Nani Atakuwa Mwenye Kukubaliwa na Yehova?
“Endeleeni kujifanyizia wokovu wenu wenyewe . ..; kwa maana Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya raha njema yake, anatenda ndani ya nyinyi ili nyinyi mnie na kutenda pia.”—WAFILIPI 2:12, 13, NW.
1, 2. Ni katika hali gani Yesu alipokea tangazo la kibali cha kimungu, na kwa nini jambo hilo litupendeze sisi?
ILIKUWA hatua ya badiliko kubwa katika historia. Yohana Mbatizaji alikuwa amekuwa akihubiri ujumbe wa Mungu na kuwazamisha katika maji wenye kutubu. Ndipo mwanamume mmoja akakaribia ambaye Yohana alimjua kuwa mwadilifu; yeye alikuwa Yesu. Hakuwa na dhambi aliyohitaji kutubia, hata hivyo aliomba abatizwe ili “kutimiza yote ambayo ni ya uadilifu.”—Mathayo 3:1-15, NW.
2 Baada ya Yohana kukubaliana naye kwa moyo wa kiasi halafu Yesu akaja juu kutoka majini, “mbingu zilifunuka, na akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa.” Zaidi ya hilo, “kulikuwako sauti kutoka katika mbingu iliyosema: ‘Huyu ndiye Mwanangu, mpendwa, ambaye mimi nimekubali.’ “(Mathayo 3:16, 17; Marko 1:11, NW) Lo, tamko rasmi lililoje! Sisi sote huona shangwe kufurahisha mtu fulani tunayestahi. (Matendo 6:3-6; 16:1, 2; Wafilipi 2:19-22; Mathayo 25:21) Basi, wazia jinsi wewe ungehisi ikiwa Mungu mwenye nguvu zote angetangaza, ‘Mimi nimekukubali wewe!’
3. Sisi tunapaswa kuhangaikia nini kuhusu kibali cha Mungu?
3 Je! leo inawezekana mtu awe mwenye kukubaliwa na Mungu? Mathalani, chukua mtu ambaye ‘hana tumaini, hana Mungu duniani,’ mwenye ‘kutengwa mbali na uzima wa Mungu.’ (Waefeso 2:12; 4:18, ZSB) Je! yeye anaweza kutoka kwenye hali hiyo aje kwenye ubarikiwa wa kukubaliwa na Yehova? Ikiwa ndivyo, jinsi gani? Acheni tuone.
Maneno Yake Yalimaanisha Nini?
4. (a) Ni nini maana ya neno la Kigiriki la ‘mwenye kukubaliwa’ katika tangazo la Mungu? (b) Kwa nini utumizi walo katika kisa hiki una upendezi wa pekee?
4 Kumbukumbu za maandishi ya Gospeli juu ya maneno ya Mungu “Nimekubali [Yesu]” zinatumia kitenzi cha Kigiriki eu·do·keʹo. (Mathayo 3:17; Marko 1:11; Luka 3:22) Kinamaanisha “kuwa mwenye kufurahika sana, kuchukua kitu kwa njia yenye kupendeleka, kupata upendezo katika,” na namna yake ya nomino ina maana ya “nia njema, ufurahio mwema, upendeleo, utakio, tamaa.” Eu·do·keʹo haihusu kibali cha kimungu tu. Mathalani, Wakristo katika Makedonia ‘walipendezwa’ kushirikiana kifedha pamoja na wengine. (Warumi 10:1; 15:26; 2 Wakorintho 5:8; 1 Wathesalonike 2:8; 3:1) Na bado, kibali ambacho Yesu alipokea kilionyeshwa na Mungu, si na wanadamu. Mtajo huo umetumiwa kwa kurejezea Yesu peke yake baada ya yeye kubatizwa. (Mathayo 17:5; 2 Petro 1:17) Kwa kupendeza, Luka 2:52, NW, inatumia neno tofauti—khaʹris—katika kunena juu ya Yesu akiwa kijana asiyebatizwa ambaye alipokea “upendeleo” kutoka kwa Mungu na wanadamu.
5. (a) Ni jinsi gani kulivyo na ithibati ya kwamba wanadamu wasiokamilika wanaweza kukubaliwa na Mungu? (b) Ni nani walio “watu wenye nia njema”?
5 Je! inawezekana pia wanadamu wasiokamilika kupata kibali cha Mungu? Kwa kufurahisha, jibu ni ndiyo. Yesu alipozaliwa, malaika walitangaza hivi: “Utukufu katika mahali pa juu kwa Mungu, na duniani amani miongoni mwa watu wenye nia njema [eu·do·kiʹas].” (Luka 2:14) Katika Kigiriki cha uhalisi, malaika walikuwa wanaimba juu ya baraka ambayo ingekuja kwa “watu wenye kufikiri kuzuri” au “watu ambao Mungu huwakubali.”a Profesa Hans Bietenhard anaandika hivi juu ya utumizi huo wa en an·throʹpois eu·do·kiʹas: “Kifungu hicho kinarejezea watu wenye raha njema ya Mungu . . . Kwa hiyo, hapa sisi hatushughuliki na nia njema ya watu . . . Tunashughulika na enzi kuu na nia yenye neema ya Mungu, ambayo hujichagulia yenyewe jamii ya watu wa kupata wokovu.” Hivyo, kama vile ambavyo Mashahidi wa Yehova wameeleza kwa muda mrefu, Luka 2:14 inaonyesha kwamba kupitia wakfu na ubatizo, inawezekana wanadamu wasiokamilika kuwa watu wa nia njema, watu wanaokubaliwa na Mungu!b
6. Ni nini ambacho bado tunahitaji kujifunza juu ya kibali cha Mungu?
6 Hata hivyo, huenda ikawa wewe unang’amua tofauti kubwa sana iliyopo kati ya kuwa ‘adui za Mungu ambao akili zao ziko juu ya kazi zilizo mbovu’ na kukubaliwa kuwa washirika wa Mungu wetu mwenye haki na hekima. (Wakolosai 1:21, NW; Zaburi 15:1-5) Kwa sababu hiyo, ingawa huenda wasiwasi ukakutoka usikiapo kwamba wanadamu wanaweza kuwa wenye kukubaliwa, huenda ukataka kujua yanayohusika. Tunaweza kujifunza mengi juu ya hilo kutokana na mishughuliko ya Mungu ya zamani.
Yeye Alikaribisha Watu
7. Kutoka 12:38 inatoa kionyeshi gani juu ya mwelekeo wa Mungu?
7 Kwa karne kadhaa kabla ya tangazo la Luka 2:14, Yehova alikaribisha watu waje na kumwabudu. Bila shaka, Mungu alikuwa akishughulika pamoja na taifa la Israeli peke yalo, lililokuwa limejiweka wakfu kwake. (Kutoka 19:5-8; 31:16, 17) Ingawa hivyo, kumbuka kwamba Israeli walipopiga miguu wakitoka kwenye utumwa wa Misri, ‘kundi kubwa la watu waliochangamana nao walikwea pamoja nao.’ (Kutoka 12:38) Sasa watu hao wasio Waisraeli ambao huenda wakawa walifanya mishughuliko pamoja na watu wa Mungu na kushuhudia yale mapigo juu ya Misri walichagua kwenda pamoja na Israeli. Inaelekea kuwa baadhi yao walikuja kuwa waongofu kamili.
8. Ni namna gani mbili za wageni waliokaa katika Israeli, na kwa nini kulikuwa na tofauti katika jinsi Waisraeli walivyoshughulika pamoja nao?
8 Agano la Sheria lilikubali hali ya watu wasio Waisraeli kuhusiana na Mungu na watu wake. Watu fulani wa kigeni walikuwa walowezi wenye kukaa tu katika bara la Israeli, ambamo ilikuwa lazima watii sheria za msingi, kama zile zilizokuwa dhidi ya kuua na zenye kutaka mwadhimisho wa Sabato. (Nehemia 13:16-21) Badala ya kuwakubali kwa moyo kabisa walowezi hao kuwa akina ndugu, Mwisraeli alitumia hadhari ya kiakili alipokuwa akinena au kushughulika pamoja nao, kwa maana walikuwa bado si sehemu ya taifa la Mungu. Mathalani, ingawa Mwisraeli hakuruhusiwa kununua na kula mzoga usiotolewa damu wa mnyama aliyejifia mwenyewe, watu hao wa kigeni wasiokuwa waongofu wangeweza kufanya hivyo. (Kumbukumbu 14:21; Ezekieli 4:14) Baada ya muda baadhi ya walowezi hao wa kigeni wangeweza kufuata mwendo wa wakaaji wengine wa kigeni waliokuja kuwa waongofu waliotahiriwa. Hapo tu ndipo walipotendewa kama akina ndugu katika ibada ya kweli, wakipasishwa wajibu wa kushika Sheria yote nzima. (Walawi 16:29; 17:10; 19:33, 34; 24:22) Ruthu, yule Mmoabi, na Naamani, yule mkoma Msiria, walikuwa watu wasio Waisraeli ambao Mungu aliwakubali.—Mathayo 1:5; Luka 4:27.
9. Ni jinsi gani Sulemani alivyothibitisha mwelekeo wa Mungu kuelekea watu wa kigeni?
9 Katika siku za Mfalme Sulemani, tunaona pia mwelekeo wa Mungu wa kukaribisha watu wasio Waisraeli. Sulemani alipokuwa akizindua hekalu, alisali hivi: “Hata na mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako . . . na kuomba kuielekea nyumba hii; basi, usikie huko mbinguni, . . . ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe kama watu wako Israeli.” (1 Wafalme 8:41-43) Ndiyo, Yehova alikaribisha sala za wageni wenye weupe wa moyo ambao walimtafuta. Labda hao pia wangejifunza sheria zake, wajitiishe kwenye kitendo cha tohara, na kuwa washiriki wanaokubaliwa wa watu wake wabarikiwa.
10. Wayahudi wangekuwa wameshughulika jinsi gani pamoja na towashi Mwethiopia, na kwa nini tohara ilimpa manufaa?
10 Mwanamume mmoja aliyefanya hivyo nyakati za baadaye alikuwa mweka-hazina wa Malkia Kandake katika Ethiopia ya mbali. Inaelekea kuwa, aliposikia kwanza habari za Wayahudi na ibada yao, mtindo wake wa maisha au njia zake za kidini hazikukubalika kwa Yehova. Kwa hiyo Wayahudi wangalilazimika kuonyesha kipimo fulani cha uvumilio wakati mwanamume huyu wa kigeni alipokuwa miongoni mwao akijifunza Sheria ili ajue matakwa ya Mungu. Kuna ithibati ya kwamba alifanya maendeleo na mabadiliko yaliyohitajiwa ili kustahili tohara. Matendo 8:27 inatuambia kwamba “alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu.” (Kutoka 12:48, 49) Hiyo ingeonyesha kwamba wakati huo alikuwa mwongofu kamili. Hivyo alikuwa katika msimamo wa kukubali Mesiya na kuwa mwanafunzi wake aliyebatizwa, kwa njia hiyo akijipatanisha na mapenzi ya Mungu yenye kupiga hatua za maendeleo.
Watu Wasioitikadi na Kundi la Kikristo
11, 12. (a) Ni badiliko gani zaidi lililotukia wakati Mwethiopia huyo alipobatizwa? (b) Ni jinsi gani hilo lilivyolingana na Wafilipi 2:12, 13?
11 Yesu aliambia wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Mwongofu Mwethiopia aliyetajwa sasa hivi alikuwa tayari ana maarifa juu ya Yehova na juu ya roho takatifu. Kwa hiyo mara Filipo alipokwisha kumsaidia aelewe Yesu na kumkubali kuwa ndiye Mwana wa Mungu wa kimesiya, angeweza kubatizwa. Hivyo angekuwa mshiriki mkubaliwa wa watu wa Yehova waliokuwa wanafuata Kristo. Kiasili, yeye angekuwa na wajibu kwa Mungu, kutakwa ‘ashike mambo yote yaliyoamriwa’ kwa Wakristo. Lakini kupasishwa wajibu huo kulikuja pamoja na tazamio zuri sana: wokovu!
12 Baadaye, Paulo aliandika kwamba Wakristo wote walihitaji ‘kuendelea kujifanyizia wokovu wao wenyewe kwa hofu na kutetemeka.’ Hata hivyo, iliwezekana kufanya hivyo, “kwa maana Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya [uradhi, UV] raha njema [eu·do·kiʹas] yake, anatenda ndani ya nyinyi ili nyinyi mnie na kutenda.”—Wafilipi 2:12, 13, NW.
13. Wakristo wangekuwa wameshughulika jinsi gani pamoja na wale wasiofanya haraka ya kubatizwa kama ya yule towashi Mwethiopia
13 Si wote waliokuja kuonana na Wakristo wa kweli waliokuwa tayari na wenye ustahili mwingi kama Mwethiopia yule hata wasonge haraka kwenye ubatizo. Baadhi yao, wakiwa si Wayahudi wala waongofu, walikuwa na maarifa kidogo au hawakuwa na yoyote juu ya Yehova na njia zake; wala maadili yao hayakuongozwa na viwango vyake. Wao wangeshughulikiwa jinsi gani? Wakristo walipaswa kufuata kielelezo cha Yesu. Kwa uhakika yeye hakutia moyo kufanya au hata kuachilia dhambi. (Yohana 5:14) Na bado, yeye alivumilia watenda dhambi waliovutiwa kuja kwake na waliotamani kupatanisha njia zao pamoja na zile za Mungu.—Luka 15:1-7.
14, 15. Zaidi ya Wakristo waliopakwa mafuta, ni namna gani za watu waliohudhuria mikutano katika Korintho, na huenda ikawa walitofautiana jinsi gani kuhusu maendeleo ya kiroho?
14 Kwamba Wakristo walishughulika kwa kuvumilia wale waliokuwa wakijifunza juu ya Mungu inaonekana wazi kutokana na maelezo ya Paulo juu ya mikutano katika Korintho. Katika kuzungumzia utumizi wa zawadi za kimuujiza za roho ambazo hapo kwanza zilikuwa alama ya kwamba Ukristo ulikuwa na baraka ya Mungu, Paulo alitaja “waaminio” na “wasioamini.” (1 Wakorintho 14:22) “Waaminio” (waitikadi, NW) walikuwa wale waliokubali Kristo na kubatizwa. (Matendo 8:13; 16:31-34) “Wakorintho wengi waliposikia, waliamini, wakabatizwa.”—Matendo 18:8.
15 Kulingana na 1 Wakorintho 14:24, ‘wasioamini au watu wajinga [watu wa kikawaida, NW]’ walikuja mikutanoni pia katika Korintho na kukaribishwa humo.c Inaelekea kuwa walitofautiana katika maendeleo yao ya kujifunza na kutumia Neno la Mungu. Huenda ikawa baadhi yao walikuwa wangali wakitenda dhambi. Huenda ikawa wengine walikuwa wamepata kipimo fulani cha imani, wakawa tayari wamefanya mabadiliko fulani katika maisha zao, na, hata kabla ya ubatizo, wakawa wameanza kuambia wengine mambo waliyokuwa wamejifunza.
16. Ni jinsi gani watu hao wangeweza kupata manufaa kwa kuwa miongoni mwa Wakristo kwenye mikutano ya kundi?
16 Bila shaka, hakuna wowote wa watu hao wasiobatizwa waliokuwa “katika Bwana.” (1 Wakorintho 7:39) Ikiwa wakati wao uliopita ulihusisha ndani kasoro nzito za kiadili na kiroho, inaeleweka kuwa ingeweza kuwachukua muda ili wajipatanishe na viwango vya Mungu. Kwa wakati uliopo, maadamu wao hawakujaribu kupindua imani na usafi wa kundi wakiwa na nia ya madhara, wao walikaribishwa. Mambo waliyoona na kusikia mikutanoni yangeweza ‘kuwakaripia’ wakati ‘siri za mioyo yao zilipokuwa zikidhihirika.’—1 Wakorintho 14:23-25, NW; 2 Wakorintho 6:14.
