Yule Msanii Mkuu—Yehova!
“WASANII hupaka rangi picha nyingi sana za macheo na machweo ya jua, na kazi zao huuzwa kwa mamia, hata maelfu, ya dola. Hata hivyo, Yehova Mungu, yule Msanii Mkuu na Mwanzilishi wa macheo na machweo ya jua, hutupatia sisi picha moja kila siku—bila malipo. Picha zilizo za awali zinapita kwa mbali nakala zinazotolewa kutokana nazo. Je! hiyo isisababishe sisi tumthamini yeye kuwa ndiye Muumba? Hiyo ndiyo sababu iliyotolewa na mwangalizi mmoja mwenye kusafiri wa Mashahidi wa Yehova katika Hawaii wakati wa moja ya hotuba alizotolea kundi moja.
Mwanamke mmoja asiyeamini kuna Mungu, mwenye kuzuru Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza, alikuwa katika hadhirina. Yeye alitia maanani njia ya kusababu kwa mhudumu huyo, lakini mashaka imara juu ya kuwako kwa Mungu yakawa yangali yanabakia-bakia. Hata hivyo, alipokuwa akiendesha gari kutoka kazini kurudi kwenye maskani yake karibu miaka miwili baadaye, mwendo wake ulipunguzwa sana na magari mengi ya wakati huo wenye pirikapirika nyingi. Hiyo ikasababisha aone machweo ya jua ambayo pindi hiyo yalikuwa ya kutazamisha sana. Fikira zake zikarudi kwenye ile hotuba ya mwangalizi mwenye kusafiri.
Yeye anasimulia hivi: “Badala ya kuudhika kwamba hayo magari mengi yalinipunguzia sana mwendo, mimi niliona yale machweo ya jua yenye upendezi mwingi, na yakanikumbusha yaliyokuwa yamesemwa na mnenaji juu ya kumthamini Yehova Mungu kuwa Msanii na Muumba. Yalinifanya nianze kufikiri ya kwamba, ‘Labda aliyosema ni kweli; kweli huenda ikawa kuna Muumba.’ Nilifikiria hilo nilipoendelea kuelekea kwenye maskani yangu, na usiku huo nikampigia simu rafiki yangu ambaye hapo awali alikuwa amenialika niende kwenye Jumba la Ufalme. Nilianza kujifunza Biblia, na sasa mimi naabudu Yehova akiwa Mungu na Muumba wangu.”
Kama mtunga zabuii, si kwamba tu mwanamke huyu alikuja kumthamini Yehova kuwa Msanii Mkuu wa uumbaji bali alikuja pia kuimba sifa zake. Mtunga zaburi aliandika hivi: Sifuni Yehova kutoka kwenye mbingu. . . Sifuni yeye, nyinyi jua na mwezi. Sifuni yeye, nyinyi nyote nyota za nuru. . . . Acheni hivyo visifu jina la Yehova; kwa maana yeye mwenyewe aliamuru, navyo vikaumbwa.—Zaburi 148:1-5, NW.