‘Vita Ni vya Yehova’
“Mimi ninakujia wewe kwa jina la BWANA [Yehova, NW) wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”— 1 SAMWELI 17:45.
1, 2. (a) Ni wito gani wa ushindani unaokabili jeshi la Israeli likiwa chini ya amri ya Mfalme Sauli? (b) Wanaume wa jeshi la Israeli wanaitikiaje wito wa ushindani wa Goliathi, na sasa ni nani anayetokea katika tamasha ile?
MAJESHI mawili yenye uweza yakabiliana ng’ambo-ng’ambo ya bonde la Ela, kusini-magharibi mwa Yerusalemu. Upande mmoja liko jeshi la Israeli, likiongozwa na Mfalme Sauli aliyewekwa katika cheo hivi karibuni. Upande ule mwingine liko jeshi la Wafilisti lenye bingwa wao aliye pandikizi la mtu, Goliathi. Inaelekea kwamba jina Goliathi linamaanisha “Mwenye Kutokea Wazi Sana.” Yeye ana urefu wa kama meta 2.7 na silaha zimemjaa tele. Goliathi anawapaazia Israeli sauti ya ukaidi wenye makufuru. —1 Samweli 17:1-11.
2 Nani atakabiliana na wito wa ushindani wa Goliathi? “Na watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana.” Lakini tazama—kijana mbichi anatokea kwenye tamasha ile! Jina lake ni Daudi, ambalo linamaanisha “Mpendwa.” Yeye alithibitika kuwa “mpendwa” kwa Yehova pia kwa sababu ya bidii yake ya kufuata uadilifu kishujaa. Tayari Samweli amekwisha kumpaka Daudi mafuta awe mfalme wa wakati ujao wa Israeli, na roho ya Yehova inafanya kazi juu yake kwa nguvu nyingi.—1 Samweli 16:12, 13, 18-21; 17:24; Zaburi 11:7; 108:6.
3. Daudi anajitayarishaje kwa vifaa vya vita, lakini Goliathi ana vifaa vya jinsi gani?
3 Anapomsikia Goliathi ‘akiwatukana majeshi ya Mungu aliye hai,’ Daudi anajitolea akapigane na jitu lile. Sauli anapotoa idhini, Daudi anachomosha mwendo lakini bila yale mavazi ya kidesturi wala silaha alizopewa na Sauli. Kifaa alicho nacho ni fimbo ya uchungaji, kombeo, na mawe matano tu yaliyo laini—tofauti na Goliathi, ambaye amechukua mkuki wenye kichwa cha kilogramu 7 na aliyevaa kinga ya koti lenye mabamba ya shaba la kilogramu 57! Huku Goliathi mwenye uweza na mchukuangao wake wakiwa wanasogea mbele, ‘Mfilisti huyo anamlaani Daudi kwa miungu yake.’—1 Samweli 17:12-44.
4. Daudi anajibuje wito wa ushindani wa jitu hilo?
4 Daudi anajibuje? Yeye anavurumisha wito huo wa ushindani ulirudie jitu hilo, akipaaza sauti hivi: “Wewe unanijia na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana [Yehova, NW] wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana [Yehova, NW] atakutia mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana [Yehova, NW] haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana VITA NI VYA BWANA [YEHOVA, NW], naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”—1 Samweli 17:45-47.
5. Tokeo la vita ile ni nini, na sifa inaendea nani?
5 Daudi anasogea mbele kijasiri kwenye vita. Jiwe la kombeo lake lafyatuka kuelekea kwenye shabaha, na Goliathi abwagika chini ardhini. Ndiyo, Yehova amethawabisha imani na ushujaa wa Daudi kwa kuelekeza fataki ndogo hiyo kwenye kipaji cha uso wa jitu hilo bila kukosea! Daudi anapiga mbio kwenda mbele, anachomoa upanga wa Goliathi mwenyewe katika ala, na kupiga na kung’oa kichwa cha mchokozi huyo. Wafilisti wanakimbia kwa mvurugiko. Kweli kweli, ingeweza kusemwa: “VITA NI VYA BWANA [YEHOVA, NW]”!—1 Samweli 17:47-51.
6. (a) Kwa nini Yehova amehifadhi maelezo marefu ya vita hiyo ya kale? (b) Watumishi wa Mungu wanahitaji uhakikishio gani wanapovumilia mnyanyaso kutoka kwa adui wanaoweza kulinganishwa na Goliathi?
6 Kwa nini Yehova amehifadhi katika Neno lake usimulizi huo wa vita ulio na maelezo marefu, ingawa vita hiyo ilifanywa miaka 3,000 iliyopita? Mtume Paulo anatuambia hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi [uvumilivu, NW] na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Leo, watumishi wengi waaminifu wa Mungu wanavumilia suto na mnyanyaso wa moja kwa moja kutoka kwa adui ambao wanaweza kulinganishwa na Goliathi. Kadiri ambavyo mibano ya adui inaongezeka, ndivyo sisi sote tunavyohitaji ule uhakikishio wenye kufariji kwamba “VITA NI VYA BWANA [YEHOVA, NW]”
Suala la Enzi Kuu
7.Ni suala gani lenye umaana wa kuhangaikiwa na watu wote wa Mungu katika mataifa yote, na kwa nini?
7 Goliathi alijileta mbele akitamba-tamba kwa kumkaidi Mungu wa Israeli. Vivyo hivyo, katika karne hii ya 20 mfumo wa kisiasa wa serikali yenye chama kimoja umekuja mbele, ukitokeza wito wa ushindani kwa enzi kuu ya Yehova na kujaribu kuchokoza watumishi wake ili wajitiishe kuabudu Serikali. Hilo ni suala lenye umaana wa kuhangaikiwa na watu wa Mungu katika mataifa yote. Kwa nini iwe hivyo? Kwa sababu Nyakati za Watu Wasio Wayahudi, au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” zilimalizika katika 1914, hiyo ikiingiza mbio kipindi kilichopo cha “taabu kubwa ya mataifa, pamoja na mfadhaiko.” (Luka 21:24-26; NW, King James Version) Nyakati za Watu Wasio Wayahudi zilianza wakati mataifa yalipoanza kukanyaga-kanyaga Yerusalemu la kidunia katika 607 K.W.K. na zikahusisha ndani miaka 2,520 iliyofuata hadi 1914, wakati ambapo Yehova alimketisha Yesu kwenye kiti cha ufalme ili awe Mfalme wake wa Kimesiya katika Yerusalemu la kimbingu. —Waebrania 12:22, 28; Ufunuo 11:15, 17.a
8. (a) Wafalme wa dunia walijibuje amri ya kiunabii kwamba ‘watumikie Yehova kwa hofu’? (b) Ni mabingwa gani wa kilimwengu wanaodhihaki Yehova vikali na kuchokoza mashahidi wake leo?
8 Badiliko kubwa lilitukia katika 1914. Mataifa wasio Wayahudi hawangeweza tena kutawala bila kukatizwa na Mungu. Lakini je! “wafalme” wenye kutawala wakati huo walitii amri ya kiunabii kwamba ‘watumikie Yehova kwa hofu,’ wakitambua Mfalme wake aliyetawazwa karibuni? Sivyo! Badala ya hivyo, wao ‘walitungamana pamoja wakiwa mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mpakwa-mafuta wake,’ Yesu. Kwa kufuatia tamaa za makuu yao wenyewe, walikuja kuwa katika “ghasia” katika ile Vita Kuu ya 1914-18. (Zaburi 2:1-6, 10-12, NW) Hadi leo hii, utawala wa ulimwengu ni suala moto-moto mbele ya aina ya binadamu. Ulimwengu wa Shetani unaendelea kutokeza mabingwa wa kisiasa, wanaolinganika na watu wa ujamaa mmoja na Goliathi, Warefaimu. Tawala hizo za kutumia mabavu zinamdhihaki vikali Yehova na kujaribu kuchokoza mashahidi wake wajitiishe, lakini kama sikuzote, vita na ushindi ni vya Yehova.—2 Samweli 21:15-22.
