Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 10/15 kur. 9-14
  • Ubatizo—Wonyesho wa Imani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ubatizo—Wonyesho wa Imani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Imani Inahitajiwa
  • Mwendo wa Maisha Unaohitaji Imani
  • Maana ya Ubatizo Wako
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Jinsi Ubatizo Unavyoweza Kutuokoa Sisi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Ubatizo—Takwa la Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • “Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 10/15 kur. 9-14

Ubatizo​—Wonyesho wa Imani

“Kwa moyo mtu huamini apate haki, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la waziwazi la wokovu.”​—Kum. 10:10, NW.

1. Kulingana na Mathayo 28:19 NW, Mtu anaonyeshaje kwamba amekuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo?

BWANA Yesu Kristo ndiye aliyetuwekea kielelezo cha kubatizwa. Wote wanaotaka kuwa wanafunzi wake wanapaswa kuzamishwa hivyo. Jambo hilo laonekana wazi katika amri aliyotoa Mwana wa Mungu akiwapa wafuasi wake baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu. Twasoma hivi: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.”​— Mt. 28:19, NW.

2. (a) Maana ya ubatizo wa maji ni nini? (b) Ili ubatizo uwe na maana ya kweli, ni jambo gani linalohitajiwa kwa mtu?

2 Ubatizo wa maji unafananisha nini? Unamaanisha kwamba inajulikana mbele ya watu kwamba mtu amejikana na kujiweka wakf kabisa kwa Yehova Mungu kama mwanafunzi wa Yesu Kristo. Ili tendo hilo liwe la maana machoni pa Baba yetu wa kimbinguni, lapaswa kufanywa kwa hiari (kwa kupenda) na kwa kujitoa kabisa. Tendo la kubatizwa si ndilo peke yake lililo la lazima ili kupata wokovu, bali pia kila kitu kinachohusiana na mpango wa ubatizo. Ni lazima mtu atubu dhambi zake, aongolewe, au kugeuka kabisa kutoka kwa mwendo mbaya, kukana kabisa kuwa yeye hana uenyeji juu yake mwenyewe kwa kujiweka wakf kabisa kwa Yehova Mungu, na kuwa mtumishi wa Aliye Juu Zaidi na Mwanawe. (Mt. 16:24; Matendo 2:38; 3:19; 1 The. 1:9, 10) Kwa kupatana na Warumi 10:9, anayetaka kubatizwa, kabla ya kuzamishwa majini, anatazamiwa akubali waziwazi kuwa anayafahamu vizuri mambo hayo. Kifungu hicho cha maneno ya Maandiko chasema hivi: “Kwa maana ukitangaza waziwazi ‘neno hilo, kwa kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kuamini moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kwa wafu, utaokolewa.” (NW)

3. Maneno ya 1 Petro 3:21, NW, yanathibitisha jambo gani kuhusiana na ubatizo?

3 Maneno ya 1 Petro 3:21 (NW) yanathibitisha kwamba mpango wote wa ubatizo, kutia ndani wonyesho huo wa imani, ni wa lazima ili kupata wokovu. Mtume huyo aliandika hivi: “Lile linalolingana na hili pia linaokoa ninyi sasa, yaani, ubatizo, (si kuondolewa kwa uchafu wa mwili, bali ombi linalofanywa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema,) kupitia kwa ufufuo wa Yesu Kristo.”

4. Usemi “kupitia kwa ufufuo wa Yesu Kristo” una maana gani?

4 Kwa wazi, tendo la kuzamishwa peke yake si ndilo linalookoa. Ingawa maji yanaweza kusafisha uchafu, wokovu hautokani na “kuondolewa kwa uchafu wa mwili” kwa kujisafisha kidini nje-nje. Petro alionyesha kwamba wokovu unapatikana “kupitia kwa ufufuo wa Yesu Kristo.” Hiyo yamaanisha kwamba yule anayebatizwa anapaswa kuamini kwamba wokovu unapatikana kwa sababu tu Mwana wa Mungu alikufa mauti ya kutoa dhabihu na kisha akafufuliwa katika siku ya tatu. Vilevile ni jambo la lazima amkubali Yesu kuwa Bwana mwenye mamlaka kamili ya kuhukumu walio hai na waliokufa, kwa kuwa Petro aliendelea kusema hivi: “Yeye yu katika mkono wa Mungu wa kuume, kwa kuwa alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na uwezo vyote vilitiishwa chini yake.”​—1 Pet. 3:22, NW.