Kubaki Katika Kukubaliwa na Mungu kwa Ajili ya Wokovu
17. Luka 2:14 ilikuwa na utimizo gani katika karne ya kwanza?
17 Kupitia kuhubiri peupe kwa Wakristo waliobatizwa katika karne ya kwanza, maelfu walisikia habari njema. Wao walitia imani katika mambo waliyosikia, wakatubu juu ya mwendo wao wa zamani, wakabatizwa, wakifanya “tangazo la peupe la wokovu.” (Warumi 10:10-15, NW; Matendo 2:41-44; 5:14; Wakolosai 1:23) Hakukuwa na shaka kwamba wabatizwa wa huko nyuma walikuwa na kibali cha Yehova, kwa maana yeye aliwapaka mafuta kwa roho takatifu, akiwafanya wawe wana wa kiroho wa kimalezi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi [eu·do·kiʹan] wa mapenzi yake.” (Waefeso 1:5) Hivyo, katika muda wa karne hiyo kile ambacho malaika walitabiri kwenye uzaliwa wa Yesu kilianza kuthibitika kuwa kweli: “Amani miongoni mwa watu wenye nia njema [au, watu walio na kibali cha Mungu].”—Luka 2:14, NW.
18. Kwa nini Wakristo wapakwa mafuta hawangeweza kuchukua hivi hivi tu msimamo wao wenye ukubali pamoja na Mungu?
18 Ili kudumisha amani hiyo, hao “watu wenye nia njema” walihitajiwa kabisa ‘waendelee kujifanyizia wokovu wao wenyewe kwa hofu na kutetemeka.’ (Wafilipi 2:12, NW) Hiyo haikuwa rahisi, kwa maana walikuwa wangali wanadamu wasiokamilika. Wangeelekeana usoni na vishawishi na mambo yenye kuwabana wafanye makosa. Kama wao wangejiachilia kwenye kosa, wangepoteza kibali cha Mungu. Hivyo, kwa upendo Yehova alipanga kuwe na wachungaji wa kiroho ambao wangesaidia makundi na kuyahami pia.—1 Petro 5:2, 3.
19, 20. Mungu alifanya maandalizi gani ili Wakristo waliobatizwa waweze kuendelea kuwa watumishi wake wakubaliwa?
19 Wazee hao wa kundi wangethamini moyoni ushauri wa Paulo: “Mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho [ambao mna sifa za kufaa kiroho, NW] mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe.” (Wagalatia 6:1) Kama tuwezavyo kuelewa, mtu aliyeichukua hatua ya maana ya ubatizo angepasishwa wajibu mkubwa zaidi, hata kama vile ilivyokuwa kwa mgeni aliyekuja kuwa mwongofu mtahiriwa katika Israeli. Hata hivyo, kama Mkristo aliyebatizwa alikosa, angeweza kupata msaada wenye upendo ndani ya kundi.
20 Kikundi cha wazee katika kundi kingeweza kumtolea msaada mmoja aliyetumbukia katika kosa zito. Yuda aliandika hivi: “Wahurumieni wengine walio na shaka, na wengine waokoeni kwa kuwanyakua katika moto; na wengine wahurumieni kwa hofu, mkilichukia hata vazi lililotiwa uchafu na mwili.” (Yuda 22, 23) Mshiriki wa kundi aliyebatizwa ambaye alisaidiwa hivyo angeweza kuendelea kuona shangwe juu ya kibali cha Yehova na amani ambayo malaika walikuwa wameinena kwenye uzaliwa wa Yesu.
21, 22. Kungetokea nini kama mtu fulani angekuja kuwa mtenda dhambi asiyetubu, na washiriki washikamanifu wa kundi wangetenda jinsi gani?
21 Kulikuwako visa ambapo mkosaji hakuonyesha toba, ingawa si kwa kawaida. Hapo wazee wangelazimika kumwondosha nje ili kuhami lile kundi safi lisichafuliwe. Jambo hilo lilitokea Korintho kwa mwanamume mmoja aliyebatizwa ambaye alizidi kuwa katika uhusiano usio wa kiadili. Paulo alishauri kundi hivi: “Acheni kabisa kuchangamana katika uandamani pamoja na waasherati, si kumaanisha kabisa kabisa pamoja na waasherati wa ulimwengu huu au watu wenye pupa na wanyakuzi au waabudu sanamu. Ama sivyo, nyinyi kwa kweli mngelazimika kutoka ndani ya ulimwengu. Lakini sasa mimi ninaandikia nyinyi mwache kabisa kuchangamana katika ushirika pamoja na yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyakuzi, hata msiwe mnakula pamoja na mtu huyo.”—1 Wakorintho 5:9-11, NW.
22 Kwa kuwa mwanamume huyo Mkorintho alikuwa amechukua hatua ile ya maana ya ubatizo, akawa mwenye kukubaliwa na Mungu na mshiriki wa kundi, kuondoshwa kwake nje kulikuwa jambo zito. Paulo alionyesha kwamba Wakristo hawakupaswa kuendeleza uandamani pamoja naye, kwa maana yeye alikuwa amekataa msimamo wake wenye ukubali pamoja na Mungu. (Linganisha 2 Yohana 10, 11.) Petro aliandika hivi juu ya hao wenye kuondoshwa nje: “Ingalikuwa afadhali kwao kama wasingalijua kamwe njia hiyo ya uadilifu, kuliko kuijua na kisha kuiacha na kupoteza amri takatifu waliyopokea. Ipo mithali isemayo: ‘Mbwa huyarudia matapishi yake mwenyewe.’”—2 Petro 2:21, 22, HNWW.
23. Katika karne ya kwanza, ni nini iliyokuwa hali ya ujumla miongoni mwa Wakristo kwa habari ya kubaki wakiwa na kibali cha Mungu?
23 Ni wazi Yehova hangeweza tena kuwa na rai ya kwamba watu hao walikuwa na kibali, kwa maana wao walikuwa wameondoshwa nje kwa kuwa wakosaji wasioonyesha toba. (Waebrania 10:38; linganisha 1 Wakorintho 10:5.) Ithibati inaonyesha ni wachache tu waliotengwa na ushirika. Walio wengi ambao walipata “fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu” na ‘wakachaguliwa kuwa wana wa kimalezi kulingana na raha njema ya mapenzi yake’ walibaki wakiwa waaminifu.—Waefeso 1:2, 5, 8-10.
24. Ni upande gani wa habari hii unaostahili kuangaliwa zaidi?
24 Ndivyo ilivyo kwa msingi katika wakati wetu, pia. Ingawa hivyo, acheni tufikirie jinsi ‘wasioitikadi au watu wa kikawaida’ wanavyoweza kusaidiwa wakubaliwe na Mungu leo na mambo yanayoweza kufanywa kuwasaidia wakikosa wanapokuwa mwendoni. Makala inayofuata itashughulika na mambo hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Linganisha “watu ambao yeye awakubali,” New Testament, na George Swann; “watu ambao yeye anafurahia,” The Revised Standard Version.
b Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Oktoba 15, 1964, kurasa 629-33.
c “Yule ἄπιστος (apistos, ‘asiyeitikadi’) na ιδιώτης (idiotes, ‘mmoja asiye na uelewevu,’ ‘muuliziaji-uliziaji’) wote wawili wamo katika tabaka ya wasioitikadi kwa kutofautishwa na waokolewa wa kanisa la Kikristo.”—The Expositor’s Bible Commentary, Buku 10, uku. 275.
Wewe Unakumbuka?
◻ Kulingana na Maandiko, ni tangu wakati gani na kwa njia gani wanadamu wanaweza kukubaliwa na Mungu?
◻ Rai ya Mungu ilikuwa nini juu ya watu wa kigeni miongoni mwa watu wake, lakini kwa nini Waisraeli walihitaji kusawazisha hadhari pamoja na uvumilio?
◻ Sisi tunaweza kukata shauri gani kutokana na uhakika wa kwamba ‘wasioitikadi’ walikuja kwenye mikutano ya Kikristo katika Korintho?
◻ Ni jinsi gani Mungu amefanya uandalizi ili kusaidia Wakristo waliobatizwa wabaki wakiwa watumishi wake waliokubaliwa?