Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Ushahidi wa Vivi Hivi Wazaa Matunda
YESU alifungua maongezi yaliyoongoza kwenye ushahidi wa vivi hivi lakini wenye matokeo sana aliposema hivi kwa mwanamke Msamaria kisimani: “Nipe maji ninywe.” (Yohana 4:7) Sisi leo twaweza vivyo hivyo kuwa wenye matokeo sana tukiwa chonjo kuona fursa zote za kutoa ushahidi wa vivi hivi. Ndugu mmoja katika Australia aliwasha cheche ya maongeo ya vivi hivi kwa kusoma andiko la siku akiwa amekalia benchi ya bustani ya starehe. Mwanamume mtaka kujua aliona kichapo hicho na akasema alipendezwa pia na Maandiko. Alikuwa Mkatoliki asiye mtendaji aliyekuwa amefundishwa mageuzi katika shule ya Kikatoliki na sasa hakujua la kuamini. Ndugu huyo alipanga kumtafutia kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?a Siku mbili baadaye alipeleka kitabu hicho mahali pa kazi pa mwanamume huyo, lakini akakuta ametoka nje. Mhazili (sekretari) wake alinyakua kitabu hicho, akisema: “Tumekuwa tukingojea kitabu hiki.”
Saa mbili baadaye ndugu huyo akapokea simu kutoka kwa yule mwanamume akiomba nakala mbili zaidi za kitabu Creation na kuomba Shahidi huyo amzuru katika ofisi yake. Ndugu huyo alipoenda kwenye ofisi hiyo, alikuta mwanamume huyo na wengine wawili. Funzo la Biblia lilianzwa pamoja na wao, kutia na mhazili, na ikapangwa kwamba ndugu huyo awatembelee mara mbili kwa juma. Katika majuma yaliyofuata, rafiki msichana wa mwanamume huyo, akiwa ‘Mkristo aliyezaliwa tena,’ aliendelea kupeleka vibarua vya kuuliza maswali ya Biblia. Mwishowe, alijiunga na funzo hilo, hali moja na mwanabiashara mwenzi wa mwanamume huyo na rafiki yake, aliyekuwa mwamini mageuzi.
Waliendelea na mafunzo yao ya Biblia kwa ukawaida kwa miezi mitano, huku funzo la pili kila juma likiongozwa katika bustani ya starehe. Halafu rafiki mvulana wa yule mhazili akajiunga na kikundi hicho. Muda mfupi baada ya hapo, mwenzi wa kwanza wa mwanamume huyo na rafiki yake walihamia Idaho katika United States, ambako waliendelea kujifunza. Majuma machache baadaye, yule mwanamume wa kwanza alifikiwa na mtu asiyemjua kabisa, akamwuliza ilikuwa imekuwaje kwa mazungumzo ya Biblia katika bustani ya starehe. Yaonekana kwamba yeye alikuwa amekuwa akisikiliza mafunzo yao. Alifanyiwa mipango ili ajifunze pia.
Tokeo la yote haya lilikuwa nini? Miezi kumi na minane kuanzia kuonana kwao mara ya kwanza katika bustani ya starehe, mwanamume yule wa kwanza na rafiki yake msichana, ambaye hapo kwanza alikuwa ‘Mkristo aliyezaliwa tena,’ wakawa wamefunga ndoa na kubatizwa. Yule mhazili na rafiki yake mvulana walifunga ndoa pia na kubatizwa. Yule mwanabiashara mwenzi na rafiki yake walioenda United States wakabatizwa, na sasa mmoja wao atumikia akiwa painia msaidizi kwa ukawaida. Yule aliyesikiliza mazungumzo ya Biblia yenye kuendelea katika bustani ya starehe aliendelea na mafunzo. Halafu akahamia Ailandi, na alikuwa akitazamia kubatizwa!
Yote haya yalitukia kwa sababu ndugu mmoja alitumia kwa manufaa pumziko lake la chakula cha mchana ili kutoa ushahidi wa vivi hivi, na Yehova akabariki jitihada zake. Sisi na tutumie kwa manufaa hayo hayo kila fursa ya kueneza habari njema kwa wale wanaoona njaa ya ujumbe wa Ufalme wa Yehova!
[Maelezo ya Chini]
a Kimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.