5. Mtu anapataje kuwa na “dhamiri njema”?

5 Kisha, pia, Petro alishirikisha “ombi linalofanywa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema” na ubatizo. Ili kupata dhamiri njema, wote wanaozamishwa wanapaswa kutubu dhambi zao, wageuke kuacha mwendo wao mbaya na kujiweka wakf kabisa kwa Mungu kupitia kwa Kristo. Ubatizo ni wonyesho wa waziwazi wa kujiweka wakf kulikoongozwa na moyo ambako sasa kunafanywa na mtu na wonyesho wa imani aliofanya kwa kinywa chake. Baada ya kufanya yote ambayo Yehova Mungu anataka, mwanafunzi huyo aliyebatizwa anapata dhamiri njema. Maadamu anadumisha hiyo dhamiri njema yu katika hali ya wokovu. Hukumu ya kulaani ya kimungu haitapitishwa juu yake.

6. (a) Mpango wa ubatizo unalingana na jambo gani? (b) Imani inahusikaje?

6 Walakini mtume huyo alimaanisha nini aliposema, “lile linalolingana na hili”? Kulingana na mstari unaotangulia, nafsi nane za kibinadamu, kutia ndani Noa, ‘zilichukuliwa salama katika maji ya gharika’ (1 Pet. 3:20, NW) Maji yale yale ambayo yaliwaharibu wale waliokuwa nje ya safina, yaliokoa Noa na washiriki saba wa jamaa yake kutokana na kizazi kiovu. Hata hivyo, pasipo imani, Noa asingeweza kupata wokovu huo mkuu. Waebrania 11:7, HNWW, latuambia hivi: “Kwa imani Noa alionywa na Mungu juu ya mambo ya baadaye ambayo hakuweza kuyaona bado [yaani, hakukuwa vionyesho vyenye kuonekana kuhusiana na kuja kwa gharika ya duniani pote na kuharibiwa kwa uhai wa kibinadamu na wa wanyama]. Alimtii Mungu akajenga ile safina ambamo aliokolewa yeye pamoja na jamaa yake. Kutokana na [imani hiyo] ulimwengu ulihukumiwa, naye Noa akapokea uadilifu unaotokana na imani.” Kama vile tu Noa alivyohitaji imani ili aijenge safina, wote wanaokuwa wanafunzi waliobatizwa wa Yesu Kristo wanapaswa kuwa na imani waweze kustahimili mikazo itakayoletwa juu yao na ulimwengu usio na imani na mungu wake.​—Yohana 12:31; 2 Kor. 4:4.

Sababu Imani Inahitajiwa

7. Katika Luka 14:26-33, Yesu Kristo alitoa shauri gani, na sababu gani?

7 Wote wanaokuwa wanafunzi wa Yesu Kristo waliojiweka wakf na kubatizwa wanaweza kutazamia magumu. Ndiyo sababu Mwana wa Mungu alitoa shauri lifuatalo:

“Kama mutu akija kwangu, asipochukia baba yake, na mama, na muke, na watoto, na ndugu zake, waume na wake, hata uzima wake pia, hawezi kuwa mwanafunzi wangu. Na mutu ye yote asiyechukua [mti wake wa mateso], na kunifuata, hawezi kuwa mwanafunzi wangu. Maana ni nani kwenu, akitaka kujenga munara, asiyeketi kwanza na kuhesabu bei kama ana vitu vya kumaliza kazi? Ao ikiwa amekwisha kuweka misingi, hawezi kumaliza, na watu wote wanaoangalia, wanaanza kumuzihaki, wakisema: Mutu huyu alianza kujenga, lakini hakuweza kumaliza. Ao mufalme gani, akikwenda kupigana na mufalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana naye anayekuja juu yake na watu elfu makumi mbili? Kama sivyo, atatuma wajumbe kuomba salama, yule mufalme akiwa angali mbali. Vivyo, kila mumoja wenu, asipoacha vitu vyake vyote, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”—Luka 14:26-33, ZSB.

Kwa kupatana na maneno hayo, wote wanaobatizwa wanahitaji kutangulia kufikiria kwa akili timamu mambo yanayohusika.

8. Maoni yetu juu ya watu wa ukoo yanapaswa kuwa nini, na sababu gani?

8 Bila shaka, Yesu hakuwa akisema kwamba wanafunzi wake walipaswa kuchukia watu wao wa ukoo. Kwani, katika Mahubiri ya Mlimani, aliwaonya kwa upole kwamba ‘tuwapende adui zetu na wenye kutuudhi.’ (Mt. 5:44) Basi, kwa kweli, twapaswa kuwaonyesha upendo mwingi zaidi watu wetu wa ukoo wasioamini, tukiwa na shauku na wenye nia kufanya yo yote yawezekanayo katika kuwasaidia wapate uzima wa milele. (Linganisha Warumi 9:1-3) Lakini mtu anayekuwa mwanafunzi aliyebatizwa anapaswa ‘kuwachukia’ katika maana ya kuwapenda kidogo zaidi kuliko anavyompenda Yesu Kristo. Sababu gani jambo hilo ni la lazima? Huenda watu wa ukoo wake wasipendezwe na mwendo wake. Huenda wakamwonyesha kwamba akibatizwa, watamkana. Kwa hiyo inataka imani kusadiki kwamba kujiweka wakf kwa Yehova na kubatizwa hakutamletea hasara bali faida.

9. Wanafunzi wa Yesu Kristo walio wakf na kubatizwa wanafurahia faida gani?

9 Mtu anapataje faida kwa kujiweka wakf na kubatizwa kama mwanafunzi wa Yesu Kristo? Kuna uradhi wa kufahamu kwamba tunafanya yale yanayokubaliwa na Yehova Mungu na Mwanawe. Kuwa na kibali yao ni bora zaidi kuliko jambo jingine lo lote. Wala rafiki zetu wala watu wa ukoo wetu hawawezi kutupa msaada usioshindwa, uongozi usio na kasoro na uzima wa milele. Walakini Yehova Mungu hufanya mambo yote hayo yapatikane kwetu kupitia kwa Mwanawe. Vilevile twapata ndugu, dada, mama na watoto katika maana ya kiroho. Yesu Kristo alitoa uhakikisho huu: “Kweli ninawaambia ninyi, Hakuna mutu aliyeacha nyumba, ao ndugu waume, ao ndugu wanawake, ao mama, ao baba, ao watoto, ao mashamba, kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba na ndugu waume, na ndugu wanawake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na mateso, na katika [taratibu ya mambo inayokuja], uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30, ZSB) Yakilinganishwa na yale tunayopata, yale tuwezayo kupoteza machoni pa walimwengu ni takataka tu.​—Flp. 3:8.

10. Ili kuwa wanafunzi wake waaminifu, sababu gani ni jambo la lazima kumpenda Yesu Kristo zaidi ya nafsi zetu wenyewe, na sababu gani jambo hilo linahitaji imani?

10 Vilevile sababu gani Mwana wa Mungu alitaja kwamba twapaswa kumpenda zaidi ya nafsi zetu? Hiyo ni kwa sababu ya yale tunayopaswa kutazamia kutoka kwa watu wasioamini. Timotheo wa pili 3:12 lasema hivi: “Wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.” Kama tungejipenda wenyewe zaidi ya tunavyompenda Mwana wa Mungu, tusingekuwa na nia ya kuteseka kwa kutusiwa na kupigwa au, ikiwa lazima, kufa kwa ajili ya kuwa wanafunzi wake. Bila shaka inahitaji imani ili kuchukua hatua hiyo ya ubatizo, tukifahamu kwamba katika wakati fulani ujao inaweza kumaanisha kupoteza maisha yetu. Imani hiyo inatia ndani uhakika thabiti katika tumaini la ufufuo. (Matendo 24:15) Ndiyo, wanadamu wanaweza kutuua, walakini hawawezi kutwaa haki yetu ya kuwa nafsi zilizo hai. Yehova Mungu peke yake ndiye awezaye kufanya hilo, kuharibu kwa umilele wote haki yetu ya kuwa hai. Kwa sababu hiyo, Yesu alitoa kitia moyo hiki: “Musiwaogope wale wanaoua mwili lakini hawawezi kuua nafsi; lakini zaidi mwogope yeye anayeweza kuharibu nafsi na mwili vilevile katika Gehena.”​—Mt. 10:28, ZSB.

11. Sababu gani imani inahitajiwa tunapokabili magumu ya kiuchumi kwa sababu ya kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo?

11 Tusipoyaona maisha yetu kuwa yenye thamani sana, twaweza vilevile kusimama imara wakati wa magumu ya kiuchumi. Katika nyakati za kisasa, wengine wa watumishi wa Mungu wamepoteza kazi zao kwa ajili ya kushikilia kwa ushikamanifu matakwa ya kimungu. Sana sana tunapokabili matatizo katika kujiruzuku, twahitaji imani kusadiki kwamba Baba yetu wa kimbinguni atajibu ombi hili: “Utupe leo chakula chetu tunachohitaji.” (Mt. 6:11, HNWW) Wote wanaobatizwa wanapaswa kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu aweza na atawaruzuku watu wake nyakati za uhitaji.

Mwendo wa Maisha Unaohitaji Imani

12. Mtu anapaswa kujitahidi kufanya maendeleo gani baada ya kubatizwa?

12 Ingawa imani inahitajiwa ili kuwa mwanafunzi aliye wakf na kubatizwa wa Yesu Kristo, huo ni mwanzo tu wa maisha ya mtu kama Mkristo. Baada ya kubatizwa, twataka kuendelea kukua katika imani na kufanya maendeleo katika kuonyesha matunda mengineyo ya roho ya Mungu—upendo, furaha, amani, uvumilivu, fadhili, wema, upole na kujiweza. Tutataka kuwa wenye juhudi katika kuwaeleza wengine imani yetu. (Gal. 5:22, 23, NW; 2 Pet. 1:5-8) Wanafunzi wapya wanapaswa kukumbuka kwamba wao wangali watoto wa kiroho nao wapaswa kuweka moyoni shauri la mtume Petro: “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni, fanyizeni nia ya kutamani sana maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni lile neno, ili kupitia kwalo mpate kukua kwenye wokovu, mradi mmeonja kwamba Bwana ni mwenye fadhili.”​—1 Pet. 2:2, 3, NW.

13. Mtu anaweza kusitawishaje tamaa ya chakula cha kiroho?

13 Ili kusitawisha tamaa ya kweli ya chakula cha kiroho, mtu anapaswa kuchukua wakati wa kufikiria kwa kuthamini yale ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wamefanya kwa ajili yake na kisha kuuruhusu moyo wake umchochee ajilishe Maandiko kwa ukawaida. Mengi zaidi yanatiwa ndani zaidi ya kusoma Biblia tu. Mtu anapaswa kufikiria kwa njia ya sala yale yaliyotajwa ndani, naye binafsi atumie maishani shauri lililoongozwa na Mungu. Kujifunza Maandiko kwa msaada wa vifaa vya kujifunza Biblia kiwe ni kimoja au viwili hakutoshi ili kumfanya mtu afahamu Neno la Mungu kabisa. Maandiko yanaeleza mengi, mengi sana ili kutujenga na kututia nguvu kiroho.

14. Waamini wapya wanapaswa kushirikiana na nani, na sababu gani?

14 Mashirika mazuri katika kundi la Kikristo ni jambo la muhimu vilevile ili tufanye maendeleo ya kiroho. Rafiki wenye kutamanika sana ni waamini wenzi ambao mafikira yao ni ya kiroho, watu wanaofurahia kuzungumza Neno la Mungu na wenye tamaa nyingi ya kusaidia wanadamu wenzao. Mtume Paulo alimwandikia Timotheo, mzee katika kundi la Kikristo maneno haya: “Katika nyumba kubwa kuna mabakuli na vyombo vya kila namna: vingine ni vyombo vya fedha na dhahabu, vingine vya mbao na udongo, vingine ni vya matumizi ya pekee, na vingine kwa matumizi ya kawaida. Basi, kama mtu atajitakasa kwa kujitenga mbali na mambo hayo yote maovu, atakuwa chombo cha matumizi ya pekee, kwa sababu amewekwa wakfu, amfaa Bwana wake na yupo tayari kwa kila kazi njema. Epa tamaa za ujana, fuata uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na watu wote ambao wanamwomba Bwana kwa moyo safi.” (2 Tim. 2:20-22, HNWW) Kwa hiyo mtume huyo alifananisha kundi kama ambavyo lilikuwa limesitawi katika siku zake na nyumba yenye vyombo vya namna zote. Kama lingekuwa jambo la lazima kwa mzee kujiepusha na ‘visivyo vya heshima,’ asivifanye rafiki zake wa karibu, hakika hilo ni jambo la muhimu hata zaidi kwa watoto wa kiroho ambao ‘akili zao zingali hazijazoezwa kwa kutumiwa kupambanua mema na mabaya.’ (Ebr. 5:14) Ni rahisi sana kwao kuvutwa na mambo yenye kuharibu.​—Linganisha 2 Petro 2:18.

15. Rafiki wazuri wanaweza kutambuliwaje?

15 Hiyo maana yake si kwamba twapaswa kuwa na maoni yenye mashaka juu ya washiriki wa kundi. Si jambo gumu kutambua rafiki wazuri. Yesu Kristo alisema. hivi: ‘Kinywa hunena yale yaujazayo moyo.’ (Luka 6:45) Kwa wazi, wale ambao usemi wao unatuchochea kweli kweli “katika upendo na kazi nzuri” ndio rafiki washikamanifu. (Ebr. 10:24) Kushirikiana nao kwaweza kufanya mtu akue kwenye kukomaa kwa Kikristo.

16. Twaonyeshaje imani ya Kikristo?

16 Kwa kuwa mwanzo wa mwendo wetu wa maisha kama Wakristo ni wonyesho wa imani, njia yetu yote ya maisha yapaswa kweli kweli kuwa yenye kuonyesha imani isiyotikisika katika Yehova Mungu na Mwanawe. Imani hiyo inaonyeshwa kwa matendo yanayopatana nayo. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Muwe watenda wa neno, wala si wasikiaji tu, mukijidanganya wenyewe.” (Yak. 1:22, ZSB) Mengi zaidi yanahitajiwa kutoka kwetu zaidi ya kusikiliza kwa heshima katika mikutano ya kundi na kutoa maelezo ya kuthamini juu ya mambo yaliyosikiwa. Twapaswa kutumia shauri lote la Mungu, nalo jambo hilo linataka matendo, utendaji, nia ya kuangalia mahitaji ya wengine ya kiroho, kimoyo na kimwili. Jambo hilo latutaka tushiriki vilevile katika kazi kubwa ya kuhubiri ambayo lazima itimizwe kabla “mwisho” kuja.​—Yak. 1:27; 1 Yohana 3:16, 17; Mt. 24:14, NW, 21, 22.

17. Kwa sababu ya mfano wa Yesu juu ya mpanzi, twaweza kujiuliza maulizo gani?

17 Kwa kupatana na mfano wa Yesu wa mpanzi, sisi wanafunzi wa Yesu tuliobatizwa twataka kujionyesha kuwa “udongo mzuri.” “Neno la ufalme” lililopandwa mioyoni mwetu lapaswa kuwa lenye kuzaa matunda. Je! twachukua kila nafasi kutoa ushuhuda, hivyo kuzaa matunda katika namna ya kusema juu ya ufalme wa Mungu? (Mt. 13:3-9, 18-23) Kwa kupatana na Ufunuo 22:1, 2, ambapo sehemu ya mpango wa Yehova wa kutoa uzima unafananishwa na miti yenye kuzaa matunda yake kila mwezi, je! tunafanya jitihada tuliyoazimia ya kutoacha mwezi upite bila sisi kushiriki katika kuwaambia wengine juu ya imani yetu? Vilevile, jambo la maana ni kujitahidi kufikia mioyo ya watu wa ukoo wasioamini na rafiki kwa njia ya kutoa ushuhuda wenye kutegemezwa na mfano mzuri katika kuishi kwa Kikristo. Huku tukikataa kuacha yale tunayofahamu kuwa sawa, je! lisingekuwa jambo zuri kuepuka kubishana sana isivyofaa juu ya siku za kuzaliwa, sikukuu na mambo kama hayo pamoja nao? Je! si vizuri zaidi kukaza akili juu ya kushiriki pamoja nao mawazo yanayofaa, yenye kujenga kutoka katika Maandiko kwa kadiri hali za kufanya hivyo zinavyojitokeza? Fadhili zetu, kupendezwa kikweli na msaada mara nyingi vyote vyaweza kutoa ushuhuda wenye nguvu zaidi kuliko maneno mengi.​—Linganisha Warumi 12:17-21.

18. Kwa sababu gani uanafunzi wa Kikristo unathawabisha?

18 Hakika uanafunzi wa Kikristo unaambatana pamoja na madaraka mazito. Lakini maisha yetu ni yenye kuthawabisha kama nini! Hata sisi tunapata amani ya akili na ya moyoni kwa kufahamu kwamba tuna kibali ya Baba yetu wa kimbinguni na ya Mwanawe. Maisha yetu yameongozwa kwa kusudi katika jitihada za kuendeleza hali njema ya milele ya wanadamu wenzetu. Kwa uhakika, twatazama mbele kwenye ‘uzima utakaokuja,’ wakati wa milele wenye kuishi kwa furaha katika taratibu mpya ya Mungu yenye haki. (1 Tim. 4:8) Imani yetu, ambayo ni ya lazima sana katika kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo aliye wakf na kubatizwa, yaweza kutuongoza kupata wakati huo ulio bora sana.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki