Endeleeni Kupanda Mbegu—Yehova Ataikuza
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA FRED METCALFE
MAPEMA katika 1948, katika utumishi wangu wa nyumba kwa nyumba,Nilitembelea shamba dogo mpakani mwa Cork kusini mwa Ailandi.Nilipomwelezea mkulima mimi ni nani, aliiva uso. Alipandwa na hasira kaliakapaza sauti kwamba mimi ni Mkomunisti, akakimbia kuchukua uma wake wa kulimia. Bila kufikiri tena, niliondoka mbio kutoka shamba hilo nikairukiabaisikeli ambayo nilikuwa nimeiacha upande wa barabara. Mlima ulikuwa wima sana,lakini niliiendesha kasi iwezekanavyo kwenye mteremko huo, bila kuangalia nyuma,kwa kuwa niliwaza mkulima huyo akinirushia uma wake wa kulimia kama mkuki mfupi.
NILIKUWA nimezoea maitikio-tendo kama hayo miaka miwili tangu nije Jamhuri ya Ailandi kutoka Uingereza nikiwa painia wa pekee katika 1946. Kikundi kidogo cha wahubiri wa Ufalme ambacho nilijiunga nacho, kikiwa na idadi ya 24 tu, kilikuwa tayari kimeona mashambulio mengi ya uadui na uchongezi. Lakini nilikuwa na hakika kwamba roho ya Yehova hatimaye ingeleta matokeo.—Wagalatia 6:8, 9.
Hata hivyo, kabla sijasimulia jinsi mambo yalivyoendelea, acha niwaambie kidogo juu ya maisha yangu ya mapema na mazoezi yaliyoniimarisha chini ya hali zenye kujaribu kama hizo.
Mfano na Mazoezi Mazuri ya Wazazi
Baba yangu alipata kweli mapema katika 1914. Wakati alipokuwa anasafiri kurudi nyumbani kutoka kwenye mchezo wa kandanda katika Sheffield, Uingereza, alisoma trakti ya Biblia iliyoeleza hali ya wafu. Alikuwa tayari amezuru makanisa mengi ili kupata majibu kwa maswali yake lakini hakufaulu. Yale aliyoyasoma katika trakti hiyo, yalimsisimua. Alipeleka ombi la kupata mabuku sita ya Studies in the Scriptures ambayo trakti ilikuwa imetangaza, akayasoma kwa bidii, mara nyingi hadi saa za mapema za asubuhi. Baba aling’amua kweli kwa haraka.
Upesi alianza kushiriki pamoja na kundi la mahali petu la Mashahidi wa Yehova, ushirika uliodumu miaka zaidi ya 40, mwingi wa muda huo akitumika akiwa mwangalizi-msimamizi. Kwa furaha baba yangu, ndugu zake wawili na dada zake wote watatu walikubali kweli. Mmoja wa Ndugu zake alimshuhudia msaidizi kijana wa duka, naye na dada yake pia wakawa Wakristo waliojiweka wakfu na kupakwa-mafuta. Baba yangu na ndugu yake waliwaoa wanawake hao wawili.
Katika familia yetu nilikuwa mmoja wa wavulana wanne waliolelewa katika “malezi na onyo la upole la Bwana.” (Waefeso 6:4, King James Version) Ninaterema kwamba wazazi wangu waliweka bidii nyingi katika kukuza kweli ndani yetu. Wakati huo hakukuwa vichapo ambavyo vilikusudiwa hasa kusaidia wazazi kufundisha watoto kweli za Biblia; lakini tulikuwa na funzo la Biblia la familia la kawaida mara mbili kila juma kwa kutumia kitabu The Harp of God, na pia mazungumzo ya kawaida juu ya andiko la siku.—Kumbukumbu 6:6, 7; 2 Timotheo 3:14, 15.
Mama yangu na baba yangu walikuwa mfano wa ajabu pia katika kuthamini kwao mikutano na katika bidii yao katika huduma. Kuongezea sifa zake nzuri za kiroho, baba yangu alikuwa pia mfurahifu, ambayo aliwapitishia watoto wake. Kazi ngumu ya wazazi wangu iliongoza kwenye matokeo mazuri. Wana wao wote wanne, sasa wakiwa katika miaka yao ya 60, bado wanamtumikia Yehova kwa furaha.
Kuingia Utumishi wa Painia
Katika Aprili 1939, nikiwa na umri wa miaka 16, nilimaliza shule na kuwa painia wa kawaida. Baba yangu alijiunga nami katika utumishi wa painia na akanipa mazoezi ya juu sana. Tukiwa tunasafiri kwa baisikeli, tulieneza kikamili eneo lililokuwa umbali wa kilometa 11 kuzunguka nyumbani kwetu. Kila siku sote wawili tulichukua vijitabu 50, na hatukurudi nyumbani mpaka tulipokuwa tumeviangusha.
Miaka miwili baadaye nilipata pendeleo kuwa miongoni mwa mapainia wa pekee wa kwanza waliopewa migawo katika Uingereza. Ilikuwa shangwe kupokea baraka hiyo, lakini ilihuzunisha sana kuacha usalama wa furaha wa nyumba ya kitheokrasi. Wakati ulipopita na kwa msaada wa Yehova, nilijirekebisha.
Utumishi wangu wa painia ulikatizwa na Vita ya Ulimwengu 2 wakati nilipofungwa pamoja na Mashahidi wengine vijana, juu ya suala la kutokuwamo. Katika gereza la Durham, niliwekwa sehemu ya YP (“Young Prisoner,” Mfungwa Kijana). Hiyo ilimaanisha nilipaswa kuvaa suruali fupi—kwa wazi ikiwa hasara katika hali ya baridi. Hebu wazia Wilf Gooch (ambaye sasa ni mratibu wa Halmashauri ya Tawi katika Uingereza), Peter Ellis (mshirika wa Halmashauri ya Tawi ya Uingereza), Fred Adams, na mimi—sote tukiwa na urefu wa meta 1.8 hivi—tukisimama pamoja tukiwa tumevaa suruali fupi kama wavulana wa shule!
Mgawo—Ailandi
Nilipainia katika sehemu tofauti-tofauti za Uingereza kwa miaka mitatu, baada ya kuachiliwa kwangu kutoka gerezani. Halafu nikapokea mgawo ambao ungethibitika kuwa wenye kujaribu na wenye kuridhisha sana—Jamhuri ya Ailandi. Yote niliyoyajua kuhusu Ailandi ya kusini ni kwamba karibu kila mtu huko alikuwa Mkatoliki wa Kiroma. Lakini nilipuuza maelezo mabaya yaliyotolewa na wengine na sikusita kukubali mgawo huo. Huo ulikuwa wakati wa kupanua ibada ya kweli, na nilikuwa na hakika kwamba Yehova, kupitia roho takatifu yake angenisaidia.
Wengi wa Mashahidi katika Jamhuri ya Ailandi walikuwa katika mji mkuu, Dublin, pakiwa na mmoja au wawili tu waliotawanyika penginepo. Hivyo, watu wengi walikuwa hata hawajaona mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilianza kazi katika mji wa Cork, pamoja na mapainia wa pekee wengine watatu. Haikuwa rahisi kupata msikilizaji. Katika Misa yao, mapadri walionya daima dhidi yetu, wakituita “Maibilisi Wakomunisti.” Magazeti ya habari pia yalionya dhidi ya utendaji wetu mbalimbali.
Siku moja kinyozi alikuwa akikata nywele zangu akitumia wembe ulionyoka (mkali mno usio na kifuniko). Katika mazungumzo yetu, aliniuliza juu ya jambo nililokuwa ninafanya katika Cork. Nilipomwambia, alipandwa na hasira akanitukana. Mkono wake ulikuwa unatetemeka kwa hasira, nami nikawazia ni-kitembea nje ya duka hilo huku kichwa changu kilichokatwa kimeshikiliwa na mkono wangu! Kilikuwa kitulizo kama nini kuondoka dukani mwake nikiwa mzima!
Jeuri ya Wafanya Ghasia
Nyakati nyingine tulihitaji kukabili jeuri ya wafanya ghasia. Kwa mfano, siku moja katika Machi 1948, tulikuwa wenye shughuli katika utumishi wa nyumba kwa nyumba wakati wafanya ghasia waliposhambulia mwenzi wangu, Fred Chaffin. Akiwa anafuatiliwa na umati huo, Fred alikimbilia kituo cha basi akasihi dereva wa basi na kondakta wamsaidie. Badala yake, walijiunga katika shambulio hilo. Fred alikimbia mbele zaidi barabarani akaweza kujificha nyuma ya ukuta mrefu ambao ulizunguka nyumba ya padri.
