Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Zile Habari Njema Zasitawi Katika Saiprasi Ujapokuwako Upinzani
MTUME Paulo alihubiri zile habari njema za Ufalme katika Saiprasi. (Matendo 13:4-12) Hiyo ilikuwa katika 47-48 W K. Leo, zile habari njema zinahubiriwa katika kisiwa hicho chenye sura nzuri na Mashahidi wa Yehova 1,154, na katika Aprili wa mwaka huu, watu 2,570 walihudhuria ile ibada ya Ukumbusho, jambo ambalo linaonyesha kwamba kuna watu wengi wenye mioyo ya ufuataji haki na wenye kumwogopa Mungu katika kisiwa hicho. Lakini ingawa wengi wa watu wa huko wanakaribisha ujumbe wa Biblia wenye amani unaotokezwa na Mashahidi wa Yehova, viongozi wa kidini wa Orthodoksi la Kigiriki wanapinga kazi hii, sawa tu na wale viongozi wa kidini Wayahudi katika siku ya Yesu. (Yohana 15:20) Afisi ya tawi ya Saiprasi inaandika hivi: “Kwa kadiri isiyopata kuonekana tena, Kanisa Orthodoksi la Kigiriki linaonyesha limepiga moyo konde ili kufanyia fujo utendaji wetu wa kuhubiri.” Halafu ripoti hiyo inaeleza jinsi hao viongozi wa kidini wanasumbua-sumbua akina ndugu katika huduma yao ya nyumba kwa nyumba na kujaribu kuwachokoza ili kujaribu kuwahusisha ndani ya ubishi. Halafu wanawashtaki kwamba walisababisha fujo, lakini akina ndugu wanakataa kuchokozeka halafu wanaenda zao.
Kweli kweli, mara nyingi upinzani wa viongozi wa kidini huwarukia wao wenyewe, kama vile ono lifuatalo linavyoonyesha: “Miezi michache iliyopita, mwanamke mmoja alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na hivi majuzi mume wake akajiunga naye. Ndipo mwanatheolojia mmoja alipozuru mume na mke hao, akitumainia kuwasadikisha waache funzo lao la Biblia. Mwatheolojia huyo alijaribu kuwaeleza juu ya Utatu. Baada ya muda yule mume akamkatiza na kusema: ‘Mimi sielewi ni jinsi gani Yesu, ambaye sasa yuko mbinguni akiwa katika mwili wenye mnofu, kama vile wewe unavyodai, angeweza wakati ule ule kuwa ni mtu mmoja na Mungu ambaye yumo katika umbo la roho.’ Jibu la mwanatheolojia huyo lilikuwa, ‘Eeh, si lazima uelewe kila kitu.’ Mtu huyo mwenye kupendezwa akasema: ‘Lakini mimi naelewa kwamba Yesu ndiye Mwana wa Mungu wala siye Mungu mwenyewe. Mimi sitaki kusikia tena juu ya Utatu.’ Kusikia hivyo mwanatheolojia huyo akasimama na kusema hivi kwa hasira: ‘Wewe pia umefika mbali na funzo lako la Biblia. Huwezi kubadilika
Sasa yule mke anahudhuria mikutano yote na alibatizwa kwenye “Tumaini [Itibari] Katika Yehova” Mkusanyiko wa Wilaya Mume anaendelea na funzo lake na anahudhuria mikutano fulani.
“Hivyo, wajapofanya jitihada zao, viongozi wa kidini hawatimizi mradi wao,” inataarifu ripoti hiyo kutoka kwenye afisi ya tawi ya Saiprasi. “Bali, kile tunachoona ni kwamba sasa watu wenye kupendezwa wanahudhuria mikutano zaidi ya wakati mwinginewo wote. Wakati ule ule, akina ndugu wamezidi kupiga moyo konde kuwaletea wenye mioyo ya ufuataji haki zile habari njema.” Yehova anategemeza washikamanifu wake kama alivyoahidi angefanya kwenye Yeremia 1:19: “Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema BWANA [Yehova, NW], ili nikuokoe”