Watumishi Wenye Ujana Katika Nyakati za Biblia
BIBLIA husema juu ya vijana wengi wazuri waliochukua kwa uzito utumishi wao kwa Mungu na ambao walibarikiwa sana kwa kufanya hivyo. Tuwe tu vijana au wazee na wenye mvi, vielelezo hivi vizuri vya Kibiblia vyaweza kuandaa kitia-moyo kikubwa.
Yusufu alikuwa na miaka 17 tu alipouzwa utumwani Misri. Akiwa huko, mbali na familia yao na mahali asipoonwa na wale waliomjua, Yusufu alithibitisha ukamilifu wake. Mke wa Potifa alipojaribu kumtongoza Yusufu, yeye alisema hivi: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” Hata mbele ya Farao mwenye uwezo, ambaye katika siku yake alikuwa ndiye mwenye nguvu nyingi kuliko wengine wote, Yusufu alishika fursa hiyo kumpa Mungu sifa kwa fasiri ya ndoto za Farao. Alibarikiwa sana. Mungu alimtumia kuokoa Wamisri na familia yake pia wasife kwa njaa na kuleta baba yake, Yakobo na nyumba yake huko chini katika Misri.—Mwanzo 37:2; 39:7-9; 41:15, 16, 32.
Musa na Wengine Walikuwa Waaminifu Ujanani
Binti ya Farao alimchukua Musa awe kama mtoto wake mwenyewe, lakini mama na baba ya Musa wakaweza kumfundisha juu ya Mungu wa kweli. Biblia husema kwamba alipokua akawa mtu mzima, Musa ‘alikataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo.’ Mungu alitumia Musa kutoa watu wake Misri, ili waipokee Sheria huko Sinai, na kuandika sehemu kubwa ya Biblia. Hata uwe una umri gani, je! wewe unasitawisha azimio la kutumikia Mungu kama alivyofanya Musa?—Waebrania 11:23-29; Kutoka 2:1-10.
Maandiko yatuambia juu ya “wadogo-wadogo” waliosikiliza pamoja na wengine wote taifani wakati Israeli waliposomewa Sheria ya Mungu. (Kumbukumbu 31:10-13, NW) “Wote wenye ueledi wa kutosha kusikiliza” walisimama “kuanzia mapambazuko mpaka adhuhuri” ili waisikie Sheria katika siku za Nehemia. (Nehemia 8:1-8, NW) Hata ikiwa walio wadogo-wadogo hawakuelewa kila jambo, wangeweza kuthamini kwamba walipaswa kumpenda, kumwabudu, na kumtii Yehova Mungu. Hata uwe una umri gani, je! wewe umesikiliza kwenye mikusanyiko na makusanyiko ambako Neno la Mungu lilizungumzwa? Je! umejifunza umaana wa kumtii yeye, kama walivyofanya Waisraeli hao wachanga?
Daudi, Yosia, na Yeremia
Mungu alimchagua Daudi, aliye mchanga kabisa kati ya ndugu wanane, kwa utumishi maalumu na kusema hivi juu yake: “Nimemwona Daudi, mwana wa Yese, mtu anayeupendeza moyo wangu, atakayefanya mapenzi yangu yote.” Mungu alimchagua awe “mchungaji” wa watu wake, na Daudi alifanya utumishi huo, ali akithibitisha upendo wake kwa Yehova muda wa miaka mingi. Aliandika zaidi ya Zaburi 70 na akawa babu wa kale wa Yesu Kristo. Uwe u kijana au mzee, je! wewe huthamini njia za Mungu, na je! wewe hufanya mambo atamaniyo, kama alivyofanya Daudi?—Matendo 13:22; Zaburi 78:70, 71; 1 Samweli 16:10, 11; Luka 3:23, 31.
Yosia alipata kuwa mfalme akiwa na miaka minane tu. Akiwa na miaka karibu 15, “akali mchanga, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babaye.” Kabla hajafika umri wa miaka 20, Yosia alianza kampeni dhidi ya ibada bandia. Baadaye, aliagiza hekalu litengenezwe kulikoharibika, naye akarudisha ibada safi barani. Twasoma hivi: “Siku zake zote hawakuacha kumfuata BWANA [Yehova, NW], Mungu wa baba zao.” Sisi sote hatuwezi kuwa mfalme kama Yosia, lakini twaweza kutumikia Mungu na kusimama imara dhidi ya ibada bandia, hata tuwe tuna umri gani.—2 Nyakati 34:3, 8, 33.
Mungu mweza yote alimwambia Yeremia hivi: “Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa.” Yeremia aliteta kwamba alikuwa mchanga mno kuwa nabii: “Aa, Bwana MUNGU [Yehova, NW]! tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Yehova aliitikia hivi: “Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru.” Kwa miaka zaidi ya 40 Yeremia alifanya lilo hilo, na hata alipotaka kuacha, hakuweza kukoma. Neno la Mungu ‘limekuwa kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yake.’ Ikawa ni lazima tu aseme! Hata uwe una umri gani, je! wewe unasitawisha aina ya imani aliyokuwa nayo Yeremia, ukisonga mbele katika utumishi wa Mungu jinsi alivyofanya?—Yeremia 1:4-8; 20:9.
Danieli, Yesu, na Timotheo
Je! wewe hujasikia juu ya Danieli? Huenda akawa alikuwa na umri wa chini sana kuliko miaka 20 alipotwaliwa pamoja na “watoto” wengine wakiwa watekwa kwenye baraza la mfalme wa Babuloni, Nebukadreza mwenye uwezo. Japo ujana wa Danieli, yeye alikuwa na azimio la kumtii Mungu. Danieli na waandamani wake walikataa kujichafua kwa vyakula ambavyo vingaliweza kuvunja Sheria ya Mungu au viwe vimenajisiwa na desturi za kipagani. Kwa miaka zaidi ya 80, Danieli hakuyumba-yumba kamwe, akadumisha ukamilifu kufikia hatua ya kukataa kuacha kusali kwa Mungu, hata ingawa tokeo la jambo hilo lingekuwa katika kutupwa kwenye simba. Je! wewe huchukua utumishi wako na sala zako kwa Mungu kwa uzito wa kadiri hiyo? Wapaswa kufanya hivyo.—Danieli 1:3, 4, 8, NW; 6:10, 16, 22.
Akiwa na umri wa miaka 12, Yesu alipatwa akiwa ameketi katikati ya walimu wa kidini hekaluni Yerusalemu, “akiwasikiliza na kuwauliza maswali. Nao wote waliomsikia [kijana Yesu] walistaajabia fahamu zake na majibu yake.” Je! mazungumzo ya Kimaandiko ya wanaume wazee hekaluni yangalikupendeza wewe kama vile Yesu? Je! wengine wangalistaajabia uelewevu wako na majibu yako? Leo, Mashahidi wengi wachanga ambao hujifunza, kusikiliza kwa uangalifu, na kushiriki katika mikutano ya Kikristo wana maarifa ya Kimaandiko ambayo huwashangaza wenye umri mkubwa zaidi.—Luka 2:42, 46, 47.
Je! wewe ni kama Timotheo, ambaye akiwa mtoto alifundishwa “maandiko matakatifu”? Alipokuwa mwanamume mchanga, Timotheo ‘aliripotiwa vema na akina ndugu’ katika angalau makundi mawili. Mtume Paulo alimchagua Timotheo asafiri pamoja naye, si ili awe mpagazi tu, bali ili amsaidie Paulo kufundisha wengine. Je! wewe ungechaguliwa kwa mapendeleo ya jinsi hiyo? Je! utendaji wako ‘huripotiwa vema,’ si katika kundi lako mwenyewe tu bali pia katika mengine?—2 Timotheo 3:15; Matendo 16:1-4, NW.
Wewe Wataka Aina Gani ya Wakati Ujao?
Je! yawezekana vijana leo wawe waaminifu kama walivyokuwa Yusufu, Musa, Daudi, na wengine? Ndiyo, yawezekana. Ni kweli kwamba vijana wengi wapendezwa na raha tu. Lakini wengine wanatumia ujana wao kwa hekima, wakipata kujua Mungu na mapenzi yake kwao. Wao huutimiza unabii wa Biblia: “Watu wako watajitolea wenyewe kwa nia siku ya jeshi lako. . . . Wewe una andamano lako la wanaume wachanga kama matone ya umande.”—Zaburi 110:3, NW.
Vijana wazuri jinsi hiyo huonyesha hekima izidiyo miaka yao, kwa kuwa Mungu aweza kuwasaidia wafanikishe maisha yao ya wakati uliopo na vilevile kuwapa wakati ujao mtukufu katika ulimwengu mpya unaokuja. (1 Timotheo 4:8) Ingawa hivyo, kijana wa ki-siku-hizi aweza kusitawishaje imani kama wale vijana watajwao katika Biblia? Ikiwa ungependa kujua, twakualika uisome makala “Vijana Wenye Furaha Katika Utumishi wa Yehova, kuanzia ukurasa 10 wa gazeti hili.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Musa kijana hakushawishwa na utajiri wa Misri
Daudi mwenye ujana alikuwa mwenye kukubalika kwenye moyo wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 6]
Ingawa Yeremia alihisi “ni mtoto tu,” kwa moyo mkuu alihubiri ujumbe usiopendwa na wengi
Akiwa na umri wa miaka 12, Yesu alistaajabisha wazee wake kwa uelewevu wake wa Neno la Mungu
[Picha katika ukurasa wa 7]
Katika Israeli hata walio wadogo-wadogo walisikiliza Sheria ya Mungu iliposomwa. Wewe je?