Je! Wewe Una Akili Iliyofunguka Kupokea Mawazo Mapya?
WATU fulani hufunga akili yao isipokee wazo jipya lolote. Huenda wakalikataa kwa sababu linatofautiana na rai yao. Mathalani, mwanamke fulani katika Denmark aliandikia Hjemmet jarida la kila juma na kusema: “Sisi husumbuliwa daima na Mashahidi wa Yehova kwenye mlango wetu. Wao huniudhi vibaya sana, lakini nashindwa ni njia gani ya kuwaondosha. . . . Kwani usumbuaji wao hauwezi kuharamishwa na sheria?”
Wajapani wa katikati ya karne ya 19 walikuwa na rai ya kwamba ‘wanasumbuliwa’ wakati mlango wao ulipobishwa hodi na Wanamagharibi. Katika macho ya wengi wao, kila kitu kilichohusiana na wenye kujidukiza katika nchi yao kilikuwa bure au hata chenye madhara. Kama vile mithali moja ya Mashariki isemavyo, “Tuhuma hufanya giza lionekane likiwa na madubwana.” Kielezi kilitolewa vizuri juu ya hali ya akili ya Wajapani katika michoro ya kuonyesha alivyokuwa Amiri Perry. Kati ya michoro 50 hivi ambayo imebakia, 2 au 3 tu ndiyo inayomwakilisha akiwa ofisa-manowari wa kikawaida wa United States. Ile mingine inamwonyesha kuwa zimwi lenye pua ndefu au dubwana lenye uso uliogeuka rangi, kama vile kielezi hiki kinavyoonyesha.
Hata hivyo, nchi yao ilipofunguliwa, Wajapani wenye akili zilizofunguliwa walikuja kung’amua kwamba wageni hao hawakuwa washenzi. Baadhi yao waliposafiri katika utume wa kwanza wa Kijapani wa kwenda United States, ilikuwa kana kwamba magamba yalianguka kutoka machoni mwao walipojionea wenyewe utamaduni wa Magharibi. Maofisa wa ngazi za juu zaidi waliendelea kulalamika juu ya jinsi Waamerika walivyokosa uungwana kulingana na rai ya Wajapani. Lakini kizazi kilicho kichanga zaidi kilifanya hukumu yenye usawaziko zaidi juu ya utamaduni ule mpya.
Hadimu mwenye umri wa miaka 19 wa ofisa mmoja mkuu aliandika baadaye hivi: “Walio wengi wa wajumbe 70 Wajapani katika utume huu waliwaonea uchungu au wakawachukia [Waamerika]. Hata hivyo, tuliposhuhudia hali zenyewe hasa, watu mmoja mmoja miongoni mwetu tuling’amua kwamba tulikuwa tumekosea na tukajuta kwa sababu ya kufungia moyoni hisia kama hizo. Kushusha hadhi ya wageni kwa kuwaona kama mbwa au farasi na kuwatenda ufidhuli kutawafanya tu wachukue sifa mbaya ya kwamba sisi hatuna rehema wala uadilifu.” Je! wewe umefungua wazi akili yako ili utazame mawazo mapya kwa mwelekeo ulio kama wa hadimu huyo kijana usio wa kutoa hukumu kabla ya uchunguzi.
Kielelezo cha Waberoya
Katika karne ya kwanza W.K., Wayahudi wengi walifungia moyoni maoni yasiyo ya kiakili ya kuhukumu mafundisho ya Kikristo kabla ya kuyachunguza. Kwa njia fulani-fulani, maoni hayo yalilandana na yale ya Wajapani waliojitenga na ulimwengu wa nje kwa maoni mabaya ya kuhukumu kabla ya uchunguzi. “Kila mahali [Ukristo] unanenewa,” ndivyo walivyodai Wayahudi katika Roma la kale. (Matendo 28:22) Kwa habari ya Wakristo fulani katika jiji la Thesalonike, Wayahudi wenye maoni ya kuegemea upande mmoja tu walipaaza sauti hivi: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako.”—Matendo 17:6.
Hata hivyo, walikuwako watu wenye nia ya kutazama ng’ambo ya maoni yao ya kuhukumu kabla ya uchunguzi. Mathalani, wakaaji wa Beroya waliitikiaje habari njema zilizohubiriwa na mtume Paulo na Sila mshirika wake? Kuhusu Waberoya, Luka mwandikaji wa Biblia alisema hivi: “Watu hawa walikuwa waungwana [washarifu katika akili, JVW] kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Je! wewe ni ‘msharifu katika akili’ kama Waberoya?
Tafadhali fikiria kisa cha Masaji. Wakati mmoja, yeye alikuwa na uhasama mkali kuelekea Ukristo. Alikuwa kama wale watu wenye kujitenga waliopinga Japani isifunguliwe wazi. Mke wake, Sachiko, alipoanza kujifunza Biblia, mume huyo alimpinga kijeuri. Hata alifikiria kuua jamaa yake kisha ajiue mwenyewe. Kwa sababu ya jeuri yake, jamaa yake ililazimika kukimbilia maskani ya ndugu mkubwa wa Sachiko kaskazini mwa Japani.
Mwishowe, Masaji aliamua kufungua kidogo akili yake na kuchunguza dini ya mke wake. Baada ya kusoma fasihi fulani ya Biblia, aliona uhitaji wa kufanya mabadiliko. Alipokuwa akijifunza Maandiko, mwelekeo wake wenye jeuri ulibadilika ukawa wa kuonyesha tunda la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Masaji alisitasita kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa sababu alihofu kwamba Mashahidi wangeweza kutafuta kisasi kwa sababu ya jeuri aliyofanya dhidi yao. Lakini mwishowe alipozuru Jumba la Ufalme, alikaribishwa kwa uchangamfu mwingi sana hata akabubujisha machozi.
Ndiyo, kuyashinda maoni ya kuhukumu mapema na kuchunguza mawazo mapya kunaweza kupanua upeo wa mtazamo wetu na huenda kukatunufaisha kwa njia nyinginezo. Hata hivyo, je! hiyo inamaanisha kwamba ni lazima tufungue akili zipokee kila wazo jipya linalotokea?
Uwe Mchaguzi
Kujitenga kwa Japani kulipomalizika, mawazo mapya yalimiminika nchini. Baadhi ya hayo yalinufaisha Wajapani, lakini wangalikuwa na hali nafuu zaidi kwa kutokuwa na mengine-mengine. “Kwa kutenda dhidi ya madhumuni ya Amiri Perry,” akasema jemadari Douglas MacArthur wa United States alipoikubali hatua ya Japani ya kusalimu amri baada ya Vita ya Ulimwengu 2, “Japani iligeuza maarifa ya Magharibi yakawa chombo cha kutumiwa kwa uonevu na utumwa.” Kwa kuiga washauri wa Magharibi, Japani ikajitia katika mwendo ulioiongoza katika mfululizo wa vita. Vita hivyo vilifikia upeo katika Vita ya Ulimwengu 2, na kuelekea mwishoni mwayo makombora mawili ya atomi yakaangushwa juu ya eneo la Wajapani.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo? Kwamba inatupasa kuwa wachaguzi katika kukubali mawazo mapya. Ingefaa tuige Waberoya ‘walioyachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo [yaliyofunzwa na Paulo] ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Neno la Kigiriki ambalo hapa limetafsiriwa ‘kuchunguza’ linamaanisha ‘kufanya utafiti wa uangalifu na wa kufuata mambo kama yalivyo hasa kama vile inavyokuwa katika taratibu za kuchunguza mambo ya kisheria.” (Word, Pictures in the New Testament, kilichotungwa na A. T. Robertson) Badala ya kukubali kwa upofu kila wazo jipya tunalotokezewa, tunahitaji kufanya utafiti wa uangalifu na wa kufuata mambo kama yalivyo hasa, sawa na vile hakimu angefanya katika kusikia kesi ya kisheria.
Tukiwa wachaguzi, hatutafanywa tuyumbeyumbe na kila mtindo unaopita au na mawazo mapya ambayo kwa kweli ni yenye madhara. Mathalani, ile iliyoitwa adili mpya ya miaka ya 1960 ilionekana kwa watu fulani kana kwamba ilikuwa wazo jipya la kuvutia. Lakini uchunguzi mwingi wa uangalifu ungaliifunua kuwa ni ukosefu wa adili wenye madhara tangu zamani, uliokuwa umetokezwa kwa jina jipya. Pia, katika Ujeremani yenye matatizo ya kiuchumi katika miaka ya 1920, bila shaka wengi waliuchukua Unazi kwa rai ya kwamba ulikuwa wazo jipya la kusisimua, lakini ulileta maumivu makali weee!
Linalofurahisha ni kwamba Mungu ameandaa kiwango kinachoweza kutumiwa kutahini mawazo mapya. Hicho ni Neno lake lililovuviwa, Biblia. Kutumia miongozo yalo kuhusu maisha ya jamaa na mahusiano ya kibinadamu kutatusaidia tuchunguze mengi ya mawazo mapya yanayosikiwa leo kutoka kwa washauri wa mambo ya kijamii, washauri wa mawazo ya akilini, na wengine wanaodai kuwa ni wastadi katika mambo hayo. (Waefeso 5:21-6:4; Wakolosai 3:5-14) Shauri la Biblia kwa habari ya uhusiano wetu pamoja na Mungu na jirani linatupatia njia ya kuchunguza mengi ya mawazo mapya yanayoenezwa sasa kuhusu dini. (Marko 12:28-31) Maarifa sahihi ya Biblia yatatuweka tayari kupambanua kama wazo fulani jipya lina thamani halisi au halina. Hapo ndipo tutakapoweza ‘kuhakikisha mambo yote na kushika sana lililo bora.’—1 Wathesalonike 5:21, NW.
Mashahidi wa Yehova huzuru jirani zao kuwatia moyo wajifunze juu ya Biblia na hivyo waweze kuhukumu mawazo mapya kwa njia inayofaa. Mashahidi huonyesha wazi pia fikira za Biblia zilizo mpya kwa wengi. Miongoni mwazo ni ukweli unaohusu nyakati tunamoishi na mambo ambayo kwa kweli yatapata aina ya binadamu wakati ujao. (Mathayo 24:3-44; 2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 21:3, 4) Kwa hiyo usichague kufuata mwelekeo wa kujitenga wakati Mashahidi wanapotembelea maskani yako. Badala ya hivyo, mbona usifungue mlango wako na kusikiliza wanayosema? Usifunge akili yako kuizuia isipokee mawazo yanayoweza kuwa na manufaa ya milele kwako.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Library of Congress photo LC-USC62-7258