Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Yehova Ategemeza Watumishi Wake Waaminifu
YESU alisema: “Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi [wameninyanyasa mimi, NW], watawaudhi ninyi.” (Yohana 15:20) Lakini watumishi waaminifu wa Yehova wanahakikishiwa kwamba yeye atawategemeza. (Zaburi 18:2; Nahumu 1:7) Katika nchi moja ya Kiafrika ambako kazi yenye amani ya Mashahidi wa Yehova imezuiliwa vikali, Yehova alitegemeza watumishi wake wakiwa katika kukabiliana na mapigo na kukamatwa, kama ripoti inayofuata inavyoonyesha:
“Mwangalizi wa mzunguko na ndugu wanne wa hapa walikamatwa kimabavu na kutupwa ndani ya chumba kidogo ambacho kwa kawaida huwekwa akiba kwa ajili ya mbwa watanga-tangaji,” yasema ripoti hiyo. “Wao waliwekwa humo kwa siku 123 wakiwa na mavazi yao ya ndani na hata hawakuruhusiwa kwenda nje chooni.” Mbunge mmoja alipata habari za hali hizo zisizo za kibinadamu na akaanza kuteta, na mwishowe, baada ya siku 123, akina ndugu waliachiliwa. Yehova aliwategemeza ndugu hao waaminifu kwa roho yake.
Ono jingine kutoka nchi iyo hiyo linaonyesha matokeo yenye manufaa ya kazi yetu ya kuhubiri. Ripoti inasimulia hivi: “Katika kijiji kimoja, watu wa huko walikuwa na sifa ya kuwa wajeuri na waasi. Hata hivyo, baada ya Mashahidi wa Yehova kuhubiri huko, wengi walikuja kustahi wenye mamlaka wa huko na wakaanza kushiriki katika kazi ya kijumuiya ya kuzitengeneza barabara kila juma.” Chifu mmoja wa huko alitaka kujua sababu iliyotokeza badiliko hilo la mwelekeo wa watu naye akaambiwa hivi: “Ilikuwa kwa sababu ya fundisho la ‘pasta’ wa Mashahidi wa Yehova.” “Siku moja chifu huyo alinialika kwenye nyumba yake,” anasema Shahidi, “naye akanitia moyo niendeleze hiyo kazi njema. Alinipa zawadi ya kuku mkubwa nikamle pamoja na jamaa yangu.” Katika pindi nyingine, meya wa huko alikuja kumzuru ndugu huyo, naye ndugu akamwalika ndani na kumpa ushuhuda. Meya “aliomba magazeti na kusema, ‘Sisi hatufikiri nyinyi hufanya dhara lolote. Endeleeni kukata-kata rufani. Sisi hatuna maagizo ya kuwakamata. Mimi nafikiri karibuni Serikali itashughulikia tatizo lenu.”’
Painia wa pekee anaandika hivi: “Baada ya mashtaka kutoka kwa mwandishi wa chama cha kisiasa, chifu wa hapa aliagiza nikamatwe na kutiwa gerezani katika kijumba kichafu-kichafu kilichotiwa taka na mkojo na samadi ya wanyama. Niliwekwa katika giza hilo kwa siku tano. Nilipokuwa njiani kwenda humo, nilipelekea Yehova sala na kukumbuka Zaburi 50:15. Walinzi huko walinihurumia na hawakufunga kabisa mlango ili niweze kupumua kidogo hewa safi. Baada ya siku tano za kuwa katika gereza hilo, nilitahiniwa waliponipa mbuzi nimpelekee chifu wa kwetu, bila mtu wa kunisindikiza. Kwa kuwa sikutoroka, nilipewa uhuru kila siku kuanzia saa 9:00 alasiri hadi saa 1:00 jioni. Ningeweza kukutana pamoja na akina ndugu, na tungeweza kuhubiri pamoja. Ingawa nilipata kuwa mgonjwa katika wakati huo mgumu na adui zangu wakatumaini kwamba ningekufa, Yehova hakuniacha kamwe. Ono hilo limenileta karibu na Yehova, nami nina uhakika kwamba mnyanyaso hautanitenganisha mimi kamwe na watu wa Yehova.”—Linganisha Warumi 8:35-39.
Mashahidi wa Yehova wanathamini jinsi Mungu huwategemeza katika nyakati za magumu. Wanawathamini pia wale wanaowaonyesha fadhili wanapokuwa wakiendesha kazi hii iliyo ya maana zaidi ya kuokoa uhai ya kuhubiri habari njema. Yehova hatasahau kamwe fadhili hizo.—Mathayo 25:40.