Wakati huo huo nilikuwa nimeenda kuchukua baisikeli yangu. Ili kurudi katikati ya mji, nilipitia barabara ya upande, lakini nilipotokea kwenye barabara kuu wafanya ghasia walikuwa wakingojea. Wanaume wawili walininyang’anya mkoba wangu wakarusha hewani vilivyokuwamo. Halafu wakaanza kunipiga ngumi na mateke. Ghafula mwanamume mmoja akatokea. Alikuwa polisi mwenye nguo za kawaida, naye akakomesha shambulio hilo, akapeleka mimi na washambulizi hao kwenye stesheni ya polisi.
Shambulio hilo liliandaa msingi wa “kuitetea Injili [habari njema, NW] na kuithibitisha.” (Wafilipi 1:7) Kesi ilipokuja mahakamani, polisi aliyekuwa ameniponyoa, yeye mwenyewe akiwa Mkatoliki wa Kiroma, alitoa ushuhuda, na watu sita wakashtakiwa kushambulia. Kesi ilionyesha kwamba tulikuwa na haki ya kwenda mlango kwa mlango na ilitumika kama kuzuizi kwa wengine ambao wangefikiri kutumia jeuri.
Mwanzoni ilifikiriwa kuwa jambo la hatari sana kupeleka akina dada wakiwa mapainia mahali kama Cork. Hata hivyo, mara nyingi ilionekana kwamba ingekuwa afadhali kwa akina dada kuwazuru wanawake wenye kupendezwa. Kwa hiyo, kabla tu ya shambulio hilo, Sosaiti ilikuwa imewapa dada mapainia wawili wazuri mgawo wa kuja Cork. Mmoja, Evelyn MacFarlane, baadaye alikuja kuwa misionari na akafanya kazi nzuri sana katika Chile. Yule mwingine, Caroline Francis, ambaye alikuwa ameuza nyumba yake huko London ili kupainia katika Ailandi, alikuja kuwa mke wangu.
Mbegu za Kweli Zachipuka
Ingalikuwa rahisi kufikiri kwamba tulikuwa tunapoteza wakati wetu bure tukipanda mbegu za ukweli wa Ufalme chini ya hali kama hizo. Lakini kuona kweli ikichipuka hapa na pale, kuliendeleza uhakika wetu katika nguvu ya Yehova kufanya mambo yakue. Kwa mfano, wakati mmoja Sosaiti ilipeleka jina na anwani za mtu aliyekuwa ameandika akiomba nakala ya kitabu Let God Be True. Anwani hiyo ilikuwa katika Fermoy, mji mdogo kilometa 35 hivi kutoka mji wa Cork. Kwa hiyo Jumapili moja asubuhi nikaenda zangu kutafuta mtu huyo.
Nilipofika Fermoy, nilimwuliza mtu mmoja anipe maelezo ya njia. “Loo,” alisema, “hiyo ni kilometa 14 nyingine mbele.” Nikaanza mwendo tena na hatimaye nikafika kwenye shamba lililo kwenye barabara ndogo ya jimbo. Yule mwanamume kijana aliyepeleka ombi la kitabu alikuwa amesimama kwenye lango la shamba. Nilipojitambulisha alisema hivi: “Kitabu hiki ni cha thamani sana kama dhahabu ya uzito wacho!” Tulikuwa na mazungumzo mazuri, na hata ni kama sikuona urefu wa kilometa 50 wa safari yangu ya baisikeli kurudi nyumbani. Hata sasa, baada ya miaka 40 baadaye, ninapata furaha nyingi ninapokutana na yule mwanamume “kijana,” Charles Rinn, kila mwaka katika mikusanyiko. Leo, kuna makundi kumi katika eneo hilo la Cork.
Muda wa miaka ya 1950, Caroline nami tulitawanya mbegu nyingi za kweli katika maeneo ya katikati ya Ailandi. Kitia-moyo cha kuendelea kuvumilia kilikuja katika 1951 wakati watu wapole kama “Granny” Hamilton na binti-mkwe wake walipoitikia upesi. “Granny” Hamilton alikuja kuwa mhubiri wa kwanza aliyebatizwa katika Wilaya ya Longford.—1 Wathesalonike 2:13.
Mahali pa kukaa palikuwa tatizo. Mara tu mkazo ulipotolewa kwa wenyeji wa nyumba, walituomba tuondoke. Kwa hiyo, tukiwa tumepoteza mahali pa kukaa patatu kwa mfululizo wa upesi, tulinunua hema, shiti ya kutandika chini, na mafumba (mifuko ya kulalia) tukayabeba nasi ndani ya gari aina ya Y-model Ford. Tulisimamisha hema popote tulipoweza mwishoni mwa kutoa ushuhuda kila siku. Baadaye tulipata gari-nyumba lenye urefu wa meta 4. Lilikuwa dogo sana, likiwa na vifaa vichache vya ki-siku-hizi—tulihitaji kutembea nusu kilometa ili kupata maji ya kunywa—na halikuwa limezuiwa ili joto lisitoke, lakini kwetu sisi lilikuwa utajiri. Ufurahifu wangu ulijaribiwa siku moja nilipoteleza kwenye mzizi wa mti wenye umajimaji na kuanguka kinyumenyume ndani ya kisima kirefu, chembamba, lakini kisicho na kina kirefu sana. Hata hivyo, tuliwapa mwangalizi wa mzunguko na mke wake mahali pa kukaa katika gari-nyumba hilo walipotuzuru.
Nyakati nyingine watu wenye mioyo mizuri walionyesha fadhili isiyotarajiwa. Kwa mfano, tulienda Sligo magharibi mwa Ailandi katika 1958, miaka minane baada ya mume na mke mapainia kufukuzwa mjini. Tulisali kwa ajili ya msaada wa Yehova ili tupate mahali pazuri pa gari-nyumba, na baada ya saa nyingi za kutafuta-tafuta tulikuta mahali pakubwa pa kuchimbua mawe, pasipotumiwa. Mwanamume aliyekuwa akichunga ng’ombe mbele kwenye kijia alituambia kwamba familia yake ndio waliokuwa wenye mahali hapo pa kuchimbua mawe. “Je! tunaweza kupatumia?” tukaomba, tukimwambia kwamba sisi tulikuwa wawakilishi wa sosaiti ya Biblia. Alisema hiyo ingekuwa sawa.
Muda mfupi baadaye aliuliza hivi: “Ninyi ni wa sosaiti gani ya Biblia?” Huo ulikuwa muda wa wasiwasi. Tulimwambia kwamba tulikuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa kitulizo kikubwa kwetu, alibaki kuwa mwenye urafiki. Majuma machache baadaye, alitupa risiti ya kodi ya mwaka mmoja kwa mahali hapo. “Hatutaki pesa zozote,” alisema. “Lakini tunajua upinzani ambao nyinyi watu hukabili, kwa hiyo ikiwa yeyote anahoji haki yenu ya kuwa hapa, huo ndio ushuhuda wenu.”
Tulipokuwa Sligo, tulisikia juu ya mwanamume fulani, mwenye duka na mchezaji kandanda anayejulikana sana, ambaye alikuwa ameonyesha kupendezwa kwa kadiri wakati mapainia waliotangulia walipokuwa bado mjini. Hata hivyo, alikuwa amekuwa na kupashana habari kudogo kwa miaka minane, kwa hivyo hatukujua jinsi alivyokuwa sasa. Tabasamu kunjufu usoni mwa Mattie Burn nilipojitanguliza kwake ilitoa jibu. Mbegu za kweli zilizopandwa miaka mingi kabla ya hapo hazikuwa zimekufa. Yeye bado ni mshirika wa kundi dogo lenye utendaji katika Sligo.
Mielekeo Yenye Kubadilika
Mahali pamoja palipoonyesha kwa ufupi mwelekeo wa uadui wa wengi kutuelekea palikuwa mji wa Athlone. Wakati kutoa ushuhuda kwa uzito kulipoanzwa hapo katika miaka ya 1950, mapadri walipanga ili wote walioishi katika sehemu moja ya mji watie sahihi ombi linalosema kwamba hawakutaka Mashahidi wa Yehova kutembelea milangoni mwao. Walilipeleka kwa serikali, wakifanya kazi huko Athlone kuwa ngumu sana kwa miaka kadhaa. Wakati mmoja kikundi cha vijana walinitambua kuwa Shahidi na wakaanza kurusha mawe. Niliposimama mbele ya dirisha la duka, mwenyewe alinialika ndani ya duka lake—hasa ili alinde dirisha lake kuliko kunilinda mimi—akaacha niondoke kupitia njia ya nyuma ya kutokea.
Hata hivyo, hivi karibuni, katika Agosti 1989, nilipoongoza hotuba ya maziko katika Athlone kwa ajili ya ndugu mwaminifu, sikuwa na budi kushangaa juu ya jinsi Yehova alivyofanya mambo yakue huko. Zaidi ya washirika wa kundi, watu 50 hivi wa mahali hapo walisikiliza kwa heshima hotuba hiyo ya maziko katika Jumba la Ufalme zuri ambalo akina ndugu walikuwa wamejenga.
Mazoezi ya Pekee Kwenye Shule ya Gileadi
Katika 1961, nilialikwa kwenye masomo ya miezi kumi huko Watchtower Bible School of Gilead. Masomo hayo ya pekee yalikuwa kwa ajili ya akina ndugu tu, kwa hiyo Caroline nami tulihitaji kufikiria mwaliko huo kwa sala. Hatukuwa tumetenganishwa kwa miaka 12. Tena, kwa kuwa mke wangu alikuwa na tamaa sana ya kuhudhuria Shule ya Gileadi na kuwa misionari, alitamauka sana kwa kutoalikwa. Lakini, kwa kuwa mwenye akili ya kuchukua mambo kiheshima, aliweka faida za ufalme kwanza na akakubali niende. Masomo hayo yalikuwa pendeleo la ajabu. Lakini ilikuwa shangwe kurudi nyumbani na kujishughulisha na kazi katika ofisi ya tawi ya Sosaiti, kuwapa kitia-moyo Mashahidi 200 au zaidi waliokuwa wakipanda na kutia maji Ailandi katika miaka ya mapema ya 1960.
Miaka mingine baadaye, katika 1979, Caroline alipata kwenda kwenye ofisi kuu ya Mashahidi wa Yehova katika New York nilipoalikwa kwenye masomo ya pekee kwa ajili ya washiriki wa Halmashauri ya Tawi. Kilikuwa kilele cha kile ambacho kilitokea kuwa sehemu ya mwisho ya uhai wake. Miaka miwili baadaye alikufa. Kwa muda wa ile miaka 32 tuliyotumikia pamoja katika utumishi wa wakati wote, Caroline hakupoteza kamwe wala bidii yake katika utumishi wa Yehova wala uhakika wake kwamba Yeye angeweza kufanya mambo yakue.
Nilimkumbuka kwa hamu sana. Jambo moja lililonisaidia nikabiliane lilikuwa makala katika gazeti la Amkeni! ya wakati huo, yenye kichwa “Kujifunza Kuishi Bila Mpendwa Wako.” (Agosti 8, 1982) Machozi yalinijia machoni wakati wowote nilipofikiri juu ya mwenzi wangu aliyepotea, lakini nilifanya yale ambayo makala hiyo ilidokeza na nikaendelea kuwa na shughuli katika utumishi wa Yehova.
Baraka ya Yehova Yaendelea
Mwaka mmoja kabla ya hilo, katika Aprili 1980, nilikuwako wakati Ndugu Lyman Swingle wa Baraza Linaloongoza alipozindua jengo jipya la tawi katika Dublin. Ilisisimusha kama nini kuona wahubiri 1,854 wa shamba hili, ambalo kwa wakati huo lilikuwa lenye kutia ndani Ailandi Kaskazini pia! Na sasa, miaka kumi baadaye, Kitabu-Mwaka kinaripoti kilele cha 3,451 kwa 1990!
Wakati huo huo nimekuwa na baraka nyingine zaidi. Nilipokuwa nikitumikia nikiwa mfunzi wa Shule ya Huduma ya Ufalme, nilikutana na Evelyn Halford, dada mwenye kuvutia na mwenye bidii ambaye alikuwa amehamia Ailandi kutumika penye uhitaji mkubwa zaidi. Tulioana katika Mei 1986, naye amethibitika kuwa tegemezo halisi kwangu katika utendaji wangu wote wa kitheokrasi.
Kati ya miaka yangu 51 ya utumishi wa wakati wote tangu nilipoacha shule, 44 imetumika katika Ailandi. Inachangamsha kuona wengi niliowasaidia ambao bado wanamtumikia Yehova, wengine wakiwa wazee na watumishi wa huduma. Naweza kusema bila kusita kwamba shangwe moja kubwa zaidi ambayo mtu aweza kuwa nayo ni kusaidia mtu mwingine kwenye njia ya uhai.
Limekuwa jambo la kuimarisha imani, kuona ibada ya kweli ikikua katika mahali pamoja baada ya pengine katika Ailandi, ujapokuwa upinzani mkali. Sasa, wahubiri 3,500 hivi wanashiriki pamoja na zaidi ya makundi 90 nchini pote. Kweli kweli, hakuna mpaka wa yale ambayo Yehova anaweza kufanya. Yeye atafanya mambo yakue ikiwa tutapanda na kutia maji kwa bidii. (1 Wakorintho 3:6, 7) Mimi najua ukweli wa hilo. Nimeliona likitokea Ailandi.
[Picha of Fred and Evelyn Metcalfe katika ukurasa wa 25]
[Picha of Fred Metcalfe katika ukurasa wa 28]