Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 9/1 kur. 14-19
  • Sheria ya Kristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sheria ya Kristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Agano Jipya
  • Sheria Iliyo ya Uhuru
  • Yesu na Mafarisayo
  • Je, Sheria ya Kristo Ni Yenye Uendekevu?
  • Jumuiya ya Wakristo Yachafua Sheria ya Kristo
  • Kujifunza Kutokana na Makosa ya Jumuiya ya Wakristo
  • Sheria ya Kabla ya Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • “Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”
    Mkaribie Yehova
  • Je! Tuko Chini ya Zile Amri Kumi?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 9/1 kur. 14-19

Sheria ya Kristo

“Nalikuwa . . . mwenye sheria mbele za Kristo.”—1 WAKORINTHO 9:21.

1, 2. (a) Mengi ya makosa ya wanadamu yangeweza kuepukwaje? (b) Jumuiya ya Wakristo ilishindwa kujifunza nini kutokana na historia ya Dini ya Kiyahudi?

“WATU na serikali hawajajifunza kamwe chochote kutokana na historia, wala kutenda kulingana na kanuni zilizopatikana kwayo.” Ndivyo alivyosema mwanafalsafa Mjerumani wa karne ya 19. Kwa kweli, mwendo wa historia ya kibinadamu umefafanuliwa kuwa “mfuatano wa makosa,” mfululizo wa makosa na taabu zisizopendeza, ambazo nyingi zazo zingaliepukwa ikiwa tu wanadamu wangalikuwa tayari kujifunza kutokana na makosa yaliyopita.

2 Kukataa huko-huko kujifunza kutokana na makosa ya wakati uliopita kwaonyeshwa katika mazungumzo haya ya sheria ya kimungu. Yehova Mungu aliweka sheria iliyo bora zaidi badala ya ile Sheria ya Kimusa—sheria ya Kristo. Hata hivyo, viongozi wa Jumuiya ya Wakristo, wanaodai kufundisha na kuishi kulingana na sheria hiyo, wameshindwa kujifunza kutokana na makosa mabaya sana ya Mafarisayo. Hivyo Jumuiya ya Wakristo imepinda na kutumia vibaya sheria ya Kristo sawa na vile Dini ya Kiyahudi ilivyoifanya Sheria ya Musa. Hilo lingewezekanaje? Kwanza, acheni tuizungumzie sheria hii yenyewe—hiyo ni nini, ni nani inaowaongoza na jinsi gani, na ni nini kinachoitofautisha na Sheria ya Kimusa. Kisha tutachunguza jinsi Jumuiya ya Wakristo imeitumia vibaya. Na tujifunze kwa njia hiyo kutokana na historia na kufaidika nayo!

Agano Jipya

3. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu agano jipya?

3 Isipokuwa Yehova Mungu, ni nani mwingine ambaye angeweza kuboresha Sheria iliyo kamilifu? Agano la Sheria ya Kimusa lilikuwa kamilifu. (Zaburi 19:7) Hata hivyo, Yehova aliahidi hivi: “Angalia, siku zinakuja, . . . nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao.” Amri Kumi—kitovu cha Sheria ya Kimusa—ziliandikwa juu ya mabamba ya mawe. Lakini kuhusu agano jipya, Yehova alisema hivi: “Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika.”—Yeremia 31:31-34.

4. (a) Ni Israeli jipi linalohusika katika agano jipya? (b) Ni nani wengine zaidi ya Waisraeli wa kiroho walio chini ya sheria ya Kristo?

4 Ni nani ambao wangeingizwa katika agano hilo jipya? Bila shaka si “nyumba ya Israeli” halisi, iliyomkataa Mpatanishi wa agano hilo. (Waebrania 9:15) La, “Israeli” jipya lingekuwa “Israeli wa Mungu,” taifa la Waisraeli wa kiroho. (Wagalatia 6:16; Warumi 2:28, 29) Kikundi hicho kidogo cha Wakristo watiwa-mafuta kwa roho kingeungwa baadaye na “mkutano mkubwa” kutoka kwa mataifa yote ambao ungejitahidi pia kumwabudu Yehova. (Ufunuo 7:9, 10; Zekaria 8:23) Ingawa hawashiriki katika agano jipya, wao pia wangekuwa chini ya sheria. (Linganisha Mambo ya Walawi 24:22; Hesabu 15:15.) Wakiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” wote wangekuwa ‘wenye sheria mbele za Kristo,’ sawa na alivyoandika mtume Paulo. (Yohana 10:16; 1 Wakorintho 9:21) Paulo aliliita agano hilo jipya “agano lililo bora.” Kwa nini? Kwanza, lilitegemea ahadi zilizotimizwa badala ya vivuli vya mambo yajayo.—Waebrania 8:6; 9:11-14.

