Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! zile habari zinazohusu kukubaliwa na Mungu zinamaanisha kwamba Wakristo wanaweza kunena na mtu ambaye wakati mmoja alionwa kuwa “mshirika anayekubaliwa” lakini baadaye ikampasa kuepukwa kwa sababu ya ukosaji?
Ndiyo, zinamaanisha hivyo. Mnara wa Mlinzi wa Novemba 15,1988 ulionyesha kwa nini inafaa Kimaandiko turekebishe maoni yetu juu ya mtu asiyebatizwa ambaye hushiriki katika huduma ya peupe pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hapo kwanza, mtu wa jinsi hiyo aliitwa “mshirika anayekubaliwa.” Ikiwa baadaye mtu huyo alivunja sheria za Mungu bila kutubu, kundi lilifanywa chonjo kwa kujulishwa jambo hilo, nao wangeepuka ushirika au maongezi pamoja naye.
Kama vile habari za hivi majuzi zilivyoonyesha, Biblia inataka kwamba hatua hiyo ya nidhamu ichukuliwe katika kisa cha watu waliobatizwa ambao ni wakosaji wasiotubu. (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Hata hivyo, wajibu wa kutoa hesabu kwa mtu asiyebatizwa anayefuatia ukosaji si sawa na ule wa mmoja aliyebatizwa. (Luka 12:48) Yeye hajabatizwa na hivyo hajawa mwenye kukubaliwa machoni pa Mungu, kwa hiyo kutenga na ushirika hakufai katika kisa chake. Kwa msingi, sasa yeye ni mlimwengu na anaweza kushughulikiwa kulingana na hivyo alivyo.
Namna gani, basi, juu ya mmoja aliyekuwa akiitwa “mshirika anayekubaliwa’’ lakini asiyestahili tena huduma ya peupe kwa sababu ya mwendo wake wenye kosa? Kwa kuwa hajatengwa na ushirika anapaswa kutendewa kuwa mlimwengu kama vile alivyo.a Bila shaka, Mnara wa Mlinzi wa Novemba 15 ulishauri katika ukurasa 19 kwamba ni lazima hadhari inayofaa izoewe na Wakristo washikamanifu. Wao wanang’amua kwamba huenda mtu asiyebatizwa akawa hasa alishiriki katika ukosaji ajapokuwa na maarifa juu ya matakwa ya Mungu. Lazima Wakristo wakomavu wawe waangalifu juu ya kufanya starehe za kirafiki pamoja na mtu wa jinsi hiyo. Maswali yakitokea juu ya kadiri ya ushirikiano ambao unaweza kufanywa pamoja naye, mengi yayo yanaweza kutatuliwa kwa kufuata mashauri ya kimungu. Tunaweza kufikiria mashauri kama lile linalopatikana kwenye 1 Wakorintho 15:33 na Mithali 13:20 na kujiuliza hivi: ‘Ni ushirika gani ambao ingefaa niwe nao pamoja na mlimwengu asiyeishi kwa kufuata viwango vya Kikristo?’ Wazee wakiona kwamba mlimwengu wa namna hiyo anakuwa tisho la namna yoyote, wanaweza kuwaonya faraghani wale walio kundini wanaoonekana ni kama wanatiwa hatarini.
Baada ya muda fulani, huenda mtu asiyebatizwa ambaye hapo kwanza alikuwa “mshirika anayekubaliwa” akaonyesha ushuhuda wa kiasi cha kutosha juu ya kutubu, na huenda akatamani kuwa tena na funzo la Biblia. (Matendo 26:20) Anaweza kunena na wazee wa kundi ambako sasa yeye anahudhuria, nao watampangia kuwa na funzo la Biblia, ikionekana kuwa inafaa kufanya hivyo. Jambo hilo litatumika pia ikiwa wakati ujao mtu anaondolewa ustahili wa kuwa mhubiri asiyebatizwa na baadaye anaonyesha kutubu. Kwa kawaida, ni sharti yeye anene na wazee wale wawili walioshughulikia ukosaji wake au wale wengine wawili ambao baraza la wazee liliwachagua ili warudie kuangalia jambo hilo ikiwa aliomba liangaliwe.
Kwa kufaa, Mnara wa Mlinzi ulieleza kwamba mambo ni tofauti kidogo katika kisa cha wazazi wanaotunza watoto wadogo nyumbani—wale ambao kulingana na sheria wangali ni watoto wadogo wanaowategemea ili wawaandalie riziki ya kimwili. (Waefeso 6:1-4) Maandiko yanaweka juu ya wazazi wajibu wa kuagiza na kuongoza watoto wao. Kwa hiyo wazazi (au mzazi anayeitikadi) wanaweza kuchagua kuongoza funzo la Biblia la faraghani pamoja na mtoto mwenye kukosa au kumhusisha katika programu ya jamaa ya funzo la Biblia na zungumzo.
Ingawa habari hizo za hivi majuzi za Mnara wa Mlinzi zinataka kuwe na rekebisho katika kufikiri kwetu na mishughuliko yetu, hilo linafanywa kwa kupatana na Maandiko yaliyo na manufaa “kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”—2 Timotheo 3:16, 17, NW.
◼ Kulingana na Tito 1:6, ni lazima watoto wote wa mwanamume wawe wamebatizwa ndipo yeye astahili kuwa mzee katika kundi?
Katika sura ya kwanza ya Tito, mtume Paulo alitoa mpangilio wa sifa za wanaume wanaotumikia wakiwa wazee wa kundi. Moja ilikuwa kwamba ndugu awe “asiye na shtaka,. . . mwenye watoto wanaoitikadi.”
Hiyo haingeweza kumaanisha kwamba ni lazima watoto wote wa mzee wawe wamebatizwa, kwa maana huenda baadhi yao wakawa ni vitoto vichanga. Kwa hiyo kwa fikiria yenye kiasi ni lazima Tito 1:6, NW, iwe inamaanisha kwamba watoto wadogo wa mwanamume wanapaswa wawe wamebatizwa ama wawe wanajifunza ukweli wa Biblia, wawe wanaukubali na kuutumia na kusonga kuelekea ubatizo, huku wakiwa chini ya ustahiki wa kijamaa. (1 Wakorintho 7:14) Mzee anapaswa awe akijaribu kufanya wanafunzi kutoka kwa watoto wake, nao wakiwa “hawakushtakiwa kuwa na ufisadi wala utundu.”b
Tunaweza kuthamini jambo hilo vizuri zaidi kwa kuangalia jinsi Biblia inavyotumia neno “mwitikadi.—Bila shaka, huenda mtu akawa ana imani, au aitikadi, katika mambo mengi. (Matendo 26:27, 28; 2 Wathesalonike 2:3, 11; Yakobo 2:19) Lakini tunapata ‘kuitikadi’ kukihusianishwa sana-sana na kuukubali Ukristo na kubatizwa. (Matendo 8:13; 18:8; linganisha 19:1-5.) Ubatizo hasa ndio huonyesha kwamba mtu ni mwitikadi. Matendo 2:41,44; 4:4,32.
Huenda watoto fulani wa mzee wakawa bado hawajawa tayari kwa ubatizo, kimwili, kihisia-moyo au kiroho. Hata hivyo, Tito 1:6, NW, inaeleza juu yao kuwa ni “watoto wanaoitikadi” ikiwa wanafanya maendeleo kuelekea ubatizo, kupatana na umri na hali yao.
[Maelezo ya Chini]
a Ikiwa mtu fulani aliye katika hali hiyo hana habari juu ya maoni haya yaliyorekebishwa, ingekuwa fadhili kumrejeza kwenye makala hizo za Mnara wa Mlinzi.
b Ona pia Mnara wa Mlinzi wa Agosti 15, 1972, uku. 384.