Je! Tunahitaji Msaada Kuielewa Biblia?
APRILI wa mwaka jana afisi ya tawi ya Sosaiti katika Brazil iliipokea barua inayofuata:
“Mimi ninawaandikia niwaeleze kwa heshima kwamba mimi ni mwuzaji magazeti ya kila siku wa hali ya chini, mtengenezaji sinema, mpigaji picha, . . . nami nimefanya kila jambo nililotaka kulifanya. Lakini imekuwa kwamba ninakosa jambo lililo la maana zaidi: Imani katika Mungu. Tayari kwa muda wa miaka miwili nimekuwa nikisoma vitabu vya Watch Tower Bible and Tract Society, nami nayapenda mafundisho ya ‘mashahidi wa Yehova,’ na ningependa kuwa mmoja wao, kisha nifanyie wanadamu jambo fulani jema. Nimechoka kuandika hati za sinema, hadithi za kusomwa na makala ambazo hata zinachochea watu wafanye umalaya, waue wengine, watumie dawa za kulevya, wafanye mashambulio, na kila jambo baya ambalo magazeti ya kila siku huchapa katika ukurasa wayo wa kwanza, unaosomwa kwa bidii nyingi na watu wazima na watoto. Lazima mimi nibadilike. Bado kuna wakati wa mimi kutumia uwezo wa kufikiri ambao Mungu amenipa nifaidi ndugu zangu.
“Kwa sababu hiyo, ningependa kuwaomba kwa hamu nyingi mnipe habari juu ya jambo ninalopaswa kulifanya nianze kufuata mafundisho ya ‘Mashahidi wa Yehova.’
“Kwa heshima, nikingojea jibu lenu lenye fadhili.”
Je! ingalitosha kumwambia mwanamume huyu asome tu Biblia pamoja na wengine ambao wangependa kufanya kama yeye? Inaonekana kwamba yeye alikuwa amekuwa akisoma Biblia kwa kiasi fulani. Lakini aliona wazi kwamba alihitaji kupata msaada zaidi.
Yeye alikuwa kama yule mwanamume Mwethiopia anayetajwa na Luka mwandikaji wa Injili kwenye Matendo, sura ya 8. Mwethiopia huyo alikuwa anaendelea kusoma kwa sauti katika unabii wa Isaya, huku akiwa anaendeshwa katika gari la kuvutwa na farasi. Kwa kuharakishwa na roho takatifu ya Mungu, Filipo mweneza evanjeli alilikaribia gari. Alipomsikia mwanamume huyo akisoma maneno ambayo leo ni sehemu ya Isaya sura ya 53, Filipo alimwuliza: “Je! yamekuelea haya unayosoma?” Mwethiopia akajibu: “Nitawezaje kuelewa; mtu asiponiongoza?”—Matendo 8:30, 31.
Ndiyo, Mwethiopia huyo mwenyewe asingeweza kamwe kumtambua mwenye kutajwa na Isaya alipoandika: “Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake.” Kwa hiyo Filipo alimweleza kwamba unabii huo ulitimizwa katika Yesu Kristo. Mwanamume huyo akaukubali uhakikisho uliotolewa kisha akaomba abatizwe mara tu nafasi ya kwanza ikipatikana.—Matendo 8:32-38.
UHITAJI WA KUELEZA MAANA YA MAANDIKO
Uhitaji uu huu wa uongozi unaonyeshwa katika maandishi yanayohusu wawili wa wanafunzi wa Yesu. Wanaume hao walikuwa njiani kwenda Emau, siku ya tatu baada ya kufa kwa Yesu. Wao waliyafahamu Maandiko ya Kiebrania, lakini bado hawakuweza kuelewa kwa nini Yesu alilazimika kupatwa na mateso na kufa. Wakati Yesu alipowafuata akawafikia, hawakumjua kwa kuwa Yesu alikuwa na umbo tofauti. Yesu alifanya nini kuwasaidia wanafunzi hawa wenye nyuso zenye huzuni?
Maandishi ya Biblia yanasema, “Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe.” Halafu ikawaje? Baada ya Yesu kumaliza kujitambulisha na kutoweka wasimwone tena, wao walisema: “Je! mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko?”—Luka 24:27, 32.
Muda mfupi baadaye siku iyo hiyo wanafunzi wawili hao walikutana na mitume wale 11 katika chumba fulani Yerusalemu wakawaeleza yote waliyoona. Wakiwa bado katika kuzungumza mambo hayo, kwa ghafula Yesu aliwatokea katikati yao. Je! Yesu aliwapa nuru zaidi? Ndivyo, kwa maana aliwaeleza hivi: “Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia, nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii, na Zaburi. Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko.” —Luka 24:44, 45.
Hali inayomhusu Apolo, ambaye “alikuwa hodari katika maandiko,” inaonyesha pia uhitaji wa kupata uongozi kutokana na chanzo kinachofaa. Apolo alikuwa mhubiri mwenye ufasaha mwingi na mwenye kusadikisha watu habari za kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi. Lakini bado ilikuwa lazima watu wawili waliooana, ambao walikuwa wameshirikiana karibu-karibu na mtume Paulo, wampe uongozi wa Maandiko. Wakristo hawa waliooana walipomsikia Apolo akihubiri, waliweza kuona kwamba yeye alihitaji kufahamishwa vizuri zaidi mafundisho fulani. Kwanza, yeye alijua habari za ubatizo wa Yohana Mbatizaji tu.—Matendo 18:24-26.
NJIA YA KIBINADAMU YA KUPITISHIA HABARI
Kutokana na mambo hayo yaliyoonwa inaweza kuonekana kwamba Yehova Mungu alifanya Biblia iandikwe kwa njia ambayo mtu anahitaji kupashana habari na njia Yake ya kupitishia habari kabla hajaweza kuielewa kwa ukamili na usahihi. Ni kweli tunahitaji msaada wa roho takatifu ya Mungu, lakini msaada wayo unatujia pia hasa kwa kushirikiana na njia ya kupitishia habari ambayo Yehova Mungu anaona anafaa kuitumia.—1 Kor. 2:6-10.
Ikionyesha kwamba Mungu angekuwa na kundi lenye mpango wa tengenezo ambalo kupitia kwalo maagizo yangetolewa, Biblia inasema hivi: “Naye alitoa wengine kuwa mitume; na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; ili tusiwe tena watoto.”—Efe. 4:11-14.
Katika karne ya kwanza, mpango huo wa kundi ulitegemewa kwa uongozi. Kwa mfano, jambo hili linaonekana wakati ulizo lilipotokea juu ya kama watu wasio Wayahudi wenye kugeuka walipaswa kutahiriwa. Wakati huo, je! mtume Paulo alisema jambo kama hili: ‘Sikieni, Yesu Kristo alinitokea mimi binafsi, naye amenionyesha maono yasiyoweza kuonekana kwa nguvu za kibinadamu, akanipa zawadi ya unabii na ya kuwa na roho kisha akaniwezesha kufanya matendo hodari; basi acheni mimi niwaeleze jinsi mambo yalivyo juu ya ulizo hili la kutahiri’? Aka, hakusema hivyo!
Mtume Paulo na wenzake walikwea Yerusalemu wakaenda kuiuliza baraza inayoongoza ya kundi la Kikristo, yenye mitume na wanaume wazee. Na mwenye kujulisha habari za uamuzi uliofanywa juu ya kutahiri hakuwa mtume Paulo bali Yakobo, ndugu-mzazi-mmoja wa Yesu, ambaye wakati huo inaonekana alikuwa ndiye mwangalizi-msimamizi wa kundi la Yerusalemu. Baada ya hapo, Paulo, Sila na wengine waliwapelekea kina ndugu maamuzi hayo.—Matendo 15:1-35.
Namna gani juu ya safari za Paulo za umisionari? Je! yeye alijitegemea kwa kufanya alivyotaka mwenyewe asifuate mgawo aliopewa na Yehova wa kuwa mtume kwa kikundi fulani cha watu? Hapana, bali yeye aliukubali mgawo wake kwa utii, na baadaye mgawo huo ulitambuliwa na “nguzo” za baraza inayoongoza Yerusalemu, kama isemavyo Wagalatia 2:9: “Walipokwisha kuijua ile neema niliyopewa; Yakobo, na Kefa, na Yohana, wenye sifa kuwa ni nguzo, walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika; ili sisi tuende kwa Mataifa, na wao waende kwa watu wa tohara.”—Matendo 9:15; 13:1-4; 22:17-21.
Baadaye, wakati Paulo alipokuja Yerusalemu kwa mara ya mwisho, Wayahudi wa hapo walikuwa wamepokea habari za udanganyifu kumhusu yeye. Kwa hiyo “wazee” katika Yerusalemu walimshauri Paulo juu ya jambo la kufanya katika jitihada ya kuzinyamazisha habari hizo. Naye Paulo aliukubali uongozi wao kwa haraka.—Matendo 21:17-36.
Ili kutusaidia tufahamu Neno la Mungu katika “siku za mwisho” hizi, kwa upendo Yehova Mungu ametutolea tengenezo lenye kuonekana lililo chini ya Kristo —“mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Jinsi ambavyo Yehova Mungu amefanikisha utendaji mbalimbali unaoendeshwa chini ya tengenezo hilo haiwezi kuacha shaka katika akili za Wakristo walio wakf kwamba kibali ya Yehova Mungu i juu yalo.—Mt. 24:45-47.
MAONI YA UUNGWANA WA AKILI
Tutakionaje chakula cha kiroho kinachotolewa na huyu “mtumwa mwaminifu mwenye akili”? Je! tunapaswa kukitazama kwa njia ya kulaumu—‘Ndiyo-oo, huenda jambo hili likawa kweli lakini tena huenda likawa si kweli, kwa hiyo inatupasa tulichunguze sana sana tuhakikishe si kosa’? Inaonekana wengine wamekuwa na maoni hayo. Ili kuunga mkono njia yao ya kufikiri wametumia maneno ya Matendo 17:11, yanayosema hivi juu ya watu waliokuwa wamebatizwa juzi-juzi huko Beroya: “Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”
Lakini je! hilo lina maana ya kwamba Waberoya hao walikuwa wakitafuta vikosa-vikosa katika ujumbe waliokuwa wakiusikia, au kwamba nia yao ilikuwa ya kutia mashaka? Je! hilo linaweka kanuni ya kuvichukua kwa njia yenye lawama vitabu vinavyotokezwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” kwa kusudi la kupata kosa? Hata!
Kwanza, na tuangalie hali zilizokuwapo kabla ya kusemwa maneno yanayowahusu Waberoya wenye akili za uungwana. Paulo, akiambatana na Sila, alikuwa katika safari yake ya pili ya umisionari. Kwa sababu ya mateso yaliyotokea, kina ndugu huko Thesalonike waliwapeleka wasonge mbele mpaka Beroya. Katika Beroya wakakuta Wayahudi wenye mioyo minyofu walioliamini sana Neno la Mungu. Lakini walikuwa hawajawa Wakristo. Walikuwa watu wenye kupendezwa tu waliopaswa kuridhika kwa kuamini kwamba mambo aliyokuwa akiwaambia Paulo yaliungwa mkono na Maandiko ya Kiebrania.
Kufikia wakati huo, Wayahudi hao wenye kujitolea sana mambo ya kimungu katika Beroya labda hawakuwa wamesikia hata siku moja habari za Yesu Kristo. Mambo ambayo Paulo alikuwa akiwaambia yalikuwa mapya kabisa. Kwa hiyo Wayahudi hao wenye akili za uungwana katika Beroya waliyachunguza Maandiko kila siku kuhakikisha kwamba kwa kweli mitajo aliyotaja Paulo ilikuwa sehemu ya Neno la Mungu. Nao walifuatia mafunzo yao wakiwa na hali gani ya akilini? Je! ilikuwa nia ya kutiatia mashaka, wakijaribu kumhakikishia Paulo alikosea? Sivyo, wao walikuwa tofauti kabisa na watu waliomlaumu-laumu Paulo juu ya Kilima Mars, kwa maana tunasoma kwamba waliusikia ushuhuda wa Paulo “kwa uelekevu wa moyo.”—Matendo 17:11, 32.
Waberoya hawa walisikiliza kwa utayari, naam, kwa hamu nyingi, ili waamini. Hivyo wao hawakuwa na utayari wa kusikiliza tu, bali walikuwa watu wenye kutaka kuzihakikisha “habari njema” hizi kuwa za kweli. Kwa kweli, ili mtu aweze kupata imani lazima awe na “nia ya kuamini.” Ikiwa yeye amejikaza asiamini, basi hatasadikishwa na ushuhuda wo wote hata uwe mwingi namna gani; kwa maana visababu vya kutokutaka kufanya jambo vinapatikana nyakati zote mtu akivitafuta, sababu zinazoonekana kufaa na kumbe hazifai, za mtu kutaka kuepa wajibu atakaopaswa kuwa nao akikubali kuamini. Ni kama vile mtume Paulo alivyosema kwa uzuri: “Si wote walio na imani.” (2 The. 3:2) Lakini Waberoya walikuwa na nia ya kuamini. Waliyafikiria mambo waliyoyasikia wakiwa na hali ya akili ya kutaka kuyapokea. Kwa sababu hiyo, “wengi miongoni mwao wakaamini, na wanawake wa Kiyunani wenye cheo, na wanaume si wachache.”—Matendo 17:12.
Wanafunzi wa Yesu waliandikia makundi ya Kikristo barua nyingi, ya watu ambao tayari walikuwa katika “njia ya kweli.” (2 Pet. 2:2) Lakini hatusomi po pote kwamba ndugu hao walikuwa na hali ya akili ya kutaka kutia-tia mashaka, wakichunguza Maandiko kwanza kuhakikisha kwamba barua hizo ziliungwa mkono na Maandiko, kwamba waandikaji kwa kweli walijua mambo waliyokuwa wakiyasema.
MAONI YETU JUU YA YULE “MTUMWA”
Tunaweza kufaidika kutokana na kufikiria mambo haya. Tukiisha kuhakikisha ni chombo gani ambacho Mungu anatumia kama “mtumwa” wake wa kutolea watu wake chakula cha kiroho, kwa uhakika Yehova hapendezwi tukikipokea chakula hicho kama kwamba huenda kikawa na kitu fulani chenye kuumiza. Inatupasa tuwe na matumaini hakika katika njia ya kupitishia habari ambayo Mungu anaitumia. Kule kwenye makao makuu Brooklyn ambako vitabu vinavyohusu Biblia vya Mashahidi wa Yehova vinatoka ndiko kwenye wazee wengi zaidi wa Kikristo waliokomaa, wa “mabaki” na wa “kondoo wengine” pia, kuliko mahali pengine po pote duniani.
Ni kweli kwamba ndugu wanaotayarisha vitabu hivi si watu wasioweza kufanya makosa. Maandishi yao hayana roho ya Mungu kama yale ya Paulo na wale waandikaji wengine wa Biblia. (2 Tim. 3:16) Kwa hiyo, nyakati nyingine, ufahamu ulipozidi kuwa wazi imekuwa lazima kusahihisha maoni. (Mit. 4:18) Walakini, kufanya hivyo kumeleta hali ya kuendelea kulisafisha umbo la jumla la kweli yenye msingi wa Biblia ambayo Mashahidi wa Yehova wanakubali kuifuata. Muda wa miaka iliyopita, kwa kuwa marekebisho yamefanywa kwenye umbo hilo la jumla la kweli, kweli hiyo imekuwa yenye kupendeza zaidi na kutumika zaidi kwenye maisha zetu katika “siku za mwisho” hizi. Waelezaji wa Biblia wa Jumuiya ya Wakristo hata si wao wenye roho ya Mungu. Wajapofanya madai ya kuwa na maarifa mengi, wao wameshindwa kukazia waziwazi hata kweli zile za msingi za Biblia—kama vile dunia ya Paradiso inayokuja, ubora wa jina la Mungu, na hali ya wafu.
Bali, kumbukumbu ambalo tengenezo la “mtumwa mwaminifu mwenye akili” limefanya kwa miaka zaidi ya 100 iliyopita linatulazimisha kukata maneno kama Petro wakati Yesu alipouliza kama mitume wake pia walitaka kumwacha, yaani, “Twende kwa nani?” (Yohana 6:66-69) Hakuna shaka. Sisi sote tunahitaji msaada kuielewa Biblia, nasi hatuwezi kuupata uongozi wa Maandiko tunaouhitaji nje ya tengenezo la “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”