Maoni ya Biblia
Kwa Nini Ujifunze Biblia?
KUSOMA Biblia yote kutoka jalada mpaka jalada sio tendo ndogo. Je! umewahi kufanya hivyo mara moja au labda mara kadhaa? Watu wengi kwa kufaa hujivunia kuwa wamefanya hivyo. Kupata wakati wa kusoma Biblia kwapasa kuorodheshwa juu kabisa—ikiwa sio namba moja—katika orodha yetu ya mambo ya kutangulizwa maishani. Kwa sababu gani? Ili kufahamu mambo ya msingi yaliyomo katika kitabu chenye mwenezo mkubwa zaidi katika historia yote, kitabu pekee ambacho hudai kwa haki kuwa kimepuliziwa roho na Mungu.—2 Timotheo 3:16.
Hata hivyo, mtu aweza kufanya zaidi ya kusoma Biblia tu na kujua mpangilio wayo wa ujumla. Je! ni tamaa yako kumpendeza Mungu na kufurahia faida kamili za mafundisho ya kitabu hicho kitakatifu? Basi fuata shauri ambalo mtume Paulo alitoa kwa kijana Timotheo: “Ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote. Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.”—1 Timotheo 4:13, 15, 16.
Kutafakari mafundisho ya Biblia jinsi hiyo na kujiingiza kwayo kunatia ndani zaidi ya kusoma Maandiko peke yayo. Kusoma Biblia kwenyewe hakuhakikishi kwamba mtu aweza kutumia ifaavyo habari aliyopata, kama vile kusoma kitabu kuhusu ubongo wa kibinadamu kusivyomstahilisha mtu kuwa mpasuaji wa ubongo. Kwa hiyo, sikiliza shauri zaidi la Paulo kwa Timotheo: “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”—2 Timotheo 2:15.
Hufungua Mfululizo wa Uelewevu
Kujua kulitumia Neno la Mungu kwa ustadi hutaka kujifunza. Mtu anapojifunza Biblia kwa uangalifu, akifikiria yale isemayo, na kupata maana yayo, akisoma mafungu katika muktadha, na kufahamu historia yayo, ndipo mfululizo wa mwono-ndani usiotarajiwa waweza kufunguka kwake. Sasa yeye binafsi huanza kufaidika kutokana na Neno la Mungu.
Ebu tuchukue mfano unaoonyesha kuwa kwa kusoma tu sehemu ya Maandiko, huenda tusipate maana ya yale yasemwayo bila ya sisi kusoma muktadha. Kwenye Matendo 17:11 tunasoma kuhusu watu wa jiji la Ugiriki la Beroya, ambalo haliko mbali kutoka Thesalonike: “Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”
Kwa mtazamo wa kwanza tunaweza kufanya mkataa kwamba Wakristo katika Beroya walikuwa wenye kujifunza zaidi ya wale waliokuwa katika Thesalonike. Hata hivyo, angalia katika mstari wa 10 wa Matendo 17 kwamba baada ya Paulo na Sila kuwasili Beroya walienda kwenye “sinagogi la Wayahudi” kuhubiri Neno la Mungu. Na mstari wa 12 wasema kwamba “watu wengi miongoni mwao [Wayahudi] wakaamini.” Mstari huo unatusaidia tufikie mkataa tofauti. Usimulizi huo mtakatifu unatuambia kuwa sio Wakristo waliokuwa wakilinganishwa mmoja na mwenzake katika miji hiyo miwili, bali, walikuwa ni Wayahudi katika sehemu hizo.
Kwa kuongezea, je! uliona kile kilichowafanya Waberoya wawe waungwana zaidi katika mwenendo? Wao waliyachunguza Maandiko kwa bidii. Profesa Archibald Thomas Robertson, akitoa maelezo juu ya maneno hayo katika Word Pictures in the New Testament, aliandika: “Paulo aliyaeleza Maandiko kila siku kama vile katika Thesalonike, lakini Waberoya, badala ya kupuuza ufasiri wake mpya, walijichunguzia (anakrinō humaanisha kupepeta, kufanya uchunguzi wa makini na hususa kama vile katika shughuli za kisheria . . . ) Maandiko.” Uchunguzi wao haukuwa wa kijuu juu tu. Wayahudi hao Waberoya walichunguza kwa uangalifu kuhakikisha kwamba yale Paulo na Sila walikuwa wakifundisha kutoka kwa Maandiko kuhusu Yesu kuwa Mesiya aliyeahidiwa zamani yalikuwa kweli.
Kwa hiyo, kwa kufuata mfano wa Waberoya, ni jambo la maana kwamba tusisome tu Neno la Mungu bali pia tujifunze hilo —‘tukiyachunguza maandiko’—ili tupate maana ya yanayosemwa. Kwa njia hiyo tunaweza kuongeza uthamini wetu kwa Biblia, na sisi pia, kama Timotheo, tuwe watu wanaoweza ‘kuokoa nafsi zetu na wale watusikiao pia.’ Kwa nini? Kwa sababu, zaidi ya kusoma Maandiko, tumejifunza hayo ili tutende kwa utii juu ya yale tumejifunza.—Mithali 3:1-6.
Chanzo cha Thamani za Kweli na Unabii
Ebu tufikirie sababu nyingine mbili za kujifunza Biblia. Biblia haiwezi kulinganishwa na kitabu kingine katika kuandaa thamani za unyofu na za kiadili. Miaka mingi iliyopita, mfunzi Mwamerika alionelea hivi: “Mimi ninaamini kwamba kuwa na maarifa ya Biblia bila mtaala wa koleji ni wenye thamani kuliko mtaala wa koleji bila Biblia.” Ili maarifa ya Biblia yapate kuwa hazina yako, kusudi lako la kujifunza Maandiko lazima liwe kutumia maagizo na mafundisho yayo katika maisha yako ya kila siku ili ikufanye uwe mtu aliye bora zaidi, ‘awezaye kutumia kwa halali neno la kweli.’—2 Timotheo 2:15; Mithali 2:1-22.
Kwa kuongezea, katika kurasa zayo mna unabii mbalimbali uliopuliziwa roho na Mungu ambao tayari umetimizwa katika historia na mwingine ambao unapata utimizo wao katika karne yetu. Kujifunza unabii wa Biblia husaidia mtu kuelewa maana ya hali zilizopo za ulimwengu—vita, njaa, mivunjiko ya familia, uhalifu wa jeuri—na jinsi ya kuepuka kunaswa na wasiwasi kwa sababu yazo. (Luka 21:10, 11, 25-28) Kwa hiyo, tunaeleweshwa na jibu la Mungu kwa matatizo ya leo, majibu yanayofunua mahali ambapo tupo katika mkondo wa wakati na jinsi tunavyoweza kupanga kwa mafanikio kwa ajili ya wakati ujao. Majibu hayo yanatujia kupitia mfereji wa jamii ya ‘mtumwa mwaminifu na mwenye akili aliye mpakwa-mafuta’ ambaye hutumia Watchtower Society kuwa chombo chake cha utangazaji.—Mathayo 24:45-47; 2 Petro 1:19.
Zaburi 119:105 husema: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” Kwa hiyo, watu wanaojifunza kwa ukawaida maneno ya hekima yanayopatikana katika Biblia na ambao huyatumia watakuwa miongoni mwa wale watakaoelewa mapenzi na makusudi ya Mungu na, kama tokeo, wanakuwa na njia iliyoangazwa ambayo huongoza maisha yao ya kila siku kupitia bwawa la ufasiki la leo.