Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 11/15 uku. 21
  • ‘Wasiotambua Mungu na Waangamie!’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Wasiotambua Mungu na Waangamie!’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maisha ya Mapema ya Polycarp
  • Ategemeza Kweli za Msingi
  • Kazi Yake Katika Smirna
  • Ni Nani Wasiotambua Mungu?
  • Kujitahidi Kuwa Washindi
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Mababa wa Kimitume—Je, Kweli Walifuata Mafundisho ya Mitume?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • ‘Dhidi ya Maarifa—Yaitwayo Hivyo kwa Ubandia’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Wengi Hudai Kuwa na Imani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 11/15 uku. 21

‘Wasiotambua Mungu na Waangamie!’

HALAIKI ya watu ilimhesabu kuwa mwanamume asiyetambua mungu yeyote, mwenye kutafuta kuwavunja moyo wasifanye ibada na kuharibu miungu yao. Kwa kudharauliwa na kupuuzwa, yeye aliletwa mbele yao katika kusanyiko la peupe. Gavana alipoulizia habari za kisa kile, mwanamume mwenye fahari wa miaka 86 alipiga hatua kwenda mbele akakiri kwamba hali yake imetambulishwa vizuri. Jina lake lilikuwa Polycarp.

Statius Quadratus gavana Mroma wa mkoa aliendelea kwa maneno haya; “Apa kwa akili nyingi za Kaisari; badili nia yako na useme, ‘Wasiokubali Mungu yuko na waangamie!’” Ndipo Polycarp akakaza macho kwenye ule umati mkubwa wa wapagani wasiotii sheria wenye kujaza stadiamu ile. Akiwapungia mkono, yeye akaugua moyoni, akatazama mbinguni, na kusema: “Wasiokubali kuna Mungu na waangamie!” Naam, ‘Wasiotambua Mungu na waangamie!’

Ndipo mkuu huyo wa mkoa akanena kwa uharaka mkubwa zaidi, akisema: “Fanya apizo nami nitakuacha huru; mtukane Kristo.” Lakini Polycarp akaitikia hivi: “Mimi nimemtumikia Huyo kwa miaka themanini na sita, na Yeye hakunitenda kosa lolote. Nawezaje kukufuru Mfalme wangu ambaye ameniokoa?”

Ndipo matayarisho yakafanywa ili mwanamume huyo mzee auawe. Mwili wake ungeliwa na moto. Kwa nini? Kwani Polycarp alikuwa nani hasa? Na ni matukio gani yaliyoongoza kwenye kifo chake?

Maisha ya Mapema ya Polycarp

Polycarp alizaliwa karibu 69 W.K. katika Esia Ndogo, kule Smirna (jiji la Kituruki la ki-siku-hizi la Izmir). Yaripotiwa kwamba yeye alilelewa na wazazi Wakristo. Alipokuwa akikomaa akawe muungwana mashuhuri, Polycarp alijulikana sana kuwa mtu mwenye ukarimu, mwenye kujinyima, mwenye kufadhili wengine, na mwenye kujifunza Maandiko kwa bidii ya uendelevu. Baada ya muda akawa mwangalizi katika kundi kule Smirna.

Imeripotiwa kwamba katika miaka yake ya mapema kidogo, Polycarp alitumia kwa faida fursa alizopata za kujifunza moja kwa moja kutokana na baadhi ya mitume. Yaonekana mtume Yohana alikuwa mmoja wa walimu wake. Kwa uhakika, Irenaeus asimulia kwamba Polycarp “si kwamba alifundishwa na mitume tu, na akaonana na wengi waliokuwa wameona Kristo, bali pia aliwekwa rasmi na mitume awe wa Esia, awe mwangalizi katika kanisa ambalo limo Smirna.” Twaweza kuwazia ni shangwe na uradhi ulioje ambao Polycarp alipata kutokana na ushirika huo wenye kunufaisha sana. Ni lazima uwe ulisaidia kumwandaa kwa ajili ya mgawo wake akiwa mwangalizi katika kundi.—Matendo 20:28; 1 Petro 5:1-4.

Ategemeza Kweli za Msingi

Uangalizi wa Polycarp juu ya kundi ulianza katika ile miaka yenye kutatiza ya uasi-imani uliotabiriwa. (2 Wathesalonike 2:1-3) Yaonekana yeye alikuwa na nia ya kujitumikisha kabisa kwa ajili ya wengine. Hivyo, wakati Ignatius wa Antiokia, Siria, akiwa njiani kwenda kuuawa katika Roma kwa sababu ya imani, alipowaomba Wafilipi wapeleke barua fulani kwenye kundi lake la nyumbani, Polycarp wa Smirna alihakikisha kwamba imepelekwa. Wakati huo yeye alipelekea Wafilipi barua yake mwenyewe.

Katika barua ambayo Polycarp aliwaandikia Wafilipi, sisi twapata uhakikisho zaidi wa kweli fulani za Kimaandiko. Yeye awatenganisha Mungu na Kristo kuwa watu tofauti, Baba na Mwana, na kusema kwamba ni “kwa penzi la Mungu kupitia Yesu Kristo” kwamba sisi twapata wokovu. Polycarp aonya dhidi ya kupenda pesa na akumbusha wasomaji wake kwamba waasherati na wanaume ambao hulala pamoja na wanaume hawatarithi Ufalme wa Mungu. (Linganisha 1 Timotheo 6:10; 1 Wakorintho 6:9, 10.) Pia ahusisha ndani mawaidha ya kwamba wake wapende waume zao na wazee wawe “wenye huruma na rehema.” Watu wote wahimizwa ‘wawe wenye bidii katika kufuatia kile kilicho chema.’ Mwisho, Polycarp asihi sana hivi: “Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, na Yesu Kristo Mwenyewe, ambaye ndiye Mwana wa Mungu, na Kuhani Mkuu wetu wa milele, na awajenge nyinyi katika imani na ukweli, na katika usikivu wote, uanana, saburi, ustahimilivu, uvumilivu, na utakato.”

Polycarp aliyanukuu Maandiko kwa wingi. Katika barua yake kwa Wafilipi, alirejezea Mathayo, Matendo, Waroma, 1 Wakorintho, 2 Wakorintho, Wagalatia, Waefeso, 2 Wathesalonike, 1 Timotheo, 1 Petro, na yaelekea visehemu vinginevyo vya Maandiko. Hii yatupa sisi kionyeshi cha kwamba angalau watu fulani wenye kujidai kuwa Wakristo walitafuta kushikamana na kanuni za Kimaandiko wakati wa kipindi kile kigumu kilichofuata kifo cha mitume.

Kazi Yake Katika Smirna

Smirna, jiji la kale la pwani la Esia Ndogo, lilikuwa lenye shughuli nyingi likiwa kitovu cha biashara yenye ufanisi. Pia kilikuwa kitovu cha ibada ya Serikali. Mathalani, wamaliki Waroma walionyeshwa wazi kuwa miungu katika sarafu na katika maandishi ya kuchongelea. Falsafa za dini ya kipagani ziliendelezwa na wenye mamlaka ya kifalme.

Ushuhuda waonyesha kwamba hesabu fulani ya wale walioshirikiana na kundi la Smirna walikuwa maskini kimwili. Lakini wakati mmoja, wao walipongezwa kwa kuwa matajiri kiroho. Ni lazima iwe Wakristo katika Smirna walitiwa moyo sana kusikia maneno ya Yesu yaliyoandikwa na mtume Yohana! Kristo alimwambia hivi yule “malaika,” au waangalizi wapakwa-mafuta, kule Smirna: “Mimi najua dhiki na umaskini wako—lakini wewe u tajiri—na kufuru la wale ambao husema wao wenyewe ni Wayahudi, na kumbe wao sio bali ni sinagogi la Shetani. Usiwe mwenye kuogopa vitu ambavyo wewe u karibu kupatwa navyo. Tazama! Ibilisi atafuliza kutupa baadhi ya nyinyi ndani ya gereza ili nyinyi mtiwe kenyekenye kwenye mtihani, na ili nyinyi muwe na dhiki siku kumi. Jithibitishe mwenyewe kuwa mwaminifu hata mpaka kifo, na mimi nitakupa wewe taji la uhai.”—Ufunuo 2:8-10, NW.

