Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • pe sura 24 kur. 203-207
  • Je! Tuko Chini ya Zile Amri Kumi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Tuko Chini ya Zile Amri Kumi?
  • Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KWA WAISRAELI KWA KUSUDI LA PEKEE
  • “KRISTO NDIYE MWISHO WA ILE SHERIA”
  • SHERIA ZINAZOWAHUSU WAKRISTO
  • Amri Kumi Zina Maana Gani Kwako Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Zile Amri Kumi za Mungu Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Je! Ni Vibaya Kufanya Kazi Siku ya Saba ya Juma?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Sheria ya Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
pe sura 24 kur. 203-207

Sura 24

Je! Tuko Chini ya Zile Amri Kumi?

1. Ni sheria gani ambayo Musa alitumiwa kupelekea watu?

NI SHERIA gani ambazo Yehova Mungu anataka tutii? Je! ni lazima tushike ile ambayo Biblia inaita “sheria ya Musa” au, mara nyingine “ile Torati”? (1 Wafalme 2:3; Tito 3:9, NW) Hiyo inaitwa vilevile “ile sheria ya Yehova,” kwa sababu ndiye aliyeitoa. (1 Mambo ya Nyakati 16:40, NW) Musa alitumiwa tu kupelekea watu Sheria hiyo.

2. Katika sheria hiyo zimo amri gani?

2 Ndani ya ile sheria ya Musa mna sheria au amri moja moja zaidi ya 600, kutia na zile 10 zilizo kubwa. Kama Musa alivyosema: “Yeye [Yehova] aliwaamuru ninyi kushika, hata amri kumi; naye akaziandika juu ya mabamba mawili ya mawe.” (Kumbukumbu la Torati 4:13; Kutoka 31:18, King James Version) Lakini Yehova aliwapa nani ile Sheria (Torati), kutia na zile Amri Kumi? Je! aliwapa wanadamu wote? Lilikuwa kusudi gani la Sheria hiyo?

KWA WAISRAELI KWA KUSUDI LA PEKEE

3. Tunajuaje kwamba Sheria hiyo walipewa Waisraeli peke yao?

3 Sheria hiyo hawakupewa wanadamu wote. Yehova alifanya agano, au mapatano na wale wazao wa Yakobo, ambao ndio waliokuja kuwa taifa la Israeli. Yehova alilipa taifa hilo peke yake sheria zake. Biblia inasema hivyo waziwazi katika Kumbukumbu la Torati 5:1-3 na Zaburi 147:19, 20.

4. Ni kwa sababu gani taifa la Israeli lilipewa Sheria hiyo?

4 Mtume Paulo aliuliza ulizo hili: “Kwa nini, basi, ile Sheria?” Ndiyo, ni kwa kusudi gani Yehova aliwapa Waisraeli sheria yake? Paulo anajibu: “Ili kufanya makosa yaonekane wazi, mpaka ule uzao upate kufika ambao kwao ile ahadi ilikuwa imefanywa . . . Kwa hiyo ile Sheria imekuwa mfundishaji wetu [au, mwalimu] wa kutuongoza kwa Kristo.” (Wagalatia 3:19-24, NW) Kusudi la pekee la Sheria hiyo lilikuwa kulinda na kuliongoza taifa la Israeli ili wapate kuwa tayari kumkubali Kristo afikapo. Dhabihu zile nyingi zilizotakwa na Sheria hiyo ziliwakumbusha Waisraeli kwamba walikuwa watenda dhambi waliohitaji Mwokozi.—Waebrania 10:1-4.

“KRISTO NDIYE MWISHO WA ILE SHERIA”

5. Kristo alipokuja akafa kwa ajili yetu, ikawaje na ile Sheria?

5 Bila shaka, Yesu Kristo alikuwa ndiye Mkombozi aliyeahidiwa, kama vile malaika alivyotangaza wakati wa kuzaliwa kwake. (Luka 2:8-14) Hivyo Kristo alipokuja akatoa uhai wake mkamilifu uwe dhabihu, ikawaje na ile Sheria? Iliondolewa. “Sisi hatuko tena chini ya mfundishaji,” Paulo akaeleza. (Wagalatia 3:25, NW) Kuondolewa kwa Sheria hiyo kulikuwa faraja kwa Waisraeli. Ilikuwa imewafunua kuwa watenda dhambi, maana wote walipungukiwa na kiwango cha kuishika Sheria hiyo kwa ukamilifu. “Kristo kwa ununuzi alitufungua sisi katika laana ya ile Sheria,” Paulo akasema. (Wagalatia 3:10-14, NW) Hivyo Biblia inasema hivi pia: “Kristo ndiye mwisho wa ile Sheria.”—Warumi 10:4; 6:14, NW.

6. (a) Matokeo yalikuwa nini juu ya Waisraeli na wasio Waisraeli wakati ile Sheria ilipokoma, na kwa sababu gani? (b) Ni hatua gani ambayo Yehova alichukua kuelekea Sheria hiyo?

6 Kwa hakika Sheria hiyo ilitumika kama kizuizi au “ukuta” kati ya Waisraeli na mataifa mengine ambao hawakuwa chini yake. Walakini, kwa kutoa uhai wake kuwa dhabihu, Kristo “alikomesha kabisa . . . ile Sheria ya amri nyingi ambamo mlikuwamo maagizo ya kisheria, ili apate kufanyiza yale makundi mawili ya watu [Mwisraeli na asiye Mwisraeli] katika kuungana na yeye mwenyewe kuwa mtu mpya mmoja.” (Waefeso 2:11-18, NW) Kwa habari ya hatua ambayo Yehova Mungu mwenyewe alichukua kuelekea sheria ya Musa, tunasoma: “Yeye kwa fadhili alitusamehe makosa yetu yote na kuifuta kabisa ile hati iliyoandikwa kwa mkono kutupinga sisi, ambayo ndani yake mlikuwa maagizo ya kisheria [kutia na zile Amri Kumi] na ambayo ilikuwa katika upinzani na sisi [kwa sababu ya kuwalaani Waisraeli kuwa watenda dhambi]; na Yeye ameiondoa njiani isiwe kizuizi kwa kuipigilia misumari kwenye mti wa mateso.” (Wakolosai 2:13, 14, NW) Hivyo, kwa ile dhabihu kamilifu ya Kristo, Sheria hiyo ilikomeshwa.

7, 8. Ni nini kinachohakikisha kwamba Sheria hiyo haikugawanywa katika sehemu mbili?

7 Walakini, watu fulani wanasema kwamba ile Sheria imegawanywa katika sehemu mbili: Zile Amri Kumi, na sheria zile nyingine. Wao wanasema kwamba sheria zile nyingine ndizo zilizokomeshwa, lakini zile Amri Kumi zimebaki. Lakini hiyo si kweli. Katika Mahubiri yake juu ya Mlima Yesu alitumia maneno fulani kutoka zile Amri Kumi na vilevile kutoka sehemu nyingine za ile Sheria. Yeye hakuweka tofauti kati yazo. Hivyo Yesu alionyesha kwamba ile sheria ya Musa haikugawanywa katika sehemu mbili.—Mathayo 5:21-42.

8 Angalia, pia, yale ambayo mtume Paulo aliongozwa na Mungu aandike: “Sasa sisi tumefunguliwa katika ile Sheria.” Je! Wakristo Wayahudi walifunguliwa watoke katika sheria zile nyingine tu, bila kufunguliwa katika Amri Kumi? Hapana, kwa maana Paulo anaendelea kusema: “Kwa kweli mimi nisingalipata kujua dhambi kama haingalikuwa ni kwa sababu ya ile Sheria; na, kwa mfano, nisingalijua kutamani kama ile Sheria haingalisema: ‘Haikupasi kamwe utamani,’” (Warumi 7:6, 7, NW; Kutoka 20:17) Kwa kuwa amri inayosema “haikupasi kamwe utamani” ndiyo ya mwisho ya zile Amri Kumi, ni wazi kwamba Waisraeli walifunguliwa katika zile Amri Kumi pia.

9. Ni nini kinachoonyesha kwamba sheria ya Sabato ya kila juma vilevile iliondolewa?

9 Je! maana yake ni kwamba ile sheria ya kushika Sabato ya kila juma, ambayo ndiyo ya nne ya zile Amri Kumi, vilevile iliondolewa. Ndivyo ilivyo. Yanayosemwa na Biblia katika Wagalatia 4:8-11 na Wakolosai 2:16, 17 yanaonyesha kwamba Wakristo hawako chini ya sheria ya Mungu waliyopewa Waisraeli, pamoja na matakwa yayo ya kushika Sabato ya kila juma na kushika siku nyingine za pekee mwakani. Ya kwamba Wakristo hawatakwi washike Sabato ya kila juma inaweza vilevile kuonwa kutokana na Warumi 14:5.

SHERIA ZINAZOWAHUSU WAKRISTO

10. (a) Wakristo wako chini ya sheria gani? (b) Nyingi za sheria hizo zilichukuliwa wapi, na kwa sababu gani ni jambo la akili kwamba zilichukuliwa huko?

10 Je! hiyo maana yake ni kwamba, kwa vile Wakristo hawako chini ya zile Amri Kumi, hawahitaji kushika sheria zo zote? Hata kidogo. Yesu alianzisha “agano jipya” likitegemea dhabihu iliyo bora ya uhai wake mwenyewe wa kibinadamu ulio mkamilifu. Wakristo wako chini ya agano jipya hilo na wanapaswa kushika sheria za Kikristo. (Waebrania 8:7-13; Luka 22:20) Nyingi za sheria hizo zimechukuliwa katika ile sheria ya Musa. Hilo si jambo lisilotazamiwa au lisilo la kawaida. Jambo kama hilo linatukia mara nyingi wakati serikali mpya inapochukua mamlaka ya kutawala nchi fulani. Huenda ile katiba ya serikali ya zamani ikafutwa na katiba mpya ikakaa mahali pa hiyo, lakini huenda katiba hiyo mpya ikafuata nyingi za zile sheria za katiba ya zamani. Kwa njia inayofanana na hiyo, lile agano la Sheria (Torati) lilikoma, lakini nyingi za sheria zake na kanuni za msingi ziliingizwa katika Ukristo.

11. Ni sheria ama mafundisho gani waliyopewa Wakristo zinazofanana sana na zile Amri Kumi?

11 Angalia uhakika wa jambo hilo unapozisoma zile Amri Kumi katika ukurasa 203, kisha uzilinganishe na sheria na mafundisho haya ya Kikristo yanayofuata: “Ni Yehova Mungu wako ambaye inakupasa kuabudu.” (Mathayo 4:10; 1 Wakorintho 10:20-22, NW) “Jilindeni wenyewe na sanamu.” (1 Yohana 5:21; 1 Wakorintho 10:14, NW) “Baba yetu uliye katika mbingu, acha jina lako litakaswe [lisichukuliwe kwa njia isiyofaa].” (Mathayo 6:9, NW) “Watoto, watiini wazazi wenu.” (Waefeso 6:1, 2) Nayo Biblia inaonyesha waziwazi kwamba kuua mtu kwa kukusudia, kufanya uzinzi, wivi, kusema uongo na kutamani ni makosa yanayopingana vilevile na sheria walizopewa Wakristo.—Ufunuo 21:8; 1 Yohana 3:15; Waebrania 13:4; 1 Wathesalonike 4:3-7; Waefeso 4:25, 28; 1 Wakorintho 6:9-11; Luka 12:15; Wakolosai 3.5

12. Ile kanuni ya sheria ya Sabato iliendelezwaje ikaingia katika mpango wa Kikristo?

12 Ijapokuwa Wakristo hawaamriwi kushika Sabato ya kila juma, tunajifunza jambo fulani kutokana na mpango huo. Waisraeli walipumzika kwa njia halisi, lakini Wakristo wanapaswa kupumzika kwa njia ya kiroho. Namna gani? Kwa sababu ya imani na utii, Wakristo wanaacha kufanya kazi za kichoyo. Kazi hizo za kichoyo ni pamoja na jitihada za kujiwekea uadilifu wao wenyewe. (Waebrania 4:10) Pumziko hilo la kiroho halishikwi siku moja tu kwa juma bali siku zote saba. Takwa lile la sheria ya Sabato halisi la kutenga siku moja kwa ajili ya faida za kiroho liliwalinda Waisraeli wasitumie kichoyo wakati wao wote wakitafuta faida zao wenyewe za kimwili. Kufuata kanuni hiyo kila siku kwa njia ya kiroho ni ulinzi unaofaa hata zaidi juu ya kupenda vitu vya kimwili.

13. (a) Ni sheria gani ambayo Wakristo wanasihiwa waitimize, nao wanaitimizaje? (b) Ni sheria gani ambayo Yesu alikazia? (c) Ni sheria gani iliyo msingi wa sheria nzima ya Musa?

13 Hivyo Wakristo wanahimizwa ‘kuitimiza ile sheria ya Kristo,’ badala ya kuzishika zile Amri Kumi. (Wagalatia 6:2) Yesu alitoa amri na maagizo mengi, na kwa kutii amri na maagizo hayo tutakuwa tunashika au kutimiza sheria yake. Hasa, Yesu alikazia umaana wa upendo. (Mathayo 22:36-40; Yohana 13:34, 35) Ndiyo, kupenda wengine ni sheria ya Kikristo. Ndio msingi wa sheria yote ya Musa, kama Biblia isemavyo: “Ile Sheria yote inasimama ikiwa imetimizwa katika usemi mmoja, yaani: ‘Lazima wewe umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”—Wagalatia 5:13, 14; Warumi 13:8-10, NW.

14. (a) Tutapata faida gani kwa kujifunza na kuzifuata kanuni za sheria ya Musa? (b) Upendo utatuongoza tufanye nini?

14 Ile sheria iliyotolewa kupitia Musa, pamoja na Amri Kumi za sheria hiyo, ilikuwa fungu la sheria zenye uadilifu kutoka kwa Mungu. Na hata kama hatuko chini ya sheria hiyo leo, zile kanuni za kimungu zinazoitegemeza bado ni zenye faida kubwa kwetu. Kwa kujifunza kanuni hizo na kuzifuata tutazidi kumthamini yule Mpaji-sheria mkuu Yehova Mungu. Lakini hasa imetupasa tujifunze na kufuata katika maisha zetu sheria na mafundisho ya Kikristo. Kumpenda Yehova kutatuongoza tutii yote anayotutaka tuyafanye sasa.—1 Yohana 5:3.

[Sanduku katika ukurasa wa 203]

ZILE AMRI KUMI

1. “Mimi ni Yehova Mungu wako . . . haikupasi kamwe uwe na miungu mingine yo yote mbele za uso wangu.

2. “Haikupasi kamwe ujifanyie mwenyewe mfano wa kuchongwa wala umbo lililo kama kitu cho chote kilicho katika mbingu juu au kilicho duniani chinichini au kilicho katika maji chini ya dunia. Haikupasi kamwe uviinamie wala kushawishwa kuvitumikia.

3. “Haikupasi kamwe ulichukue jina la Yehova Mungu wako kwa njia isiyofaa . . .

4. “Ukiikumbuka siku ya sabato kuiona kuwa takatifu, inakupasa kutoa utumishi na kufanya kazi yako siku sita. Lakini ile siku ya saba ni sabato kwa Yehova Mungu wako. Haikupasi ufanye kazi yo yote, wewe wala mwana wako wala binti yako.

5. “Heshimu baba yako na mama yako ili siku zako zipate kuwa ndefu juu ya ardhi ambayo Yehova Mungu wako anakupa wewe.

6. “Haikupasi kamwe kuua mtu kwa kukusudia.

7. “Haikupasi kamwe ufanye uzinzi.

8. “Haikupasi kamwe uibe.

9. “Haikupasi kamwe ushuhudie uongo ukiwa shahidi juu ya mwanadamu mwenzako.

10. “Haikupasi kamwe utamani nyumba ya mwanadamu mwenzako. Haikupasi kamwe utamani mke wa mwanadamu mwenzako, wala mtumwa wake mwanamume wala kijakazi wake wala ng’ombe dume wake wala punda wake wala cho chote kilicho mali ya mwanadamu mwenzako.”—Kutoka 20:2-17, NW.

[Picha katika ukurasa wa 204, 205]

TIle Sheria ilitumika kuwa ukuta kati ya Waisraeli na mataifa yale mengine

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki