Habari Njema kwa Aina ya Binadamu Yote!
“MIMI nikaona malaika mwingine akiruka katika mbingu ya kati, na yeye alikuwa na habari njema za milele kujulisha wazi kuwa taarifa teremeshi kwa wale ambao hukaa juu ya dunia, na kwa kila taifa na kabila na ulimi na kikundi cha watu.” (Ufunuo 14:6, NW) Kwa maneno hayo, mtume Yohana mzee alieleza njozi yake ya kiunabii iliyovuviwa, njozi yenye kutimizwa katika siku yetu wenyewe. Ni kitulizo kama nini kujua kwamba kuna habari njema katika kipindi hiki cha uhalifu wenye kuongezeka, uchafuzi, uvamizi-haramu, vita, na mashaka yaliyoenea sana kuhusu hali ya uchumi! Lakini ni habari gani zingeweza kuwa njema sana hivi kwamba zahitaji malaika azitangaze? Ni taarifa gani zingeweza kuwa za kuteremesha kwa kiasi cha kustahili kujulishwa wazi kwa kila taifa na kabila na ulimi na kikundi cha watu?
Twaweza kujibu hilo tukirudisha fikira nyuma kwenye pindi nyingine ambapo malaika alitangaza habari njema yeye binafsi. Hii ilikuwa wakati karne ya kwanza K.W.K. ilipokuwa ikikaribia mwisho, karibu miaka mia moja kabla Yohana hajaona njozi yake. Wachungaji walikuwa nje makondeni wakiwa pamoja na makundi yao karibu na Bethlehemu, na malaika akatokea atangaze kuzaliwa kwa Yesu, akisema: “Ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote; maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana.”—Luka 2:10, 11.
Kwa kweli uzaliwa wa Yesu ulikuwa “habari njema ya furaha kuu.” Yeye alikua akawa ndiye Kristo na Mwokozi aliyeahidiwa, yule aliyetoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ili waamini wenye mioyo ifaayo wapate kuishi. Zaidi ya hilo, alipaswa awe Mfalme wa Ufalme wa Mungu, “Mwana-Mfalme wa Amani,” ambaye chini ya utawala wake haki na amani ingekuja mwishowe kwa aina ya binadamu. (Isaya 9:6, HNWW; Luka 1:33) Kwa kweli, uzaliwa wake ulikuwa habari njema zilizostahili kutangazwa na malaika!
Yesu Ni Mfalme
Kule nyuma katika karne ya kwanza, Yesu alitimiza mengi ya makusudi ambayo Mungu alimkusudia, lakini hakutawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu wakati huo. Kama vile gazeti hili limeonyesha wazi mara nyingi, jambo hilo halikutukia mpaka 1914. Kama vile utimizo wa unabii uonyeshavyo wazi, katika mwaka huo Ufalme wa Mungu ulisimamishwa imara katika mbingu. (Ufunuo 12:10, 12) Ingawa zilikuwako habari mbaya sana katika 1914—kutokea kwa Vita ya Ulimwengu 1—uzaliwa wa Ufalme wa Mungu ulikuwa ndizo habari bora zaidi. Ndiyo sababu Yesu alitoa unabii huu kwa siku yetu: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:14.
Je! unabii wa Yesu umetimizwa? Jibu ni ndiyo! Na njozi ya kiunabii ya Yohana imetimizwa pia. Ni kweli kwamba sisi hatuwezi kumwona malaika asiyeonekana ambaye Yohana alimwona. Lakini Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakionekana sana kwa kuwa wametangaza habari njema ambazo yule malaika anazo “kwa kila taifa na kabila na ulimi na kikundi cha watu.” Katika mabara 212 na visiwa vya bahari, sauti zao zimesikiwa. Na umati wa watu unaitikia. Maono ya baadhi ya watu hawa yataonyesha ni jinsi gani hasa habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu zilivyo.