Je! Helo Ina Moto?
“KWENYE hatua fulani katika miaka ya sitini ya karne hii, Helo ilitoweka.” Ndivyo alivyosema mtungaji Mwingereza David Lodge katika kitabu chake Souls and Bodies, na maneno yake yaonyesha kufikiri kwa Wakatoliki na Waprotestanti wengi wakati wa miongo iliyofuata vita ya ulimwengu ya pili. Kwa muda, mengi ya makanisa yale makubwa-makubwa yalipunguza ufundishaji wa fundisho lao rasmi la helo yenye moto yakiwa katika jitihada za kujipatanisha na violezo vya fikira za ki-siku-hizi.
Wazo la kuadhibiwa baada ya kufa lilikuwa halikubaliki kwa watu hasa kwa sababu wazo la dhambi yenyewe lilipata kuwa lisiloeleweka katika akili zao. Alipohojiwa katika 1984, Ratzinger Kardinali Mroma alisema: “Mwerevuko wetu... wakaza fikira juu ya hali zinazopunguza uzito wa makosa na kutetea uhaki wayo kwa jaribio la kufanya watu wawe bila hisia ya kujali kuwa na hatia, kuwa na dhambi . . . , ambayo ndicho kitu halisi chenye kuhusianishwa na helo na Pargatori.”
Je! leo yawezekana kuamini kwamba dhambi ni kitu halisi bila kulikubali fundisho la adhabu baada ya kifo katika pargatori na helo? Kitabu cha hivi majuzi, Abrege de la foi catholique (Muhtasari wa Imani ya Kikatoliki), kilichofanyiwa dibaji na Decourtray Kardinali Mfaransa, kiliuliza swali hilo kinaganaga kabisa: “Je! yahitajiwa kabisa kuiamini helo?” Jibu likawa: “Haiwezekani kuliepa suala hilo la kuogopesha sana kuhusu helo.” Kichapo Vatican Council II —More Postconciliar Documents (1982) chanukuu “Itikadi ya Watu wa Mungu” kuwa ikitaarifu hivi: “Sisi twaamini . . . [kwamba] wale ambao wameitikia upendo na huruma ya Mungu wataingia katika uhai wa milele. Wale ambao wamezikataa watapewa fungu la kuwa kwenye moto usiozimwa kamwe.”
Kwa hiyo, zijapokuwako jitihada zote za kitheolojia kuthibitisha vingine, moto wa helo ungali sana ni sehemu ya fundisho rasmi la Kikatoliki ambalo lashikiliwa kishupavu. Hata hivyo A New Dictionary of Christian Theology (1983) yanena juu ya “aibu” na “ukosefu wa starehe” ambao fundisho la laana ya milele husababishia washiriki wengi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo leo. Wao hutatizwa kupatanisha fundisho hili la ushupavu pamoja na lile wazo la Mungu wa upendo. Wao hujiuliza hivi kwa mshangao: ‘Je! kweli helo yenye moto ni fundisho la Kikristo na la Kibiblia? Ikiwa sivyo, lilianzia wapi?’
[Picha katika ukurasa wa 3]
Bourges Cathedral, France