Jambo Bora Zaidi la Kufanya na Maisha Yangu
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA BOB ANDERSON
Karibu miaka kumi iliyopita, marafiki fulani waliniuliza: “Kwa nini umeendelea kwa muda mrefu ukiwa painia, Bob?” “Ee,” nilitabasamu na kusema, “mwaweza kufikiria jambo lolote bora zaidi la kufanya kuliko upainia?”
NILIKUWA na umri wa miaka 23 katika 1931 nilipoingia katika utumishi wa painia. Sasa niko katika mwaka wangu wa 87 na bado napainia. Ninajua nisingalifanya jambo jingine bora zaidi na maisha yangu. Acha nieleze ni kwa nini.
Katika 1914 trakti iliachwa nyumbani kwetu. Ilitangazwa na International Bible Students, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Shahidi huyo aliporudi, mama yangu alimuuliza kwa makini juu ya moto wa helo. Mama alikuwa amelelewa kuwa Mmethodisti mshupavu wa Wesley lakini hakuweza kamwe kupatanisha fundisho hili la mateso ya milele na Mungu wa upendo. Mara tu alipojifunza ukweli wa jambo hilo, yeye alisema: “Nahisi furaha zaidi kuliko vile nimewahi kuhisi maishani mwangu!”
Mama yangu aliacha mara moja kufundisha kwenye shule ya Jumapili ya Methodisti naye akajiunga na kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia. Alianza kuhubiri katika mji wa nyumbani kwetu wa Birkenhead, unaoelekeana na bandari ya Liverpool upande wa pili wa Mto Mersey, na baada ya muda mfupi alikuwa akiendesha baiskeli kwa kawaida kwenye miji mingi jirani. Alitoa ushahidi katika eneo hili pana kwa muda uliobaki wa maisha yake naye akaja kujulikana vizuri sana, akiwekea watoto wake kielelezo chema. Alikufa mwaka wa 1971 akiwa mzee wa umri wa miaka 97, akiwa Shahidi mtendaji hadi mwisho.
Dada yangu, Kathleen, na mimi tulihamishwa kutoka shule ya Jumapili ya Methodisti kuandamana na mama kwenye mikutano yake pamoja na Wanafunzi wa Biblia. Baadaye, wakati baba yangu aliandamana nasi pia, wazazi wangu walipanga funzo la Biblia la familia la kawaida katika kitabu The Harp of God. Funzo kama hilo lilikuwa jambo jipya katika siku hizo, lakini msingi huu wa mapema katika kweli za msingi za Biblia ulithawabisha sana, kwa kuwa dada yangu na mimi sote tuliingia katika utumishi wa painia mwishowe.
Mama alishikamana na wazo kwamba kutazama “Photo-Drama of Creation” katika Liverpool katika 1920 kulikuwa hatua ya badiliko la kiroho kwetu sisi watoto, naye alisema kweli. Ingawa nilikuwa mchanga sana, utoaji huo uliacha maono dhahiri akilini mwangu. Jambo la kutokeza katika kumbukumbu langu ni ile sehemu inayoonyesha maisha ya Yesu, hasa vile ilivyomwonyesha akitembea kuelekea kifo chake. Ono hilo lote lilinisaidia kukaza fikira juu ya kazi iliyo ya maana zaidi maishani—kuhubiri!
Mapema katika miaka ya 1920, nilianza kugawa trakti pamoja na mama yangu Jumapili alasiri. Kwanza tuliagizwa kuziacha kwenye nyumba; baadaye tuliambiwa tuwape wenye nyumba halafu turudie wale waliopendezwa. Sikuzote nimeona jambo hili kuwa msingi wa mapema wa ziara zetu za kurudia na utendaji wa funzo la Biblia, ulio wenye mazao sana leo.
Kuingia Katika Utumishi wa Painia!
Kathleen na mimi tulibatizwa katika 1927. Nilikuwa nikifanya kazi nikiwa mchanganuaji wa madawa katika Liverpool wakati, katika 1931, nilisikia azimio la kukubali jina Mashahidi wa Yehova. Mara nyingi nilikuwa nimewaona makolpota wa Sosaiti (sasa waitwao mapainia) wakihubiri katika eneo la biashara katika Liverpool, na kielelezo chao kilinivutia sana. Jinsi nilivyotamani kuwa huru na ushirika wa kilimwengu, ili nitumie maisha yangu katika utumishi wa Yehova!
Wakati wa kiangazi cha mwaka huohuo, rafiki yangu Gerry Garrard aliniambia kwamba alikuwa amekubali mgawo wa kuhubiri katika India, kutoka kwa msimamizi wa pili wa Watch Tower Society, Joseph F. Rutherford. Kabla tu hajasafiri kwa meli, alikuja kuniona naye akazungumza juu ya pendeleo la utumishi wa wakati wote. Alipokuwa akiniaga, alinitia moyo zaidi akisema, “Nina hakika utakuwa painia hivi karibuni, Bob.” Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Nilijiandikisha katika Oktoba mwaka huo. Ilikuwa shangwe iliyoje, uhuru ulioje, kuendesha baiskeli kupitia vijia vya mashambani, nikihubiri kwenye jumuiya zilizotengwa! Wakati huo nilijua kwamba nilikuwa nikiingia katika kazi iliyo ya maana sana ambayo ningepata kufanya.
Mgawo wangu wa painia wa kwanza ulikuwa katika South Wales nilipojiunga na Cyril Stentiford. Baadaye Cyril alimwoa Kathleen, nao walipainia pamoja kwa miaka kadhaa. Binti yao Ruth, pia aliingia utumishi wa painia hatimaye. Kufikia 1937, nilikuwa Fleetwood, Lancashire—nikiwa mwenzi wa Eric Cooke. Hadi wakati huo, mapainia walihubiri maeneo ya mashambani pekee ya Uingereza, nje ya eneo la kutaniko. Lakini Albert D. Schroeder, aliyekuwa mwenye daraka la kazi ya ofisi ya tawi ya Sosaiti ya London wakati huo, alifanya uamuzi wa kutuhamisha kwenda jiji la Bradford, Yorkshire. Huu ulikuwa wakati wa kwanza ambapo mapainia katika Uingereza walikuwa wamegawiwa kusaidia kutaniko hususa.
Katika 1946, Eric alienda kwenye Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower naye akagawiwa kwenda upande wa Kusini wa Rhodesia, sasa Zimbabwe, naye na mkeye bado wanatumika kwa uaminifu wakiwa wamishonari katika Durban, Afrika Kusini.
Mwaka wa 1938 ulinikuta katika mgawo mwingine, wakati huu nikiwa mtumishi wa eneo (sasa aitwaye mwangalizi wa mzunguko) wa kaskazini-magharibi mwa Lancashire na Wilaya ya Lake yenye kupendeza. Huko nilikutana na Olive Duckett, na tulipooana, alijiunga nami mara moja katika kazi ya mzunguko.
Ireland Wakati wa Miaka ya Vita
Mara baada ya Uingereza kutangaza vita dhidi ya Ujerumani katika Septemba 1939, mgawo wangu ulibadilishwa niende Ireland. Kuandikishwa jeshini kulikuwa kumeanza katika Uingereza lakini si katika upande wa kusini wa Jamhuri ya Ireland, ambayo ilibaki ikiwa nchi isiyokuwamo wakati wa vita. Jamhuri ya Ireland na Ireland Kaskazini zilikuwa ziwe mzunguko mmoja. Hata hivyo, kulikuwa na vizuizi, na ilikuwa lazima kupata vyeti vya ruhusa ya kusafiri ili kuondoka Uingereza kwenda sehemu yoyote ya Ireland. Wenye mamlaka waliniambia ningeweza kwenda, lakini ningelazimika kukubali kurudi Uingereza mara moja wakati umri wangu wa kuandikishwa jeshini ulipofika. Nilikubali kwa maneno, lakini kwa kushangaza, wakati cheti changu cha ruhusa kilipotoka, hakikuwa na masharti yoyote pamoja nacho!
Wakati huo, kulikuwa na Mashahidi wazidio 100 tu katika Ireland nzima. Tulipofika Dublin katika Novemba 1939, Jack Corr, aliyekuwa painia muda mrefu, alitulaki. Alituambia kwamba kulikuwa na mapainia wengine wawili katika mji ulio karibu-karibu na watu wachache wenye kupendezwa katika Dublin, karibu 20 kwa ujumla. Jack alikodi chumba katika Dublin kwa ajili ya mkutano ambako wote walikubali kukutana kwa ukawaida kila Jumapili. Mpango huu uliendelea hadi kutaniko lilipoanzishwa 1940.
