Utamwambia Nini Mbudha?
1 Katika nchi nyingine, zaidi ya nusu ya wale wanaobatizwa ni kutoka Ubudha. Ni nini kinachowavutia waingie katika kweli? Unaweza kumwambiaje Mbudha habari njema?
2 Mwonyeshe Hangaikio la Kweli: Watu wengi ambao zamani walikuwa Wabudha walisema kwamba si kusababu kwingi kulikowavutia kwenye kweli. Badala yake, walivutiwa na jinsi walivyohangaikiwa kikweli. Mwanamke Mwesia aliyeishi Marekani alivutiwa sana na urafiki wa dada aliyemtembelea hivi kwamba akakubali kujifunza. Hakujua Kiingereza vizuri, lakini dada huyo alikuwa mwenye subira. Mwanamke huyo alipokuwa amechoka au hakuweza kujifunza, dada huyo angemtembelea kirafiki tu na kupanga funzo lifanywe wakati mwingine. Hatimaye mwanamke huyo, wana wake wawili, na mama yake mzee walibatizwa. Alirudi nchi ya kwao na kusaidia wengi wajifunze kweli. Mmoja wa wana wake sasa hutumikia katika ofisi ya tawi. Hizo zilikuwa baraka zilizoje kutokana na kuonyesha ‘fadhili za Yehova na upendo kwa ajili ya binadamu’!—Tito 3:4.
3 Kufikiri kwa Wabudha: Kwa ujumla Wabudha hukubali maoni mengine, lakini hawaoni likiwa jambo la lazima kushikilia fundisho fulani. Kwa hiyo, itikadi zao wakiwa mmoja-mmoja hutofautiana. Fundisho moja la kawaida la dini ya Buddha ni kwamba maisha yamejaa mateso, lakini kupitia kuelimishwa, mtu anaweza kukomesha mzunguko wenye kuendelea wa kuzaliwa tena katika maisha yasiyofaa. Inasemekana kwamba ili mtu aondolewe kwenye mzunguko huu, lazima afikie Nirvana, hali isiyoweza kufafanuliwa kwa sababu si mahali au tukio, bali badala yake, ni hali isiyo na maumivu wala uovu. (Ona broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa?, ukurasa wa 9-10.) Jambo hilo latuonyesha nini? Kwamba halingekuwa jambo lenye matokeo kubishana na watu juu ya falsafa ya Kibudha. Badala yake, zungumzia matatizo ya kawaida yanayowahangaisha watu wote.
4 Kazia Mambo Yanayowahusu Nyote Wawili: Kwa kuwa Wabudha kwa kawaida huhusianisha maisha ya duniani na mateseko, huenda wakaliona lile wazo la uhai wa milele duniani kuwa upuuzi. Hata hivyo, sisi sote huwa na tamaa na kufurahia maisha ya familia, kuona kuteseka kukiondolewa, na kujua maana ya maisha. Ona jinsi mahitaji hayo yanavyoweza kukaziwa.
5 Unaweza kujaribu utangulizi huu:
◼ “Leo twaishi katika ulimwengu ambamo watu wengi wasio na hatia huteseka. Unaamini ni nini kinachohitajiwa ili kumaliza maumivu na taabu za wote? [Ruhusu jibu.] Kuna ahadi ya kale ambayo hunifariji sana. [Soma Ufunuo 21:4.] Bila shaka, wakati huo haujafika bado, lakini ufikapo, tungependa kuuona, sivyo?” Halafu utoe kichapo kinachoeleza jinsi ambavyo kuteseka kutakavyokwisha.
6 Kwa mtu mwenye umri mkubwa zaidi waweza kusema:
◼ “Labda unahangaishwa kama mimi na wingi wa mawazo yaliyopotoka na matokeo yake ambayo yanaathiri watoto wetu. Kwa nini kuna ongezeko kubwa la ukosefu wa adili miongoni mwa vijana? [Ruhusu jibu.] Je, ulipata kujua kwamba hali hiyo ilitabiriwa katika kitabu kilichoanza kuandikwa zamani sana kabla ya kuanzishwa kwa Uislamu, Ukristo, na Uhindu? [Soma 2 Timotheo 3:1-3.] Ona kwamba hali hizi zaendelea kuwapo ijapokuwa elimu inaendelea kuongezeka. [Soma mstari wa 7.] Kichapo hiki kilinisaidia kuelewa kweli ambayo watu wengi sana hawajui. Je, ungependa kukisoma?” Toa kitabu au broshua ifaayo.
7 Kwa kawaida Wabudha hustahi Biblia kuwa maandishi matakatifu. Kwa hiyo isome moja kwa moja. (Ebr. 4:12) Ikiwa hapendelei uvutano wa tamaduni za Magharibi, mtajie kwamba waandikaji wote wa Biblia walikuwa Waesia.
8 Ni Vichapo Gani Ambavyo Huwa na Matokeo Zaidi? Trakti iliyochapishwa hasa kwa ajili ya Wabudha, Will Suffering Ever End? imechapwa katika lugha za Kichina, Kijapani, Kisinhale, na Kithai. Kwa kuongezea, wahubiri wengi wamefanikiwa kutumia fasihi zifuatazo: vitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, na Siri ya Kupata Furaha ya Familia; broshua Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai—Wewe Waweza Kulipataje?, na “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”; na kama bado yapatikana trakti Habari za Ufalme Na. 35, Je, Watu Wote Watapata Kupendana? Wabudha wengi ambao sasa wanajifunza kweli wanajifunza broshua Anataka kwanza kisha kitabu Ujuzi.
9 Ijapokuwa inasemekana kwamba wamishonari Wabudha walifika Athene karibu miaka 400 kabla ya Paulo kuhubiri huko, haijulikani kwa uhakika kama alikutana na mtu aliyefuata mafundisho ya Budha. Hata hivyo, twajua jinsi ambavyo Paulo alihisi kuhusu kuhubiria watu wa aina zote. Alijifanya kuwa “mtumwa kwa wote” ili ‘apate kwa vyovyote kuokoa wengine.’ (1 Kor. 9:19-23) Twaweza kufanya vivyo hivyo kwa kupendezwa kibinafsi na watu na kwa kukazia tumaini tulilo nalo sote tunapomtolea ushahidi kila mtu tunayekutana naye.