Asili ya Helo
“HELO,” chaeleza New Catholic Encyclopedia, ndilo neno ambalo “hutumiwa kumaanisha mahali pa waliolaaniwa milele.” Ensaiklopedia moja ya Kiprotestanti yafafanua helo kuwa “mahali pa adhabu ya wakati ujao kwa waovu.”a Lakini imani katika mahali hapo pa adhabu baada ya kifo si ya makanisa yale makubwa-makubwa ya Jumuiya ya Wakristo tu. Ilianza karne nyingi kabla ya Jumuiya ya Wakristo kutokea.
Helo ya Mesopotamia
Miaka 2,000 hivi kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, Wasumeri na Wababuloni waliamini kuna ulimwengu wa chini ya ardhi ambao waliuita Bara Liendewalo Bila Kurudi. Imani hii ya kale yaonyeshwa katika mashairi ya Kisumeri na Kiakkadi yajulikanayo kuwa “Utenzi wa Gilgameshi” na “Kushuka kwa Ishtari Kwenda Kwenye Ulimwengu wa Chini ya Ardhi.” Mashairi hayo yaeleza kwamba makao haya ya wafu ni nyumba ya giza, “nyumba ambayo hakuna wowote walioiingia hutoka humo.”
Kuhusu hali zilizomo, andishi la kale la Kiashuri linataarifu kwamba “ulimwengu huo wa chinichini ulijawa na hofu kuu.” Mwana-mfalme Mwashuru aliyesemwa kuwa alionyeshwa makao haya ya wafu yaliyo chini ya ardhi alishuhudia kwamba “miguu [yake] ilitetemeka” kwa sababu ya mambo aliyoona. Akieleza juu ya Nergal, yule mfalme wa ulimwengu wa chini ya ardhi, aliandika hivi: “Yeye alinipigia ukelele mkali wa hasira kuu.”
Dini za Misri na Mashariki
Wamisri wa kale waliamini kutokufa kwa nafsi, na walikuwa na wazo lao wenyewe juu ya ulimwengu wa baada ya kifo. The New Encyclopcedia Britannica yataarifu hivi: “Maandishi ya maziko ya Wamisri yaonyesha njia ya kwenda kwenye ulimwengu ufuatao kuwa; yenye kujawa na hatari za kutisha: madubwana ya kutia hofu, maziwa ya moto, malango yasiyoweza kupitwa isipokuwa kwa kutamka mizungu ya kiuchawi, na mwendesha-kivuko mkorofi ambaye kusudio lake ovu ni lazima lizuiliwe kwa mizungu ya kiuchawi.”
Dini za Wahindi-Wairani zilisitawisha imani mbalimbali kuhusu adhabu baada ya kifo. Kwa habari ya dini ya Kihindu, Encyclopcedia Universalis (Ensaiklopedia ya Ulimwengu Wote Mzima) ya Kifaransa yataarifu hivi: “Kuna maelezo yasiyohesabika kuhusu zile helo 21 zenye kuwaziwa na Wahindu. Watenda dhambi humezwa na hayawani-mwitu na nyoka, huchomwa moto kwa jitihada nyingi, hukatwa visehemu-sehemu kwa msumeno, huteswa-teswa na kiu na njaa, huchemshwa katika mafuta, au husagwa-sagwa wawe poda katika vyombo vya chuma au vya jiwe.”
Dini ya Jaini na ya Kibuddha, zote mbili zina fasiri zazo kuhusu helo, ambamo watenda dhambi wasiosikitika huteswa-teswa. Dini ya Zoroasta, iliyoanzishwa katika Iran, au Uajemi, ina helo fulani pia—mahali penye baridi na mnuko mbaya ambapo nafsi za watenda dhambi huteswa-teswa.
Kwa kupendeza, ingeonekana kwamba mateso-mateso yaliyo katika helo ya fasiri za Kimisri, Kihindu, Kijaini, Kibuddha na Kizoroasta si ya milele. Kulingana na dini hizi, baada ya kipindi cha kuteseka, nafsi za watenda dhambi husonga mbele kwenye mahali au hali nyingine, ikitegemea wazo la dini hususa kuhusu tukio la mwisho kwa mwanadamu. Mawazo yao kuhusu helo yafanana na pargatori ya Ukatoliki.
Helo za Kigiriki, Kietruska, na Kiroma
Wagiriki wa kale waliamini kwamba nafsi (psy·kheʹ, neno ambalo walilitumia pia kwa kipepeo) huendelea kuishi baada ya kifo. Waliiita Hadesi makao ya wafu na wakaamini kwamba ilitawalwa na mungu mwenye jina ilo hilo. Katika kitabu chake Orpheus—A General History of Religions, mwanachuo Mfaransa Salomon Reinach aliandika hivi kuhusu Wagiriki: “Imani yenye kuenea sana ilikuwa kwamba [nafsi] iliingia majimbo yenye moto mkali baada ya kuuvuka mto Styx katika mashua ya Charon mwendesha-kivuko wa zamani, aliyetoza nauli ya [sarafu] obolusi, iliyowekwa katika kinywa cha mtu yule mfu. Katika majimbo yenye moto mkali ilienda mbele ya wale mahakimu watatu wa mahali hapo . . . ; ikiwa ilishutumiwa kwa matendo yayo ya uhalifu, ilikuwa lazima iteseke katika Tartaro. . . . Wagiriki hata walivumbua Limbo moja, yale makao ya watoto waliokufa katika utoto mchanga, na Pargatori moja, ambapo adhabu fulani iliyo pole ilizitakasa nafsi.” Kulingana na The World Book Encyclopedia, nafsi zilizoishia Tartaro “zilipatwa na mteseko-teseko wa milele.”
Katika Italia Waetruska, ambao mwerevuko wao ulitangulia ule wa Waroma, waliamini pia kuna adhabu baada ya kifo. Dictionnaire des Religions (Kamusi ya Dini) yataarifu hivi: “Utunzaji mwingi sana ambao Waetruska waliwafanyia wafu wao waelezwa na wazo lao kuhusu yale majimbo ya chinichini. Kama Wababuloni, wao walipafikiria hapa kuwa mahali pa kuteseka-teseka na kukata tamaa kwa roho za wafu. Kitulizo cha pekee kwao kingeweza kupatikana kutokana na matoleo ya upatanisho yenye kufanywa na wazao wao.” Kichapo kingine cha marejezo chajulisha wazi hivi: “Makaburi ya Waetruska yaonyesha tamasha za maogofyo makubwa yaliyofanya kutokee michoro ya Kikristo kuhusu helo.”
Waroma walichagua kufuata ile helo ya Kietruska, wakiiita Orkusi au Infernusi. Pia waliazima hadithi za ubuni wa Kigiriki kuhusu Hadesi, yule mfalme wa ulimwengu wa chini ya ardhi, wakimwita Orkusi, au Pluto.
Wayahudi na Maandiko ya Kiebrania
Namna gani juu ya Wayahudi kabla ya siku ya Yesu? Kwa habari yao, twasoma hivi katika Encyclopcedia Britannica (1970): “Kuanzia karne ya 5 K.K. na kuendelea, Wayahudi walikuwa katika mwonano wa karibu-karibu pamoja na Waajemi na Wagiriki, wote wawili wakiwa na mawazo yaliyositawishwa sana kuhusu maisha ya baada ya kifo. . . . Kufikia wakati wa Kristo, Wayahudi walikuwa wamejipatia imani ya kwamba nafsi mbovu zingeadhibiwa katika Gehena baada ya kifo.” Hata hivyo, Encyclopcedia Judaica yataarifu hivi: “Hakuna dokezo lolote la wazo hili la baadaye kuhusu Gehena hupatikana katika Andiko.”
Taarifa hii ya mwisho ni sahihi. Hakuna dokezo lolote katika Maandiko ya Kiebrania kuhusu kuadhibiwa kwa nafsi katika moto wa helo baada ya kufa. Fundisho hili la kuogopesha sana ni la tangu kule nyuma kwenye dini za Babulonia zilizotokea baada ya Gharika, wala si la Biblia. Fundisho la Jumuiya ya Wakristo kuhusu kuadhibiwa katika helo lilianza na Wababuloni wa mapema. Lile wazo la Kikatoliki kuhusu kuteseka katika pargatori ili kupata ondoleo la dhambi ni la tangu kule nyuma kwenye dini za mapema za Misri na Mashariki. Limbo iliigwa kutokana na hadithi ya ubuni wa Kigiriki. Sala na matoleo kwa ajili ya wafu zilikuwa zoea la Waetruska.
Lakini ni nini msingi wa mafundisho haya ya mtu kuadhibiwa akiwa na fahamu zake baada ya kifo?
[Maelezo ya Chini]
a Cyclopcedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature ya M’Clintock na Strong, Buku 4, ukurasa 165.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kuuvuka Styx kama kulivyoelezwa katika “Inferno” ya Dante
[Hisani]
Dover Publications, Inc.