Ireland Kaskazini, ikiwa sehemu ya United Kingdom, ilikuwa vitani pamoja na Ujerumani, hivyo tukiwa tunahamia kaskazini kuelekea Belfast, tulikuwa na vyeti vya kupokea posho na vipindi vya kuzimiwa taa usiku vya kukabiliana navyo. Ijapokuwa ndege za Nazi zililazimika kuruka umbali wa kilometa 1,600 ili kufika Belfast na kurudi kwenye makao yazo katika Ulaya, zilifaulu kupiga bomu jiji hilo kwa matokeo. Wakati wa shambulio la kwanza, Jumba la Ufalme letu lilipata madhara na nyumba yetu ikaharibiwa tulipokuwa tukiwatembelea ndugu katika sehemu nyingine ya jiji, hivyo tulipona kiajabu. Usiku huohuo, familia ya Mashahidi ilikimbilia mahali pa usalama pa watu wote. Walipofika hapo, walikuta pakiwa pamejaa watu ikawabidi kurudi nyumbani kwao. Mahali hapo pa usalama palipigwa bomu moja kwa moja, na wote waliokuwamo wakauawa, lakini ndugu zetu waliokoka wakiwa na majeraha na machubuko machache. Wakati wa hii miaka migumu ya vita, hakuna mmoja wa ndugu zetu aliyeumia sana, jambo ambalo tulishukuru Yehova kwalo.
Ugavi wa Chakula cha Kiroho
Vita ilipokuwa ikiendelea, vizuizi viliongezeka sana, na mwishowe upekuzi wa barua ukaamuriwa. Hii ilimaanisha kwamba Mnara wa Mlinzi lilizuiliwa na halikuruhusiwa kuingia nchini. Ingawa tulishindwa tungefanyaje, mkono wa Yehova haukuwa mfupi. Asubuhi moja nilipokea barua kutoka kwa “binamu” katika Kanada aliyekuwa akiniandikia kuhusu mambo ya kifamilia. Mimi sikujua hata kidogo yeye alikuwa nani, lakini mwishoni mwa barua alisema alikuwa ametia ndani “makala ya Biblia yenye kupendeza” ili niisome. Ilikuwa nakala ya Mnara wa Mlinzi, lakini kwa sababu ilikuwa na jalada lisilo na maandishi, ilikuwa haijaondolewa na upekuzi.
Mara hiyohiyo mke wangu na mimi, na kwa msaada wa Mashahidi wa hapo, kutia ndani Maggie Cooper aliyekuwa amekuwa katika kazi ya “Photo-Drama” tulianza kunakili makala hizo. Upesi tulijipanga ili kupeleka nakala 120 kotekote nchini, mara magazeti ya Mnara wa Mlinzi yenye jalada lisilo na maandishi yalipokuwa yakifika kwa ukawaida kutoka kwa marafiki wengi wapya katika Kanada, Australia, na Marekani. Hatukukosa kamwe toleo moja wakati wa kipindi chote cha vita, kwa sababu ya bidii nyendelevu na fadhili yao.
Pia, tuliweza kuwa na makusanyiko. Mkusanyiko wa 1941 ulikuwa wenye kutokeza wakati kichapo kipya Children kilipotangazwa. Ilionekana kwamba mpekuzi hakuzuia kitabu ambacho alifikiri kilihusu watoto, hivyo tuliweza kuingiza ugavi wetu nchini bila taabu yoyote! Katika pindi nyingine, tulichapisha kijitabu Peace—Can It Last? nchini kwa sababu haikuwezekana kuingiza nakala kutoka London. Ijapokuwa vizuizi vyote hivyo tulivyowekewa, tulitunzwa vizuri kiroho.
Kuushinda Upinzani
Kasisi aliyekaa katika nyumba ya kutunzia wagonjwa ya Belfast iliyosimamiwa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimpelekea mkeye nakala ya kitabu Riches katika Uingereza. Mkeye aliipinga kweli, na katika majibu yake alielewesha wazi jambo hilo. Yeye alisema pia kwamba tulikuwa “tengenezo lisilo la kizalendo.” Mpekuzi wa barua aliona hilo naye akaripoti jambo hilo kwenye Idara ya Upelelezi wa Uhalifu. Kama tokeo, niliitwa kwenye kituo cha polisi kutoa maelezo na nikaambiwa nilete nakala ya kitabu Riches. Kwa kupendeza, kitabu hicho kiliporudishwa mwishowe, niligundua kwamba sehemu zilizokuwa zimepigwa mstari zote zilihusu Kanisa Katoliki ya Kiroma. Nilihisi kwamba hili lilifaa, maana nilijua kwamba polisi walikuwa macho dhidi ya utendaji wa IRA (Jeshi la Jamhuri ya Ireland).
Nilihojiwa kwa makini kuhusu kutokuwamo kwetu nyakati za vita, kwa kuwa polisi waliona vigumu kuelewa msimamo wetu. Lakini wenye mamlaka hawakuchukua kamwe hatua yoyote dhidi yetu. Baadaye nilipoomba ruhusa ya kufanya kusanyiko, polisi alisisitiza kutuma polisi wawili wapeleka-habari. Nilisema, “Tutawakaribisha!” Hivyo walikuja na kuketi mkutano wote wa alasiri, wakiandika maandishi yaliyofupizwa. Mwishoni mwa kipindi hicho, wakauliza, “Kwa nini tulitumwa hapa? Tunafurahia kila kitu!” Walikuja tena siku iliyofuata na kwa shukrani wakakubali kuchukua nakala iliyotolewa bure ya kijitabu chetu Peace—Can It Last? Sehemu nyingine ya kusanyiko ilipita bila tukio lolote.
Mara tu vita ilipokwisha na vizuizi vya kusafiri vikaondolewa, Pryce Hughes kutoka Betheli ya London akaja Belfast. Aliandamana na Harold King, aliyegawiwa baadaye kwenda China akiwa mishonari. Baada ya miaka sita ya kutengwa mbali na ofisi ya tawi ya London, sisi sote tulitiwa moyo sana na hotuba walizotoa ndugu hawa. Muda mfupi baadaye, Harold Duerden, painia mwingine mwaminifu, alitumwa kutoka Uingereza ili kuimarisha kazi ya Ufalme katika Belfast.
Kurudi Uingereza
Tulikuwa tumekuja kuwapenda ndugu wa Ireland, na ilikuwa vigumu kurudi Uingereza. Lakini mke wangu na mimi tuligawiwa kurudi Manchester na baadaye tukahamia Newton-le-Willows, mji mwingine wa Lancashire ambapo uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi. Lois, binti yetu, alizaliwa katika 1953, na ilichangamsha moyo kumwona akiingia huduma ya painia akiwa na umri wa miaka 16. Baada ya kuolewa na painia fulani David Parkinson, waliendelea na utumishi wao wa wakati wote katika Ireland Kaskazini, kwa njia nyingi wakifuatia hatua ambazo Olive na mimi tulikuwa tumechukua. Sasa, wao pamoja na watoto wao, wamerudi Uingereza, na sisi sote tunatumika katika kutaniko lilelile.
Yajapokuwa mabadiliko katika hali zetu, sikuacha kamwe kupainia—Olive hakutaka hilo kamwe, wala mimi sikutaka. Sikuzote nimehisi kwamba rekodi yangu ya upainia imewezekana kwa sababu ya mke wangu kwa sababu bila, utegemezo wake wa daima wenye upendo, singaliweza kamwe kuendelea na utumishi wa wakati wote. Bila shaka, sote wawili tunachoka haraka sana sasa, lakini kutoa ushahidi bado ni shangwe, hasa tunapokuwa pamoja, tukiongoza mafunzo ya Biblia na majirani wetu. Muda wa miaka mingi, tumependelewa kusaidia watu mmoja-mmoja karibu mia moja wawe watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, na kubatizwa. Hiyo imekuwa shangwe kama nini! Nakiri idadi hii lazima kufikia sasa iwe imeongezeka mara nyingi zaidi familia zinapaponuka mpaka vizazi vya tatu na vya nne vikawa Mashahidi pia.
Mara nyingi Olive na mimi huzungumza juu ya mapendeleo na maono yetu mengi ya miaka mingi. Imekuwa miaka yenye shangwe kama nini, na jinsi imepita kwa haraka! Najua singaliweza kupata jambo bora zaidi la kufanya na maisha yangu kuliko kumtumikia Mungu wangu, Yehova, nikiwa painia miaka hii yote. Sasa, iwe ni kutazama nyuma kwa shukrani au kutazama mbele kwa matazamio, naona kwamba maneno ya Yeremia ni yenye maana sana: “Ni huruma za BWANA kwamba hatuangamii, kwa kuwa rehema zake hazikomi. Ni mpya kila siku asubuhi. . . . Kwa hiyo nitamtumaini yeye.”—Maombolezo 3:22-24.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Bob na Olive Anderson