Je! Talaka Inapasa Kuruhusiwa?
KATIKA Juni 1986 wapiga kura katika Jamhuri ya Ailandi walipiga kura iliyokaribia kwenda sare, ya 3 kwa 2, ili kuunga mkono marufuku yao juu ya talaka. Hiyo ilifanya Jamhuri iwe nchi ya peke yake katika Ulaya ya Magharibi ambamo bado sheria hairuhusu talaka.
Kuna ithibati ya kwamba, ijapokuwa kuna wimbi la mielekeo na fikira za kufadhili maoni ya wengine, maoni ya watu walio wengi juu ya lile suala la talaka lenye kuwasha hasira kwa urahisi yangali yanaongozwa na malezi yao. Asili ya kijamii, elimu, na mambo ya kijamii, yote yanashiriki sehemu fulani. Lakini kati ya mambo yote, dini, au ukosefu wa dini, linabaki likiwa ndilo jambo kubwa lenye kuongoza zaidi.
Maoni yako ni nini juu ya talaka? Ikiwa mume na mke waliofunga ndoa wanahisi wakiwa taabani sana kwa kuishi pamoja na ni wazi hawapatani utu, je! inawapasa waruhusiwe kukomesha taabu yao kwa kujipatia talaka? Wewe ungejibu swali hili jinsi gani? La maana zaidi, ungetegemeza jibu lako juu ya msingi gani?
Maoni Mbalimbali Yanayohitilafiana
Kwa wale mamilioni ambao wanashikilia viwango vya Katoliki ya Roma, hakuna mambo ya talaka hata kidogo. “Katika ndoa ya Kikristo,” inaeleza The Catholic Encyclopedia, “hakuwezi kamwe kuwa na talaka kamili [yenye haki ya kufunga upya ndoa], angalau baada ya ile ndoa kuwa imeingia katika ukamilisho wa kimalazi.” Hata hivyo, Kanisa Katoliki la Roma linaruhusu kutangua ndoa kwa kutegemea hali fulani, na utaratibu huu unatumiwa mahali pengi. Mathalani, katika Aprili 1986 The Denver Post liliripoti hivi: “Wakatoliki wa mahali wanaomba mitanguo mingi sana ya ndoa hivi kwamba Dayosisi Kuu ya Denver inatumia dola 250,000 kuongeza wafanya kazi na katika uendeshaji wa kompyuta moja ili kuwezana na wingi wa kazi waliyo nayo.” Ripoti hiyo ilizidi kusema kwamba “katika Dayosisi ya Denver, kuna kesi za mitanguo 700 za miaka mitatu iliyopita ambazo bado hazijashughulikiwa.”
Waprotestanti katika mamia ya madhehebu kuzunguka ulimwengu wanaelekeana na namna nyingi sana za sheria na virekebi vya kanisa kuhusu talaka. Hata hivyo, kwa ujumla wenye mamlaka wa Kiprotestanti wanaruhusu talaka kwa kutegemea sababu nzito-nzito tu. Lakini ile inayoweza kuonwa kuwa nzito inaweza kutofautiana sana katika kanisa moja na jingine. Makosa kama uzinzi, ukatili, na kumtoroka yule mwingine yanakubaliwa kwa ujumla kuwa sababu za talaka, lakini si hayo tu. Madhehebu fulani sasa yana sherehe na ibada za talaka yakiwa na tenzi za kuimbwa na sala kama katika arusi. Katika sherehe moja kama hiyo, “nadhiri za ndoa zinafutwa. Mume na mke wanampokeza mhudumu pete zao za arusi. Ibada ile inamalizika kwa tangazo rasmi kutoka kwa mhudumu kwamba ndoa ile imevunjwa, na wale wawili wanasukana mikono kwa kusalimiana,” inaripoti The New York Times.
Wayahudi wana mapokeo yenye kufikilizwa na mahakama za kidini. Sheria za kirabi zinaruhusu talaka ama kwa mwafaka wa watu wale wawili ama kwa kutegemea sababu za kuwa na kasoro za kimwili au mwenendo usiovumilika. Hata hivyo, talaka ile inaonwa kuwa halali wakati tu yule mume anapotoa “geti,” au cheti cha talaka, nacho kinaweza kuanzisha ushindani mkali. Wakiwa na mfundo moyoni, waume fulani hukataa kutoa hati ile, au wanaitumia kama mbinu ya kung’ang’ania jambo fulani. “Tatizo hili limeacha maelfu ya wanawake Wayahudi wenye kicho kingi wakiwa katika muhali wenye maumivu mengi ya ndoa,” akasema Msimamizi wa Baraza la Jiji la New York, Andrew Stein, katika hotuba moja kwa kusanyiko la marabi, wanasheria, na wengine. Bila ile geti, linaonwa kuwa jambo lisilo halali mwanamke yule kuolewa upya, na mtoto ye yote anayezaliwa naye anapata sifa mbaya ya kuitwa mamzeri, au mwana-haramu, katika Taifa la ki-siku-hizi la Israeli.
Kwa habari ya watu wasio wa dini na wasioamini kuna Mungu, ambao inachukuliwa kwamba wanaendesha mambo yao kulingana na sheria ya bara, bado suala hilo si rahisi. Hiyo ni kwa sababu sheria za talaka zinatofautiana nchi na nchi na hata eneo na eneo ndani ya nchi ile ile moja. Mwenye mamlaka mmoja anaorodhesha sababu zipatazo 50 ambazo talaka halali inaweza kupatwa katika sehemu mbalimbali za United States. Hizo zinatia ndani “mwenendo mbaya sana na uovu,” “kutokuelekea vya kutosha kwamba ndoa itahifadhiwa,” na “mke kukataa kuhama pamoja na mume kwenda kwenye eneo hili.” Katika nyakati za majuzi, vidalili vyote vya kuona uhitaji wa kupambanua yaliyo mema na mabaya vimeondolewa na ile ambayo kwa kawaida inaitwa talaka isiyotegemea kosa lo lote.
Ingali Ni Hali Yenye Kutatanisha
Hata ingawa nyingi za sheria na virekebi hivi mbalimbali vinavyohitilafiana kuhusu talaka vinasemwa kuwa vinategemea msingi wa Biblia, je! vimefanikiwa kuimarisha ndoa au kuongezea furaha ya kibinadamu? Hesabu inayoongezeka ya talaka—talaka moja kwa kila ndoa mbili katika nchi fulani-fulani—inaandaa jibu la wazi. Si kwamba tu sheria hizi zimekosa mafanikio katika kuimarisha kifungo cha ndoa, bali zimeongezea pia taabu na mteseko katika maisha za mamilioni ya watu.
Kwa sababu hiyo, ni jambo la maana wale wanaojali kikweli kufanya yaliyo mema watafute kujua Biblia inasema nini hasa juu ya habari hii.