini—ama wa Mungu mwenyewe ama wa ndege, mnyama, samaki, au kitu cho chote kingine. Ibada yao ya ndama wa dhahabu muda mfupi baada ya kutoka kwao Misri huenda ikawa ilitokana na uvutano wa Kimisri.—Kutoka 32:1-28; Kumbukumbu 4:15-20.
Itikadi Katika Kutokufa
Wamisri walikuwa waitikadi imara katika kutokufa. Hivyo, watawala wa Misri walitayarisha makaburi yenye madoido mengi, yaliyojazwa mahitaji ya maisha na anasa nyingi, wakitumainia kujipatia furaha ya milele katika maisha ya baadaye. Zile piramidi ndicho kielelezo cha kutokeza zaidi juu ya zoea hilo.
Vito vya kidhahabu, mavazi, fanicha, divai, chakula, vijungu, masanduku ya pembe-ndovu, na hata vibamba vya mawe ya kusagia rangi ya macho (wanja) viliwekwa vyote kwa ujalifu katika makaburi ya Wamisri. Iliitikadiwa kwamba vitu hivyo vingeweza kutumiwa katika maisha ya baada ya makaburini. Katika nyakati za mapema zaidi, watumwa waliuawa na kuzikwa pamoja na mabwana-wakubwa zao, wawatumikie wao baada ya kifo. Mkusanyo mmoja wa maandishi yenye nguvu za kiuganga ambao umejulikana kuwa “Kitabu cha Wafu” umepatwa ndani ya maelfu ya majeneza ya Kimisri. Ilitumainiwa kwamba maandishi hayo yangesaidia mtu mfu ashinde zile hatari za namna-namna za maisha ya baadaye.
Maoni ya Waisraeli yalikuwa tofauti kama nini! Wao walijua kwamba, kama vile Biblia ingesema baadaye, kwamba “wafu hawajui neno lo lote.” Na wakati mwanadamu anapokufa, “siku hiyo mawazo yake yapotea.”a Tumaini lao kwa maisha ya wakati ujao lilikuwa katika ufufuo.—Mhubiri 9:5,10; Zaburi 146:4; Ayubu 14:13-15.
Nani Aliishi Lini?
Wachunguzi wa vitu vya kale vya Wamisri wanatambua “nasaba” 31 za wafalme Wamisri na kusema juu ya ule Ufalme wa Zamani (Nasaba 3-6), ule Ufalme wa Kati (Nasaba 11,12), na ule Ufalme Mpya (Nasaba 18-20). Lakini njia hiyo ya kukadiria hesabu iko mbali na usahihi. Hiyo inahusisha ndani maandishi yenye kutiliwa mashaka na yenye kutegemea vijipande-vijipande vya habari zisizo kamili na huenda hata yakawa yanatia ndani wafalme kadha waliokuwa wanatawala katika majimbo tofauti wakati ule ule mmoja, badala ya kuwa walifuatana-fuatana kutawala mmoja baada ya yule mwingine.b
Wakati Musa alipoanza kuandika vile vitabu vya kwanza vya Biblia, yeye alifuata ile ambayo inaonekana ilikuwa ndiyo desturi ya Wamisri wenyewe ya kurejeza kwenye mfalme wao kwa kumwita “Farao,” bila kutumia jina la kibinafsi. Hivyo, sisi hatujui jina la Mafarao ambao Abrahamu na Yusufu walijua au ni yupi aliyetawala wakati wa kutoka kwa Israeli katika Misri. Hata hivyo, ule mtajo wa cheo “Farao” ulianza baadaye kufuatanishwa pamoja na jina la mfalme mwenyewe, hiyo ikiwezesha kuhusianisha matukio ya Kibiblia pamoja na orodha ya wafalme Wamisri. Hapa pana baadhi ya Mafarao wenye upendezi hususa kwa mwanafunzi wa Biblia:
Akhenaton (wa ile inayoitwa ati Nasaba ya 18) alikuwa mwabudu mwenye hari wa ile sahani-jua Aton. Katika 1887 mkusanyo wa bao za udongo zipatazo 377 ulipatwa kule Tel el-Amarna, zapata kilometa 320 kusini mwa Cairo. Bao hizo zinazopendeza zilikuwa barua za kibalozi zilizopokewa na Akhenaton na baba yake Amenhotep wa 3. Zilizotiwa ndani zilikuwa barua kutoka kwa watawala wa Yerusalemu, Megido, Hazori, Shekemu, Lakishi, Hebroni, Gaza, na mikoa-miji mingine katika Palestina. Labda zikiwa zimeandikwa muda mfupi kabla ya Israeli kuingia Kanaani, barua hizo zilifunua mizozano ya kivita na matendo mabaya ya siri. Hizo pia zilionyesha kwamba kila mji ulikuwa na mfalme wao mwenyewe, kama vile kitabu cha Biblia cha Yoshua kinavyoonyesha.
Tutankhamen, mwana-mkwe wa Akhenaton, ndiye yule “Mfalme Tuti” mwenye sifa kubwa ambaye samani za kaburi lake la kidhahabu lenye fahari nyingi zilifukuliwa na wachimbuzi wa vitu vya kale na zimeonyeshwa katika majumba mbalimbali ya kuhifadhia vitu vya kihistoria. Samani hizo ni wonyesho wa kutokeza wa ule utajiri wa Mafarao. Utajiri kama huo ndio ambao mapema zaidi Musa alikuwa ameupa kisogo wakati yeye ‘alipokataa kuitwa yule mwana wa binti wa Farao, akichagua kutendwa vibaya pamoja na wale watu wa Mungu badala ya kuwa na ule mfurahio wa muda tu wa dhambi.’—Waebrania 11:24, 25, NW.
Merneptah alikuwa wa ile “Nasaba ya 19.” Juu ya kifaa-kumbukumbu cha ushindi kilichopatwa katika hekalu moja kule Thebes, Farao huyo aliandika kwamba “Israeli amelazwa ukiwa, mbegu yake haipo.” Huo ndio mtajo mmoja tu unaosema waziwazi juu ya Israeli kama taifa zima uliopata kuonekana katika maandishi ya kale ya Kimisri. Ingawa ni dhahiri hayo ni majisifu ya bure tu, dai hilo linaonekana kama linaonyesha kwamba ule ulemezo wa Waisraeli juu ya Kanaani ulikuwa tayari umetukia. Hivyo, mlemezo huo wa 1473 K.W.K. lazima uwe ulitukia kati ya wakati ambao Akhenaton alipokea zile barua za Tel el-Amarna na zile siku za Merneptah.
Shishak (Sheshonk wa 1, “Nasaba ya 22”) ndiye Farao wa kwanza kutajwa kwa jina katika Biblia. Akiwa na kani ya kijeshi yenye magari-vita na wapanda-farasi, yeye alivamia Yuda, akatisha Yerusalemu, na ‘akachukua zile hazina za ile nyumba ya Yehova na zile hazina za ile nyumba ya mfalme. Kila kitu yeye alichukua.’ (2 Nyakati 12:9, NW) Tukio hilo linahakikishwa na mchoro wa kuchongwa ulio juu ya ukuta wa kusini mwa hekalu la Amon kule Karnaka (-Thebes ya kale). Mchoro huo unaonyesha wafungwa 156 waliotiwa pingu, kila mmoja akiwakilisha mji au kijiji kimoja kilichotekwa, kutia na Megido, Shunemu, na Gibeoni. Miongoni mwa mahali-mahali palipotekwa, Shishaki hata anaorodhesha ule “Uwanja wa Abramu”—rejezo lililo la mapema zaidi kuhusu Abrahamu katika maandishi ya kumbukumbu za Kimisri.
Serikali Kubwa Nyingine za Ulimwengu Zainuka
Mwishowe, mahali pa Misri palichukuliwa na Ashuru ikiwa ndiyo serikali kubwa yenye kutawala ulimwengu. Lakini Misri ilibaki ikiwa kani yenye nguvu nyingi za kisiasa. Hoshea, yule mfalme wa mwisho wa ule ufalme wa Israeli wa kaskazini wenye makabila kumi, alitunga hila pamoja na Mfalme So wa Misri katika jitihada isiyofanikiwa ya kupindua lile kongwa la Ashuru. (2 Wafalme 17:3, 4) Miaka baadaye, wakati wa utawala wa Mfalme Hezekia wa Yuda, Mfalme Tirhakah wa Ethiopia (labda yule mtawala Mwethiopia wa Misri, Farao Taharka) alipiga miguu kijeshi kuingia Kanaani na kwa muda akaondoshea kando shambulio la Senakeribu mfalme Mwashuru. (2 Wafalme 19:8-10) Maandishi ya kila mwaka ya Senakeribu mwenyewe, ambayo yalipatwa katika Ashuru, yanaonekana kuwa yanarejeza kwenye jambo hilo wakati yanaposema hivi: “Mimi binafsi niliteka wakiwa hai. . . wale waendesha-magari-ya-vita wa yule mfalme wa Ethiopia.” Jiwe la Senakeribu la Taasisi ya Kimashariki, Chuo Kikuu cha Chicago.
Isaya nabii wa Yehova alikuwa ametabiri kwamba Misri ingeingizwa ndani ya “ule mkono wa bwana-mkubwa mwenye ugumu” na kwamba mfalme “mwenye imara” angetawala juu ya Wamisri. (Isaya 19:4, NW) Ukweli wa unabii huo unahakikishwa na hati moja ya Kiashuru ambamo Esari-haddoni mwana wa Senakeribu anajisifu kuhusu mlemezo wake juu ya Misri, akisema: “Mfalme wa nchi hiyo, Tirhakah, mimi nilijeruhi mara tano kwa mirusho ya mishale na nikatawala juu ya nchi nzima yake.”
Farao Neko alipiga miguu kijeshi kuelekea kaskazini wapata mwaka 629 K.W.K. ili akazuie yale majeshi yaliyokuwa yakija kutoka juu ya serikali kubwa ya tatu ya ulimwengu, Babuloni. Biblia inasema kwamba Yosia wa Yerusalemu alijaribu bila hekima kukomesha kani za Kimisri kule Megido na akashindwa na kuuawa.c (2 Nyakati 35:20-24) Yapata miaka minne baadaye, katika 625 K.W.K., Farao Neko mwenyewe alishindwa na Wababuloni kule Karkemishi. Biblia na hata Maandishi-Tarehe ya Kibabuloni yanarejeza kwenye tukio hilo, ambalo liliwapa Wababuloni ukubwa wa kuwa juu ya Esia ya magharibi.
Katika 525 K.W.K. Misri ilikuja chini ya udhibiti wa ile serikali kubwa ya nne ya ulimwengu, Umedi-Uajemi. Karibu karne mbili baadaye, katika 332 K.W.K., Aleksanda Mkuu alitokea katika tamasha na akaleta Misri chini ya ile serikali kubwa ya tano ya ulimwengu, Ugiriki. Aleksanda ndiye aliyeweka msingi wa ule mji wa Aleksandria katika eneo la delta ya Naili katika Misri, ambapo, wapata mwaka 280 K.W.K., tafsiri ya kwanza ya Biblia kutoka Kiebrania kuingia katika Kigiriki ilianza. Tafsiri hiyo, ambayo ilikuja kujulikana kuwa ile Septuagint, ndiyo Biblia iliyotumiwa na wafuasi wa Yesu katika ulimwengu wenye kusema Kigiriki.
Katika wakati wa Roma, ile serikali kubwa ya sita ya ulimwengu, Yesu aliletwa Misri akiwa mtoto mchanga ili kumwokoa yeye kutoka kwa Herode mwenye wivu. (Mathayo 2:13-15) Wamisri walikuwa katika Yerusalemu siku ile ya Pentekoste 33 W.K. kusikia yale mahubiri mazuri ajabu ya habari njema za Kikristo. Na yule Mkristo mfasaha wa maneno wa karne ya kwanza Apolo alikuja kutoka huku—Matendo 2:10; 18:24.
Ndivyo, Misri na Wamisri wamekuwa na sehemu mashuhuri katika historia ya Biblia, na vitu vingi vilivyogunduliwa kwa uchimbuzi vinahakikisha mambo ambayo Maandiko yanasema juu ya bara hilo la kale. Kweli kweli, Misri ilikuwa mashuhuri sana hivi kwamba katika vifungu fulani vya kiunabii, hiyo inafananisha ulimwengu wote ulio chini ya utawala wa Shetani. (Ezekieli 31:2; Ufunuo 11:8) Lakini Misri ya kale, ijapokuwa yenye imara ikiwa serikali kubwa ya ulimwengu, haikuweza kamwe kuondoshea kando ule utimizo wa makusudi ya Yehova. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa pia juu ya ile serikali kubwa ya pili ya ulimwengu ya historia ya Biblia, Ashuru, kama vile sisi tutaona katika toleo la wakati ujao la gazeti Mnara wa Mlinzi.
[Maelezo ya Chini]
a The Jewish Encyclopedia inasema: “Ile itikadi ya kwamba nafsi inaendeleza kuwako kwayo baada ya kukoma kwa mwili. . . haifundishwi waziwazi mahali popote katika Andiko Takatifu.”
b Kwa zungumzo linalopendeza juu ya matatizo yanayoshirikishwa na orodha hizo, ona kile kitabu Aid to Bible Understanding, kurasa 324-325, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
c Hilo lilikuwa moja ya yale mapigano ya kukata maneno yaliyofanywa kule Megido, jambo ambalo linaongoza mahali hapo patumiwe kama mfano wa pigano la mwisho kabisa la Mungu la kukata maneno dhidi ya mataifa ya kibinadamu yenye uasi, katika Har–Magedoni, au Armagedoni.—Ufunuo 16:16.
[Ramani katika ukurasa wa 23]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mediterranean Sea
Carchemish
Euphrates
Megiddo
Jerusalem
Alexandria
GOSHEN
Memphis
Nile
LOWER EGYPT
Thebes
[Credit Line]
Based on a map copyrighted by Pictorial Archive (Near Eastern History) Est. and Survey of Israel
[Picha katika ukurasa wa 24]
Mungu wa Kimisri akionyeshwa kuwa na mwili wa kibinadamu na kichwa cha ndege-kipanga
[Credit Line]
Courtesy of the British Museum, London
[Picha katika ukurasa wa 25]
Sehemu ya “Kitabu cha Wafu’’ ambacho kilipatwa ndani ya jeneza moja la Kimisri
[Credit Line]
Courtesy of the Superintendence of the Museo Egizio, Turin
Jeneza la Kimisri na kifuniko cha mwili uliogandishwa kuhifadhiwa
[Credit Line]
Courtesy of the Superintendence of the Museo Egizio, Turin
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mfalme Tutankhamen akiwa pale karibu na mungu Amoni aliyeketi
[Credit Line]
Courtesy of the Superintendence of the Museo Egizio, Turin