Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Habari Njema za Ufalme Kutoka Kule Chini
KAMA ilivyo katika mabara mengine 211, habari njema za UfaIme zinapigiwa mbiu kwa bidii na Mashahidi wa Yehova kule chini katika Australia. Mashahidi wa huko ambao ni zaidi ya 49,000 wanaona shangwe ya kuwa na baraka nyingi. Watu wengi wa mataifa tofauti-tofauti wamehamia huko miaka iliyopita, hivi kwamba sasa makundi 58 ya watu wa rangi nyinginezo yanaripoti utumishi wa shambani. Maono ya kutia moyo yanasimuliwa na ofisi ya tawi la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi.
Mkimbizi Mvietnam
Mkimbizi Mvietnam, ambaye sasa anaishi Australia, alilelewa katika mazingira ya ibada ya wazee waliokufa zamani, dini ya Konfyushasi, na dini ya Buddha, pamoja na falsafa ya Mashariki na ya Magharibi. Yeye alikuwa askari katika jeshi la Vietnam ya Kusini mpaka 1975. Katika 1979 alilazimika kukatwa mkono wa kushoto kwa sababu ya kivimbe hatari kilichofura katika kiwiko chake. Kwa kutamani sana uhuru, alikimbia Vietnam katika 1983, akiwa pamoja na watu wengine 24, katika mashua ndogo. Baada ya kabiliano la kuogopesha sana pamoja na maharamia wa baharini, mashua yao ilielea-elea ovyo katika Bahari ya China ya Kusini kwa siku sita zenye joto kali, mpaka mwishowe wakafika Malesia. Aliruhusiwa kuingia Australia baada ya kukaa miezi mitano katika kambi ya wakimbizi. Miezi mitatu baadaye alikutana na ukweli. Maneno ya Yesu kwenye Yohana 8:32 yakajibu tamaa yake ya kina kirefu ya kutaka uhuru: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” Akina ndugu walimwonyesha upendo mwingi. Leo yeye ni Shahidi wa Yehova na ni chombo kinachotumika kusaidia Wavietnam wengine wengi wajifunze ukweli unaoweka mtu huru.
Mwaborijini Aitikia Ukweli
Katika Australia ya kaskazini-magharibi ndugu painia kijana na mwenzake walitembelea mwana-mke Mwaborijini katika eneo la kikabila linaloitwa kibanda cha sufi. Baada ya kusikia sababu yao ya kumtembelea, mwanamke huyo akachukua ufunguo uliozungushiwa shingo yake na kufungua kasha kubwa la chuma. Acha washangae walipoona humo ndani mbili za broshua zetu za Mnara wa Mlinzi na nakala ya zamani ya Biblia miongoni mwa vitu vyake vichache. Wakaketi chini, wakaweza kuanzisha funzo kwa kutumia moja ya broshua hizo. Ingawa mwanamke huyo hasomi wala haandiki, yeye alizithamini kweli kweli broshua alizokuwa amezipata kabla ya hapo. Sasa funzo la ukawaida linaongozwa, naye anafurahia sana.
Kupiga Simu Kiaksidenti
Katika jiji la Sydney, lenye wakaaji milioni tatu, kisichana wa miaka mitatu alikuwa akichezea simu na akapiga namba fulani bila lengo lolote. Kumbe namba hiyo ilikuwa ya Shahidi. Dada alijibu, naye kwanza akafikiri mwenye kupiga alikuwa mjukuu wake. Ndipo aliposikia sauti ya mtu mzima. Huyo alikuwa ni mama ya kisichana yule, aliyeomba radhi kwa ajili ya binti yake. Maongezi yakafuata, na muda huo dada yetu akatoa ushuhuda. Bibi huyo alipaaza mshangao huu: “Mimi nilikuwa nikitumainia Mashahidi wangekuja tena mlangoni kwangu. Nataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova!” Akaendelea kusema kwamba miezi miwili tu kabla ya hapo, yeye alikuwa amezuru Peru na kuvutiwa na shangazi yake na jamaa yake ambao sasa ni Mashahidi wa Yehova. Bibi huyo alisema: “Watoto wa watu wa ukoo wangu walikuwa maibilisi wadogo, lakini sasa wao ni malaika wadogo!” Mipango ilifanywa kuwe na funzo la Biblia, na bibi huyo mwenye kupendezwa anazidi kufanya maendeleo mema—yote hayo kwa sababu ya simu ya kiaksidenti iliyopigwa na kisichana chake.