“Sauli” wa Ki-Siku-Hizi
9. Ni nani leo wamelingana na namna ya Mfalme Sauli ya kutenda mambo, na kwa njia gani mbali-mbali?
9 Mfalme Sauli anaingia wapi katika habari hii? Mapema kidogo, kwa sababu ya uasi wake, Yehova alikuwa amepiga moyo konde ‘kurarulia mbali utawala wa kifalme wa Israeli utoke kwake.’ (1 Samweli 15:22, 28, NW) Sasa, Sauli alikuwa ameshindwa kutegemeza enzi kuu ya Yehova alipokabiliwa na wito wa ushindani wa Goliathi. Zaidi ya hilo, baada ya hapo alianza kunyanyasa Daudi, aliyemshinda Goliathi na kupakwa mafuta na Yehova achukue mahali pa Sauli. Makasisi walio katika mstari wa utawala wa Jumuiya ya Wakristo wametenda namna hiyo hiyo kwa ulinganifu wa kustaajabisha! Wao wameasi dhidi ya ukweli wa Biblia, wakiwa sehemu ya ule uasi-imani mkuu ‘usiotii habari njema’ juu ya Bwana wetu Yesu na Ufalme wake unaokuja. Wao wameshindwa kabisa kabisa kutetea enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima na wamewanyanyasa kwa uchungu mwingi mashahidi wapakwa-mafuta wa Yehova na waandamani wao, ule umati mkubwa. Yehova ataondolea mbali waasi-imani hao ‘katika ghadhabu yake.’—2 Wathesalonike 1:6-9; 2:3; Hosea 13:11.
10. (a) Katika 1918, ni mwongozo gani rasmi wa makusudio uliotangazwa kwa chapa katika London na kikundi cha makasisi mashuhuri? (b) Badala ya kufuatisha matendo yenye kulingana na ule mwongozo rasmi wa 1918, makasisi wamefuatia mwendo gani?
10 Wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, njia za kuacha msimamo unaofaa za makasisi wa Jumuiya ya Wakristo zilionekana wazi. Ni wazi kwamba unabii wa Yesu katika Mathayo sura 24 na 25, na Luka sura ya 21 ulikuwa ukitimizwa. Kwa uhakika, katika 1918 kikundi cha makasisi mashuhuri katika London, Uingereza, wenye kuwakilisha Makanisa ya Kibaptisti, Kikongreshenali, Kipresbiteri, Kiepiskopali, na Kimethodisti, kilitangaza kwa chapa mwongozo rasmi wa makusudio yao. Mwongozo huo ulitaarifu hivi: “Mgogoro mkubwa uliopo unaelekeza kwenye mwisho wa nyakati za Mataifa wasio Wayahudi.” Lakini wao hawakufuatisha matendo yenye kulingana na tangazo hilo. Tayari, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walikuwa wamehusika kwa kina kirefu katika kuunga mkono pande zote mbili za vita ya ulimwengu ya kwanza. Badala ya kutambua kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme, wao walijitiisha kwenye fikira ya mataifa ya kilimwengu—kwamba watu wanapaswa waendelee kutawalwa na serikali kubwa za kisiasa za mataifa wasio Wayahudi zilizo na mgawanyiko, hata na watawala wakatili kama Goliathi, badala ya kuungamana chini ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 25:31-33.
Hakuna Kuacha Msimamo Unaofaa!
11. Ni akina nani wamekuwa hawakuacha msimamo unaofaa kuhusu suala la enzi kuu, nao wanafuata kielelezo cha nani?
11 Je! watumishi wa Mungu wanaomfuata kwa bidii nyingi huacha msimamo unaofaa kuhusu suala hilo la enzi kuu? Hata kidogo, kama inavyoonyeshwa wazi na maandishi ya Biblia! (Danieli 3:28; 6:25-27; Waebrania 11:32-38; Ufunuo 2:2, 3, 13, 19) Wakristo washikamanifu leo wanategemeza enzi kuu na Ufalme wa Yehova yajapokuwako mashutumu yale yote ya ukatili na minyanyaso ambayo Goliathi mchokozi wa ki-siku-hizi anarundika juu yao. Hivyo, wao wanafuata katika hatua za Yesu, “Mwana wa Daudi,” ambaye alifanya kijasiri vita ya kiroho kwa ajili ya enzi kuu ya Yehova, wakati ule ule akidumisha hali ya kutokuwamo kabisa kuelekea mapambano na siasa za ulimwengu. Katika sala kwa Baba yake, Yesu alitaarifu kwamba wafuasi wake pia, Wakristo wa kweli, “si sehemu ya ulimwengu.”—Mathayo 4:8-10, 17; 21:9; Yohana 6:15; 17:14, 16; 18:36, 37, NW; 1 Petro 2:21.
12. (a) Ni akina nani ambao wamepiga na kuangusha Goliathi wa ki-siku-hizi, na jinsi gani hivyo? (b) Kumekuwa na athari gani juu ya watu wa Yehova kwa sababu ya kuwa na rai ya kwamba “Goliathi” ni mfu?
12 Mabaki ya Kidaudi ya Wakristo wapakwa-mafuta leo wamempiga na kumwangusha Goliathi wa ki-siku-hizi. Jinsi gani hivyo? Kwa njia ya kwamba wamejitangaza bila shaka lolote kuwa upande wa Yehova wa ubishani unaohusu utawala wa ulimwengu. “AZIMIO (Lililopitishwa na Shirika la Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa Waliokuwa Katika Mkusanyiko kule Cedar Point, Ohio, Jumapili, Septemba 10, 1922)” liliweka kigezo cha kufuatwa. Lilitia ndani mambo yanayofuata:
“10. Zaidi ya hilo sisi tunashikilia na kushuhudiza kwamba hii ndiyo siku ya kisasi cha Mungu dhidi ya milki ya Shetani inayoonekana na isiyoonekana;
“11. Kwamba haiwezekani kusimamisha upya ulimwengu au utaratibu wa zamani; kwamba wakati ndio huu umefika wa kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu kupitia Kristo Yesu; na kwamba mamlaka na matengenezo yote yasiyojitiisha kwa nia ya kupenda chini ya utawala mwadilifu wa Bwana yataharibiwa.”
“Mwana wa Daudi,” akiwa Kichwa cha kundi la Kikristo, bila shaka ndiye alielekeza kuvurumishwa kwa “jiwe” hilo la ukweli wa Ufalme. (Mathayo 12:23; Yohana 16:33; Wakolosai 1:18) Maazimio yaliyopitishwa kwenye mikusanyiko ya kila mwaka kuanzia 1922 hadi 1928 yalikazia msimamo huo. Kulingana na rai ya watu wa Yehova, “Goliathi” alilala akiwa mfu, akiwa amekatwa kichwa. Utawala wa kibinadamu wenye kutumia mabavu umekuwa hoi usiweze kulazimisha watetezi wa enzi kuu ya Yehova waache msimamo unaofaa.—Linganisha Ufunuo 20:4.
13. (a) Makasisi wa Jumuiya ya Wakristo waliachaje msimamo unaofaa wakati wa uonevu uliokuwa katika Ujeremani ya Hitler? (b) Kitabu Mothers in the Fatherland kiliripoti nini juu ya Mashahidi wasioacha msimamo unaofaa?
13 Kielelezo cha ki-siku-hizi kinachotokeza wazi kuonyesha uchokozi wa tawala za kisiasa zilizo kama Goliathi kilitukia katika Ujeremani ya Nazi. Dini zile kubwa-kubwa, za Kikatoliki na Kiprotestanti pia, ziliacha msimamo unaofaa kwa njia yenye ole kwa kuuangukia Unazi miguuni, kumfanya mtawala wa nchi hiyo awe sanamu ya ibada, kusalimu bendera yake ya swastika, na kubariki askari zake walipochomosha mwendo wakachinje waitikadi wenzao katika mataifa jirani. Wenye kuitwa Wakristo eti kutoka imani zote—lakini si Mashahidi wa Yehova—walinaswa katika juhudi hiyo ya kizalendo. Kitabu Mothers in the Fatherland kiliripoti hivi: “[Mashahidi wa Yehova] walipelekwa kwenye kambi za mateso, elfu moja kati yao wakauawa, na elfu nyingine wakafa kati ya 1933 na 1945. . . . Wakatoliki na Waprotestanti walisikia wakichagizwa na makasisi wao wawe na ushirikiano pamoja na Hitler. Ikiwa walikinza, walifanya hivyo dhidi ya maagizo yaliyotoka kwenye kanisa na serikali pia.” Lo, Kanisa na Serikali zikawa na hatia ya damu iliyoje!—Yeremia 2:34.b
14. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hunyanyaswa mara nyingi?
14 Hadi leo hii, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuonewa kikatili katika mabara mengi, sawa na vile Yesu alivyotabiri. Lakini chini ya mastakimu zote, Wakristo hao wanafuliza kuhubiri kwa bidii “habari njema hizi za ufalme.” (Mathayo 24:9, 13, 14) Ingawa hali iko hivyo, ajabu ni kwamba katika nchi zilizo nyingi Mashahidi wanatambuliwa kuwa raia wafuata-haki, wenye maisha safi, walio vielelezo katika kuunga mkono sheria na utengemano. (Warumi 13:1-7) Hata hivyo wao huteswa mara nyingi. Kwa nini? Kwa kuwa ibada ni ya Yehova peke yake, wao hujiepusha kuinamia viwakilishi vya Serikali au kuvisalimu. (Kumbukumbu 4:23, 24; 5:8-10; 6:13-15) Bila kuacha msimamo unaofaa, wao wanaabudu Yehova, “yeye peke yake,” wakifanya Yehova awe Bwana Mwenye Enzi Kuu wa maisha zao. (Mathayo 4:8-10; Zaburi 71:5; 73:28, NW) Wakiwa “si sehemu ya ulimwengu,” wao wanadumisha kutokuwamo kwa Kikristo kuelekea siasa na vita vya ulimwengu.—Yohana 15:18-21; 16:33.
15, 16. (a) Ni kielelezo cha nani ambacho Mashahidi wa umri wote wanaweza kufuata wakati Goliathi wa ki-siku-hizi anapowatisha, na kielezi cha jambo hilo kilitolewaje na msichana Mkristo wa miaka sita? (b) Wazazi Wakristo wanataka kuzoeza wadogo-wadogo wao wawe kama nani?
15 Goliathi wa ki-siku-hizi huwatisha mara nyingi washika-ukamilifu hawa, ambao wanatanguliza ibada ya Yehova mbele ya mazoea ya kuabudu sanamu. (Linganisha Ufunuo 13:16, 17.) Lakini Mashahidi, vijana kwa wazee, wanaweza kufuata kielelezo cha Daudi kwa kujibu bila hofu wito huo wa ushindani. Katika bara moja la Latini Amerika, msichana Mkristo wa miaka sita alikuwa amepokea mazoezi bora kwenye maskani yao tangu utoto mchanga. (Linganisha Waefeso 6:4; 2 Timotheo 3:14, 15.) Hiyo ilikuwa imechangia kumfanya awe mwanafunzi aliye na akili nyingi zaidi katika darasa lake shuleni. Lakini dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia ilisababisha ajiepushe kushiriki katika sherehe za kuabudu sanamu darasani. Alipoeleza msimamo wake, mwalimu alipaaza sauti ya mshangao ya kwamba msichana wa umri wake ni mchanga mno asiweze kuwa na dhamiri! Mtoto huyo wa miaka sita alimthibitisha mwalimu kuwa mwenye makosa kwa kutoa ushuhuda wa kuvutia.
16 Inatumainiwa kwamba wazazi wote Wakristo watazoeza wadogo-wadogo wao ili wafuate kielelezo cha Daudi kijana kwa kuchukua msimamo wao wakati mamlaka ya kilimwengu iliyo kama Goliathi inapowatisha. Wao na wawe kama wale watoto watatu waaminifu Waebrania, kama Danieli na wengine wengi walio katika maandishi ya Biblia katika ‘kushika dhamiri njema’ kishujaa kwa upatano na kanuni za Biblia.—1 Petro 2:19; 3:16; Danieli 3:16-18.
Kulingana na Maoni ya Wanahistoria
17. (a) Mwanahistoria Mwingereza Toynbee alionya kwamba ni tukio gani lingekuja kuwako? (b) Jamii ya Goliathi wa ki-siku-hizi inatahinije ushikamanifu wa watu wa Mungu?
17 Mwanahistoria Mwingereza Arnold Toynbee anayejulikana sana alionya juu ya tukio ambalo lingekuja kuwako katika wakati wetu la “namna yenye kuchukiza ya ibada fulani ya kipagani ya serikali za kitaifa zilizo na enzi kuu,” akieleza hilo pia kuwa “mchachuko mkali wa divai mpya ya demokrasi katika viriba vikuukuu vya ukabila.” Wale wanaodai kwamba taifa lao ni bora kuliko mengine yote, hata kufikia hatua ya kuabudu Serikali, wametumiwa na watawala kwa faida yao wenyewe na wakashurutishwa kufuata mawazo ya aina moja tu ili watekeleze miongozo yao, iwe ni myema au mibaya. Tokeo ni kwamba, jamii ya Goliathi imeinuka ili kutahini ushikamanifu wa watu wa Mungu, ambao wanapenda bara la uzaliwa wao lakini wanakataa kuabudu Serikali na vifananisho vyayo.
18. Mkristo mwenye kudhamiria mambo anapaswa kujibu maswali gani ya upekuzi?
18 Kama ilivyokuwa katika Ujeremani ya Nazi, leo kuna maswali ya upekuzi ya kujibiwa na Mkristo mwenye kudhamiria mambo: Je! mimi napaswa kuitikadi kwamba taifa ninamoishi linapendelewa na Mungu kuliko taifa jingine lolote? Hasa sasa, katika kipindi hiki kilicho hatari zaidi ya vyote katika historia ya kibinadamu, je! ni jambo linalofaa na la kiakili kuwa narai ya kwamba kisehemu kimoja cha dunia hii ni bora kuliko visehemu vingine vyote? Au kuona kijisehemu cha jamaa ya kibinadamu kuwa bora kuliko vijisehemu vingine vyote?
19. Mwanahistoria aliye mkubwa wa wote, Yehova, anatuambia nini juu ya kufikiri na kutenda kana kwamba taifa moja la wanadamu ni bora kuliko kila taifa jinginelo?
19 Acheni tufikirie rai ya Mwanahistoria aliye mkubwa wa wote—Yehova Mungu, Mtungaji wa Biblia. Mtume Petro anatuambia hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” Na je! haitupasi sikuzote tutende kupatana na taarifa iliyovuviwa ya mtume Paulo kwamba Mungu “alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote [dunia nzima inayokaliwa, NW]?” Mbona taifa moja la wanadamu lifikiri na kutenda kana kwamba hilo ni bora kuliko kila taifa jinginelo? Akinena juu ya wanadamu wote, Paulo alisema: “Sisi tu wazao wa Mungu.”—Matendo 10:34, 35; 17:26, 29.
20. Ni kitu gani ambacho hakitawatolea tena watu wa Mungu wito wa ushindani katika mfumo mpya wa Yehova, na funzo letu linalofuata litazungumzia nini?
20 Katika mfumo mpya wa Yehova, wapendao uadilifu hawatatokezewa tena wito wa ushindani na mifumo ya kisiasa ya serikali zenye chama kimoja iliyo kama Goliathi, kwa maana kiburi na chuki ya vikundi vyenye mizozo yatakuwa mambo ya zamani. (Zaburi 11:5-7) Hata wawe wanaishi wapi duniani, tayari watu wa Mungu wamekwisha kuacha nyuma mambo hayo ya utukuzo wa taifa, kwa kutii amri ya Yesu kwamba ‘wapendane, kama vile alivyowapenda.’ (Yohana 13:34, 35; Isaya 2:4) Funzo letu linalofuata linaonyesha huo ni upendo wa aina gani!
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate zungumzio lenye maelezo marefu la hii orodha ya matukio ya Biblia, ona kurasa 129-139 za kitabu “Ufalme Wako Uje,” kinachotangazwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti ya New York.
b Ili upate vielelezo vya kuchochea kuhusu ukamilifu wa Mashahidi wa Yehova, vijana kwa wazee, katika kujibu wito wa ushindani wa “Goliathi” wa Nazi, ona Kitabu cha Utendaji 1986 kurasa 46-49, 76-81.
Maswali kwa Kupitia
◻ Ni nini kinachofananishwa na Goliathi jitu lenye uchokozi?
◻ Ni kwa njia gani mbalimbali watumishi wa Mungu hawaachi msimamo unaofaa kuhusu suala la enzi kuu?
◻ Kwa nini watu wa Mungu wanaweza kusema kwamba Goliathi wa ki-siku-hizi amekwisha kupigwa akaangushwa?
◻ Ni akina nani wanaofuata namna ya Mfalme Sauli ya kutenda mambo, na jinsi gani?
◻ Ni jinsi gani watu wa Yehova wametenda kama Daudi kwa kukabiliana na uonevu wa Goliathi wa ki-siku-hizi?