5. Ni nini kusudi la agano jipya, na kwa nini litafanikiwa?

5 Kusudi la agano hilo ni nini? Ni kutokeza taifa la wafalme na makuhani ili kubariki wanadamu wote. (Kutoka 19:6; 1 Petro 2:9; Ufunuo 5:10) Agano la Sheria ya Kimusa halikutokeza kamwe taifa hilo kwa maana kamili, kwa kuwa Israeli kwa ujumla liliasi nalo likapoteza fursa yalo. (Linganisha Warumi 11:17-21.) Hata hivyo, agano jipya hakika litafaulu, kwa kuwa linahusianishwa na aina tofauti kabisa ya sheria. Tofauti katika njia zipi?

Sheria Iliyo ya Uhuru

6, 7. Sheria ya Kristo huandaaje uhuru mkubwa zaidi kuliko ilivyofanya Sheria ya Kimusa?

6 Sheria ya Kristo hushirikishwa na uhuru mara kwa mara. (Yohana 8:31, 32) Hiyo hurejezewa kuwa “sheria ya watu huru” na “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” (Yakobo 1:25; 2:12, NW) Bila shaka, uhuru wote miongoni mwa wanadamu ni wa kadiri. Licha ya hilo, sheria hii hutoa uhuru mkubwa zaidi kuliko ile iliyoitangulia, Sheria ya Kimusa. Jinsi gani?

7 Kwa kielelezo, hakuna anayezaliwa chini ya sheria ya Kristo. Mambo kama jamii na mahali pa kuzaliwa hayahusiki. Wakristo wa kweli huchagua mioyoni mwao kwa hiari kukubali nira ya utii kwa sheria hiyo. Kwa kufanya hivyo, wao huona kwamba hiyo ni nira ya fadhili, mzigo mwepesi. (Mathayo 11:28-30) Ikiwa mwakumbuka, Sheria ya Kimusa ilikusudiwa pia kumfundisha mtu kwamba yeye ni mwenye dhambi na mwenye uhitaji mkubwa wa dhabihu ya fidia ili imkomboe. (Wagalatia 3:19) Sheria ya Kristo hufundisha kwamba Mesiya amekuja, akalipa bei ya fidia kwa kutoa uhai wake, na kutufungulia njia tuweze kuwekwa huru kutoka katika utumwa mbaya sana wa dhambi na kifo! (Warumi 5:20, 21) Ili kufaidika, twahitaji ‘kudhihirisha imani’ katika dhabihu hiyo.—Yohana 3:16, NW.

8. Sheria ya Kristo hutia ndani nini, lakini kwa nini kuishi kulingana nayo hakuhitaji kujua kwa moyo mamia ya sheria halali?

8 ‘Kudhihirisha imani’ huhusisha kuishi kulingana na sheria ya Kristo. Hilo hutia ndani kutii amri zote za Kristo. Je, hilo humaanisha kujua moyoni mamia ya sheria na maagizo? La. Ingawa Musa, mpatanishi wa agano la kale, aliandika Sheria ya Kimusa, Yesu, Mpatanishi wa agano jipya, hakuandika hata sheria moja. Badala ya hivyo, aliishi kulingana na sheria hiyo. Kupitia mwendo wake wa maisha ulio mkamilifu, aliacha kigezo ili wote wafuate. (1 Petro 2:21) Huenda hiyo ndiyo sababu ibada ya Wakristo wa mapema ilirejezewa kuwa “ile Njia.” (Matendo 9:2; 19:9, 23; 22:4; 24:22) Kwao, sheria ya Kristo ilitolewa kielelezi katika maisha ya Kristo. Kumwiga Yesu kulikuwa kutii sheria hiyo. Upendo wao mwingi kwake ulimaanisha kwamba sheria hiyo kwelikweli iliandikwa mioyoni mwao, jinsi ilivyotolewa unabii. (Yeremia 31:33; 1 Petro 4:8) Na aliye mtiifu kwa sababu ya upendo hahisi kamwe kuwa anaonewa—sababu nyingine inayofanya sheria ya Kristo iweze kuitwa “sheria ya watu huru.”

9. Ni nini kiini chenyewe cha sheria ya Kristo, na ni jinsi gani sheria hiyo huhusisha amri mpya?

9 Ikiwa upendo ulikuwa wa maana katika Sheria ya Kimusa, huo ndio kiini chenyewe cha sheria ya Kikristo. Kwa njia hiyo sheria ya Kristo hutia ndani amri mpya—lazima Wakristo wawe na upendo wa kujidhabihu kuelekea mmoja na mwenzake. Wao wapaswa kupenda kama alivyopenda Yesu; aliutoa uhai wake kwa hiari kwa niaba ya rafiki zake. (Yohana 13:34, 35; 15:13) Kwa hiyo yaweza kusemwa kwamba sheria ya Kristo ni wonyesho wa theokrasi ulio wa juu hata zaidi kuliko vile Sheria ya Musa ilivyokuwa. Kama vile jarida hili limeonyesha hapo mbele: “Theokrasi ni utawala wa Mungu; Mungu ni upendo; kwa hiyo theokrasi ni utawala wa upendo.”

Yesu na Mafarisayo

10. Ufundishaji wa Yesu ulitofautianaje na ule wa Mafarisayo?

10 Basi, haishangazi hata kidogo kwamba Yesu alipambana na viongozi wa kidini Wayahudi wa siku yake. Waandishi na Mafarisayo hawakuwa wamefikiria kamwe “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” Walijaribu kudhibiti watu kupitia maagizo yaliyofanyizwa na mwanadamu. Mafundisho yao yakawa yenye kuonea, ya kulaumu, yasiyofaa. Tofauti kabisa na hivyo, mafundisho ya Yesu yalikuwa yenye kujenga na ya kufaa sana! Alifundisha mambo yenye kutumika naye akashughulikia mahitaji na mahangaiko halisi ya watu. Alifundisha kwa njia sahili na akiwa na hisia za kutoka moyoni, akitumia vielezi vya maisha ya kila siku na kufundisha kutokana na mamlaka ya Neno la Mungu. Kwa njia hiyo, “makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake.” (Mathayo 7:28) Ndiyo, ufundishaji wa Yesu ulifikia mioyo yao!

11. Yesu alionyeshaje kwamba Sheria ya Kimusa ilipaswa kutumiwa kwa kiasi na kwa rehema?

11 Badala ya kuongezea Sheria ya Kimusa maagizo zaidi, Yesu alionyesha jinsi Wayahudi walipaswa kuwa wakitumia Sheria wakati wote—kwa kiasi na rehema. Kumbukeni, kwa kielelezo, ile pindi alipofikiwa na mwanamke aliyekuwa akitokwa damu. Kulingana na Sheria ya Kimusa, yeyote ambaye mwanamke huyo aligusa angekuwa najisi, kwa hiyo bila shaka hakupaswa kuchangamana na umati wa watu! (Mambo ya Walawi 15:25-27) Lakini alitaka sana kuponywa hivi kwamba alipitia katikati ya umati naye akagusa vazi la nje la Yesu. Kutokwa damu kukakoma mara moja. Je, Yesu alimkemea kwa ajili ya kuikiuka Sheria? La; badala ya kufanya hivyo, alielewa hali yake mbaya na akaonyesha kwa matendo ile amri kubwa kupita zote ya Sheria—upendo. Kwa hisia-mwenzi alimwambia mwanamke huyo hivi: “Binti, imani yako imekuponya, enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena.”—Marko 5:25-34.

Je, Sheria ya Kristo Ni Yenye Uendekevu?

12. (a) Kwa nini tusikate maneno kwamba Kristo ni mwendekevu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba kufanyizwa kwa sheria nyingi huongoza kwenye kufanyizwa kwa njia nyingi za kuzikiuka?

12 Basi, je, tukate maneno kwamba kwa kuwa sheria ya Kristo ‘ni ya uhuru,’ ni yenye uendekevu, ilhali Mafarisayo, wakiwa na mapokeo yao yote ya mdomo, angalau waliwekea mienendo ya watu mipaka yenye ukali? La. Mifumo ya kisheria ya leo yatolea kielezi kwamba mara nyingi kadiri sheria zilivyo nyingi, ndivyo watu hupata njia nyingi katika hizo za kuzikiuka.a Katika siku ya Yesu wingi wa sheria za Mafarisayo ulitia moyo kutafuta njia za kuzikiuka, kule kufanya kazi kijuu-juu tu bila upendo, na kule kukuza sura ya nje ya kuwa mwenye kujihesabia uadilifu ili kufunika ufisadi wa ndani.—Mathayo 23:23, 24.

13. Kwa nini sheria ya Kristo inatokeza kiwango cha juu zaidi cha mwenendo kuliko mfumo wowote wa sheria ulioandikwa?

13 Kwa kutofautisha, sheria ya Kristo haikuzi mitazamo hiyo. Kwa hakika, kutii sheria yenye kutegemea kumpenda Yehova na inayotiiwa kwa kuiga upendo wa Kristo wa kujidhabihu kwa ajili ya wengine hutokeza kiwango cha juu zaidi cha mwenendo kuliko kitokezwacho kwa kufuata mfumo rasmi wa kisheria. Upendo hautafuti njia za kukiuka jambo; huo hutuzuia tusifanye madhara ambayo mfumo wa sheria huenda usikataze waziwazi. (Ona Mathayo 5:27, 28.) Kwa njia hiyo, sheria ya Kristo itatuchochea kuwafanyia wengine mambo—kuonyesha ukarimu, ukaribishaji-wageni, na upendo—katika njia ambazo hakuna sheria yoyote rasmi ingeweza kutuchochea tufanye.—Matendo 20:35; 2 Wakorintho 9:7; Waebrania 13:16.

14. Kuishi kulingana na sheria ya Kristo kulikuwa na tokeo gani juu ya kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?

14 Kwa kadiri ambavyo washiriki walo waliishi kulingana na sheria ya Kristo, kutaniko la Kikristo la mapema lilifurahia hali yenye uchangamfu, yenye upendo, yenye uhuru kadiri fulani kutoka katika mitazamo migumu, yenye kuhukumu, na ya kinafiki iliyoenea sana katika masinagogi ya siku hiyo. Ni lazima iwe washiriki wa makutaniko hayo mapya kwa kweli walihisi kwamba walikuwa wakiishi kulingana na “sheria ya watu huru”!

15. Ni zipi baadhi ya jitihada za mapema za Shetani za kufisidi kutaniko la Kikristo?

15 Hata hivyo, Shetani alitamani kulifisidi kutaniko la Kikristo kutoka ndani, jinsi tu alivyokuwa amelifisidi taifa la Israeli. Mtume Paulo alionya juu ya watu walio kama mbwa-mwitu ambao ‘wangesema mapotovu’ na kuonea kundi la Mungu. (Matendo 20:29, 30) Yeye alilazimika kukabiliana na Wayudaiza (wageuzao watu wafuate Dini ya Kiyahudi), waliojitahidi kubadili uhuru wa kadiri wa sheria ya Kristo na utumwa wa Sheria ya Kimusa, iliyokuwa imetimizwa katika Kristo. (Mathayo 5:17; Matendo 15:1; Warumi 10:4) Baada ya mtume wa mwisho kufa, hakukuwa na kizuizi tena dhidi ya uasi-imani huo. Kwa hiyo ufisadi ukaenea sana.—2 Wathesalonike 2:6, 7.

Jumuiya ya Wakristo Yachafua Sheria ya Kristo

16, 17. (a) Ufisadi ulikuwa wa namna gani mbalimbali katika Jumuiya ya Wakristo? (b) Sheria za Kanisa Katoliki ziliendelezaje maoni yaliyopotolewa juu ya ngono?

16 Sawa na Dini ya Kiyahudi, ufisadi ulikuwa wa namna mbalimbali katika Jumuiya ya Wakristo. Hiyo pia ikawa mawindo ya mafundisho yasiyo ya kweli na maadili malegevu. Na mara nyingi jitihada zayo za kulinda kundi layo dhidi ya mavutano ya nje zilithibitika kuwa zenye kubabua chochote kilichosalia cha ibada ya kweli. Sheria ngumu na zisizo za kimaandiko zikakua upesi.

17 Kanisa Katoliki limeongoza katika kuunda idadi kubwa ya sheria za kanisa. Sheria hizo zilikuwa zimepotolewa hasa juu ya mambo yanayohusu ngono. Kulingana na kitabu Sexuality and Catholicism, kanisa lilitwaa falsafa ya Kigiriki ya Ustoiki, iliyoshuku aina zote za raha. Kanisa lilikuja kufundisha kwamba raha yote ya kingono, kutia ndani ile ya mahusiano ya ndoa ya kawaida, ilikuwa yenye dhambi. (Tofautisha Mithali 5:18, 19.) Ngono ilidaiwa kuwa ya uzazi tu, wala si ya raha ya kingono. Kwa njia hiyo sheria ya kanisa ililaumu njia yoyote ya kuzuia mimba kuwa dhambi nzito sana, nyakati nyingine ikihitaji adhabu ya kutubisha ya miaka mingi. Zaidi, ukuhani ulikatazwa kuoa, amri ambayo imetokeza ongezeko kubwa la ngono haramu, kutia na kuwatenda watoto vibaya.—1 Timotheo 4:1-3.

18. Matokeo ya kuongezeka kwa sheria za kanisa yalikuwa nini?

18 Kadiri sheria za kanisa zilivyoongezeka, zilikusanywa kuwa vitabu. Vitabu hivyo vikaanza kuifunika na kuchukua mahali pa Biblia. (Linganisha Mathayo 15:3, 9.) Sawa na Dini ya Kiyahudi, Ukatoliki uliyashuku maandishi ya kibinadamu na kuyaona mengi yayo kuwa tisho. Upesi maoni hayo yakapita mno onyo la Biblia lifaalo juu ya habari hiyo. (Mhubiri 12:12; Wakolosai 2:8) Jerome, mwandikaji wa kanisa wa karne ya nne W.K. alipaaza sauti hivi: “Ee Bwana, nikipata wakati wowote tena kuwa na vitabu vya kilimwengu au kuvisoma, nimekukana.” Baada ya muda, kanisa likajitwalia kazi ya kukagua vitabu—hata vitabu juu ya habari za kilimwengu. Kwa njia hiyo katika karne ya 17 mwastronomia Galileo alilaumiwa kwa sababu ya kuandika kwamba dunia hulizunguka jua. Kusisitiza kwa kanisa kuwa mamlaka ya mwisho katika kila jambo—hata katika maswali juu ya astronomia—hatimaye kungedhoofisha imani katika Biblia.

19. Makao ya watawa yaliendelezaje umabavu ulio mgumu?

19 Uundaji-sheria wa kanisa ulisitawi katika makao ya watawa ambapo, watawa wa kiume walijitenga na ulimwengu huu ili waishi katika hali ya kujikana. Makao mengi ya watawa ya Katoliki yalishikamana na “Kanuni ya Mtakatifu Benedict.” Abati (jina lililotokana na neno la Kiaramu “baba”) alitawala akiwa na mamlaka kamili. (Linganisha Mathayo 23:9.) Ikiwa mtawa alipokea zawadi kutoka kwa wazazi wake, abati alikuwa akiamua ikiwa mtawa huyo au mwingine ndiye angeipokea. Zaidi ya kulaumu maneno machafu, kanuni moja ilikataza porojo na mizaha yote, ikisema hivi: “Hakuna mwanafunzi yeyote atakayeongea mambo hayo.”

20. Ni nini kinachoonyesha kwamba Uprotestanti pia ulichochea umabavu usio wa kimaandiko?

20 Uprotestanti, uliojitahidi kupindua mambo yenye kupita kiasi ya Ukatoliki, upesi ukawa stadi vilevile wa kufanyiza sheria za kimabavu zisizo na msingi katika sheria ya Kristo. Kwa mfano, mpinduzi wa kidini mkuu John Calvin alikuja kuitwa “mfanya sheria wa Kanisa lililofanywa upya.” Aliongoza kanisa la Protestanti la Geneva akiwa na sheria ngumu nyingi ambazo zilitekelezwa na “Wazee” ambao “kazi” yao, akaandika Calvin, “ni kusimamia maisha ya kila mmoja.” (Tofautisha 2 Wakorintho 1:24.) Kanisa lilidhibiti hoteli mbalimbali na kuamua ni vichwa gani vya mazungumzo vilivyoruhusiwa. Kulikuwa na adhabu kali kwa makosa kama kuimba nyimbo zisizo na staha au kucheza dansi.b

Kujifunza Kutokana na Makosa ya Jumuiya ya Wakristo

21. Matokeo ya ujumla ya mwelekeo wa Jumuiya ya Wakristo wa ‘kupita yaliyoandikwa’ yamekuwa nini?

21 Je, kanuni na sheria zote hizo zimeilinda Jumuiya ya Wakristo dhidi ya ufisadi? Tofauti kabisa! Leo Jumuiya ya Wakristo imegawanyika katika mamia ya mafarakano, kuanzia yale yenye kufuata sheria sana hadi yale yaliyo yenye uendekevu sana. Yote hayo, kwa njia moja au nyingine, ‘yamepita yale yaliyoandikwa,’ yakiruhusu kufikiri kwa kibinadamu kuongoze kundi na kuingilia sheria ya kimungu.—1 Wakorintho 4:6.

22. Kwa nini uasi wa Jumuiya ya Wakristo haukumaanisha mwisho wa sheria ya Kristo?

22 Hata hivyo, historia ya sheria ya Kristo haina mwisho wenye msiba. Yehova Mungu hataruhusu kamwe wanadamu duni waifagilie mbali sheria ya kimungu. Sheria ya Kikristo ina nguvu sana leo miongoni mwa Wakristo wa kweli, nao wana lile pendeleo kubwa la kuishi kulingana nayo. Lakini baada ya kuchunguza kile ambacho Dini ya Kiyahudi na Jumuiya ya Wakristo zimefanyia sheria ya kimungu, twaweza kwa kufaa kuuliza, ‘Twaishije kulingana na sheria ya Kristo huku tukiepuka ule mtego wa kuchafua Neno la Mungu kwa kusababu kwa kibinadamu na kanuni zinazodhoofisha maana yenyewe ya sheria ya kimungu? Sheria ya Kristo yapaswa kutupa maoni gani yenye usawaziko leo?’ Makala inayofuata itashughulikia maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

a Ni Mafarisayo hasa waliotokeza namna ya Dini ya Kiyahudi iliyoko leo, kwa hiyo haishangazi kwamba Dini ya Kiyahudi bado hutafuta njia za kukiuka vizuizi vyavyo vingi vilivyoongezwa vya Sabato. Kwa kielelezo, mgeni kwenye hospitali ya Kanisa Othodoksi kwenye siku ya Sabato aweza kuona kwamba lifti husimama yenyewe kwenye kila orofa ili abiria waepuke kufanya “kazi” yenye dhambi ya kubonyeza kibonyezo cha lifti. Madaktari fulani Wayahudi huandika mapendekezo yao ya madawa kwa wino utakaotoweka baada ya siku chache. Kwa nini? Mishnah huhesabu kuandika kuwa “kazi,” lakini hiyo hufafanua “kuandika” kuwa kuacha alama ya kudumu.

b Servetus, aliyepinga baadhi ya maoni ya kitheolojia ya Calvin, alichomwa mtini akionwa kuwa mzushi.

Ungejibuje?

◻ Ni nini kiini chenyewe cha sheria ya Kristo?

◻ Njia ya Yesu ya kufundisha ilitofautianaje na ile ya Mafarisayo?

◻ Shetani alitumiaje mwelekeo mgumu wa kufanyiza sheria ili kufisidi Jumuiya ya Wakristo?

◻ Ni yapi baadhi ya matokeo yanayofaa ya kuishi kulingana na sheria ya Kristo?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu aliitumia Sheria ya Kimusa kwa kiasi na kwa rehema

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki