Ukaribishaji-Wageni wa Melita Waleta Mibaraka
MELITA (Malta) ilikuwa kituo kizuri cha nchi kavu kwa mtume Paulo alipovunjikiwa meli katika karne ya kwanza W.K. Wakaaji wa kisiwa hicho walipokea yeye na wasafiri wenzake “kwa njia yenye msaada.” Kwa uhakika, Wamelita (Wamalta) hawa waliwaonyesha wasafiri hao “fadhili ya kibinadamu izidiyo ile ya kawaida.”—Matendo 28:1, 2, NW.
Baadaye, Publio, mwanamume mkuu wa kisiwa hicho alipokea Paulo na waandamani wake kwa ukaribishaji-wageni na ‘kuwapa upokezi wa kihisani kwa siku tatu.’ Habari zilipoenea kwamba mtume ameponya baba ya Publio homa na kuhara damu, “wale watu wengine katika kisiwa hicho waliokuwa na magonjwa walianza pia kumjia na kuponywa.” (Matendo 28:7-9, NW) Lakini Paulo alifanya mengi zaidi. Alipanda mbegu za ukweli katika mioyo ya watu hao, na hilo likatokeza mibaraka mingi kwa wanakisiwa hao wenye ukaribishaji-wageni. Leo, jambo hilo hilo linatendeka katika Melita. Sasa njoo uone.
Wageni Wenye Kuzuru Waleta Habari Njema
Ikionwa kutoka hewani, Melita hung’aa kama johari iliyowekwa katika ile bahari buluu ya Mediterania. Afikapo Uwanja wa Ndege wa Luga, mgeni mwenye kuzuru huona bara lililokaushwa na jua likionekana kana kwamba lina ujanijani kidogo tu. Atuapo chini, yeye hupata kujua kwamba kisiwa hiki cha kilometa 11 kwa 16 ndiyo makao ya wakaaji wakadiriwao kuwa 347,000. Makuba na vinara-chongoka vya makanisa na makathedro mengi sana ya Melita hufunua kwamba dini imekuwa huko tangu zamani. Lakini katika karne hii ya 20, Wamelita wamenufaikaje kutokana na ziara za Mashahidi wa Yehova?
Mwangalizi mmoja mwenye kusafiri ambaye jina lake ni David alitembelea makao ya Juliana akamkuta akiwa na utayari wa kuitikia ujumbe wa Ufalme. “Mimi nilikuwa nimeudhika sana na mhusiko wa kanisa katika siasa,” asema Juliana, “na kwa hiyo mimi nikajaribu kutafuta katika Biblia ukweli juu ya serikali ya Mungu. Lakini nilipokuwa nikiisoma, kuna mambo ambayo sikuweza kuelewa kwa urahisi. Wazia jinsi nilivyoamshwa kupendezwa wakati mtembeleaji huyu kwenye mlango wangu alipouliza kama nilijua Ufalme wa Mungu ni nini! Mara hiyo, nilimwomba anionyeshe jibu katika Biblia yangu ya Kikatoliki. Akafanya hivyo. Siku hiyo hiyo nikajua nimeupata ukweli.”
Shahidi wa huko alipanga funzo la Biblia na Juliana. David aliporudi Melita miezi sita baadaye, ulikuwa mshangao ulioje kukaribishwa na Juliana ndani ya Jumba la Ufalme! Baada ya muda mfupi mwanamke huyo akawa tayari kuwa mhubiri wa habari njema za Ufalme.
Mume wa Juliana, Francis, alikuwa pia amevurugwa na mafundisho ya kanisa. Mume huyo alipokuwa akimzuru Juliana katika pindi ambapo Juliana alikuwa hospitalini, alimkuta huyo mke wake akisikiliza mirekodi ya kanda za hotuba za watu wote za Biblia zilizotolewa kwenye Jumba la Ufalme. Aliposikia habari juu ya familia, Francis aliona jinsi ushauri wa Kibiblia ulivyo timamu, na tokeo ni kwamba, yeye aliamua kuanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Muda si muda akajua tatizo lililokuwa lazima litatuliwe. Lilikuwa nini?
Kwa miaka kama 20, Francis alikuwa amefanya kazi akiwa mchukua-pesa kwenye ju-mba la kamari. Sasa aling’amua kwamba kazi iliyohusisha kucheza kamari haipataniki na kanuni za Kikristo ambazo hulaani vikali pupa na choyo. (Warumi 13:9, 10; 1 Wakorintho 6:9, 10) “Ingawa kwanza nilikosa imani iliyohitajiwa ili kubadili kazi yangu,” akiri Francis, “nilisali nipate msaada wa Yehova. Mwishowe, nilipata kazi nyingine ambayo huniwezesha nitunze mke na mwana wangu, Sandro.” Leo, Francis hutumikia akiwa mzee katika kundi la kwao la Mashahidi wa Yehova.
Faraja Kutokana na Maandiko
Rose alikuwa ameolewa na George akiwa mwenye furaha kwa miaka sita wakati mume huyo alipopatwa na msiba wa kifo katika aksidenti. Mwanamke huyo hakupata faraja hata kidogo katika kazanio la padri kwamba Mungu alikuwa amemchukua George kwa sababu ya kuwa mwenye wivu kwa upendo ambao mwanamke huyo alikuwa nao kwa mumeye. Rose alishuka moyo sana hivi kwamba alifikiria kuua watoto wake watatu halafu ajiue mwenyewe.
Lakini ni badiliko lililoje lililompata Rose wakati Shahidi jirani jina lake Helen alipoanza kuongoza naye funzo la Biblia! Muda si muda Rose alifarijiwa na lile fundisho la Kimaandiko la ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Wakati ule ule, kitia-moyo kilikuja kutoka kwa Peter, mwangalizi mwingine mwenye kusafiri. Rose alinufaika sana kutokana na hotuba zake juu ya ufufuo. Kwa kuchochewa na tumaini hili, Rose alijiunga na Helen katika kutoa ushahidi wa peupe, na wote wawili sasa hutumikia wakiwa mapainia wa kawaida, au wahubiri Ufalme wa wakati wote.
Kitia-Moyo cha Kuwa Wenye Bidii
Joe alitoka katika familia kubwa, kwa maana alikuwa na ndugu na dada 12. Kwa kutiwa moyo na mwangalizi mwenye kusafiri, kwa bidii aliwatolea ushahidi watu wa ukoo wake ambao ni wengi. “Mwanzoni,” yeye asema, “familia yetu ilijua kwamba mambo niliyowaeleza kutokana na Biblia yalikuwa ya akili. Lakini walipoona kwamba upendezi wangu wa kuwa Shahidi uliongezeka, walibadili nia, na wote wakawa dhidi yangu—hasa baba yangu.” Je! mtazamo wao uliizima bidii ya Joe?
Hata kidogo! Mathalani, wakati mtoto wa mmoja wa dada zake alipokuwa mgonjwa na karibu kufa, Joe alimtolea ushahidi dada yake, akasema naye kwa uhakika juu ya tumaini la ufufuo. Sasa dada huyu ni Shahidi aliyebatizwa wa Yehova. Halafu, mmoja wa ndugu wakubwa zaidi wa Joe na familia yake wakaonyesha kupendezwa na ukweli. Kisha ndugu aliye mkubwa kabisa na familia yake wakachukua msimamo upande wa Ufalme wa Mungu. Wakati uo huo, baba ya Joe alikuwa akipatwa na kasirani nyingi zaidi na zaidi. Dada mchanga kabisa wa Joe alipoanza kujifunza Biblia, baba huyo alimwondosha Joe katika makao ya familia. Bila kuzuiwa na hilo, Joe akatumia kila pindi kuwazuru watu wa ukoo wake na kuongea juu ya ujumbe wa Biblia. Bado, baba yake alitenda kwa kasirani na kusema: “Mbona usiseme na padri? Yeye ndiye aijua Biblia vizuri kabisa!” Joe alijibu kwamba angeterema kufanya hivyo ikiwa baba yake angeandamana naye. Ziara yao ilikuwa na tokeo gani?
“Tulipanga siku na wakati,” Joe asimulia, “lakini padri alitaka kujua angejitayarisha kwa ajili ya habari gani, akieleza kwamba kwa kuwa alikuwa ameondoka kwenye seminari miaka saba mapema, sasa angehitaji kufanya utafiti fulani. . . . Lakini baada ya juma moja, mwezi mmoja, na hata miezi miwili, padri hakutimiza mwadi wake. Baba yangu alipoona hilo, alibadili nia yake juu ya kanisa na pole kwa pole akang’amua kwamba mambo niliyokuwa nimejifunza kutokana na Biblia yalikuwa ya kweli.” Mwishowe baba ya Joe aliukubali ukweli, hiyo ikifanya hesabu ya washiriki wa familia yake wenye kujitia katika utumishi wa Yehova iwe 29.
Ushauri Wenye Msaada Waleta Mibaraka
Akisema kwa idili juu ya mwangalizi mwingine mwenye kuzuru, mhudumu painia aliyefunga ndoa jina lake Ignatio aeleza hivi: “Paul na mke wake walikuja kukaa nasi. Walitusaidia sisi wote wawili katika uhusiano wetu wa ndoa na pia katika huduma ya shambani. Sikuzote yeye [Paul] alikazia umaana wa kuhubiri.”
Ignatio akumbuka lililotukia wakati Paul alipokutana na wazee wa kundi na watumishi wa huduma wakati wa ziara yake ya mwisho. “Niliposema nilitaka kuondoa wakati fulani kwenye kazi ya kuhubiri asubuhi hiyo ili nilitayarishe sehemu yangu katika programu kwenye mkutano fulani,” asema Ignatio, “Paul alisema kwamba yeye angeenda katika utumishi wa shambani kama ilivyopangwa hata kama mimi singeweza kuandamana naye. Hapo basi, mimi nikaamua kwenda pia. Yehova alibariki uamuzi wangu kama nini! Asubuhi hiyo nilianzisha funzo la Biblia, na kutokana nalo, sasa watu sita wamo katika ukweli.”—Linganisha 3 Yohana 4.
Badilishano la Kitia-Moyo
Kila wakati mzee mwenye kusafiri azurupo Mashahidi wenzake katika Melita, wao humpokea kwa ukaribishaji-wageni na huwa na hamu ya kunufaika kutokana na kitia-moyo na himizo lake. (Linganisha 3 Yohana 5-8.) Tokeo ni kwamba, Wamelita wengi zaidi na zaidi wanachukua msimamo imara upande wa Yehova Mungu na Ufalme wake. Kufikia mwisho wa mwaka wa utumishi wa 1989, 389 kati ya wanakisiwa hawa wenye ukaribishaji-wageni walikuwa wamefanya hivyo. Sasa wakiwa wamepangwa kitengenezo kuwa makundi matano yenye kusitawi (manne katika Melita na moja katika kisiwa cha hapo karibu cha Gozo), kwa ujasiri wao hupiga mbiu ya zile habari njema.
Waangalizi wote wenye kusafiri waliogawiwa kuzuru Melita katika miaka ya majuzi wamehisi kama mtume Paulo, aliyewaambia hivi Wakristo Waroma: “Mimi natamani sana kuwaonya nyinyi, ili kwamba mimi nipate kuwapa nyinyi zawadi fulani ya kiroho ili nyinyi mfanywe imara.” Kwa kweli ziara zao zimetokeza “badilishano la kitia-moyo” chenye kuburudisha. (Warumi 1:11, 12, NW) Zaidi ya hilo, utendaji mbalimbali wa kuhubiri Ufalme kwa Mashahidi wa Yehova unawaletea mibaraka mingi ya kiroho wale watu wa Melita wenye ukaribishaji-wageni.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 24, 25]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
GOZO
COMINO
MELITA (MALTA)
Valleta
Bahari ya Mediterania
km 8
ml 5