Uenzi wa Kipainia—Muda wa Maisha Yote
Katika chumba nadhifu kisicho na vitu vya madoido mengi katika Cardiff, Wales, Funzo la Kitabu la Kundi limemalizika sasa hivi. Kiongozi wa funzo anawashukuru kwa ajili ya ukaribishaji wao wale dada mapainia wawili, Maud Clark na Mary Grant, ambao sasa wamo katika umri wao wa miaka 90 na kitu, na kuwatia moyo wasimulie mambo ya kule nyuma . . .
Maud: Sasa ni miaka 65 tangu Mary na mimi tulipokutana kwanza na tukaanza kupainia pamoja.
Mary: Ndiyo, ilikuwa katika 1923, katika usiku baridi wenye theluthi, wa Januari! Wewe unakumbuka, Maud? Mimi nilikuchukua wewe kutoka kwenye kituo cha reli cha Much Wenlock nikakupeleka moja kwa moja kwenye makao yangu. Tulikula kitu kidogo, halafu tukajifunza pamoja Tabernacle Shadows. Asubuhi iliyofuata tukapanda baiskeli zetu kwenda kuhubiria wakulima wa Shropshire.
Mionano ya Mapema
Maud: Bila shaka nakumbuka, tulikuwa tayari kwa jambo hilo. Wajua, sisi wawili tulikuwa tumekuwa tukipainia kwa muda fulani. Hata nilipokuwa kisichana tu, sikuzote Neno la Mungu lilinipendeza. Kwani, naweza kukumbuka nikitaja kutokana na kumbukumbu langu zaburi saba kanisani ili nipate Biblia ya bure! Ilikuwa katika 1908, nilipokuwa na umri wa miaka 11, kwamba dada yangu mkubwa zaidi alisoma kile kitabu The Divine Plan of the Ages na kuliacha kanisa tulilokuwa tukihudhuria, akawa Mwanafunzi wa Biblia. Kweli za Biblia zikawa maongezi yetu kwenye maskani yetu. Lakini baba yangu alipokufa, mimi nilianza kujiuliza, ‘Wafu wako wapi?’
Ulikuwa msisimuko ulioje kupata jibu nilipoenda kuona The Photo-Drama of Creation, iliyoonyeshwa katika Sheffield mji wa maskani yetu! Katika picha hizo zenye mwendo, zilizotayarishwa ziambatane sawia na maneno ya rekodi za kinanda, mimi niliona yule mwana wa mwanamke Mshunami akiinuliwa kutoka kifoni. Ndiyo, nilijifunza kwamba wafu hawajui neno lo lote mpaka wanapofufuliwa.—2 Wafalme 4:32-37.
Nilijiuzulu haraka kutoka Kanisa la Kianglikani na nikaanza ile tuliyoita kazi ya uchungaji, nikitoa fasihi (vitabu) ya Kibiblia mle mle katika eneo nilimojulikana kwa kugawa magazeti ya kanisa. Mimi nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova katika Agosti 1918 kwenye kusanyiko moja katika jiji la hapo karibu la Leeds.
Baada ya kutumia nyakati nyingi za malikizo yenye furaha pamoja na dada makolpota wawili katika Derbyshire, niliamua kabisa akilini kufanya utumishi wa painia uwe kazi yangu ya maisha. Katika Agosti 1922, nilianza mgawo wangu wa kwanza: Biggleswade katika Bedfordshire.
Mmoja wa makolpota alisema kwa mimi hivi: “Ukiweza kuvumilia kwa muda wa miezi sita ya kwanza, utakuwa unaweza kuendelea.” Miezi hiyo ya kwanza-kwanza haikuwa rahisi. Nilipata aksidenti nikiwa nimepanda baiskeli yangu. Ndipo mwandamani wangu wa kwanza painia akarudia maskani ya kwao. Lakini mimi nilipiga moyo konde niendelee, kwa hiyo nikaandikia Sosaiti nikiomba mwenzi. Na Yehova akanipa mimi Mary!
