Maisha na Huduma ya Yesu
Daraka la Uanafunzi
BAADA ya kuondoka kwenye nyumba ya Farisayo mashuhuri, ambaye inaonekana wazi ni mshiriki wa Sanhedrini, Yesu anasonga mbele kuelekea Yerusalemu. Umati mkubwa wa watu unamfuata. Lakini makusudio yao ni nini? Ni nini hasa kinachohusika katika kuwa mfuasi wake wa kweli?
Wanapokuwa wakisafiri, Yesu anageukia umati wa watu hao na labda anawashtua anaposema: “Ikiwa mmoja yeyote ananijia mimi na hachukii baba yake na mama na mke na watoto na akina ndugu na dada, ndiyo, na hata nafsi yake mwenyewe, yeye hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”
Yesu anamaanisha nini? Hamaanishi kwamba wafuasi wake wanapaswa kuwachukia kihalisi watu wa ukoo wao. Bali, ni lazima wao wawachukie katika maana ya kuwapenda kwa kadiri ndogo kuliko vile wanavyompenda yeye. Yakobo baba mtangulizi wa Yesu anasemwa kuwa ‘alichukia’ Lea na akapenda Raheli, jambo ambalo lilimaanisha kwamba Lea alipendwa kwa kadiri ndogo kuliko Raheli dada yake.
Fikiria, pia, kwamba Yesu alisema mwanafunzi anapaswa kuchukia “hata nafsi yake mwenyewe,” au uhai. Hapo tena, analomaanisha Yesu ni kwamba ni lazima mwanafunzi wa kweli ampende Yeye hata kuliko vile anavyopenda uhai wake mwenyewe. Hivyo Yesu anakazia kwamba kuwa mwanafunzi wake ni daraka zito. Si jambo la kufuatwa bila ufikirio wa uangalifu.
Magumu na mnyanyaso yanahusika katika kuwa mwanafunzi wa Yesu, kama vile yeye anavyoendelea kuonyesha: “Awaye yote asiyebeba mti wa mateso wake na kuja baada ya mimi hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” Hivyo, ni lazima mwanafunzi wa kweli awe na nia ya kupita chini ya himila ile ile ya kusutwa ambayo Yesu alivumilia, hata kutia ndani, ikihitajiwa kabisa, kufa mikononi mwa adui za Mungu, jambo ambalo muda si muda Yesu atalifanya.
Kwa hiyo, kuwa mwanafunzi wa Kristo ni jambo ambalo umati wa watu wanaomfuata yeye wanahitaji kulichanganua kwa uangalifu. Yesu anakazia uhakika huo kwa kutumia kielezi. “Kwa kielelezo,” yeye anasema, “ni nani kati ya nyinyi ambaye anataka kujenga mnara asiyeketi kwanza na kuhesabu-hesabu gharama, aone kama yeye ana vya kutosha kuukamilisha? Ama sivyo, huenda yeye akalaza msingi wao lakini asiweze kuumaliza, na watazamaji wote huenda wakaanza kumdhihaki, wakisema, ‘Mtu huyu alianza kujenga lakini hakuweza kumaliza.’”
Kwa hiyo Yesu anaupa umati wa watu hao wenye kumfuata kielezi cha kwamba kabla ya kuwa wanafunzi wake, inawapasa wawe wameamua imara kwamba wanaweza kutimiza yanayohusika, sawa na vile mtu anayetaka kujenga mnara huhakikisha kabla ya kuanza kwamba ana asilimali ya kuukamilisha. Akiandaa kielezi kingine, Yesu anaendelea kusema:
“Au ni mfalme gani, akiwa anapiga miguu kwenda kukutana na mfalme mwingine katika vita, asiyeketi kwanza na kufanya shauri kama yeye akiwa pamoja na askari elfu kumi anaweza kukabiliana na yule ambaye anakuja dhidi yake akiwa pamoja na elfu ishirini? Ikiwa, kwa uhakika, yeye hawezi kufanya hivyo, basi huyo anapokuwa angali kule mbali yeye hupeleka nje baraza la mabalozi na kusihi akiomba amani.”
Ndipo Yesu anapokazia wazo la vielezi vyake, akisema: “Hivyo, nyinyi mwaweza kuwa na uhakika kwamba, hakuna mmoja kati ya nyinyi ambaye hasemi nenda-salama kwa mali zake zote anaweza kuwa mwanafunzi wangu.” Jambo hilo ndilo umati wa watu wenye kumfuata, na, ndiyo, kila mtu mwingine yeyote anayejifunza habari za Kristo, lazima awe na nia ya kulifanya. Lazima wao wawe tayari kudhabihu kila kitu walicho nacho—mali zao zote, kutia na uhai wenyewe—kama wangetaka kuwa wanafunzi wake. Je! wewe una nia ya kufanya jambo hilo?
“Chumvi, kwa uhakika, ni bora,” Yesu anaendelea kusema. Katika Mahubiri ya Mlimani aliyoyatoa, yeye alisema kwamba wanafunzi wake ndio “chumvi ya dunia,” kumaanisha kwamba wao wana uvutano wenye hifadhi juu ya watu, sawa na vile chumvi halisi ilivyo kihifadhi. “Lakini hata ikiwa chumvi inapoteza imara yayo, itakolezwa kwa kitu gani? Haifai wala kwa ajili ya udongo wala kwa ajili ya mbolea,” Yesu anamalizia. “Watu huitupa nje. Acheni yule aliye na masikio ya kusikiliza, asikilize.”
Kwa hiyo Yesu anaonyesha kwamba ni lazima hata wale ambao wamekuwa wanafunzi wake kwa muda fulani wasidhoofike katika hali yao ya kupiga moyo konde kuendelea mbele. Wakifanya hivyo, watakuwa bure tu, wawe kitu cha kudhihakiwa na ulimwengu huu na wasiofaa mbele za Mungu, kwa uhakika, wawe suto juu ya Mungu. Kwa sababu hiyo, wao watatupwa nje kama chumvi isiyo na imara, iliyochafuliwa. Luka 14:25-35; Mwanzo 29:30-33; Mathayo 5:13, NW.
◆ Ni nini maana ya mtu ‘kuchukia’ watu wa ukoo wake na yeye mwenyewe?
◆ Yesu anatoa vielezi gani viwili, navyo vinamaanisha nini?
◆ Ni nini wazo la maelezo ya Yesu ya kumalizia kuhusu chumvi?