Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 7/15 kur. 21-23
  • ‘Lakini Mimi Sipendi Yehova!’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Lakini Mimi Sipendi Yehova!’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Moyo, Dhamiri, na Imani
  • Yawezekana Kupona
  • Jinsi Wengine Wawezavyo Kusaidia
  • Mrudishie Yehova Moyo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Jipatie Moyo Unaompendeza Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kuazimia Kumtumikia Yehova kwa Moyo Kamili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Kumwendea Daktari wa Moyo Aliye Hodari Kupita Wote Nyakati Zetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 7/15 kur. 21-23

‘Lakini Mimi Sipendi Yehova!’

BOB alikuwa kivulana tu mama yake alipopata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa miaka kadhaa, aliandamana naye kwenye Jumba la Ufalme na hata katika kazi ya kuhubiri, ingawa hakubatizwa kamwe. Hata hivyo, alipofikia miaka ya utineja, aliacha kushirikiana na Mashahidi. Aliharibu kabisa maisha yake kwa kujikwaa-kwaa katika hali za mabaya mbalimbali. Ingawa angali anadai kuamini mengi ya mambo aliyojifunza kutokana na Biblia, jambo hili halijatosha kumfanya atake kurudia tengenezo la Yehova. Kwa nini Bob anahisi hivi?

Fikiria kielelezo kingine. David alikuwa amekuwa mhudumu wa wakati wote kwa miaka kadhaa. Pindi kwa pindi, masuala yalimpita-pita akilini kuhusu mafundisho fulani ya Biblia. Lakini sikuzote alitatua matatizo hayo kwa kusababu ya kwamba kama vile ilivyo katika kufaulu kuunda umbo la kitu katika mchezo wa kuunganisha vijipande vilivyotenganishwa, mtu hachoki na kuacha eti kwa sababu kijipande kimoja au viwili haviingiani hapo kwanza. Yeye aliridhika kumngojea Yehova ili apate uelewesho. Lakini muda si muda, David alidai kwamba hakuweza kuridhika tena kungojea. Kwa kujiuzulu mapendeleo yake ya utumishi, upesi aliuacha ukweli. Ni nini kilichobadili kufikiri kwake?

Kwa uhakika, inavunja moyo kuwaona wapendwa wetu wakichoka na kuiacha mbio ya uhai. Bila shaka, sisi tunataka kufanya yote tuwezayo tuwasaidie. (2 Wakorintho 12:15; Wagalatia 5:7) Lakini ni nini hasa husababisha mtu aangukie mbali kutoka kwenye ukweli? Jambo gani laweza kufanywa kusaidia mtu huyo arudi mbioni? Na mtu apaswa kufanya nini maelekeo hayo yakianza kusitawi ndani yake?

Moyo, Dhamiri, na Imani

Kuna jambo moja lenye kustahili kuangaliwa juu ya wale ambao wameacha ukweli. Walio wengi hawafanyi hivyo kwa sababu hawaamini tena ndio ukweli. Tofauti na hivyo kabisa, wengi wao husema, “Najua huu ndio ukweli, lakini . . . “au, “Ikiwa kuna ukweli wowote, mimi najua kwamba ndio huu.” Mle ndani kwenye kina cha mioyo yao, wengi wao wangali wanaamini kwamba yale ambayo wamejifunza kutokana na Biblia ndio ukweli. Lakini kwa njia fulani wamelegeza mkono wao na kupoteza bidii yao. Yakobo alisema: “Imani pasipo matendo imekufa.” —Yakobo 2:26.

Imani ya kweli yahusisha mengi kuliko kuwa tu na maarifa au kuamini kwamba jambo fulani ni kweli. Badala ya kuwa utaratibu fulani wenye kutendeka akilini tu, imani yahusisha moyo wa kitamathali, kwa maana Biblia yatuambia: “Kwa moyo mtu hujizoeza imani kwa ajili ya uadilifu.” (Warumi 10:10, NW) Basi, kwa sababu nzuri Biblia inaonyesha kwamba chanzo cha tatizo huwa moyo wakati mtu aanzapo kuacha njia inayofaa. Kama vile mtume Paulo alivyoonya: “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai.”—Waebrania 3:12.

Ili tupate ushuhuda wa kwamba moyo unahusika kwa kina kirefu, ingefaa tumsikilize Diane, aliyekuwa ameangukia mbali. Wakristo wenzake walipojaribu kumsaidia, yeye alitoa jibu hili la kutoboa wazi, “Siwezi kumrudia Yehova. Mimi simpendi!” Yeye alijua kwamba jambo moja tu ambalo lingemsaidia akae karibu na Yehova Mungu ni kumpenda kama Mtu na kama Mmoja anayeustahiki ujitoaji wake. Kwa uhakika, upendo wa aina hii ndio uliomsukuma kuweka maisha yake wakfu kwa Yehova hapo kwanza. Lakini kwa njia fulani hakuhisi akiwa tena na upendo huo. Alijua kwamba bila huo, kama angerudi angekuwa akifanya mambo kwa kujiburuta-buruta tu. Lakini mtu hupotezaje upendo aliokuwa akiuhisi kwa kina kirefu hivyo?

Basi, Paulo alitaja “moyo mbovu wa kutokuamini.” Katika visa fulani, ukosefu huo wa imani hutokana na kuruhusu moyo utamani kitu ambacho Yehova Mungu hukataza au kukinza jambo fulani analoamuru. Hivyo moyo hugawanyika na huwa si kamili tena kuelekea Yehova. Halafu, kwa kuhisi kwamba mwendo wa mtu haukubaliwi na Mungu, njia rahisi ya kuepuka mkabiliano zaidi huwa ni “kujitenga na Mungu aliye hai.” (Linganisha Mwanzo 3:8-10.) Badala ya kutubu, “moyo mbovu” husukuma mtu kufuta Yehova na kusudi lake kutoka maishani mwake. Hivyo mtu asiye na imani huchoka na kuuacha ukweli.

Katika visa vingine, badala ya kuteswa na michomo mikali ya dhamiri kwa sababu ya mwendo fulani, mtu huacha mwendo wake umsukume kwa hila kutafuta njia ya kiakili ya kujiponyosha kwa kutumia mashaka, kutafuta-tafuta makosa, au hata uasi-imani. Akiweza kujisadikisha kwamba muundo mzima wa imani yake una makosa, huwa hahisi tena wajibu wa kuishi ndani ya mipaka yao. Watu mmoja mmoja wa jinsi hiyo huitupilia kando dhamiri njema na ‘kuangamia kwa habari ya Imani.’—1 Timotheo 1:19.

Bila shaka, huenda mtu akachoka na kuacha ukweli kwa sababu nyingineyo. Lakini yoyote iwayo, karibu mara zote huwa yahusisha moyo. Kwa sababu hii, shauri hili ni la wakati unaofaa kweli kweli: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.”—Mithali 4:23.

Yawezekana Kupona

Ushujaa wahitajiwa ili kukubali wazi kwamba mielekeo yetu wenyewe ya kimakosa ndiyo iliyokuwa mzizi wa kupoteza imani yetu. Lakini kukubali hivyo ndiyo hatua ya kwanza kuelekea kujitengenezea njia ya kurudia uhusiano imara pamoja na Yehova. Alilojionea Steve, painia mmoja katika Uingereza, linatoa kielezi kizuri cha jambo hili.

Ingawa Steve hakupata kamwe kuanguka kutoka kwenye ukweli, wakati mmoja alianza kuhisi utupu na ukosefu wa usadikisho. Alipowahubiri wengine, maneno yake yalisikika matupu masikioni mwake mwenyewe. Steve alipokuwa miongoni mwa ndugu na dada zake wa kiroho, alihisi akikosa starehe, kana kwamba hakuwa mmoja wao.

Furaha kwa Steve ni kwamba, yeye alitambua kuwa ndiye mwenye tatizo. “Sikufanya lile kosa la kukaa mbali na wengine ili nifikirie mambo, kana kwamba kilikuwako chanzo fulani cha uvuvio ndani ya mnofu usiokamilika ambacho kingeandaa majibu yenye kufaa,” akumbuka Steve. (Linganisha Warumi 7:18.) Bali, aling’amua kwamba ni lazima apekue moyo wake na kuing’oa mizizi ya tamaa za udanganyifu zenye kumwongoza auache ukweli. Alianza na msingi wenyewe hasa, akajitahidi kuthibitisha upya upendo wake kwa Mungu na imani yake katika Neno Lake. Leo, Steve anatumikia kwa furaha akiwa misionari.

Jinsi Wengine Wawezavyo Kusaidia

Si kila mtu ambaye amepoteza au anapoteza mshiko wake imara juu ya ukweli huona mambo waziwazi kama vile Steve alivyoyaona. Kwa uhakika, mara nyingi upotezo huu wa mwono wazi wa kiroho ndio huongoza kwenye anguko la mwisho. Hapa ndipo Wakristo wenzi waweza kusaidia. (Warumi 15:1; Wagalatia 6:1) Lakini ni njia gani bora zaidi ambayo jambo hili laweza kufanywa?

Ni wazi kwamba haitoshi kumwalika au kumtia moyo mtu huyo arudi. Vipingamizi vyahitaji kutambuliwa na kuondolewa. Ni lazima jitihada zifanywe kuvutia moyo wa mtu huyo aliyedhoofika au akawa asiyetenda. Mazungumzo ya moyo kwa moyo, ya kutoboa wazi lakini yenye fadhili, huenda yakasaidia mtu huyo. Kutumia maandiko kama 1 Timotheo 1:19, Waebrania 3:12, na Yeremia 17:9, 10 huenda kukamsaidia kupekua mle chini kwenye kina cha moyo wake na kuona kinachosababisha ‘ajitenge na Mungu aliye hai.’

Visababishi vikiisha kutambuliwa, ni lazima jitihada zielekezwe kuvishughulikia. Moyo mgonjwa wa kimwili hutaka utunzaji na labda upasuaji wenye maumivu ili mgonjwa aponyoshe uhai wake. Ndivyo ilivyo kuhusu moyo ulio mgonjwa kitamathali. Tamaa mbaya, maelekeo ya kujitegemea, au mambo mengine yanayosababisha moyo upotoke ni lazima yaondolewe ili uwe wenye kuitikia tena. Hata ingeweza kufaa Wakristo watendaji wasali pamoja na mtu huyo asiye mtendaji, hata kujifunza naye Biblia ikiwa wazee wanaona inashaurika kufanya hivyo. Kwa njia hizo tu ndivyo moyo unavyoweza kurudishwa katika hali inayofaa na mtu yule aje kumpenda tena Yehova.—Mithali 2:1-5.

Hivi ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha Diane. Mazungumzo pamoja na Wakristo wakomavu yalimsaidia kutambua alilohitaji kufanya ili kuamsha upya upendo wake kwa Yehova. Aking’amua kwamba ilikuwa lazima apate kumjua Yehova tena kindani, Diane alikubali msaada uliotolewa. Baada ya kujifunza Biblia kwa karibu mwaka mmoja, yeye na mume wake wakawa tena wasifaji wa Yehova wenye kutenda.

Kwa kuwa upendo wahusisha kitendo, mara nyingi jambo ambalo huthibitika kusaidia zaidi ni kufanya yanayosemwa na Yehova na kujionea mwenyewe msaada wake wenye upendo. Ndiyo, utendaji husaidia mtu apate upya upendo uliosukuma moyo wake hapo kwanza. (Zaburi 34:8) Huenda jambo hili likaanza na kuchukua hatua za utendaji ili kupambana na tamaa zenye makosa au kusahihisha maelekeo yasiyofaa ya moyo. Kila ushindi unaopatikana katika pigano hili ni hatua moja ya kukaribia zaidi kuurudisha moyo kwa Yehova. (Mithali 23:26; 1 Petro 2:1-3) Kwa kadiri moyo unavyozidi kuvutwa, ndivyo inavyozidi kukua tamaa ya kushiriki na wengine yaliyomo. Kwa sababu hiyo, mara tu wale waliokuwa wahubiri wa Ufalme wasio watendaji wakiisha kustahili, yapasa wasaidiwe kushiriki katika kazi ya kuhubiri, kwa maana “kwa moyo mtu hujizoeza imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanyiza tangazo la peupe kwa ajili ya wokovu.” —Warumi 10:10, NW.

Kwa wowote ambao huhisi kwamba hawampendi tena Yehova, barabara ya kurudia maisha ya kimungu huenda ikawa ndefu na ngumu. Hata hivyo, mapono ya kiroho ya Steve na ya Diane ni ushuhuda wa kwamba badiliko la moyo linaweza kutukia. Ndiyo, kurudia hali ya kwanza kwawezekana kupitia kazi inayotendwa na roho ya Yehova, utumizi wa Neno lake, na kufanya upya ushirikiano pamoja na tengenezo lake. Sisi tunatumaini na kusali kwa moyo mweupe kwamba watu hao wanaweza kusaidiwa washangilie tena katika ibada ya Yehova na utumishi mtakatifu kama wale wanaompenda Yehova kwa moyo mzima.—Marko 12:30; 1 Wakorintho 13:8; 3 Yohana 1-4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki