Watangazaji wa Ufalme Waripoti
Yehova Alibariki Msimamo Wao Thabiti kwa Ajili ya Sheria Yake
KATIKA nchi moja ya Mashariki ya Kati, baba mmoja alikuwa akitengeneza tairi iliyotoboka kando ya barabara wakati gari moja lilipogonga mwanaye wa miaka minne kisha likatia kasi kukimbia. Yule mtoto mjeruhiwa akiwa amepakatwa na mamaye, baba alielekea kwenye hospitali ya karibu zaidi, kumbe akaelekezwa kwenda hospitali nyingine iliyoko kilometa 25 kutoka hapo. Daktari aliamua kwamba mvulana huyo alikuwa akivuja damu kwa ndani mwilini, na kwamba alihitaji upasuaji na kutiwa damu mishipani. Madaktari wengine wanane walikubali wote kwamba aliihitaji. Kwa kujua sheria ya Mungu dhidi ya utiwaji damu mishipani, wazazi hao walikataa. “Tunawapa dakika tano tu za kuamua ama sivyo hatutagusa mtoto wenu hata kama baadaye mtakubali atiwe damu mishipani,” daktari huyo akatisha. Wakati uo huo, tumbo la mtoto liliendelea kufura na alikuwa akifikia hali hatari.
Ndugu wa kimwili wa baba huyo, ambaye hayumo katika ukweli, alimkaza baba huyo aruhusu ule utiaji damu mishipani. Hata alisema: “Tafadhali mfikirie mvulana huyu kuwa si wako bali wangu. Kwa kuwa dhamiri yako inakusumbua wewe, mimi ndimi nitakuwa mwenye daraka la kulaumiwa, kutia na daraka la kulipia gharama ya hospitali, kumpa mtoto damu inayohitajiwa. Huyu ndiye mwana wako wa peke yake.” Mkazo huo ulikuwa mgumu kuhimili, lakini wazazi hao walikuwa thabiti katika uamuzi wao.
Wao walichukua mvulana huyo na kuondoka wakitafuta hospitali fulani, lakini wakapotea njia. Kwa nasibu waliona ishara ya hospitali nyingine wakaiendea, ingawa hiyo siyo waliyokuwa wakitafuta. Baada ya kuona mvulana huyo, daktari alisema: “Ule mfuro wa tumbo la mtoto huenda ukawa au usiwe ni ishara ya kuvuja damu ndani mwilini. Mwache mvulana alale, na kesho tutafanya machunguzi yanayohitajiwa ili kujua.” Machunguzi yalionyesha kwamba hakukuwa na kuvuja damu, bali mfuro ule ulisababishwa na aksidenti ile. Hakukuwa na uhitaji wa upasuaji. Kwa kweli, daktari huyo alisema kwamba upasuaji ungaliweza kuwa hatari sana. “Asante kwa Yehova,” wakasema wazazi wale, “kwa usalama wa mwana wetu na kwa kutuelekeza kwenye hospitali inayofaa na kwa daktari anayefaa.”
Miaka kumi baadaye, ni nini limekuwa tokeo la hali hii? Baba huyo anasimulia hivi: “Ndugu yangu wa kimwili ambaye alinikaza mimi katika hospitali alikuja kuthamini msimamo wetu na akaona mwelekezo wa Yehova katika kisa hiki. Hiyo iliamsha kupendezwa kwake na ukweli, naye akaukubali, na sasa yeye amebatizwa na anatumikia akiwa mzee katika kundi. Mke na watoto wake wanatumikia Yehova kwa bidii pamoja naye. Wale ndugu zangu wengine wawili wamo katika ukweli pia pamoja na jamaa zao, na mmoja wao anatumikia akiwa mtumishi wa huduma. Baba na mama yangu walibatizwa hivi majuzi ijapokuwa ni wazee kwa umri. Kwa hiyo, ingawa lilikuwa tukio baya sana kwa mke wangu na mimi, kwa sababu ya hilo washiriki wapatao 30 wa jamaa yangu wamekubali ukweli; tayari wengine wao wamebatizwa na wanatumikia wakiwa wazee na watumishi wa huduma. Wengine wanaelekea kwenye ubatizo. Mwana wangu, ambaye sasa ana umri wa miaka 14, ni mhubiri mwenye afya na bidii, naye anatazamia ubatizo. Mke wangu na mimi tunatolea Yehova asante kama nini kwa kutusaidia tufanye uamuzi unaofaa kwa kupatana na sheria yake iliyotaarifiwa kwenye Matendo 15:29!”
[Picha katika ukurasa wa 27]
‘Endeleeni kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu’