Jumuiya ya Wakristo Yafichuliwa Kuwa Ndiyo Mwendelezaji wa Ibada Bandia
“Hili ndilo taifa ambalo watu walo wamekuwa hawakutii sauti ya Yehova Mungu walo, na wamekuwa hawakukubali nidhamu.”—YEREMIA 7:28, NW.
1, 2. Yeremia alitenda jinsi gani kwa kujibiza mgawo wake aliopewa na Mungu?
“MOTO wa usadikisho wa kweli uliwaka ndani yake; kulikuwa na kani yenye kulazimisha kunena ukweli, kugombeza lakini pia kutegemeza.” Kwa maneno hayo wanachuo wawili Waebrania wanaeleza fungu la kazi ya Yeremia. Hata ingawa mgawo wake kutoka kwa Mungu ulikuwa mkubwa kwa kadiri ya kuogopesha, yeye alijua kwamba ilikuwa lazima atimize daraka lake kuelekea taifa la Yuda. Ni kama vile yeye mwenyewe alivyojisemea: “Kwa maana neno la Yehova lilipata kuwa kwangu kisababishi cha suto na cha kufanyiwa mzaha mchana kutwa. Na mimi nilisema: ‘Mimi sitamtaja yeye, na mimi sitasema zaidi katika jina lake.’ “Ndiyo, mkazo na mnyanyaso huo ni kama ulipata kumzidia mno. Lakini je! yeye alichoka akaacha?—Yeremia 20:8, 9a, NW.
2 Yeremia aliendelea kusema: “Na katika moyo wangu lilithibitika kuwa kama moto unaowaka uliofungiwa katika mifupa yangu; na mimi nikachoka kulizuilia kwa ndani, na mimi nilikuwa siwezi kulivumilia.” (Yeremia 20:9b, NW) Yeremia hakuepa utume wake wa kutangaza hukumu za Mungu kwa Yuda.—Yeremia 6:10, 11.
Yeremia wa Ki-Siku-Hizi
3. Yesu na wanafunzi wake walionyesha mwelekeo gani kuelekea mgawo wao?
3 Yeremia, Kristo Yesu na wanafunzi wa Kikristo wa mapema walitangaza bila woga kwa Wayahudi na mataifa ujumbe usiopendwa na wengi juu ya Ufalme wa Mungu. Ingawa hapo kwanza walikuwa wametiwa jela kwa kuhubiri, Petro na mitume wale wengine walijibu washtaki wao wa kidini kwa ushujaa hivi: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” Kwa agizo la wenye mamlaka ya kidini, wao walipigwa mijeledi kwa sababu ya ujasiri wao. Mitume walitenda jinsi gani kwa kujibiza? “Kila siku katika hekalu na kutoka nyumba kwa nyumba wao waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya yule Kristo, Yesu.”—Matendo 5:29, 40-42; Mathayo 23:13-33, NW.
4. Ni akina nani ambao wamefuata kielelezo cha Yeremia katika karne ya 20, na wao wamefanya hivyo jinsi gani?
4 Hivyo Wakristo wapakwa mafuta wa mapema walitenda kama Yeremia. Ingawa walielekewa na magumu na adui za kidini wenye shingo ngumu, wao walitangaza hukumu za Mungu. Sasa, ni akina nani katika karne hii ya 20 ambao wamefuata kielelezo hicho hicho? Ni akina nani ambao wametangaza peupe na kutoka nyumba kwa nyumba hukumu za Mungu juu ya huu mfumo wa mambo na hasa juu ya mfanani wa Yerusalemu, Jumuiya ya Wakristo? Ithibati ya kihistoria imekuwa ikirundamana kwa zaidi ya miaka 68 kuonyesha kwamba jamii ya ki-siku-hizi ya Yeremia imekuwa ni kile kikundi kidogo lakini chenye ushujaa cha mashahidi wapakwa mafuta wa Yehova. Wao wameongezewa hesabu na kusaidiwa tangu 1935 na “mkutano mkubwa” unaokua wa mamilioni ya waandamani wenye nia, ambao pia wanajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa sauti yenye umoja, wao wametimiza fungu lao la kazi ya Yeremia kwa kulaumu wazi-wazi dini bandia kuwa ni mtego na hila.—Ufunuo 7:9, 10; 14:1-5.
Jumuiya ya Wakristo—Kwa Sababu Gani Ni Ulinganifu wa Ki-Siku-Hizi wa Yerusalemu?
5. Ni katika njia gani mbalimbali Jumuiya ya Wakristo ni kama Yerusalemu wa kale?
5 ‘Lakini,’ huenda mtu akauliza, ‘tunapata wapi ulinganifu kati ya Yerusalemu wa kale na Jumuiya ya Wakristo?’ Ni kwa sababu ya mielekeo na hali zenye ufanani zilizo katika Jumuiya ya Wakristo yenye kiburi leo. Wao wanatia itibari yao katika ‘miji mitakatifu’ yao na mahali-mahali pao patakatifu, kama vile Roma, Yerusalemu, Canterbury, Fatima, Guadalupe, na Zaragoza, kutaja pachache tu. Wao wanapenda kukweza makathedro yao, mabasilika, mahekalu, na makanisa, wakijisifu kwamba yalijengwa kwa ufundi wa kale na kwa ubuni wa kisanii, kama kwamba yanawapa wao msimamo fulani wa pekee kwa Mungu. Hata wanasema kwamba majumba yao ya kidini yalijengwa ‘kwa utukufu wa Mungu.’ Hata hivyo, ni mangapi ya majengo hayo yanayochukua jina la Yehova Mungu kikweli? Tofauti na hivyo, mtu anakumbushwa-kumbushwa juu ya wale wasanii waliochora ramani za kuyajenga, wale wachoraji na wachonga-maumbo ambao waliyapamba-pamba, wale wateja wakwasi ambao waliyalipia, au wale “watakatifu” ambao majengo hayo yamewekwa wakfu kwao. Itibari ya Jumuiya ya Wakristo katika ufundi wa kale na mapokeo ni yenye kudanganya kama ilivyokuwa itibari ya Yuda katika hekalu layo takatifu.—Yeremia 7:4.
6. Lawama la wazi ambalo Yesu alifanya juu ya viongozi wa kidini wa Kiyahudi linatumika jinsi gani kwa viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo?
6 Kwa kupatana na lawama za wazi za Yeremia juu ya makuhani na manabii wa Kiyahudi, ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo leo? Kwa kutoboa mambo wazi kama Yeremia, Yesu alitoa uelezaji fulani juu ya viongozi wa kidini wa Kiyahudi ambao unafaana na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo mpaka siku ya leo: “Wao hawazoei mambo ambayo wao wanahubiri . . . Kila jambo ambalo wao wanafanya linafanywa kuvuta fikira . . . kama kutaka kuchukua mahali pa heshima kwenye karamu nono na viti vya mbele katika masinagogi.” (Mathayo 23:3-7, The Jerusalem Bible) Ni mara nyingi kama nini tunaona viongozi wa kidini na wahubiri mashuhuri wakibariki mikutano na mikusanyano ya kisiasa na ya kutukuza utaifa kwa kuwapo katika hiyo—na kushiriki kutangazwa kimashuhuri na vyombo vya habari wakiwa pamoja na wanasiasa!
7. (a) Ni jinsi gani wahubiri fulani wanaongoza vibaya halaiki ya watu? (b) Ni mwito gani wa ushindani ambao viongozi wa kidini wameepuka?
7 Sasa, katika huu muda wa kitelevisheni, kunakuwa na wahubiri wa TV wenye kutumia njia hiyo kwa kufanya kila mbinu ya tamasha za kutazamisha halaiki ya watu na kuwavutia kisaikolojia ili kuhadaa na kukausha mifuko ya kondoo. Linafaa kama nini lile lawama la wazi la Yeremia hata sasa, yapata miaka 2,600 baadaye! “Kwa maana kutoka aliye mdogo zaidi kati yao hata kufika kwa aliye mkubwa zaidi kati yao, kila mmoja anajifanyia mwenyewe pato lisilo haki; na kutoka kwa nabii hata kufika kwa kuhani, kila mmoja anatenda kwa ubandia.” Wakati ule ule, hakuna wo wote kati yao wanaotaka kukubali ule mwito wa ushindani wa kufanya huduma ya kweli ya Kikristo, kuelekeana na watu ana-kwa-ana, kutoka nyumba kwa nyumba. Ni Mashahidi wa Yehova peke yao—jamii ya Yeremia iliyopakwa mafuta, na ule “mkutano mkubwa”—ambao wamekubali daraka hilo.—Yeremia 6:13; Matendo 20:20, 21.
Je! Jumuiya ya Wakristo Imeokoka?
8. Kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo inaitikadi kwamba iko kwenye umbali usioweza kufikiwa na Har–Magedoni?
8 Wahubiri hao wa TV wanafanya watu wasinzie kwa kuwaingiza katika hisia bandia ya kujiona salama, kwa kutumia-tumia bila uangalifu zile shime na theolojia zinazohusu “kuzaliwa tena” na zinazosema “ukiisha okoka, umeokoka sikuzote.” Mamilioni ya watu kutoka karibu kila dini na farakano la Jumuiya ya Wakristo wameongozwa kuitikadi kwamba wao ‘wamezaliwa tena’ na ‘wameokoka.’ Wanasiasa ambao hawaoni haya wanaona raha kufanya dai hilo hilo. Ndiyo, wahubiri walio mashabiki wao wanawaambia kwamba wao wana amani pamoja na Mungu kwa sababu “wameokoka”—kuwaambia hivyo ijapokuwa wana migawanyiko ya kidini, ya kisiasa na ya kutukuza utaifa, lo! Na wale watu wanapenda iwe hivyo, hata kama vile walivyofanya katika siku ya Yeremia! (Yeremia 5:31; 14:14) Wao wanafikiri wako katika umbali usioweza kufikiwa na hukumu ya Mungu ya Har–Magedoni.—Yeremia 6:14; 23:17; 1 Wakorintho 1:10; Ufunuo 16:14, 16.
9. (a) Kwa kweli “kuzaliwa tena” kunatumika kwa nani? (b) Biblia inasema nini juu ya nafsi? (Kwa maswali yote mawili, toa tegemezo zaidi kutokana na Reasoning From the Scriptures.)
9 Hata hivyo, uchunguzi wa uangalifu juu ya Neno la Mungu na mafundisho ya Kristo unaonyesha kwamba ni watu wa hesabu ndogo tu ambao wanashiriki pendeleo la kuzaliwa tena, kuzaliwa ‘kutokana na maji na kutokana na roho,’ hivyo wakashiriki utawala wa kimbingu pamoja na Kristo. (Yohana 3:3-5, NW; Warumi 8:16, 17; Ufunuo 14:1-3) “Mkutano mkubwa” wa Wakristo wa kweli leo hawahitaji kuzaliwa tena, kwa kuwa tumaini lao la uhai wa milele ni la kidunia si la kimbingu. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Zaidi ya hilo, fundisho la Jumuiya ya Wakristo linategemea taarifa bandia—kwamba mwanadamu ana nafsi isiyokufa ambayo inahitaji wokovu. Katika Biblia hamna mahali penye tegemezo kwa fundisho hilo, ambalo kwa kweli limepatwa kutokana na falsafa ya kale ya Kigiriki.a
Hawana Upendezo Katika Neno au Jina Lake
10. Wengi wa viongozi wa kidini wanaiona Biblia jinsi gani?
10 Kuna mambo mengine ya ufanani kati ya Yerusalemu wa kale na Jumuiya ya Wakristo ya ki-siku-hizi. Yeremia alitaarifu hivi: “Tazama! Neno lenyewe la Yehova limekuwa suto kwao, neno ambalo katika hilo wao hawawezi kuwa na upendezo wo wote.” (Yeremia 6:10, NW) Viongozi wa kidini wanapendelea zaidi kunukuu maneno ya wanafalsafa na wanasayansi, badala ya Neno la Yehova. Wengi wanaaibikia Biblia; wao hata wanaidhihaki kupitia “uchambuzi [wao] wa juu zaidi.” Wao wanadai kwamba Biblia ni hadithi za ubuni na ngano za kimapokeo zilizotokezwa zikiwa kama kitabu kizuri. (Yeremia 7:28) Na kwa habari ya jina la Mtungaji wayo, wao wanalitazama kwa madharau. Ni uthibitisho gani tulio nao kwa dai hilo lenye mkazo?
11. Pana utofautiano gani kati ya Jumuiya ya Wakristo na Yeremia katika utumizi wao wa jina la Mungu?
11 Ingawa tetragramatoni ya Kiebrania (יהוה) inaonekana karibu mara 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania, jina “Yehova,” au “Yahweh,” limeondolewa na mahali palo pakawekwa lile neno “BWANA” lisilo la mtu fulani mahususi katika Biblia nyingi za Kiingereza. Mathalani, jina hilo limeachwa nje kabisa katika tafsiri za sasa za Biblia katika lugha ya Afrikaans. Tafsri Franquesa-Solé ya Kihispania ilitumia;jina hilo katika chapa yayo ya asili. Wakati ile namna iliyosahihishwa ilipotangazwa, jina la kimungu likawa limetoweka, mahali palo pakiwa pamechukuliwa na Señor (Bwana). Na hata wakati tafsiri za Jumuiya ya Wakristo zinapotia ndani jina la Mungu, ni mara chache viongozi wa kidini wanapolitumia. Hata hivyo, katika ujumbe wake wa kiunabii Yeremia alitumia mara 726 jina la Mungu lenye kumpambanua!b
“Malkia wa Mbinguni” na Ibada ya Sanamu
12-14. (a) Jamaa za Kiyahudi zilihusika katika utendaji gani wa bidii? (b) Yehova aliona ibada yao jinsi gani?
12 Tunapata ulinganifu mwingine tunapochunguza ujumbe wa Yeremia kwa Yerusalemu. Wakati Yehova alipoambia nabii wake asisali kwa ajili ya wale watu, yeye alionyesha wazi sababu. “Je! kwani wewe huoni mambo ambayo wao wanafanya katika ile miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu? Wana wanaokota vijiti vya kuni, na akina baba wanawasha moto, na wake zao wanakanda mkando wa unga.” Na ni katika shughuli gani ya bidii ambamo jamaa nzima ilihusika? “Kufanya keki za kidhabihu kwa ‘malkia wa mbingu’”!—Yeremia 7:16-18; 44:15, 19, NW.
13 Kitabu kimoja cha Kiyahudi chenye mafafanuzi kinataarifu hivi: “Kidhehebu cha ‘malkia wa mbinguni’ kilifuatwa kwa hamu nyingi na waziwazi.” Inashangaza sana kwamba taifa la Yuda lilikuwa likizoea ibada ya sanamu, likiabudu mungu-mke wa kipagani, ambaye inawezekana alikuwa yule mungu-mke wa uzazi wa Kibabuloni, Ishtari, mungu wa tatu katika utatu wa nyota. Au “malkia” huyo angaliweza kuwa ni Ashtorethi, mungu-mke wa Kikanaani mwenye kulingana na huyo mwingine.—1 Wafalme 11:5, 33.
14 Kuongeza kwa ibada hiyo ya mungu-mke, wao walikuwa wakijitia katika ibada-sanamu nyingine. Yehova aliwashutumu kwa sababu hiyo, akisema: “Kwa sababu gani wao wameniudhi mimi kwa mifano yao ya kuchongwa, kwa miungu yao ya kigeni iliyo mibatili?” Ile taarifa ya kuwashtaki iliendelea kusema: “Wao wamekuwa hawakutii sauti yangu na wamekuwa hawakutembea katika hiyo, bali wao waliendelea kutembea kwa kufuata ukaidi wa moyo wao na kufuata mifano ya Baali, ambayo baba zao walikuwa wamewafundisha wao juu yayo.” (Yeremia 8:19; 9:13, 14, NW) Je! Jumuiya ya Wakristo imeanguka ndani ya mtego huo huo?
15. (a) Ni hali gani kuhusu ibada ya sanamu tunayopata katika Jumuiya ya Wakristo leo? Nukuu vielelezo vya kwenu. (b) Wakristo wa kweli wanachukua msimamo gani kuhusu Mariamu? (Ona pia Reasoning From the Scriptures, kurasa 254-61.)
15 Zuru karibu kanisa au kathedro lo lote lile —la Kiprotestanti, Kikatoliki, au Kiorthodoksi —na wewe utapata angalau mifano ya msalaba. Lakini katika makao ya Kikatoliki na Kiorthodoksi, mna mifano ya “Mariamu Mtakatifu aliye bikira daima, Mama ya Mungu wa Kweli,” akiwa katika vikao na misimamo ya namna nyingi sana.c Kila mtajo bora unarundikwa juu yake, kutia na “Malkia wa mbinguni” na “Malkia wa ulimwengu wote mzima”!d Kwa upande ule mwingine, jamii ya Yeremia, ingawa inaheshimu Mariamu kuwa mama ya Yesu na kuwa mwitikadi aliyepakwa mafuta, imefuata shauri hili la kimtume kwa uangalifu: “Jilindeni wenyewe na sanamu za kuabudiwa.”—1 Yohana 5:21; Yeremia 10:14, NW.
Utatu Wachukua Mahali pa Bwana Mmoja Mwenye Enzi Kuu Yehova
16. Ni fundisho gani lilifungulia njia ya kumstahi mno Mariamu, na jinsi gani?
16 ‘Lakini,’ huenda wewe ukauliza, ‘ibada na staha hii iliyo nyingi mno kwa Mariamu imekuja-kujaje?’ Ni kwa sababu ya hatua nyingine ya kanisa la mapema lenye uasi-imani, ya kufyonza ndani yalo waabudu wapagani. Lile wazo la kwamba kuna miungu mitatu katika mmoja lilishikiliwa mahali pengi katika ulimwengu wa kipagani. Waroma wa kale walikuwa na mahekalu yenye vikundi vya vijumba vitatu-vitatu “vilivyotolewa wakfu kwa utatu wa waungu walioshirikishwa katika itikadi mbalimbali na ibada. Hivyo ndivyo ilivyokuwa na hekalu la Jupiter Optimus Maximus katika kilima Kapitoli, lililowekwa wakfu kwa ule utatu wa miungu ya Kiroma, Jupiter, Juno na Minerva.”e
17, 18. (a) Ni kitu gani kimegandamizwa, na hivyo fundisho la Utatu likaruhusiwa kusitawi? (b) Toa hoja zaidi kutokana na Reasoning From the Scriptures.
17 Ili kuendeleza lile fundisho lenye kuibuka la “Utatu Ulio Mtakatifu Zaidi” katika karne za tatu na nne, ilihitajiwa kabisa Kanisa Katoliki ligandamize lile wazo la Kiebrania lililoelezwa waziwazi sana katika maneno ya Yeremia: “Katika njia yo yote hakuna mmoja ye yote aliye kama wewe, O Yehova. Wewe ni mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza. Lakini Yehova kwa kweli ni Mungu. Yeye ndiye Mungu aliye hai na Mfalme kwa wakati usio dhahiri.” Yesu alithibitisha kuelewa mambo jinsi hiyo aliponukuu hivi kutokana na maneno ya Musa: “Sikia, O Israeli, Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.”—Yeremia 10:6, 10; Marko 12:29; Kumbukumbu 6:4, NW.
18 Kwa kusaidiwa na woga wa ushirikina wa Kiyahudi wa kutotamka “Yahweh,” au “Yehova,” utumizi wa jina la Mungu uliachwa na Jumuiya ya Wakristo yenye uasi-imani. Hiyo iliruhusu kuwe na nafasi-wazi ya kitheolojia ambayo ‘Utatu Mtakatifu’ ungeweza kujaza.f
19. (a) Ni nini limekuwa tokeo la kukubaliwa kwa Utatu na Jumuiya ya Wakristo? (b) Ni udanganyifu gani uliokimbiliwa ili kukazilia ile hoja ya Utatu?
19 Hivyo, Jumuiya ya Wakristo imemalizia kwa ‘kutembea kwa kufuata mungu mwingine,’ mungu wa kiutatu, ambaye hakujulikana kabisa kabisa kwa Wayahudi na kwa Kristo na Wakristo wa kweli. Na ili kukazilia fumbo hilo la watatu katika mmoja, watafsiri wa Jumuiya ya Wakristo hata walikimbilia kufanya udanganyifu katika Biblia yao ya King James Version.g Zaidi ya hilo, kama tokeo lenye kutazamiwa kutokana na fundisho la Utatu, sehemu kubwa ya Jumuiya ya Wakristo imeanguka pia ndani ya ibada au staha nyingi mno ya “Malkia [wayo] wa Mbinguni.”—Yeremia 7:17, 18, New International Version.
Viongozi wa Kidini Wanaendeleza Mnyanyaso
20, 21. Ni mwendo gani ambao viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamefuata, na ni maswali gani ambayo sasa yanafaa?
20 Kulingana na yaliyotangulia, swali la Yeremia linafaa kwa viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo: “Ni jinsi gani ninyi wanaume mnasema: ‘Sisi ni wenye hekima, na sheria ya Yehova ipo pamoja nasi’? Kwa uhakika, sasa, ile stailasi bandia ya waandishi imefanya kazi kwa ubandia mtupu. . . . Tazama! Wao wamekataa neno lenyewe la Yehova, na ni hekima gani ambayo wao wanayo?” (Yeremia 8:8, 9, NW) Wao wamekataa Yehova na wawakilishi wake, mashahidi wake. Sawa na vile makuhani na manabii walivyonyanyasa Yeremia, ndivyo viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamekuwa wakichochea sehemu iliyo kubwa zaidi ya mnyanyaso wa kinyama wa Mashahidi wa Yehova muda wote wa karne hii.
21Lakini ni kwa sababu gani wao wameendeleza mnyanyaso huo? Mashahidi wamefanya nini kuchokoza hasira yao na kuchokora moto wao? Makala ya mwisho katika mfululizo huu itachunguza maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate mfikirio wenye maelezo marefu juu ya mambo haya, ona kurasa 76-80, 356-61, 379-80 katika Reasoning From the Scriptures, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.)
b Ili upate habari zaidi juu ya kugandamizwa kwa jina la kimungu, ona ile broshua ya kurasa 32 Jina la Mungu litakaloendelea Milele, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
c The Image of Guadalupe—Myth or Miracle, kilichotungwa na Jody Brant Smith, ukurasa 6.)
d The Glories of Mary, kilichotungwa na Alphonsus de Liguori, ukurasa 424.
e Las Grandes Religiones Ilustradas (Dini Zile Kubwa Zafanyiwa Kielezi), ukurasa 408.
f Ili upate funzo juu ya fundisho la Utatu, ona Reasoning From the Scriptures, kurasa 405-26.
g 1 Yohana 5:7 ni nyongeza isiyo ya kweli, na Mathayo 24:36, ambayo haina “wala Mwana,” imeyaacha nje maneno hayo kwa udanganyifu. Ona maelezo ya chini ya The Emphatic Diaglott, ukurasa 803, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., na The Codex Sinaiticus and The Codex Alexandrinus, ukurasa 27, iliyotangazwa na Wadhamini wa Jumba la Uingereza la Makumbusho.
Je! Wewe Unakumbuka?
◻ Jamii ya Yeremia ya ki-siku-hizi imetambulishwa jinsi gani?
◻ Ni nini baadhi ya ulinganifu mbalimbali ulio kati ya Yerusalemu wa kale na Jumuiya ya Wakristo?
◻ Ni jinsi gani viongozi wa kidini wamefanya watu wasinzie katika kuitikadi kwamba wao wana amani pamoja na Mungu?
◻ Ni hali gani ya kuachilia mambo na kuabudu sanamu ambayo imekuwa mfano hasa wa Jumuiya ya Wakristo?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Katika 1938 Mashahidi walikuwa wakilaumu waziwazi dini bandia
[Picha katika ukurasa wa 17]
Jumuiya Wakristo inaitibari katika mahali-mahali payo patakatifu panapoheshimiwa kwa sababu ya kudumu sana, kama vile Wayahudi walivyoitibari katika Yerusalemu
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wahubiri wa TV wa Jumuiya ya Wakristo wanafanya watu wasinzie katika kuitikadi kwamba wao ‘wameokoka’ au ‘wamezaliwa tena’