Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 1/1 kur. 20-23
  • Hazina Yenye Thamani Kubwa ya Kushiriki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hazina Yenye Thamani Kubwa ya Kushiriki
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kielelezo Chenye Kuchochea cha Mama
  • Kushiriki Hazina Yetu kwa Wakati Wote
  • Kutimiza Mradi
  • Malta na Libya
  • Mgawo Mpya
  • Makao ya Wenye Ukoma
  • Kutegemezwa na Hazina
  • Yehova Alinifundisha Kufanya Mapenzi Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Ukaribishaji-Wageni wa Melita Waleta Mibaraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Kukaza Macho na Moyo Kwenye Tuzo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Nimeazimia Kuendelea Kumtumikia Muumba Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 1/1 kur. 20-23

Hazina Yenye Thamani Kubwa ya Kushiriki

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GLORIA MALASPINA

Pwani ya Sicily ilipotokomea, mume wangu na mimi tukaanza kukazia fikira mahali tulipokuwa tukienda, Malta, iliyo kisiwa cha Mediterania. Tazamio lenye kusisimua jinsi gani! Meli ilipokuwa ikivuka bahari, tuliwazia juu ya ono la mtume Paulo alipokuwa Malta katika karne ya kwanza.—MATENDO 28:1-10.

ILIKUWA katika mwaka wa 1953, na wakati huo kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova haikuwa imetambuliwa kisheria katika Malta. Mwaka uliokuwa umepita, tulikuwa tumehitimu katika Watchtower Bible School of Gilead na tulipewa mgawo wa kwenda Italia. Baada tu ya wakati mfupi wa kujifunza Kiitalia, tulikuwa na hamu ya kuona kilichokuwa kikitungoja katika Malta.

Mwanamke mchanga kama mimi, alikujaje kuwa mishonari katika nchi ya kigeni? Acha nieleze.

Kielelezo Chenye Kuchochea cha Mama

Katika 1926, wakati familia yetu ilipokuwa ikiishi katika Fort Frances, Ontario, Kanada, mama yangu alikubali kuchukua kijitabu Millions Now Living Will Never Die kutoka kwa Mwanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo). Alikisoma kwa makini sana, na juma ilo hilo akahudhuria funzo la Biblia la kikundi, kwa kutumia gazeti la Watch Tower. Mama alikuwa msomaji wa Biblia mwenye bidii, na alikubali ujumbe wa Ufalme wa Mungu ukiwa kama hazina aliyokuwa akitafuta. (Mathayo 6:33; 13:44) Ujapokuwa upinzani wenye jeuri kutoka kwa baba, na ingawa alikuwa na wasichana wadogo watatu wa kutunza, alichukua msimamo katika yale aliyokuwa akijifunza.

Imani ya mama iliyokuwa imara kwa miaka 20 iliyofuata ilifanya mimi na dada zangu wakubwa wawili, Thelma na Viola, tulijue tumaini la ajabu la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Alikabili majaribu magumu mengi sana, lakini hatukutilia shaka haki ya mwendo aliochagua.

Katika 1931, nilipokuwa na umri wa miaka kumi tu, tulihamia shamba fulani kaskazini mwa Minnesota, Marekani. Huko hatukuweza kuwa na ushirika wa kawaida na Mashahidi wa Yehova lakini tulipata maagizo ya Kibiblia kutoka kwa mama. Utumishi wake wa kujitolea akiwa kolpota, au mhudumu wa wakati wote, ulinichochea nitake kuungana naye katika kazi hiyo. Katika 1938 dada zangu wawili na mimi tulijiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa katika kusanyiko moja katika Duluth, Minnesota.

Baada ya kuhitimu katika shule ya sekondari katika 1938, mama alinitia moyo nijifunze kazi fulani ili niweze kujisimamia kifedha huku nikiwa painia (jina jipya la kolpota). Hili lilikuwa shauri zuri, hasa kwa sababu baba aliamua kwenda zake na kutuacha peke yetu.

Kushiriki Hazina Yetu kwa Wakati Wote

Mwishowe nilihamia California, na katika 1947, nikaanza kazi ya kupainia katika San Francisco. Nilipokuwa nikifanya kazi ya kutayarishia Kusanyiko la “Mpanuko wa Mataifa Yote” katika Los Angeles, nilikutana na Francis Malaspina. Mradi wetu wenye kufanana wa umishonari uliongoza kwenye mwanzo wa uhusiano wenye upendo. Tukaoana katika 1949.

Katika Septemba 1951, Francis na mimi tulialikwa katika darasa la 18 la Gileadi. Katika siku ya kuhitimu, Februari 10, 1952, baada ya miezi mitano ya mazoezi makali, nchi tulizokuwa tutumwe zilikuwa zikitajwa kialfabeti na msimamizi wa shule, Nathan H. Knorr. Aliposema, “Italia, Ndugu na Dada Malaspina,” tayari tulikuwa tukiwazia safari hiyo!

Majuma machache baadaye, tulipanda meli katika New York tukasafiri kwa siku kumi hadi Genoa, Italia. Giovanni DeCecca na Max Larson, waliofanya kazi katika makao makuu ya Brooklyn, walikuwa hapo gatini kutusindikiza. Katika Genoa tulilakiwa na wamishonari waliofahamu magumu ya kuingia katika nchi hiyo.

Tukisisimukia kila kitu kilichokuwa karibu nasi, tuliingia katika gari-moshi hadi Bologna. Kile tulichoona tulipofika lilikuwa jiji lililoharibiwa na mabomu ya Vita ya Ulimwengu 2. Hata hivyo, kulikuwa vitu vizuri vingi pia, kama vile harufu nzuri sana yenye kuvutia iliyojaa hewa ya asubuhi ya kahawa inayochomwa na manukato ya vikolezo vya mchuzi mtamu sana uliokuwa ukitayarishwa kwa pasta za aina nyingi.

Kutimiza Mradi

Tulianza kuhubiri tukiwa tumekariri maneno ya kusema, na tuliyasema hadi ujumbe ulipokubaliwa au mlango ulipofungwa. Tamaa ya kujieleza ilitusukuma kujifunza lugha hiyo kwa bidii sana. Baada ya miezi minne, tulipewa mgawo wa kwenda kuishi katika makao mapya ya mishonari katika Naples.

Jiji hili kubwa lajulikana sana kwa mandhari yalo yenye kupendeza. Tulifurahia utumishi wetu huko, lakini baada ya miezi mingine minne, mume wangu alipewa mgawo wa kazi ya mzunguko, au kusafiri, akitembelea makutaniko kutoka Rome hadi Sicily. Baadaye, pia tulitembelea Malta na hata Libya katika Afrika Kaskazini.

Safari za gari-moshi kutoka Naples hadi Sicily katika siku hizo zilikuwa jaribu la uvumilivu wa kimwili. Tulikuwa tukisafiri katika gari-moshi lililojaa watu na wakati mwingine kusimama kwa muda wa saa sita hadi nane katika vijia vilivyojaa watu humo ndani. Hata hivyo, hilo lilitupa nafasi nzuri ya kujua tabia za watu waliokuwa karibu nasi. Nyakati nyingine chupa kubwa za divai iliyotengenezewa nyumbani zilitumika kama kiti cha kukalia kwa mwenye kuibeba, ambaye kila mara angeitumia divai hiyo kuondoa kiu yake wakati wa safari hiyo ndefu. Wasafiri wenye urafiki mara kwa mara walitushirikisha kwa kutugawia mkate na salami zao, tulithamini wonyesho huo wa uchangamfu na ukarimu wenye kutia moyo.

Katika Sicily tulilakiwa na marafiki waliobeba masanduku yetu huku wakipanda mlima bila kupumzika kwa muda wa saa tatu na nusu hadi kwenye kutaniko lililokuwa kule juu kabisa. Ukaribishaji mchangamfu wa ndugu zetu Wakristo ulitufanya tusahau uchovu wetu. Wakati mwingine tulipanda nyumbu wasioweza kujikwaa, lakini hatukuangalia chini kwenye bonde ambako tungeanguka ikiwa nyumbu angejikwaa hatua moja. Tulitegemezwa kwa kuona msimamo thabiti wa ndugu zetu katika kweli za Biblia ijapokuwa magumu waliyokuwa nayo, na upendo waliotuonyesha ulitufanya tushukuru kuwa pamoja nao.

Malta na Libya

Tukiwa twawafikiria sana ndugu zetu katika Sicily, tuliabiri kuelekea Malta. Mtume Paulo alikuwa amepata watu wakarimu huku, nasi pia tuliwapata. Dhoruba katika Ghuba la St. Paul lilitufanya tutambue hatari ambayo meli ndogo zilipata katika karne ya kwanza. (Matendo 27:39–28:10) Na bado tungesafiri kwenda Libya. Hali ingekuwaje katika nchi hii ya Kiafrika ambapo kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku?

Kwa mara nyingine tena tulikabili desturi nyingine tofauti kabisa. Mandhari na sauti za jiji la Tripoli zilinivutia akili tulipokuwa tukitembea kwenye barabara zenye nguzo ndani ya mji. Wanaume walivalia mavazi yaliyosokotwa kwa manyoya ya ngamia ili kujikinga na joto lenye kuchoma la Jangwa la Sahara wakati wa mchana na hata usiku wakati wa baridi. Tulipata kufahamu na kuheshimu jinsi watu walivyobadilikana ili wapatane na hali ya hewa ya mahali wanapoishi.

Bidii yenye uangalifu ya ndugu ilitufundisha mengi kuhusu kumtegemea Yehova kabisa na kufuata mwongozo wa walio na ujuzi zaidi juu ya kuhubiri chini ya hali kama hizo. Ndugu zetu Wakristo walikuwa watu kutoka mataifa mengi; hata hivyo walifanya kazi kwa muungano katika utumishi wao kwa Yehova.

Mgawo Mpya

Kwa sababu ya upinzani kwa kazi yetu ya kuhubiri, ilitubidi kuondoka Italia, lakini kwa furaha tulikubali mgawo mpya wa kuhubiri katika Brazili katika 1957. Francis na mimi tukajipatanisha na maisha na desturi za huko, na baada ya miezi minane, Francis alialikwa kufanya kazi ya mzunguko. Tulisafiri kwa basi, kwa ndege, na kwa miguu. Nchi hii kubwa sana, yenye urembo mwingi sana, ilitupa somo katika jiografia.

Mzunguko wetu wa kwanza ulitia makutaniko kumi katika jiji la São Paulo, pamoja na miji midogo kumi katika sehemu za ndani na kando-kando ya sehemu ya kusini ya pwani ya jimbo la São Paulo. Hakukuwa na makutaniko katika miji hiyo siku hizo. Tungetafuta mahali pa kukaa, na baada ya kutulia, tungeenda nyumba kwa nyumba tukiwa na ujumbe wa Ufalme. Pia tuliwapa vikaratasi vya ukaribishaji waje kuona moja ya sinema za mafundisho za Watch Tower Society.

Kupanda basi tukiwa na filamu, projekta, transfoma, faili, fasihi, vikaratasi vya ukaribishaji, na chombo cha kuchorea mahali pa kuonyeshea sinema kwenye vikaratasi vya ukaribishaji haikuwa kazi rahisi. Kwa kulinganisha, sanduku letu dogo la nguo halikuwa kitu kikubwa. Ilitubidi kuiweka projekta hiyo kwenye mapaja yetu ili isipasuke kwa ajili ya kutikiswa-tikiswa kwa sababu ya kusafiri kwenye barabara mbaya.

Baada ya kupata mahali pa kuonyesha sinema, tungeenda mlango kwa mlango na kuacha vikaratasi vya ukaribishaji kwa sinema. Mara nyingine tungepata ruhusa ya kuonyesha sinema ndani ya mkahawa. Nyakati nyingine tulisimamisha shiti kati ya milingoti miwili huko nje. Wahudhuriaji wenye uthamini, wengi wao wakiwa hawajawahi kamwe kuona picha zenye kusonga, wangesimama na kusikiliza kwa makini wakati Francis alikuwa akisoma maelezo. Baadaye, tungetawanya fasihi za Biblia.

Ili kufikia vijiji, tulisafiri kwa basi. Mito mingine haikuwa na daraja, kwa hiyo basi lingewekwa kwenye chelezo kubwa na kuvushwa upande mwingine. Tulishauriwa kutoka nje ya basi na, tukiona basi ikiteleza ianguke ndani ya mto turuke upande ule mwingine wa chelezo ili tusivutwe na maji mpaka ndani ya mto. Kwa shukrani, hatukupoteza basi yoyote ndani ya mto—lilikuwa jambo zuri, hasa kwa sababu mto huo ulijulikana kuwa na samaki piranha wenye kula nyama!

Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa katika New York katika 1958, tulirudi Brazili, ambapo muda mfupi baadaye tukarudia kazi ya kusafiri. Wilaya yetu ilitupeleka kwenye mpaka wa Uruguai upande wa kusini, Paraguai upande wa magharibi, jimbo la Pernambuco upande wa kaskazini, na Bahari ya Atlantiki upande wa mashariki mwa Brazili.

Makao ya Wenye Ukoma

Katika miaka ya katikati ya 1960, tulikubali mwaliko wa kuonyesha sinema moja ya Sosaiti katika makao ya wenye ukoma. Lazima nikubali kwamba kwa njia fulani nilikuwa na woga. Tulikuwa na ujuzi mdogo kuhusu ukoma, mbali na ule tuliokuwa tumesoma katika Biblia. Tulipoingia kwenye uwanja huo, uliokuwa umepakwa rangi nyeupe, tulielekezwa kwenye jumba kubwa. Mahali fulani palikuwa pametengwa kwa kamba kwa ajili yetu na chombo chetu.

Fundi wa umeme aliyekuwa akitusaidia alikuwa mwenyeji wa makao hayo aliyekuwa mwenye umri wa miaka 40. Alikuwa amepoteza mikono yake hadi kwenye kiwiko na sehemu nyingine za mwili wake, zikifanya aonekane vibaya sana. Mwanzoni niliduwaa, lakini hali yake ya shangwe na ufundi wa kufanya kazi yake ulinituliza. Upesi tulikuwa tunazungumza mambo mengi tukiwa tunamalizia matayarisho muhimu. Katika wale wagonjwa elfu moja walioishi katika makao hayo, zaidi ya mia mbili walihudhuria. Walipokuwa wakichechema na kuingia ndani, tuliona hatua mbalimbali ambazo ugonjwa wao ulikuwa umefika. Ono lenye kugusa hisia-moyo kwetu kama nini!

Tulifikiria yale Yesu alisema kwa mwenye ukoma aliyeomba hivi, “Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa.” Akimgusa mtu huyo, Yesu akamhakikishia akisema, “Nataka; takasika.” (Mathayo 8:2, 3) Baada ya programu hiyo kuisha, wengi walikuja kutushukuru kwa kuja, mwili wao ulioharibiwa ukiwa ushuhuda ulio wazi wa kuteseka kukubwa sana kwa binadamu. Baadaye, Mashahidi wenyeji walijifunza Biblia na wale waliotaka kujifunza mengi zaidi.

Katika 1967 tulirudi Marekani ili tushughulikie matatizo fulani ya afya yaliyokuwa mabaya sana. Tulipokuwa tukishughulikia hilo, tulipendelewa kushiriki tena katika kazi ya mzunguko. Kwa miaka 20 iliyofuata, nilishiriki na Francis katika kazi ya kuzunguka katika Marekani. Wakati wa kipindi hiki alifundisha pia katika Shule ya Huduma ya Ufalme.

Kilikuwa chanzo cha kitia moyo jinsi gani kwangu kuwa na mume mpendwa na mshiriki mwaminifu aliyeshughulikia mgawo wowote aliopewa! Tukiwa pamoja tulipendelewa kushiriki hazina ya kweli za Biblia katika sehemu za mabara manne.

Kutegemezwa na Hazina

Huko nyuma katika 1950, mama aliolewa na David Easter, ndugu mwaminifu aliyebatizwa katika 1924. Walitumikia pamoja kwa miaka mingi katika huduma ya wakati wote. Hata hivyo, wakati wa miaka ya mwisho-mwisho ya maisha ya mama, ugonjwa wa Kupungua Akili ulianza kujionyesha. Alihitaji utunzaji mwingi kwa sababu ugonjwa huo ulimwondolea uwezo wake wa kusababu. Dada zangu wenye utegemezo pamoja na David walichukua daraka hilo zito la kumtunza, kwa maana hawakutaka tuache mapendeleo yetu ya pekee ya utumishi wa wakati wote. Kielelezo cha uaminifu cha mama hadi kifo chake katika 1987 kilitusaidia sana kujua jinsi ya kujiendesha maishani, na tumaini alilofurahia la thawabu ya kimbingu lilitufariji.

Kufikia 1989, ningeweza kuona kwamba Francis hakuwa na nguvu kama alivyokuwa mbeleni. Hatukujua kwamba ugonjwa wa kichocho, unaojulikana sana katika sehemu nyingi za dunia, ulikuwa ukimdhuru. Katika 1990, adui huyu asiyechoka akamshinda, nikampoteza mwenzi wangu mpendwa niliyekuwa nimeshiriki naye zaidi ya miaka 40 katika utumishi wa Yehova.

Marekebisho ni sehemu ya maisha. Mengine ni rahisi, mengine ni magumu. Lakini Yehova, Mpaji wa hazina yenye thamani kubwa ya kweli za Biblia, alinitegemeza kwa njia ya tengenezo lake na upendo na kitia moyo kutoka kwa familia yangu. Bado nimeridhika nitazamapo mbele kwenye utimizo wa ahadi zote za Yehova ambazo hakika zitakuja.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mume wangu na mimi tulipokuwa wamishonari katika Italia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki