Sheria ya Kabla ya Kristo
“Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”—ZABURI 119:97.
1. Misogeo ya magimba ya kimbingu huongozwa na nini?
TANGU utoto, yamkini Ayubu alikuwa ametazama juu kwenye nyota kwa kustaajabu. Huenda ikawa, wazazi wake walikuwa wamemfundisha majina ya makundi ya nyota na yale waliyojua juu ya sheria zinazoongoza msogeo wa hayo makundinyota angani. Kwani, watu katika nyakati za kale walitumia miendo thabiti ya makundi hayo ya nyota yaliyo makubwa na yenye kupendeza, ili kutia alama majira yenye kubadilika. Lakini nyakati zote ambazo aliyaangalia makundinyota kwa kustaajabu, Ayubu hakujua ni kani zipi zenye uweza zilizoshikamanisha pamoja mifanyizo hiyo ya nyota. Kwa njia hiyo, hakuweza kumjibu Yehova Mungu alipomuuliza hivi: “Je! unazijua amri zilizoamuriwa mbingu?” (Ayubu 38:31-33) Ndiyo, nyota huongozwa na sheria—sheria zilizo sahihi na tata sana hivi kwamba wanasayansi wa leo hawazifahamu kikamili.
2. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba uumbaji wote huongozwa na sheria?
2 Yehova ndiye Mpaji-Sheria Mkuu Kuliko Wote katika ulimwengu wote mzima. Kazi zake zote huongozwa na sheria. Mwana wake mpendwa, “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” alikuwa akitii kwa uaminifu sheria ya Baba yake kabla ya ulimwengu wote mzima halisi kuwako! (Wakolosai 1:15) Malaika pia huelekezwa na sheria. (Zaburi 103:20) Hata wanyama wanaongozwa na sheria wanapotii amri za silika ambazo Muumba wao ameweka ndani yao.—Mithali 30:24-28; Yeremia 8:7.
3. (a) Kwa nini wanadamu wanahitaji sheria? (b) Yehova aliliongozaje taifa la Israeli?
3 Namna gani wanadamu? Ingawa tumebarikiwa na zawadi kama akili, adili, na hali ya kiroho, bado twahitaji kiasi fulani cha sheria ya kimungu kituongoze katika kutumia uwezo huo mbalimbali. Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walikuwa wakamilifu, hivi kwamba ni sheria chache tu zilizohitajiwa kuwaongoza. Kupenda kwao Baba yao wa kimbingu kulipaswa kuwapa sababu za kutosha za kumtii kwa moyo. Lakini walikosa kutii. (Mwanzo 1:26-28; 2:15-17; 3:6-19) Likiwa tokeo, wazao wao walikuwa viumbe vyenye dhambi vilivyohitaji sheria nyingi zaidi za kutoa mwelekezo. Kadiri wakati ulivyopita, Yehova alitimiza uhitaji huo kwa upendo. Alimpa Noa sheria hususa alizopaswa kupitisha kwa familia yake. (Mwanzo 9:1-7) Karne kadhaa baadaye, kupitia Musa, Mungu alilipa taifa jipya la Israeli mfumo wa Sheria ulioandikwa, uliotia ndani kila kitu. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwamba Yehova aliongoza taifa zima na sheria ya kimungu. Kuchunguza Sheria hiyo kutatusaidia kuelewa fungu la maana ambalo sheria ya kimungu inalo maishani mwa Wakristo leo.
Sheria ya Kimusa—Kusudi Layo
4. Kwa nini lingekuwa jambo gumu kwa wazao wachaguliwa wa Abrahamu kutokeza Mbegu iliyoahidiwa?
4 Mtume Paulo, mwanafunzi wa Sheria mwenye kuchunguza sana, aliuliza hivi: “Torati ni nini basi?” (Wagalatia 3:19) Ili kujibu, twahitaji kukumbuka kwamba Yehova alimwahidi rafiki yake Abrahamu kwamba nasaba ya familia yake ingetokeza Mbegu ambayo ingeletea mataifa yote baraka kubwa. (Mwanzo 22:18) Lakini hapa palikuwa na ugumu fulani: si Waisraeli wote, wazao wachaguliwa wa Abrahamu, waliokuwa watu wenye kumpenda Yehova. Wakati ulipopita, wengi walithibitika kuwa wenye shingo ngumu, waasi—wengine walikuwa karibu hawaongozeki! (Kutoka 32:9; Kumbukumbu la Torati 9:7) Kwao, kuwa miongoni mwa watu wa Mungu kulikuwa tu jambo la uzawa, wala si chaguo.
5. (a) Yehova aliwafundisha Waisraeli nini kupitia Sheria ya Kimusa? (b) Sheria iliundwaje ili iathiri mwenendo wa walioishika?
5 Watu kama hao wangewezaje kutokeza na kufaidika na Mbegu iliyoahidiwa? Badala ya kuwadhibiti kama roboti, Yehova aliwafundisha kupitia sheria. (Zaburi 119:33-35; Isaya 48:17) Kwa hakika, neno la Kiebrania la “sheria,” toh·rahʹ, humaanisha “maagizo.” Ilifundisha nini? Kimsingi iliwafundisha Waisraeli kuhitaji kwao Mesiya, ambaye angewakomboa kutokana na hali yao ya dhambi. (Wagalatia 3:24) Sheria pia ilifundisha hofu ya kimungu na utii. Kwa kupatana na ile ahadi ya Kiabrahamu, Waisraeli walipaswa watumikie wakiwa mashahidi wa Yehova kwa mataifa mengine yote. Kwa hiyo Sheria ilipaswa iwafundishe mfumo wa mwenendo ulio wa juu na ulio bora ambao ungemheshimu Yehova; ingewasaidia Waisraeli kujiepusha na mazoea yenye ufisadi ya mataifa yaliyowazunguka.—Mambo ya Walawi 18:24, 25; Isaya 43:10-12.
6. (a) Sheria ya Kimusa ina sheria ngapi hivi, na kwa nini hizo hazipasi kuonwa kuwa nyingi kupita kiasi? (Ona kielezi-chini.) (b) Ni ufahamu gani wenye kina tuwezao kuupata kupitia funzo la Sheria ya Kimusa?
6 Basi, haishangazi kwamba, Sheria ya Kimusa ina sheria nyingi—zaidi ya 600.a Mfumo huo ulioandikwa uliongoza nyanja za ibada, serikali, maadili, haki, na hata chakula na usafi wa kiafya. Lakini, je, hilo lamaanisha kwamba Sheria ilikuwa tu rundo la masharti na amri zenye maneno machache zisizo na hisia? La hasha! Kujifunza mfumo huo wa Sheria hutoa ufahamu mkubwa wenye kina wa utu wa Yehova wenye upendo. Fikiria vielelezo kadhaa.
Sheria Iliyoonyesha Waziwazi Rehema na Huruma
7, 8. (a) Sheria ilikaziaje rehema na huruma? (b) Yehova alitekelezaje Sheria kwa rehema katika kisa cha Daudi?
7 Sheria ilikazia rehema na huruma, hasa kwa wanyonge au walio hoi. Wajane na mayatima walichaguliwa kwa ajili ya ulinzi. (Kutoka 22:22-24) Wanyama wa kazi walilindwa dhidi ya ukatili. Haki za msingi za kumiliki mali zilistahiwa. (Kumbukumbu la Torati 24:10; 25:4) Ingawa sheria ilidai hukumu ya kifo kwa ajili ya uuaji-kimakusudi, iliwezesha rehema ipatikane katika visa vya uuaji usiokusudiwa. (Hesabu 35:11) Yaonekana kwamba, waamuzi Waisraeli walikuwa na uhuru wa kuamua adhabu iliyotozwa makosa fulani, ikitegemea mtazamo wa mkosaji.—Linganisha Kutoka 22:7 na Mambo ya Walawi 6:1-7.
8 Yehova aliwawekea waamuzi kielelezo kwa kutumia Sheria kwa uthabiti unapohitajiwa lakini kwa rehema popote iwezekanapo. Mfalme Daudi, aliyekuwa amefanya uzinzi na kuua kimakusudi, alionyeshwa rehema. Si kwamba hakuadhibiwa, kwa kuwa Yehova hakumlinda kutokana na matokeo mabaya yaliyotokana na dhambi yake. Hata hivyo, kwa sababu ya agano la Ufalme na kwa sababu Daudi alikuwa na mwelekeo wenye rehema na alikuwa na mtazamo wa moyo wenye toba ya kina, hakuuawa.—1 Samweli 24:4-7; 2 Samweli 7:16; Zaburi 51:1-4; Yakobo 2:13.
9. Upendo ulikuwa na fungu gani katika Sheria ya Kimusa?
9 Zaidi, Sheria ya Kimusa ilikazia upendo. Wazia mojawapo mataifa ya leo likiwa na mfumo wa sheria ambao kwa kweli uliamrisha upendo! Sheria ya Kimusa haikukataza uuaji-kimakusudi tu; bali pia iliamuru hivi: “Umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18) Haikukataza kule kuwatenda vibaya wakazi-wageni tu; bali pia iliamuru hivi: “Mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri.” (Mambo ya Walawi 19:34) Haikukataza uzinzi tu; bali pia ilimwamuru mume amfurahishe mkewe! (Kumbukumbu la Torati 24:5) Katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati pekee, maneno ya Kiebrania yaonyeshayo sifa ya upendo yanatumika mara 20 hivi. Yehova aliwahakikishia Waisraeli upendo wake mwenyewe—katika wakati uliopita, wakati uliokuwapo, na wakati ujao. (Kumbukumbu la Torati 4:37; 7:12-14) Kwa kweli, amri iliyo kuu zaidi ya Sheria ya Kimusa ilikuwa: “Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Yesu alisema kwamba Sheria yote hutegemea amri hiyo, pamoja na ile amri ya kupenda jirani. (Mambo ya Walawi 19:18; Mathayo 22:37-40) Si ajabu kwamba mtunga-zaburi aliandika hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”—Zaburi 119:97.
Kuitumia Vibaya Sheria
10. Kwa kiasi kikubwa, Wayahudi walionaje Sheria ya Kimusa?
10 Basi, yahuzunisha kama nini, kwamba kwa kiasi kikubwa, Waisraeli walikosa kuithamini Sheria ya Kimusa! Watu walikosa kuitii Sheria, waliipuuza, au waliisahau. Walichafua ibada safi kwa yale mazoea ya kidini yenye kuchukiza ya mataifa mengine. (2 Wafalme 17:16, 17; Zaburi 106:13, 35-38) Nao waliisaliti Sheria kwa njia nyinginezo pia.
11, 12. (a) Vikundi vya viongozi wa kidini vilifanyaje uharibifu baada ya siku za Ezra? (Ona sanduku.) (b) Kwa nini marabi wa kale waliona yahitajika “kufanyiza ua kuizunguka Sheria”?
11 Baadhi ya madhara mabaya zaidi kwa Sheria yalifanywa na walewale waliodai kuifundisha na kuihifadhi. Hilo lilitokea baada ya siku za mwandishi mwaminifu Ezra wa karne ya tano K.W.K. Ezra alipigana sana dhidi ya mavutano yenye kufisidi ya mataifa mengine na akakazia kusoma na kufundisha Sheria. (Ezra 7:10; Nehemia 8:5-8) Baadhi ya walimu wa Sheria walidai kufuata hatua za Ezra nao wakafanyiza kilichokuja kuitwa “Sinagogi Kubwa.” Kati ya misemo yalo lilikuwapo lile elekezo: “Fanyiza ua kuizunguka Sheria.” Walimu hao walisababu kwamba Sheria ilikuwa kama shamba lenye thamani. Ili yeyote asipite ndani ya shamba hilo bila ruhusa kwa kuvunja sheria zalo, walifanyiza sheria za ziada, “Sheria ya Mdomo,” ili kuwazuia watu wasikaribie makosa kama hayo.
12 Huenda wengine wakabisha kwamba viongozi Wayahudi walistahili kuhisi hivyo. Baada ya siku ya Ezra Wayahudi walitawalwa na mamlaka za kigeni, hasa Ugiriki. Ili kuzuia uvutano wa falsafa na utamaduni wa Kigiriki, vikundi vya viongozi wa kidini vilitokea miongoni mwa Wayahudi. (Ona sanduku, ukurasa 10.) Baada ya muda baadhi ya vikundi hivyo vikaanza kushindana na, hata kupita ukuhani wa Kilawi katika kuwa walimu wa Sheria. (Linganisha Malaki 2:7.) Kufikia mwaka wa 200 K.W.K., sheria ya mdomo, ilikuwa imeanza kuwa na uvutano juu ya maisha ya Wayahudi. Mwanzoni sheria hizo hazikupasa kuandikwa, zisije zikachukuliwa kuwa sawa na Sheria iliyoandikwa. Lakini hatua kwa hatua, kufikiri kwa kibinadamu kulitangulizwa mbele ya kule kwa kimungu, hivi kwamba hatimaye “ua” huo kwa kweli ulidhuru “shamba” lilelile ulilopaswa kulinda.
Uchafuzi wa Dini ya Mafarisayo
13. Viongozi fulani wa kidini Wayahudi waliteteaje kule kufanyiza kwa kanuni nyingi?
13 Marabi walisababu kwamba kwa kuwa Torah, au Sheria ya Kimusa, ilikuwa kamilifu, lazima iwe na majibu kwa kila swali liwezalo kuzuka. Maoni hayo hayakuwa yenye staha kikweli. Kwa kweli, yaliwapa marabi uhuru wa kutumia kusababu kwa kibinadamu, wakifanya ionekane kana kwamba Neno la Mungu ndilo lililokuwa msingi wa kanuni katika aina zote za masuala—baadhi yayo ya kibinafsi, mengine hafifu tu.
14. (a) Viongozi wa kidini Wayahudi walitanuaje kupita kiasi isivyo kimaandiko, ile amri ya Kimaandiko ya kujitenga na mataifa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba sheria za kirabi zilishindwa kuwalinda Wayahudi wasikubali mavutano ya kipagani?
14 Tena na tena hao viongozi wa kidini walitwaa amri za Kimaandiko na kuzitanua kupita kiasi. Kwa mfano, Sheria ya Kimusa iliunga mkono kujitenga na mataifa, lakini marabi walihubiri aina fulani ya chuki isiyo na kiasi kuelekea chochote kisicho cha Kiyahudi. Walifundisha kwamba Myahudi hapaswi kuacha mifugo yake kwenye hoteli ya Wasio Wayahudi, kwa kuwa Wasio Wayahudi “wanashukiwa kuwa hufanya ngono na wanyama.” Mwanamke Myahudi hakuruhusiwa kumsaidia mwanamke Asiye Myahudi aliye na utungu wa kuzaa kwa sababu kwa kufanya hivyo angekuwa “anasaidia kuzalisha mtoto kwa ajili ya ibada ya sanamu.” Kwa kuwa walishuku kwa kufaa majumba ya mazoezi ya Ugiriki, marabi walikataza mazoezi yote ya kimichezo. Historia yathibitisha kwamba yote hayo yalikuwa na matokeo kidogo sana katika kuwazuia Wayahudi wasikubali itikadi za Wasio Wayahudi. Kwa hakika, Mafarisayo wenyewe walikuja kufundisha fundisho la kipagani la Kigiriki la hali ya kutokufa kwa nafsi!—Ezekieli 18:4.
15. Viongozi wa kidini Wayahudi walipotoaje zile sheria juu ya utakaso na ngono ya maharimu?
15 Pia Mafarisayo walipotoa sheria za utakaso. Ilisemwa kwamba Mafarisayo wangelitakasa jua lenyewe ikiwa wangepewa fursa. Sheria yao ilishikilia kwamba kuchelewa “kwenda msalani” kungeweza kumchafua mtu! Kunawa mikono kukawa desturi tata, kukiwa na sheria juu ya mkono upaswao kunawiwa kwanza na jinsi gani. Wanawake hasa walionwa kuwa wasio safi. Kwa msingi wa amri ya Kimaandiko ya ‘kutomkaribia’ jamaa yeyote wa kimwili (kihalisi sheria dhidi ya ngono ya maharimu), marabi waliamua kwamba mume hakupaswa kutembea nyuma ya mkewe; wala kuongea naye sokoni.—Mambo ya Walawi 18:6.
16, 17. Sheria ya mdomo ilipanuaje amri ya kushika Sabato ya kila juma, kukiwa na tokeo jipi?
16 Ijulikanayo sana ni ile dhihaka ya kiroho ambayo sheria ya mdomo ilifanya dhidi ya sheria ya Sabato. Mungu alilipa Israeli amri sahili: Msifanye kazi yoyote siku ya saba ya juma. (Kutoka 20:8-11) Hata hivyo, sheria ya mdomo ikapanua sheria kwa kuongeza aina 39 tofauti-tofauti za kazi iliyokatazwa, kutia ndani kufunga au kulegeza fundo, kushona kwa kudunga mara mbili tu, kuandika herufi mbili za Kiebrania, na kadhalika. Kisha kila mojawapo ya aina hizo za kazi iliyokatazwa ilihitaji sheria nyingine zisizo na mwisho. Ni mafundo yapi yaliyokatazwa na ni yapi yaliyoruhusiwa? Sheria ya mdomo ilitoa majibu kwa maagizo ya kibinadamu. Kuponya kulikuja kuonekana kuwa kazi iliyokatazwa. Kwa kielelezo, kuunganisha kiungo kilichovunjika katika siku ya Sabato, kulikatazwa. Mtu anayeumwa jino angeweza kutumia siki kukoleza chakula chake, lakini ni lazima asiinywe hiyo siki kupitia meno yake. Hilo laweza kuponya jino lake!
17 Kwa njia hiyo kwa sababu ya kuzikwa chini ya mamia ya sheria za kufanyizwa na mwanadamu, kwa Wayahudi walio wengi, sheria ya Sabato ilipoteza maana yayo ya kiroho. Yesu Kristo, “Bwana wa sabato,” alipofanya miujiza yenye kuvutia na yenye kuchangamsha mioyo siku ya Sabato, waandishi na Mafarisayo hawakuchochewa. Walihangaikia tu kwamba alionekana kupuuza maagizo yao.—Mathayo 12:8, 10-14.
Kujifunza Kutokana na Makosa ya Mafarisayo
18. Tokeo la kuongezea Sheria ya Kimusa sheria za mdomo na mapokeo lilikuwa nini? Toa kielezi.
18 Kwa ufupi, twaweza kusema kwamba sheria na mapokeo hizo zilizoongezwa zilijibandika kwenye Sheria ya Kimusa sawa na vile kombe za bahari washikamanavyo na upande wa nje wa meli. Mwenye meli hutumia wakati na jitihada nyingi kubambua viumbe hivyo vyenye kutatiza kutoka kwenye meli yake kwa sababu hivyo hupunguza mwendo wa hicho chombo navyo huharibu rangi yacho ya kuzuia kutu. Vivyo hivyo, sheria za mdomo na mapokeo ziliilemeza na kuidhoofisha Sheria. Hata hivyo, badala ya kuondolea mbali sheria hizo za ziada, marabi waliendelea kuongeza zaidi. Kufikia wakati Mesiya alipokuja kutimiza Sheria, ile “meli” ilikuwa imebandikwa sana “kombe za bahari” hivi kwamba ilikaribia kuzama! (Linganisha Mithali 16:25.) Badala ya kulinda agano la Sheria, viongozi hao wa kidini walifanya lile kosa la kulikiuka. Lakini, mbona ule “ua” wao wa kanuni ulishindwa?
19. (a) Kwa nini ule “ua kuizunguka Sheria” ulishindwa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba viongozi wa kidini Wayahudi walikosa imani ya kweli?
19 Viongozi wa Dini ya Kiyahudi walishindwa kuelewa kwamba vita dhidi ya ufisadi hupiganwa moyoni wala si kwenye kurasa za vitabu vya sheria. (Yeremia 4:14) Ufunguo wa kupata ushindi ni upendo—upendo kwa Yehova, sheria yake, na kanuni zake za uadilifu. Upendo huo hutokeza kuchukia kilekile anachochukia Yehova. (Zaburi 97:10; 119:104) Wale ambao mioyo yao imejazwa upendo kwa njia hiyo huendelea kuwa waaminifu kwa sheria za Yehova katika ulimwengu huu mfisadi. Viongozi wa kidini Wayahudi walikuwa na pendeleo kubwa la kuwafundisha watu ili kuendeleza na kuchochea upendo huo. Kwa nini walishindwa kufanya hivyo? Yaonekana walikosa imani. (Mathayo 23:23, linganisha kielezi-chini cha NW.) Ikiwa wangalikuwa na imani katika nguvu za roho ya Yehova za kufanya kazi mioyoni mwa wanadamu waaminifu, hawangalihisi uhitaji wa kudhibiti vigumu maisha ya wengine. (Isaya 59:1; Ezekieli 34:4) Kwa kuwa walikosa imani, hawakuwapa watu imani; waliwalemeza watu na amri zilizofanyizwa na mwanadamu.—Mathayo 15:3, 9; 23:4.
20, 21. (a) Mwelekeo wa akilini wenye kuongozwa na mapokeo ulikuwa na athari gani kwa ujumla juu ya Dini ya Kiyahudi? (b) Twajifunza masomo gani kutokana na yale yaliyoipata Dini ya Kiyahudi?
20 Viongozi hao Wayahudi hawakuendeleza upendo. Mapokeo yao yalitokeza dini iliyopendezwa sana na mambo ya kijuu-juu, wakitii bila kufikiri ili waonekane—hali iliyofaa ya kutokeza unafiki. (Mathayo 23:25-28) Maagizo yao yalitokeza sababu zisizohesabika za kuwahukumu wengine. Kwa sababu hiyo Mafarisayo wenye kiburi, na wenye mamlaka walihisi kuwa walistahili kumchambua Yesu Kristo mwenyewe. Walisahau kusudi kuu la Sheria na wakamkataa yule Mesiya mmoja wa kweli. Likiwa tokeo, alilazimika kuliambia taifa la Kiyahudi hivi: “Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”—Mathayo 23:38; Wagalatia 3:23, 24.
21 Somo ni nini kwetu? Kwa wazi, mwelekeo wa akilini ulio mgumu na wenye kuongozwa na mapokeo hauendelezi ibada safi ya Yehova! Lakini je, hili lamaanisha kwamba waabudu wa Yehova leo hawapaswi kuwa na kanuni zozote kamwe isipokuwa ziwe zimeonyeshwa kihususa katika Andiko Takatifu? La. Kwa jibu kamili, acheni sasa tuchunguze jinsi Yesu Kristo alivyoanzisha sheria mpya na iliyo bora badala ya ile Sheria ya Kimusa.
[Maelezo ya Chini]
a Bila shaka, bado hiyo ni idadi ndogo sana kwa kulinganishwa na mifumo ya kisheria ya mataifa ya kisasa. Kwa kielelezo, kufikia mapema miaka ya 1990, sheria za serikali za Marekani zilijaza kurasa zaidi ya 125,000, maelfu ya sheria mpya yakiendelea kuongezwa kila mwaka.
Je, Waweza Kueleza?
◻ Uumbaji wote unaongozwaje na sheria ya kimungu?
◻ Kusudi kuu la Sheria ya Kimusa lilikuwa nini?
◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba Sheria ya Kimusa ilikazia rehema na huruma?
◻ Sababu gani wale viongozi wa kidini Wayahudi waliongezea ile Sheria ya Kimusa sheria zisizohesabika, na kukiwa na tokeo jipi?
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Viongozi wa Kidini Wayahudi
Waandishi: Walijiona kuwa waandamizi wa Ezra na wafafanuaji wa Sheria. Kulingana na kitabu A History of the Jews, “si waandishi wote waliokuwa watu wa vyeo vya juu, na majaribio yao ya kufichua maana za sheria zilizofichika mara nyingi yalizorota na kuwa amri zisizo na maana na vizuizi vya kipumbavu. Vizuizi hivyo vikawa desturi, ambayo upesi ikawa mtawala mgumu.”
Hasidimu: Jina hilo humaanisha “walio wachaji” au “watakatifu.” Walitajwa kwa mara ya kwanza kuwa kikundi karibu mwaka wa 200 K.W.K., walikuwa wenye mamlaka kisiasa, walinzi washupavu wa utakato wa Sheria dhidi ya udhalimu wa uvutano wa Kigiriki. Wahasidimu waligawanyika katika vikundi vitatu: Mafarisayo, Masadukayo, na Waesene.
Mafarisayo: Wasomi fulani huamini kuwa jina hilo hutokana na maneno “Waliotengwa,” “Wapendao mtengano.” Kwa kweli walikuwa washupavu katika jitihada zao za kujitenga na Wasio Wayahudi, lakini pia waliona jamii yao kuwa iliyotengwa—na iliyo bora kuliko—Wayahudi wa kawaida, ambao hawakujua mambo magumu ya sheria ya mdomo. Mwanahistoria mmoja alisema hivi juu ya Mafarisayo: “Kwa ujumla, waliwatenda watu kama watoto, wakiidhinisha na kufafanua mambo yaliyo madogo zaidi ya kawaida za dini ya kufuatwa.” Msomi mwingine alisema hivi: “Dini ya Mafarisayo ilitokeza rundo la kanuni halali zilizoshughulikia hali zote, kukiwa na matokeo yasiyoepukika ya kwamba zilifanya mambo madogo kuwa makubwa na kwa kufanya hivyo zilifanya mambo ya maana sana yawe madogo (Mt. 23:23).”
Masadukayo: Kikundi kilichohusiana kwa ukaribu na utawala wa kiukoo na ukuhani. Walipinga kwa bidii waandishi na Mafarisayo, wakisema kwamba sheria ya mdomo haikuwa na uhalali uleule wa Sheria iliyoandikwa. Kushindwa kwao katika bishano hilo kulionyeshwa na Mishnah yenyewe: “Mkazo mkubwa watiwa katika [kushika] maneno ya Waandishi kuliko katika [kushika] maneno ya Sheria [iliyoandikwa].” Talmud, iliyotia ndani maelezo mengi juu ya sheria ya mdomo, baadaye ilifikia hatua ya kusema hivi: “Maneno ya waandishi ni . . . yenye thamani zaidi kuliko maneno ya Torah.”
Waesene: Kikundi cha watawa waliojitenga wenyewe katika jamii zilizotengwa. Kulingana na The Interpreter’s Dictionary of the Bible, Waesene walijitenga hata zaidi kuliko Mafarisayo na “nyakati nyingine waliweza kuwa na mielekeo ya Kifarisayo kuliko Mafarisayo wenyewe.”
[Picha katika ukurasa wa 8]
Huenda ikawa wazazi wa Ayubu walimfundisha juu ya sheria zinazoongoza hayo makundinyota