Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
“Kila Andiko Ambalo Mwanamke Huyo Alisoma Liligusa Moyo Wangu”
“NENO la Mungu li hai, tena lina nguvu,” akasema mtume Paulo. (Waebrania 4:12) Hilo lilithibitika kuwa kweli katika maisha ya mwanamke mmoja wa kutoka Vietnam ambaye alilelewa akiwa Mbuddha. Hii ndiyo hadithi yake.
“Wazazi wangu, ambao wangali wako katika Vietnam, ni Wabuddha wa jina, basi mimi nililelewa nikiwa Mbuddha mpaka nilipofunga ndoa nikiwa na umri wa 22. Familia ya mume wangu ilijaribu kunilazimisha kubatizwa katika Kanisa Katoliki. Walisema kwamba mama-mkwe wangu mfu alikuwa akizuiwa kwenda mbinguni kwa sababu mimi nilikuwa Mbuddha! Kwanza nilikataa kufanya hivyo, lakini baadaye nikabatizwa ili kuwafurahisha. Hata hivyo, kwa kina kirefu ndani ya moyo wangu, nilihisi huo ukiwa mzaha kwa sababu nilichukia unafiki katika Kanisa Katoliki. Halikuwa tofauti na dini ya Kibuddha. Hiyo ilihusika katika vita na siasa kwa kadiri ile ile, na dini zote mbili zilitia moyo kuabudu mababu waliokufa.
“Kama ningalibaki katika Vietnam, ningalikuwa na nafasi kidogo sana ya kujifunza ukweli. Mimi nilikua nikawa mtu mzima wakati misukosuko ya kisiasa ilipokumba Vietnam ya Kusini, nami niliishi katika mji ulio mbali sana na Saigon. Basi ilikuwa baraka kuweza kutorokea Australia.
“Nilikuwa mmoja wa watu wa mashuani waliopata nafasi bora zaidi ya kuponyoka. Nikiwa nimemshika mtoto wangu wa miezi miwili mikononi mwangu, nililazimika kukimbia gizani niponyoke kutoka kwa polisi na kuipanda mashua ndogo ya kuvua samaki. Baada ya siku saba baharini, tulifika Malesia, ambako tulikaa kwa miezi michache katika kambi ya wakimbizi kabla ya kuja Australia.
“Baada ya miaka miwili na nusu katika Australia, mimi nilifikiwa na Mashahidi wa Yehova katika huduma yao ya nyumba kwa nyumba. Katika ziara ya kwanza, nilikubali funzo la Biblia la ukawaida kwa sababu niliona hii kuwa fursa nzuri ya kujifunza Kiingereza. Lakini mwenendo wa Shahidi aliyenikuta na ule ukweli ambao mwanamke huyo alinifunza ni mambo yaliyonivutia sana. Kila andiko alilosoma liligusa moyo wangu, nami singeweza kuona unafiki wowote katika tengenezo la Yehova. Baada ya kujifunza Biblia kwa mwaka mmoja na nusu, niliweka maisha yangu wakfu kwa Yehova nikabatizwa.
“Ni lazima niseme kwamba ukweli umebadili maoni yangu yote juu ya maisha. Mume wangu ni asiyeamini, lakini Yehova amenisaidia na kunitegemeza, pamoja na familia yangu ndogo. Yeye amekuwa Mfunzi Mkuu wangu na amenifundisha kuwa mke na mama mzuri zaidi. Mimi naendelea kumtolea Yehova asante kwamba amenisaidia kutoka giza la kiroho kuingia katika nuru ya ukweli wa Biblia.”
Kwa kweli, Neno la Mungu lililopuliziwa roho lilitokeza nguvu yenye faida katika kisa hiki. Kujifunza Biblia na kutumia yale mtu ajifunzayo huyapa maisha maana na kusudi na kuongoza kwenye uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Kama alivyosema Musa aliyepuliziwa roho, “si jambo lisilofaa kwenu; maana, ni maisha yenu.”—Kumbukumbu 32:47.y