Sala Juu ya Mlima Hiei—Je! Ni Utatuzi wa Vipingamizi vya Amani ya Ulimwengu?
JE! SALA italeta amani ya ulimwengu?“Amani haitakuja kwa kusali tu. Mambo si rahisi hivyo,” akasema Gijun Sugitani, mtengeneza ratiba ya mkutano mmoja wa sala uliofanywa katika Agosti 1987 katika Japani. “Lakini hata sifikiri kwamba amani itapatikana bila sala.” Maoni yake yalipatana kabisa na yale yaliyoshikiliwa na Wajapani wapatao 500 na wajumbe 24 wa kutoka ng’ambo waliohudhuria lile Kutano Kuu la Kidini la 1987 lililofanywa katika Kyoto, Japani.
Farakano Tendai la Kibuddha lilitetea huo mkutano wa sala kuwa ufuatisho wa ule uliofanywa katika 1986 kule Assisi (Italia) na likauratibu usadifiane tarehe pamoja na yale makumbuko ya mwaka wa 1,200 tangu Hekalu la Enryakuji lilipofunguliwa juu ya Mlima Hiei. Watu mmoja mmoja wenye mandhari-nyuma za maisha ya Kibuddha, Wakristo wa jina tu, wafuasi wa Confucius, Wahindu, Waislamu, Wayahudi, Wakalasinga, na Washinto walipokezana zamu kutoa sala juu ya mlima huo. Je! kweli kweli mkutano huo ulikuwa utatuzi wa vipingamizi vya amani ya ulimwengu?
Mkutano wa “Upangaji wa Maua”
“Kutano kuu hili ni upangaji wa maua ya kidini,” akasema Etai Yamada, yule mkuu wa makuhani na mwenyekiti mheshimiwa wa farakano la Tendai. “Hakuna lo lote la maua haya linalopoteza umbo na harufu yalo lenyewe.” Yeye alimaanisha kwamba maadamu dini hizo zimeungana kwa umoja katika tamaa ya kutaka amani ya ulimwengu, kila moja inaweza kudumisha itikadi zayo zinazopingana na zile nyingine, kama maua moja moja yaliyo katika upangaji mmoja.
Miongoni mwa “maua” mashuhuri yaliyokuwa katika mkutano huo alikuwamo mwakilishi wa Kanisa Katoliki, Francis Kardinali Arinze wa Idara ya Ukatibu wa Vatikani kwa Ajili ya Wasio Wakristo. Arinze alisoma ujumbe wa papa, ambao ulisema kwamba “amani haiwezi kupatikana bila sala, na ingawa vita huenda vikaanzwa na hesabu ndogo ya watu, kupatikana kwa amani kunahitaji ushirikiano ng umoja wa kila mtu.”—Mainichi Daily News: Agosti 5, 1987, uku. 12.
Ikiwa tumaini la kupata amani ya ulimwengu ‘linahitaji ushirikiano na umoja wa kila mtu. Mungu ambaye wao wanatolea sala ni mwenye nguvu jinsi gani? Wajumbe hao walisali kuomba amani, lakini wao wanaitikadi kwamba jitihada za kibinadamu ndizo zingeileta. Mkutano wao ungekuwa wonyesho wenye sura nzuri juu ya jitihada zao wenyewe, kama upangaji maridadi wa maua.
Inapendeza kutazama upangaji wa maua, lakini pindi ile ya pekee ikiisha, maua hayo yasiyo na mizizi yanafifia pamoja na upendezi wayo. Ule uzuri wa ua moja moja na ile fahari ya upangaji huo vinapotea baada ya muda mfupi. Tena maua hayo hayakusudiwi kuzaa tunda. Je! hilo kutano kuu lilimalizika pia likiwa kama ‘upangaji wa maua’ ambao hauzai matunda?
Viongozi wenyewe wa kidini wenye kushiriki hawakuridhika na matokeo. “Wao wangalipenda kutaja wazi zaidi hatua ambazo dini hizo zinapasa kuchukua wakati ujao lakini walisema hakukuwa na wakati wa kutosha kwa mazungumzo kama hayo,” inaripoti Asahi Evening News. Hata hivyo, tokeo kama hilo lilitazamiwa. “Shabaha yetu,” akasema Takaaki Kobayashi, mmoja wa watengeneza ratiba ya lile kutano kuu, “ni kusikia madokezo ya kila dini juu ya njia zilizo bora za kupatia amani. Kawaida iliyo ya maana sana ni kwamba kila mshiriki lazima asikilize maoni ya wengine bila kutoa maelezo au kujibiza au kutokeza majadiliano.” Jitihada yao kwenye huo mkutano wa sala ilihusiana na kusikiliza wengine tu, si kufanya kitendo. Tokeo likawa kwamba, mkutano huo “ulishindwa kuonyesha ajenda ya waziwazi ya kutimiza malengo ya hilo kutano kuu.”
Je! Lilifaa kwa Wakristo wa Kweli?
Watu wanaojitahidi kufuata Yesu Kristo huenda wakashangaa kwa kujiuliza hivi: Je! Mkristo anapaswa kujiunga katika mkutano kama huo wa sala? Uhakika wa kwamba ulifanywa juu ya Mlima Hiei, ule mlima mtakatifu wa farakano moja la Kibuddha, unatokeza mambo yanayopasa kufikiriwa. Je! wewe unaweza kuwazia Yesu Kristo akishuka chini aje kwenye mlima mtakatifu wa Kibuddha ili kutoa sala ya kuomba amani?
Mtume Paulo alionya wafuasi wa Yesu Kristo hivi: “Msipate kuwa wenye kufungwa nira isivyofaa pamoja na wasio na itikadi. Kwa maana ni ushirika gani uadilifu unao pamoja na ukosefu wa kutii sheria? Au ni hisa gani nuru inayo pamoja na giza? Zaidi, ni upatani gani ulioko kati ya Kristo na Beliali? Au ni fungu gani alilo nalo mtu mwaminifu pamoja na asiye na itikadi? Na ni mwafaka gani linao hekalu la Mungu pamoja na sanamu? . . . “ ‘Kwa hiyo ondokeni kutoka miongoni mwao, na kujitenga ninyi wenyewe,’ asema Yehova, ‘na acheni kabisa kugusa kitu kisicho safi’ ”; “na mimi nitaingiza ninyi ndani.’ ”—2 Wakorintho 6:14-17, NW.
Je! kuzitoa sala kwenye mkutano fulani wa kuchanganya imani mbalimbali juu ya mlima mtakatifu wa Kibuddha hakungekuwa sawa na ‘kuwa wenye kufungwa nira isivyofaa pamoja na wasio na itikadi’? Basi, je! hiyo inamaanisha kwamba Wakristo wa kweli wanapaswa kuchukua mambo hivi hivi tu katika sala ya kuomba amani?
Sala ya Kuomba Amani
Sivyo hata kidogo! Katika unabii wake kuhusu “sehemu ya mwisho ya zile siku,” nabii Isaya alisema juu ya wengi ambao wangesema: “Njoni, ninyi watu, na acheni sisi twende juu kwenye mlima wa Yehova,” si kwenye ule Mlima Hiei wa Kibuddha. “Mlima wa Yehova” unafananisha ibada ya kweli ya yule Mungu wa Biblia. ‘Kwenda juu’ kwenye mlima huo kunatokeza nini? Ni kwamba, Yehova “atatuagiza juu ya njia zake, na sisi tutatembea katika vijia vyake,” akasema Isaya! “Yeye [Yehova] kwa uhakika atafanya hukumu miongoni mwa mataifa,” akaongezea Isaya. Tokeo ni kwamba, kungekuwa na amani ya ulimwengu, kwa maana nabii alitabiri kwamba waabudu wa kweli watapaswa ‘kufua panga zao ziwe majembe ya plau, na mikuki yao iwe mikasi ya kupogolea; taifa halitainua upanga juu ya taifa jingine, wala hawatajifunza vita tena zaidi.’—Isaya 2:2-4, NW.
Hali hiyo tayari imeenea sana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova na karibuni itafunika dunia nzima. Lakini jinsi gani? Yehova Mungu, si wanadamu, ndiye ataleta amani ya kudumu kupitia Ufalme wake. Huo utafagia dunia iishiwe kabisa na wavunja-amani wote na kuingiza mbio dunia-paradiso. (Ufunuo 11: 15, 18) Tofauti na maneno yaliyosemwa kwenye kutano kuu la kidini lililokuwa kama “upangaji wa maua” wenye kupendeza ambao hauzai matunda, maneno ya Yehova hayamrudii kamwe bila matokeo,—Isaya 55:11.
Mbona, basi, tusali kuomba amani ikiwa Mungu ataileta bila kujali jitihada za kibinadamu? Kwa kusali kwamba Ufalme wa Mungu uje, sisi tunaonyesha kwamba sisi wenyewe tunatamani sana amani na tunaonyesha imani yetu katika njia ya Mungu ya kuileta duniani. (Mathayo 6:9, 10) Kama sisi tutaona au hatutaona amani yenye kufanyizwa na Mungu, hiyo inategemea ‘kutumaini kwetu katika Yehova.’ Kwa hiyo njoo kwenye “mlima wa Yehova” na ujiunge katika sala ya kuomba ile amani ya kweli ambayo yeye ameahidi.—Zaburi 37: 9, 11, NW.
[Picture on page 8]
Inapendeza kutazama upangaji wa maua, lakini kusudi la upangaji huo si kuzaa matunda
[Picture on page 9]
Mlima Hiei, ule mlima mtakatifu wa farakano Tendai la Kibuddha, ambapo ule mkutano wa sala ulifanywa