Utajiri wowote wa kiroho ambao huenda ukawa uliendelea miongoni mwa wenye kujiita Wakristo kule Smirna bila shaka ulihusiana moja kwa moja na uangalizi mzuri wa wazee wa kundi. Kipindi hicho kilikuwa cha jitihada ya kidini yenye msukosuko mwingi, na washiriki wa kundi walitumikia katikati ya itikadi na viibada vyenye kuhitilafiana. Eneo lao la kutolea ushahidi lilijawa na mazoea ya kishetani, kutia na ulozi na unajimu, na hivyo hali ya huko ilikuwa ya kutotambua Mungu.

Kuongezea uadui wa ile halaiki ya wapagani kulikuwako ile chuki kali yenye kuonyeshwa na Wayahudi. Wakati kuuawa kwa Polycarp kwa sababu ya imani kulipotukia katika Februari 23, 155 W.K., Wayahudi washupavu waripotiwa kuwa walisaidia kukusanya kuni. Walifanya hivi ingawa mauaji yale yalitukia katika siku ya Sabato kuu!

Ni Nani Wasiotambua Mungu?

Polycarp alikuwa amekusudia kubaki katika Smirna akabiliane na hatari ile wakati adui zake wangemjia. Lakini kwa kuhimizwa na wengine, aliondoka akaenda kwenye shamba la karibu. Alipojulikana alikokuwa, alikataa kuhama tena ili awaepe wale wenye kumtafuta lakini akasema hivi tu: “Penzi la Mungu na litendeke.”

Akiingia katika stadiamu ile, Polycarp alisimama mbele ya gavana na ule umati mkubwa wenye kasirani. Gavana alipozidi kumhimiza aonyeshe heshima ya ibada kwa Kaisari, Polycarp alisema wazi hivi: “Mimi ni Mkristo . . . Ikiwa wewe wataka kujua maana ya Ukristo, likupasalo kufanya tu ni kutaja siku fulani na usikie nitakayosema.” Gavana akajibu hivi: “Jaribu kuzisema hoja zako kwa umati wa watu.” Lakini Polycarp akasema: “Wewe ndiwe nilifikiri yastahiki kuzungumza nawe jambo hilo, kwa sababu sisi tumefundishwa kuzipa serikali na wenye mamlaka staha yote ifaayo . . . maadamu haitufanyi turidhiane msimamo wetu.” Muda mfupi baada ya hapo Polycarp alichomwa moto akafa kwa sababu hakutaka kumkana Yesu Kristo.

Mungu peke yake ndiye aweza kuamua msimamo wa Polycarp akiwa Mkristo ulikuwa wa hali gani hasa. Namna gani leo? Songamano kubwa la Wakristo wa kweli lakataa pia kumkana Kristo. Bali, wao wajulisha kwamba yeye ndiye Mfalme wa Kimesiya wa Mungu ambaye alitawazwa mbinguni. Pia Mashahidi hawa wa Yehova waonyesha wazi kwamba tuko karibu kuona utimizo wa maneno ya unabii wa Yesu kuhusu “dhiki kubwa,” tukio lenye maangamizi makuu kuliko yote ambayo ulimwengu utapata kuyajua. Hata hivyo, hii haionyeshi mwisho tu wa aina ya kibinadamu bali pia wa uovu. Kuokoka kwawezekana kuingia katika ulimwengu mpya mwadilifu wa amani na ufurahishi.—Mathayo 24:13, 21, 34; 2 Petro 3:13.

Ni nani angechagua kupigana dhidi ya wajumbe wenye habari nzuri za jinsi hiyo? Ni wale tu wasiotambua Mungu, hata ikiwa wana “namna fulani ya ujitoaji kimungu.” (2 Timotheo 3:5, NW) Mafundisho bandia ya kidini yamepofusha akili za watu fulani, na wengi ‘wanasikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani.’ (1 Timotheo 4:1) Wakristo wa kisasa wameteseka mikononi mwa wasiotambua Mungu, baadhi yao kufikia kifo. Lakini watumishi wenye imani wa Yehova hawatakata kamwe tumaini, kwa maana hatimaye watapata zawadi ya Mungu ya uhai wa milele. Kwa sasa, wapiga mbiu hawa waaminifu wa Ufalme wa Mungu wabakia wakiwa watetezi thabiti wa ukweli wa Kimaandiko.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki