Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 11/15 kur. 4-6
  • Amri Kumi Zina Maana Gani Kwako Wewe?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Amri Kumi Zina Maana Gani Kwako Wewe?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jambo Ambalo Yale Maneno Kumi Yalimaanisha kwa Israeli
  • Maoni Yaliyorekebishwa
  • Maana Yazo Kwetu
  • Je! Tuko Chini ya Zile Amri Kumi?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Zile Amri Kumi za Mungu Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Sabato
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Sheria ya Upendo Katika Mioyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 11/15 kur. 4-6

Amri Kumi Zina Maana Gani Kwako Wewe?

KATIKA muda wa miezi mitatu baada ya wao kukombolewa kutoka Misri katika 1513 K.W.K., Waisraeli walipiga kambi mbele ya Mlima Sinai jangwani. Kwa kuitwa na Yehova, nabii Musa alipanda mlima huo na kusikia ahadi ya Mungu kwamba Yeye angelifanya taifa la Israeli liwe ‘mali Yake ya pekee kati ya jamii zote za watu.’ Ndipo Musa alipowapasha watu habari hizi kupitia wanaume wazee wa taifa. “Baada ya hayo watu wote wakajibu kwa sauti moja na kusema: ‘Yote ambayo Yehova amenena sisi tuna nia ya kuyafanya.’”—Kutoka 19:1-8, NW.

Bada ya hapo, Mungu alitaarifu wazi Amri Kumi kwa Musa, akitoa dibaji ya sheria hizi kwa elezo hili: “Mimi ni Bwana [Yehova, NW], Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa.” (Kutoka 20:2) Hili Fungu la Maneno Kumi lilikuwa kwa ajili ya Waisraeli, walioambiwa hivi katika Amri ya Kwanza: “Usiwe na miungu mingine ila mimi.”—Kutoka 20:3.

Kufuata hapo, Yehova alimpa Musa maagizo katika amri nyingine za kimungu kwa Israeli. (Kutoka 20:4–23:19) Zote pamoja, zilijumlika kuwa sheria kama 600. Nao ulikuwa msisimuko ulioje kung’amua kwamba malaika wa Mungu alikuwa akienda mbele ya taifa ili kutayarisha njia ya kuingia katika Bara la Ahadi! (Kutoka 23:20-22) Yehova alijulisha wazi hivi: “Mimi nitafanya mbele ya watu wako wote mambo ya ajabu ambayo hayajafanyizwa kamwe katika dunia yote wala miongoni mwa mataifa yote; na watu wote ambao wewe upo katikati yako wataiona kazi ya Yehova, kwa sababu ni jambo lenye kuvuvia hofu ambalo mimi ninafanya kwa habari ya nyinyi.” Mungu alitaka watu wake nao wamrudishie nini? “Wewe nawe kwa sehemu yako shika jambo ambalo mimi ninakuamuru leo.” Ndiyo, utii kwa sheria na miongozo yote ya Yehova uliamrishwa.—Kutoka 34:10, 11, NW.

Jambo Ambalo Yale Maneno Kumi Yalimaanisha kwa Israeli

Kutokana na kukimbia kwao kutoka kwenye utumwa wa Kimisri wakiwa wamelindwa na Mungu, Waisraeli walikuja kujua jina la Mungu katika maana mpya. Yehova alikuwa amekuwa Mkombozi wao. (Kutoka 6:2, 3) Kwa hiyo, ile amri ya tatu ikawa na maana ya pekee kwao, kwa kuwa kwa njia hiyo walikatazwa kulichukua jina la kimungu kwa njia isiyostahiki.—Kutoka 20:7.

Lakini namna gani kuhusu ile amri ya nne, ambayo yahusiana na siku ya Sabato? Amri hii ilikazia kustahi mambo matakatifu, kama vile Yehova alivyokuwa ameonyesha alipokuwa akianzisha “mwadhimisho wa sabato” kuhusiana na kukusanya mana. (Kutoka 16:22-26) Kwa sababu Waisraeli fulani hawakutii haraka, Yehova aliwakumbusha wazi kwamba yeye ndiye alikuwa amewapa agizo hilo. “‘Ukumbukeni vizuri uhakika wa kwamba Yehova ndiye amewapa nyinyi ile sabato.’ . . . Na watu wale wakafuliza kushika sabato siku ya saba.” (Kutoka 16:29, 30, NW) Baadaye, Yehova alionyesha jinsi mpango huu usivyohusisha wengine ndani, akitaarifu hivi: “Ni ishara kati ya mimi na wana wa Israeli kwa wakati usio dhahiri.”—Kutoka 31:17, NW.

Halafu, fikiria ile amri ya kumi isiyofanana na nyinginezo, yenye kukataza tamaa yenye choyo. Hii hapa ni sheria ambayo hakuna mwanadamu angeweza kuifikiliza. Kila Mwisraeli alikuwa na wajibu wa kumtolea hesabu Mungu wake, Yehova, aliyepekua moyo wa mtu mmoja mmoja ili agundue makusudio yake.—Kutoka 20:17; 1 Samweli 16:7; Yeremia 17:10.

Maoni Yaliyorekebishwa

Yesu Kristo, aliyezaliwa ndani ya taifa la Israeli, aliambia wanafunzi wake hivi: “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza.” (Mathayo 5:17) Paulo aliwaandikia hivi Wakristo Waebrania: “Ile Sheria ina kivuli cha mambo mema yenye kuja, lakini si uhalisi wenyewe wa mambo hayo.” (Waebrania 10:1, NW) Kama wewe ungalikuwa Mwebrania aliyeongolewa ukaja kwenye Ukristo, ungalielewaje maelezo haya? Washirika fulani wa kundi la mapema la Kikristo waliamini kwamba mamia yote ya sheria zile ambazo Mungu alitoa kupitia Musa, kutia na Amri Kumi, yangali yalitumika. Lakini je! hayo yalikuwa ndiyo maoni yafaayo?

Fikiria maneno haya ya Paulo kwa Wayahudi waliokuwa wamepata kuwa Wakristo katika mkoa wa Galatia: “Sisi tulio Wayahudi kwa asili, wala si wakosaji wa Mataifa, hali tukijua ya kuwa mwanadamu hahesabiwi haki [uadilifu, NW] kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu; sisi tulimwamini Kristo Yesu ili tuhesabiwe haki [uadilifu, AW] kwa imani ya Kristo, wala si kwa matendo ya sheria; maana kwa matendo ya sheria hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki [uadilifu, NW].” (Wagalatia 2:15, 16) Kwa kweli, kuwa na msimamo wa uadilifu pamoja na Mungu hakukutegemea kutii Sheria ya Musa, kwa maana jambo hilo lilikuwa haliwezekani katika hali ya kutokamilika kwa kibinadamu. Paulo aliongezea hivi: “Wale wote walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati, ayafanye. . . . Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu.”—Wagalatia 3:10-13.

Kama wafuasi wa Kiyahudi wa Yesu hawakuwa tena chini ya laana ya Sheria, je! Wakristo wowote walikuwa na wajibu wa kushika amri zote walizopewa Israeli? Paulo aliwaandikia hivi Wakolosai: “[Mungu] alitusamehe sisi makosa yetu yote na kufuta kabisa ile hati iliyoandikwa kwa mkono dhidi yetu, ambayo ilikuwa na maamuzi rasmi na ambayo ilikuwa na upinzani kwetu; na Yeye ameiondoa njiani kwa kuipigilia misumari kwenye mti wa mateso [wa Kristo].” (Wakolosai 2:13, 14, NW) Bila shaka, Wakristo wengi wa mapema walihitaji kurekebisha kufikiri kwao na watambue kwamba walikuwa wamefanywa ‘wakawa huru kutoka vifungo vya Sheria.’ (Warumi 7:6, HNWW) Kwa kujizoeza imani katika kifo cha dhabihu ya Yesu, ambacho kilikomesha ile Sheria na kutengeneza njia ya kuanzishwa kwa “agano jipya” lililotabiriwa, wao walikuwa na tazamio la kupata msimamo wa uadilifu pamoja na Yehova.—Yeremia 31:31-34; Warumi 10:4.

Maana Yazo Kwetu

Je! hii yamaanisha kwamba Amri Kumi, zikiwa sehemu ya msingi ya ile Sheria, zimeacha kabisa kuwa na maana yoyote kwa Wakristo? Sivyo hata kidogo! Ingawa hayo Maneno Kumi hayawafungi Wakristo katika wajibu wa kisheria, sheria hizi zaendelea kutoa miongozo timamu, hali moja na amri nyinginezo za Sheria ya Musa. Mathalani, Yesu alisema kwamba amri mbili zilizo kubwa zaidi ni zile zinazotaka kupenda Mungu na jirani. (Walawi 19:18; Kumbukumbu 6:5; Mathayo 22:37-40) Katika kushauri Wakristo Waroma, Paulo alinukuu amri ya sita, ya saba, ya nane, na ya kumi, akiongezea hivi: “Na ikiwapo amri nyingine yo yote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako.”—Warumi 13:8, 9.

Kwa hiyo, basi, Amri Kumi zatumika kwa kusudi gani leo zikiwa sehemu ya Neno la Mungu lililovuviwa? Zafunua maoni ya Yehova kuhusu mambo. (2 Timotheo 3:16, 17) Fikiria zafanya hivyo jinsi gani.

Amri nne za kwanza zakazia madaraka yetu kuelekea Yehova. (Ya Kwanza) Yeye ni Mungu ambaye bado atoza ujitoaji wa pekee. (Mathayo 4:10, NW) (Ya Pili) Hakuna yeyote wa waabudu wake apaswa kutumia mifano ya ibada. (1 Yohana 5:21) (Ya Tatu) Utumizi wetu wa jina la Mungu wapaswa kuwa ufaao na wenye heshima nyingi, si wenye utovu wa staha kamwe. (Yohana 17:26; Warumi 10:13) (Ya Nne) Maisha yetu yote yapasa yawe na tegemeo lenye kuzungukia mambo matakatifu. Hii yatuwezesha sisi kupumzika, au ‘tuchukue sabato,’ kutoka kwenye mwendo wa kujihesabia uadilifu.—Waebrania 4:9, 10, NW.

(Ya Tano) Utii wa watoto kwa wazazi wao waendelea kutumika ukiwa ndilo jiwe la pembeni la umoja wa jamaa, ukiambatana na baraka za Yehova. Nalo ni tumaini zuri kama nini ambalo latolewa na hii “amri ya kwanza yenye ahadi”! Sababu si kwamba tu “upate fanaka” bali pia ‘uishi miaka mingi duniani.’ (Waefeso 6:1-3, HNWW) Kwa kuwa sasa tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu uliopo ulio mwovu, utii huo wa kumcha Mungu watolea vijana tazamio la kutokufa kamwe.—2 Timotheo 3:1; Yohana 11:26.

Kupenda jirani kutatuzuia tusimsababishie madhara kupitia matendo maovu kama (Ya Sita) kuua mtu kimakusudi, (Ya Saba) uzinzi, (Ya Nane) kuiba, na (Ya Tisa) kusema taarifa zisizo za kweli. (1 Yohana 3:10-12; Waebrania 13:4; Waefeso 4:28; Mathayo 5:37; Mithali 6:16-19) Lakini namna gani juu ya makusudio yetu? Ile amri (Ya Kumi), iliyo dhidi ya tamaa yenye choyo, yatukumbusha kwamba Yehova ataka madhumuni yetu yawe manyoofu sikuzote machoni pake.—Mithali 21:2.

Lo, twapata maana nyingi kama nini katika Amri Kumi! Kwa kuwa zategemea kanuni za kimungu ambazo hazitakuwa kamwe kuu-kuu, yatupasa tuzithamini sana kama vikumbusha vyenye thamani kubwa sana kuhusu wajibu wetu wa kupenda Mungu na jirani yetu.—Mathayo 22:37-39.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kifo cha Yesu kilikomesha ile Sheria, kutia na Amri Kumi walizopewa Waisraeli kwenye Mlima Sinai

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki