Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Kwa nini Sheria ya Mungu ilisema kwamba ilikuwa lazima mwanamume Mwisraeli aliyefanya ngono na bikira asiyeposwa afunge ndoa naye na hangeweza kumtaliki kamwe?
Kwenye Kutoka 22:16, 17 na Kumbukumbu 22:28, 29, twapata sheria hii, ambayo watu fulani wamedai kwamba yaonekana kutokuwa na huruma kuelekea wanawake. Kwa kweli, ilitia moyo kwamba kiwango cha maadili kiwe cha hali ya juu kwa wanaume na wanawake pia.
Kumbukumbu sura ya 22 ilitokeza sheria mbalimbali za kinyumbani. Mathalani, ilishughulika na hali ya mwanadamu ambaye hakumpenda tena mke wake na akadai kwamba hakuwa amekuwa bikira. Pia ilitokeza sheria za Mungu kuhusu uzinzi na kunajisi. Ndipo twasoma hivi:
“Mtu mume akimwona kijana aliye mwanamwali [bikira] ambaye hajaposwa, akamshika na kulala naye, wakaonekana; yule mtu mume aliyelala naye na ampe baba yake yule kijana shekeli hamsini za fedha, kisha na awe mkewe, kwa kuwa amemtweza; hana ruhusa ya kumwacha siku zake zote.” — Kumbukumbu 22:28, 29.
Hiki kilikuwa kisa cha kutongozwa kinguvu na/au cha uasherati. Ikiwa mwanamume asiyejali sana kufuata kanuni angehisi akiwa na uhuru mwingi sana wa kufanya ngono na bikira, bikira huyo ndiye hasa angepatwa na hasara. Zaidi ya kuwapo uwezekano wa kwamba angeweza kupata mtoto wa haramu, thamani yake ya kuwa bibi-arusi ilipungua, kwa maana huenda Waisraeli wengi wasitake kumwoa akiisha kuwa si bikira tena. Ingawa hivyo, ni jambo gani lingevunja mwanamume moyo asijione huru sana kuchezea bikira? Ni Sheria ya Mungu iliyo “takatifu na adilifu na njema.”—Warumi 7:12, NW.
Fungu la sheria za Musa lilikuwa na uandalizi wenye kuruhusu mwanamume ataliki mke wake kwa sababu fulani-fulani. (Kumbukumbu 22:13-19; 24:1; Mathayo 19:7, 8) Lakini tusomayo kwenye Kutoka 22:16, 17 na Kumbukumbu 22:28, 29 yaonyesha kwamba hiari ya kutaliki ilimalizika baada ya uasherati kufanywa kabla ya ndoa. Basi, jambo hili lingeweza kusababisha mwanamume (au mwanamke bikira) akinze kishawishi cha kushiriki katika uasherati. Mwanamume hangeweza kuhisi kwamba, “Mwanamke huyu ana sura nzuri na mwenye kusisimua, kwa hiyo nitaona raha pamoja naye hata ingawa si wa namna ile ambayo ningependa kuoa.’ Bali, sheria hii ingezuia ukosefu wa adili kwa kusababisha yeyote ambaye angetaka kuwa mkosaji apime uzito wa matokeo yenye kuendelea kwa muda mrefu ambayo yangetokana na uasherati—kulazimika kukaa pamoja na mtu yule mwingine muda wa maisha yake yote.
Pia Sheria ilipunguza tatizo la uanaharamu. Mungu alijulisha rasmi hivi: “Mwana wa haramu asiingie katika mkutano wa Bwana [Yehova, NW].” (Kumbukumbu 23:2) Kwa hiyo mwanamume aliyetongoza bikira alilazimika kumwoa, uasherati wao haungetokeza watoto wa haramu miongoni mwa Waisraeli.
Ni kweli kwamba Wakristo huishi katika muundo wa hali ya kijamii iliyo tofauti na ile ya Waisraeli wa kale. Sisi hatuko chini ya maamuzi rasmi ya Sheria ya Musa, kutia na sheria hii yenye kutaka ndoa ya watu wawili waliojitia katika uasherati huo. Hata hivyo, hatuwezi kuhisi kwamba kujitia katika uasherati wa kabla ya ndoa ni jambo dogo tu. Wakristo wapaswa kufikiria kwa uzito matokeo yenye kuendelea kwa muda mrefu, sawa na vile sheria hii ilivyowasukuma Waisraeli kufanya hivyo.
Kutongoza mtu asiyefunga ndoa huharibu haki ya mtu huyo ya kuingia ndoa ya Kikristo akiwa bikira safi (wa kiume au wa kike). Uasherati wa kabia ya ndoa huathiri pia haki za mtu yeyote ambaye huenda akaja kuwa mwenzi wa ndoa wa mtu mwenye kufanya hivyo, yaani, haki ya mtu huyo ya kufunga ndoa na Mkristo aliye safi. Zaidi ya yote, ni lazima uasherati uepukwe kwa sababu Mungu asema kwamba ni kosa; ni dhambi. Kwa kufaa mtume aliandika hivi: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati.”—1 Wathesalonike 4:3-6; Waebrania 13:4.