Mary, wewe ulichukua msimamo wa kusimama upande wa ukweli mapema kuliko mimi, sivyo?
Mary: Ndiyo, Maud. Wakati huo tulikuwa tukiishi katika Cardiff, Wales ya Kusini. Nilipokuwa na miaka 16, nyanya yangu alinialika nisome kitabu The Divine Plan of the Ages, alichokuwa amepata kwenye mkutano wa watu wote uliopangwa kitengenezo na Wanafunzi wa Biblia. Sikuzote mimi nilitaka kuielewa Biblia na kuwa misionari nikiisha kukua. Nilipokuwa nikisoma buku hilo, nilijua kwamba nilikuwa nimeupata ukweli.
Nilianza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia, mama yangu ajapokataa sana kukubalia jambo hilo. Wajua, wazazi wangu walikuwa wenye mali, na kwa kuwa wao hawakuniruhusu nifanye kazi, mimi nilizipata hali kwenye maskani yetu kuwa zenye vizuizi sana. Hata hivyo, niliweza kupata sehemu ile nyingine ya fungu lote la misaada ya kujifunzia Biblia. Mama yangu alipogundua, alichoma moto vitabu hivyo kwa kasirani na kuniambia nilikuwa mchanga mno kujua mambo kama hayo. Nililazimika kuleta-leta kwa siri kitabu kimoja kimoja ndani ya maskani yetu ili viwe badala ya hivyo vingine, baada ya kufanya ziara za asubuhi kwenye maskani ya mmoja wa Wanafunzi wa Biblia karibu kilometa 3 kutoka hapo. Nilikuwa nikivisoma kwa pupa kabla ya wale wengine nyumbani kuamka, nikivificha katika kibanda cha bustani wakati wa mchana.
Katika 1913, nilipokuwa na miaka 17, nilisafiri kwenda London kwa likizo la kuona mandhari. Jambo la kufurahisha ni kwamba, hiyo ililingana na ziara ya Ndugu Russell kwenye kusanyiko lililofanywa kule Kingsway Hall. Nikiwa huko nikaonyesha tamaa yangu ya kubatizwa. Dada kolpota aliyefanya kazi katika Cardiff alimkaribia Ndugu Russell kumwuliza kama yeye aliwaza kwamba mimi nilikuwa mchanga mno. Ndugu Russell akaniuliza nilikuwa na umri gani na kuniuliza maswali ili aone kama nilielewa Maandiko na ili aamue kama nilikuwa nimeweka maisha yangu wakfu kwa Yehova. Tokeo ni kwamba, nilivaa kanzu ndefu nyeusi nikajiunga na wataka-ubatizo wale wengine ili tupate uzamisho kwenye Tabanakulo ya London. Mimi nayakumbuka vizuri sana maneno tuliyoimba tulipokuwa tukitoka ndani ya maji:
“Nimezikwa pamoja na Kristo,
nikainuliwa naye pia,
Nini kingine kimebakia?
Kwamba tu mashindano na
ugomvi nitayakomesha
Kwamba tu nitembee kwa upya wa maisha.”
Baadaye, ndugu mmoja alinikaribia akasema: “Lazima iwe kwamba wewe ndiwe wa mwisho kuingia wa wale 144,000; una wakati mfupi sana uliobaki wa kufanya mwito na uchaguzi wako uwe hakika.” Hayo ndiyo yaliyokuwa mawazo ya wengi waliokuwa na rai ya kuuona ule mwaka wenye kukaribia, 1914, kwa tarajio kubwa. Ingawa hivyo, kwangu mimi huu ulithibitika kuwa wakati wa kutahiniwa nilipokuwa nikichukuliana na upinzani mkubwa kwenye maskani yetu. Nilihudhuria mikutano mara nyingi nilivyoweza. Katika 1916, nilifurahia lile pendeleo la kutumikia nikiwa mkaribishaji wa kike kwenye wonyesho wa Photo-Drama of Creation katika Cardiff. Baada ya kumaliza mazoezi yangu ya ukunga katika Manchester, nilianza utumishi wa painia wa wakati wote katika 1922.
Kutoa Ushuhuda Mashambani
Maud: Kule nyuma ilikuwa lazima tuwe sana na akili ya kuanzilisha mambo. Tuliambia kila mmoja kwamba tulikuwa katika kazi ya Kikristo. Watu siku hizo walikuwa wasomaji. Sisi tuliwatolea The Harp of God na mfululizo wa Studies in the Scriptures. Bila shaka, tulihitaji sanduku kubwa la kuchukulia vitabu vyote hivyo. Langu lilikuwa kubwa sana hivi kwamba siku moja nilipofika kwenye shamba moja la eneo lililojitenga, mke wa mkulima alifikiri nilikuwa mtu wa ukoo nikitoka Kanada kuzuru. Tulicheka kama nini!
Kwa kuwa upainia ulikuwa maisha yetu, tulipokea riziki yetu kutokana na ile kazi ya kugawanya vitabu vyenye ujumbe wa Biblia. Tulitumia mapato yetu kwa uangalifu na tuliishi kwa uwekevu, tukibadilishana vitabu na siagi na mazao mengine ya shambani na kuokota viazi, tanipu, na kabeji zilizoanguka kutoka kwenye mikokoteni-shamba katika vile vibarabara visivyotandazika vizuri vyenye mavumbi-mavumbi. Tukaja kuwa wastadi katika kutengeneza mipira ya baiskeli zetu ilipotoboka, na tukazidi-zidi kuwa washonaji wazuri, tukijifanyizia nguo zetu wenyewe.
Wakati akina ndugu wenye kutumikia wakiwa wahutubu wa kusafiri mbali walipokuwa wakitoa hotuba za Biblia katika miji, Mary na mimi tuliwafuata nyuma kuendeleza upendezo ambao kuhubiri kwao kuliamsha katika watu. Vikundi vidogo vya wenye kupendezwa vilichomoza katika Shrewsbury na miji mingine. Nasi tulitazamia makusanyiko kama nini! Mimi nafikiri ule mkusanyiko wa 1926 kule London ulikuwa wa kutokeza. Huko tulifurahia lile pendeleo la ziada la kugawanya kijitabu The Standard for the People katika barabara za huo mji mkuu. Ndipo taharuki yetu ilipoongezeka tulipokuwa tukisoma mambo yaliyokuwa katika barua moja kutoka kwa Sosaiti. Lilikuwa badiliko la mgawo kwetu: Ailandi ya Kaskazini.
Kupainia Maeneo Mapya
Tuliwasili katika County Antrim, Ailandi ya Kaskazini, ili kupainia miongoni mwa watu waliogawanyika kidini. Kwanza tulikaa Green-island. Kulikuwa na uchepechepe na baridi, nasi hatukuwa na mioto kwa majuma kadhaa kwa sababu ya mgomo wa wafanya kazi wa makaa-mawe katika Uingereza. Naweza kupiga picha na kuona sisi sasa, tukiwa tumeketi kwa kuvaa koti na vifunika-mikono nyakati za jioni, tukijaribu kujifunza na huku tunatetemeka-tetemeka kutokana na baridi. Ndipo kiangazi kilipokuja, na lo, tukamshukuru Yehova kama nini kwa pendeleo la kufanya kazi katika mazingira ya kupendeza ya vibonde vya Antrim. Watu huko walisikiliza vizuri ujumbe wa UfaIme. Oh, ndiyo, mara nyingi wao walitoa ubishi, lakini walikuwa wenye fadhili. “Come awa’ in” (Karibuni ndani), wao wakawa wakisema, na kuweka birika juu ya greesha (vijani-jani vilivyooza na kukaushwa na kufanyiza moto mkali) ili ichemke, na mazungumzo yetu yakaendelea.
Mary: Kwa kuwa sasa sisi pamoja tulikuwa wasichana wanne mapainia katika mgawo wetu, tuligandamana na ratiba kamili ya kitheokrasi kuhusu mikutano. Kila asubuhi tulizungumzia Andiko moja na kusoma “Azimio Langu la Asubuhi,” ambalo, kwa sehemu, lilisema ‘Kila siku mimi nitakumbuka kwenye Kiti-UfaIme cha Neema ya Kimbingu yale mapendezi makuu ya kazi ya mavuno, hususa ushiriki ambao mimi mwenyewe nimependelewa kufurahia katika kazi hiyo, na mapendezi ya wafanya kazi wenzangu wapendwa kwenye Betheli na mahali kwingineko.’ Usiku wa Jumatano tulifanya Mkutano wa Sala, Sifa na Ushuhuda wetu. Siku za Jumapili tulijifunza pamoja Mulinzi, na tulikuwa tukikusanyika kwa kuzunguka kinanda kidogo cha kuimbia ambacho mara nyingi kilipatikana katika maskani za watu, ili tuimbe kutokana na Hymns of the Millenial Dawn, kama vile:
“Usidhani umeshinda kamwe,
Usiketi kistarehe kamwe
Huachi kazi ya jasho lako
Hadi upatapo taji yako.”
Maud: Lilikuwa badiliko kama nini wakati tulipogawiwa kazi ya pekee iliyofunguka—tukawa ‘mapainia wa nyumba za kibiashara.’ Tungewezaje kweli kuwatolea ushuhuda wafanya kazi, mameneja wa benki, na watu kama hao? Yale majengo makubwa katika Belfast yalionekana kama yasiyoingilika. Lakini sisi tukakumbuka Wafilipi 4:13, NW: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” Nasi tulikuwa hatufikirii kukataa mgawo wetu. Tulipata maono mazuri sana kwa kuongea na watu hao na kuwaangushia fasihi nyingi! Kufikia 1931 tulikuwa tumemaliza nyumba zile za kibiashara na tulikuwa tumetumia miaka mitano katika Ailandi ya Kaskazini. Tulijiuliza mgawo wetu wenye kufuata ungekuwa wapi. Tulistaajabu kwamba ulikuwa zile nyumba za kibiashara za Dublin.
Twende Tarshishi au Ninawi?
Lazima tukubali wazi kwamba, kwanza, sisi tulihisi kama Yona, aliyegawiwa kuhubiria Ninawi na badala ya kufanya hivyo akaelekea upande wa Tarshishi. Tungalipendelea kupata mgawo tofauti. Baada ya muda mfupi tukang’amua ni lazima tutegemee Yehova. Hata hivyo, iliogopesha kama nini kusimama kando ya Nguzo ya Nelson katika Dublin na kuona barabara zilizojaa mapadri na watawa-kike, huku wanaume wakiinua kofia zao na wanawake wakipitana-pitana kimakasi kwa kumheshimu ‘yule Bikira mbarikiwa.’ Wakati huo kulikuwa na Wanafunzi wa Biblia wanne tu katika Dublin.
Tuliweza kupata vyumba kwenye jamaa moja ya Katoliki ya Roma. Bila shaka, tulilazimika kuficha vitabu vyetu chini ya kitanda, kwa maana padri alifanya ziara za ukawaida kwenye nyumba hiyo. Siku moja mfanya kazi mmoja wa Dublin alifika kwenye makao yetu, akisema: ‘Ninyi mliacha vitabu kwenye benki yangu.’ Alisisimuliwa sana navyo hata akaenda kila duka aone kama walikuwa wakiuza vitabu vya Hakimu Rutherford. Ndipo alipoandikia New York akapewa anwani yetu. Alipanga karamu kwa ajili ya rafiki zake wote ili awaeleze aliyokuwa amejifunza.
Baadaye mwaka huo, sisi tulihudhuria mkusanyiko mmoja katika Liverpool, Uingereza, ambako tulijifunza juu ya jina jipya letu, Mashahidi wa Yehova. Tuliporudi Dublin, tulishiriki katika ile kampeni ya kugawanya kile kijitabu The Kingdom, the Hope of the World, kilichokuwa na azimio la mkusanyiko huo. Tulifanya ziara kwenye makao yote ya watawa wa kiume na wa kike, na nyumba za kibiashara, tukitoa nakala za bure za kijitabu hicho. Zote zilikubaliwa!
Mary: Siku moja tuliona mashua ikipita kasi majini kuteremkia mto Liffey, na hiyo ikatupa sisi wazo la kuwatolea ushuhuda wafanya kazi wa meli zilizokuwa gudini. Tulipojaribu kuingia eneo la gudini, lilizuiliwa na polisi mmoja, aliyetuuliza tulikuwa tunafanya nini. Tulipomwonyesha vitabu vile, yeye akasema, “Endeleeni “Tulipata makapteni kadhaa wa meli waliotoka nchi nyinginezo, nao waliwajua Mashahidi. Tunapotazama nyuma kwenye maono hayo, tunastaajabia jinsi Yehova alivyotutunza wakati kila mmoja wetu alipoenda akiwa peke yake juu ya meli hizo.
Kutoa Ushuhuda Wakati wa Miminiko la Makombora
Maud: Katika 1939 wakati vita ilipotokea tulirudi Liverpool na kujiunga pamoja na mapainia wengine 20 walioishi kwenye maskani ya mapainia. Sasa sisi tuliishi katika muda wa mashambulizi ya angani na uangushaji wa makombora na tulitoa ushuhuda kokote ambako watu wangesikiliza. Mara nyingi tulijipata tukiwekelea sahani za santuri juu ya vinanda vyetu, tukizungumzia ujumbe wa Ufalme, halafu kupiga mbio kurudia maskani yetu ya mapainia, au kujifyatusha kutoka kificho kimoja kwenda kile kingine ili tusipatwe na ushambulizi wa angani. Muda wote wa kipindi hiki, sisi hatukupatwa na ogofyo, kwa kuwa tulikuwa tukifanya kazi ya Bwana.
Mara nyingi tulipokuwa tukitembea kwenye barabara, watu waliturushia matukano kwa sababu ya msimamo wa kutokuwamo ambao Mashahidi walidumisha wakati huo wa pigano. Mimi nakumbuka kwamba kwenye nyumba moja mwanamume kijana alisikiliza yale maneno yaliyorekodiwa katika sahani na akakubali funzo la ukawaida la Biblia. Ugumu fulani ukatokea. Alikuwa ndiyo sasa tu amejitolea kujiunga na Jeshi-Maji la Uingereza. Aliwaandikia wenye mamlaka barua akitaarifu msimamo wake wa kutokuwamo na jibu alilopokea likawa ni kuachishwa kabisa wajibu wa kuwa jeshini. Baadaye alijiunga nasi katika utumishi wa wakati wote.
Mary: Mimi sitasahau kamwe zile siku za vita, Maud. Wewe unakumbuka lililotukia tulipohamia Knutsford katika Cheshire katika 1942? Bibi mmoja alitupaazia sauti akisema, ‘Ninyi mnasaidiaje ile jitihada ya kupigana vita?’ Kabla hatujaweza kujibu, mpita-njiani mmoja akajibu, ‘Mwanamke huyu anafanya kazi ambayo sisi hatuna ushujaa wa kuifanya.’ Mwanamume mmoja mzee-mzee naye akaingilia, ‘Wao wanafanya kazi njema.’
Maud: Kweli kweli, kazi ya mafunzo ya Biblia ilikuwa ndilo jambo kubwa. Mimi nilipata Ono zuri sana nilipozuru shamba moja nikakuta bibi aliyeniambia kwamba mvulana wake mdogo alikuwa ameuawa katika aksidenti ya barabarani. Nilimwangushia kijitabu Hope for the Dead na nikaanza funzo la Biblia. Baada ya nyakati saba za kujifunza, bibi huyo alianza kuandamana nami katika kazi ya ushuhuda. Miezi michache baadaye mume wake aliukubali ukweli, na katika muda wa miaka miwili hao wawili wakauza shamba lao na kuanza kupainia. Binti yao alijiunga nao baadaye katika kazi ya wakati wote, na sasa yeye na mume wake wanatumikia katika Betheli ya London.
Kwenye lile kusanyiko la Leicester la 1941, Ndugu Schroeder alitangaza kwamba mapainia wa pekee wangepokea alawansi kidogo ya kipesa ili kuwasaidia na mahitaji yao ya maisha. Kwa karibu miaka 20, Yehova alikuwa amebariki kazi yetu ya kugawanya vitabu na kwa njia hiyo akatuandalia vitu tulivyohitaji. Yehova hakutuaibisha kamwe kwa kukosa kutusaidia. Sisi tumethibitisha kwamba “kumekuwa hakukupunguka neno moja la ahadi njema yake yote ambayo yeye ameahidi.”—1 Wafalme 8:56, NW.
Kutafuta “Kondoo” Katika Wales
1954 ulitukuta tukiwa katika Milford Haven, Wales. Kujapokuwa na upinzani wa viongozi wa kidini, sisi tulihubiri na tukapata watu fulani wenye mfano wa kondoo ambao waliitikia. Tuliwapanga kitengenezo wakawa kikundi kimoja na kuwaonyesha jinsi ya kuongoza mikutano na kutoa maelezo mafupi yenye kujaa maana. Ilikuwa pindi yenye kujaa shangwe kama nini kuona saba wakibatizwa katika josho (dipu) la kondoo lililojazwa maji yenye ujotojoto ambayo yalipelekwa hapo yakiwa katika mitungi mikubwa ya kusukasukia maziwa!
Katika mji wa Abercynon ulio bondeni katika Wales, ziara ya kufuatia mtu mwenye kupelekewa magazeti kwa ukawaida ilileta matokeo mema. Ingawa bibi yule mwenye kukubali nakala za magazeti kwa ukawaida alisema, “Mimi siitikadi unayoniambia,” yeye alikubali kuyasoma magazeti. Katika ziara ya baadaye, nilipata mume wake akiwa na shughuli nyingi za kupamba nyumba. Baada ya maongezi ya kirafiki, mipango ilifanywa kuanzisha funzo la Biblia juma linalofuata. Tulifanya urafiki na wale wana watatu wake waliokuja kujiunga katika funzo. Mwishowe, mama na wanaye wakaweka maisha zao wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Kufikia tarehe hii, washiriki 35 wa jamaa hiyo wameukubali ukweli, baadhi yao wakitumikia wakiwa mapainia wasaidizi, wa kawaida, au wa pekee na wengine wakiwa wazee.
Haya basi, sisi hawa katika Cardiff tukisimulia mambo ya kule nyuma kuhusu maisha zetu. Hatuna sikitiko lolote. Yehova amekimu kila uhitaji wetu kwa njia ya kimwili. Sisi tumekuwa na maisha mazuri ajabu tukitumikia pamoja tukiwa mapainia, na bado sisi tunahesabu utumishi wa wakati wote kuwa ndiyo hazina yetu iliyo kubwa zaidi maishani.
Sasa mioyo yetu inasisimuka kuona hesabu zenye kuongezeka za mapainia. Na kule kuwaona vijana wale wote wanaouchukua utumishi huu wenye thamani kubwa—lo, sisi tunashangilia kama nini! Mary na mimi tumepainia pamoja kwa miaka 65. Maisha zetu zimekuwa rahisi-rahisi lakini zenye shughuli nyingi, zimekuwa ngumu lakini zenye kuthawabisha. Sisi tunapendekeza kikweli kupainia muda wa maisha yote.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Maud (kushoto) na Mary wangali wanapata hazina yao iliyo kubwa zaidi katika utumishi wa wakati wote kwa Yehova