Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 12/1 kur. 28-30
  • Mimi Nilipanda Mlima Ulio Mzuri Kupita Yote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mimi Nilipanda Mlima Ulio Mzuri Kupita Yote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mzinduko
  • Funzo la Biblia
  • Kutolea Wengine Ushahidi
  • Matterhorn wa Kipekee
    Amkeni!—1996
  • Tunahitaji Milima
    Amkeni!—2005
  • “Una Utukufu Kuliko Milima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 12/1 kur. 28-30

Mimi Nilipanda Mlima Ulio Mzuri Kupita Yote

MIMI nilizaliwa na kulelewa katika mji mdogo katika milima ya Ulaya ya Mashariki. Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki Waroma, lakini hawakunifanya nihudhurie kanisa na nyumbani hatukusali pamoja wala kuongea kuhusu dini. Kwa hiyo, kama vijana wengine wengi, nilitumia wakati na nishati zangu katika michezo, elimu na usafiri.

Katika mji wetu, kulikuwako kikundi chenye utendaji mwingi cha wapanda milima kikiongozwa na mwanamume mmoja mfadhili mwenye ujuzi ambaye alijua mengi kuhusu milima. Asante zimwendee yeye, mimi nilipata kuwa mwenye ujuzi sana katika kupanda milima. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 18, na upesi niliingiwa na mapenzi mengi ya kutazama mandhari za kuvutia sana nikiwa katika vilele vya juu, nikasisimuka kukabiliana na hali zenye hatari na kuziokoka, na kufanya urafiki na wengine walioshiriki hatari hizo.

Naikumbuka pindi moja baada ya mimi kuwa katika kikundi kile kwa miaka mitano. Nilikuwa nikipanda mlima mahali ambapo mtandao wa ardhi ulikuwa rahisi, nami nikapunguza uangalifu mwingi niliokuwa nao wakati ule nilipokuwa ndiyo ninafikia kileleta. Nilipokaribia sehemu ya juu ya tungamo-mwamba, lilianza kumomonyoka. Sikuwa na la kufanya ila kuruka kando na kupaaza sauti ya onyo kwa mpandaji mwenzangu. Mwamba wenye kuanguka uliikata kamba yenye kutuunganisha pamoja, nami nikaanguka. Jambo la kufurahisha ni kwamba anguko langu lilizuiliwa na utambarare mdogo wenye nyasi meta 4 tu pale chini. Hata hivyo, si sikuzote ambapo mambo huenda vizuri jinsi hiyo katika mchezo huu!

Nikiwa na umri wa miaka 24, nilihitimu chuo kikuu nikatwaa uongozi wa kikundi kidogo cha wapanda milima katika mji wa nyumbani kwetu. Baada ya kitambo, tulichanga pamoja pesa fulani za kununua basi ndogo ili tuweze kujipeleka wenyewe na vifaa vyetu kwenye milima ya mbali zaidi. Lakini gari hilo lilikuwa katika hali mbaya, nami nilitumia miezi mitatu, mchana na usiku, nikilitengeneza. Lilipokuwa tayari, sisi sote tulitafuta-tafuta kazi hatari zenye malipo mazuri, kama kazi ya kujenga sehemu zilizoinuka sana, na kwa njia hii tulikusanya pesa hatimaye ili tufunge safari ya kwenda Iran. Huko, katika 1974, tulipanda volkeno yenye urefu wa meta 5,800 yenye kuitwa Damavand. Ingawa mpando ule ulianza kwa urahisi sana, kuelekea sehemu ya juu tulilazimika kuvumilia theluji ya kina kirefu, pumzi chache kwa sababu ya kimo kile, na mioshi yenye madhara iliyotoka katika matundu ya volkeno.

Tukiwa njiani kurudi nyumbani katika ile basi ndogo, tulipanga kupanda Mlima Ararati lakini tukalazimika kufuta jambo hilo kwa sababu ya misukosuko ya kisiasa. Katika 1975 tulienda kuteleza katika barafu katika Msafa wa Milima Alps ya Austria, na wakati ule ule, tukaanzisha shindano la kupiga picha kote kote taifani na tukaliita “Wanadamu na Milima.” Shindano hili lingali lafanywa kila mwaka. Sisi sote tulikuwa na hisia ya kwamba maisha zetu zilijawa na kusudi na zilikuwa za kuridhisha.

Mzinduko

Hata hivyo, nilipofika karibu miaka 30, nilianza kuchoshwa na upandaji milima nami nikashangaa kwa kujiuliza hivi: ‘Je! kweli maisha ndiyo aya haya tu?’ Watu fulani waliniambia nifunge ndoa, lakini mimi nilikuwa na rafiki waliokuwa wamefunga ndoa, nao hawakuonekana wakiwa wenye furaha sana. Hata wenzi wa ndoa ambao uhusiano wao ulifanyika katika ile hatari na ule msisimuko wa kupanda milima walionekana kuwa wakipoteza furaha yao katika uhalisi wa maisha ya siku baada ya siku. Mimi sikujua kwa nini ndoa zao hazikuwa na furaha, lakini ingawa mimi mwenyewe ningalipenda sana kufunga ndoa, sikutaka kukosa furaha kama wao.

Kwa kuongezea, niliona badiliko katika vijana walioenda kupanda milima. Kabla ya kwenda, sikuzote kulikuwa kumekuwako roho ya nidhamu, ushirikiano, na urafiki katika kambi za kupanda msafa wa milima Alps. Sasa, wavulana wachanga na wasio na ujuzi hawakuwa na nidhamu na hawakutosheka kufanya maendeleo ya pole kwa pole. Wao walitaka kujionyesha na kufanya mipando iliyokuwa migumu mno na hatari kwa kadiri iliyowazidi wao kwa mbali. Kwa kuhisi nikiendelea kuzinduka zaidi na zaidi, nilifanya mazungumzo ya muda mwingi na yenye kina kirefu pamoja na Bonjo rafiki yangu. Mwishowe akadokeza niongee na mpanda mlima mwenzangu, Henry.

Henry aliniazima kitabu, Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele, nami nilipokisoma, niligutuka kuona jinsi kilivyozungumza juu ya maswali yaliyokuwa yamekuwa yakinishangaza moyoni mwangu. Kumbe Henry alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo nikauliza kama ningeweza kujiunga. Alikubali, na kwa miaka miwili nikajihusisha katika kujifunza kwa bidii nyingi Biblia na fasihi zozote za Biblia ambazo ningeweza kuzipata.

Funzo la Biblia

Maarifa yangu yalipoongezeka, nilihisi shangwe yenye kuongezeka. Mimi nilikuwa na uzoeani wa kijuujuu tu pamoja na dini ya Katoliki ya Roma, lakini niligutuka kuona kwamba Ukristo wa Biblia haukutegemea sherehe, mapokeo, na hisia-moyo zisizo za kiakili. Bali, ulihusisha ndani kanuni za maadili ya hali ya juu ambazo ziliathiri kila sehemu ya maisha ya Mkristo. Kwa kuongezea, nilishangaa sana kuona kwamba Biblia husababu mambo kiakili sana na haipingani na nadharia za kisayansi ambazo zimethibitishwa sana kuwa za kweli.

Shahidi aliyeongoza mazungumzo pamoja na Henry na mimi hakutulazimisha kubadili maoni yetu na njia yetu ya maisha. Alilofanya tu ni kueleza wazi mambo yasemwayo na Biblia. Kwa sababu hiyo, mimi niliendelea kupanda milima kwa miaka miwili ya kwanza ya kujifunza. Lakini maarifa yangu yalipoongezeka kina, nikapata kung’amua kwamba upandaji milima ulikuwa kwangu kama kitu kilichonikolea mwilini. Pia aksidenti ya ule mwamba wenye kuanguka ilinikumbusha juu ya maneno ambayo Yesu alimwambia Shetani wakati Shetani alipomtolea wito wa ushindani kwamba ajivurumishe chini kutoka kwenye dari ya mnara wa hekalu: “Usimjaribu Bwana [Yehova, NW] Mungu wako.” (Mathayo 4:5-7) Niling’amua kwamba utendaji huu ulionyesha ukosefu wa staha kwa uhai ambao Yehova alikuwa amenipa.

Kwa hiyo nikampa mpandaji mwingine mwenye ujuzi daraka la kusimamia kikundi chetu cha wapanda milima na nikapata kwamba haikuwa vigumu kuvuka kutoka upande huu wa kupanda milima kwenda upande ule mwingine wa Ukristo. Nilipokuwa nikiwapa watu au nikiwauzia vifaa vyangu vyote—vyombo vya kutelezea katika barafu, vyuma vya kupandia, vichomekwa-ardhini vilivyoungana na kamba za kupandia, nyundo, misumari iliyo kama ndoana, na shoka la barafuni—nikitumia maneno ya mtume Paulo, naweza kusema kwa moyo mnyoofu kwamba sasa vitu hivyo vilikuwa “mavi” tu. (Wafilipi 3:8) Hisia ya uradhi wa kina kirefu ilikuja juu yangu nilipoweza kujiunga katika kazi ile kubwa ya kusifu jina la Mungu peupe. Katika 1977 Henry na mimi pia tulifananisha wakfu wetu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji.

Kutolea Wengine Ushahidi

Wakati huo, kulikuwako washirika 15 hivi wa kikundi kile cha wapandaji milima katika mji wetu, na polepole Henry na mimi tuliwatolea wote ushahidi. Ilikuwa shangwe iliyoje wakati ndugu yangu, aliyekuwa mshirika pia, alipoanza kujifunza Biblia, akiwa pamoja na mke wake, na akabatizwa katika 1981. Muda fulani baadaye, Bonjo alijiunga nasi, na pia mwingine mmoja, yule wa tano wa klabu cha wapanda milima. Haikuwa lazima tena tupande milima mirefu. Raha yetu iliyo kubwa zaidi ilikuwa kuwazuru katika bonde watu waliothamini ukweli wa Biblia. Pia mama yangu, aliyekuwa amekuwa akiona wasiwasi mwingi kuhusu utendaji wa ndugu yangu na mimi wa kupanda milima, alipokea badiliko hili kwa kuhisi kitulizo kikubwa. Hatimaye, yeye pia alijiunga nasi katika ile ibada safi ya Yehova.

Sasa nilikuwa nimepoteza uharaka wa tamaa yangu ya kufunga ndoa. Asante kwa Neno la Mungu, mimi nilizijua kanuni ambazo zingenisaidia nifanikishe ndoa, lakini sasa nilifurahi kuwa mseja na kutumikia Yehova bila kuvutwa fikira kando. Sulemani alijulisha wazi hivi: “Mke mwenye busara, mtu hupewa na Bwana [Yehova, NW].” (Mithali 18:22; 19:14) Kwa hiyo, mimi niliamua kumngojea Yehova kwa saburi ili anipe zawadi hii, kwa wakati wa sasa niwe ninaishi kwa njia ambayo ningekuwa mume mwenye ustahiki wakati ambapo jambo hilo lingetukia. Katika 1982 ndipo Yehova aliponipa ile baraka nzuri ajabu ya mke mzuri sana.

Mke wangu na mimi tungali twaishi katika milima, nami ningali naipenda. Lakini hangaikio letu kuu sasa ni kusaidia watu wapande mlima mwingine. Mlima upi huo? Ule wenye kutajwa katika unabii wa .Isaya: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya Bwana [Yehova, NW] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana [Yehova, NW], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana [Yehova, NW] katika Yerusalemu.” (Isaya 2:2, 3) Imekuwa shangwe iliyoje kuweza kuupanda mlima huu ulio mzuri kupita yote!—Imechangwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki