Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kuhubiri Habari Njema Katika “Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia”
“HABARI njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa kwa ajili ya ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakuja.” Ndivyo Yesu alisema kwa wanafunzi wake muda mfupi kabla ya kifo chake. Upesi baada ya ufufuo wake, alisema zaidi hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Mathayo 24:14; Matendo 1:8, NW) Leo, unabii huu mbalimbali unatimizwa katika mabara zaidi ya 200, kutia na nchi ya Peru ya Amerika ya Kusini.
Mashahidi zaidi ya 32,000 wanahubiri habari njema katika bara hilo lenye upendezi, na hakika eneo lao linatia ndani nyingine za sehemu zilizo za mbali zaidi sana za dunia: eneo lililoinuka la milima Andes, kufikia miinuko ya kati ya meta 4,000 na 4,500, na pia ile nyika yenye joto ya Amazon, ambako watu wanaweza kufikiwa kwa mashua za mtoni. Tawi la Peru linaripoti hivi:
◻ “Katika eneo la nyikani, tuna mapainia wa pekee wanane waliogawiwa kutumia mashua ndogo mbili za mtoni zinazoitwa lanchas. Mashua hizi zinavuta meta 0.3 tu ya maji, hivyo basi imewezekana kurefusha kuhubiriwa kwa habari njema katika maeneo mengi mapya katika mito iliyo midogo zaidi. Kufikia hapo, akina ndugu wanaotumia mashua hizi wameangusha mamia ya maelfu ya magazeti, vitabu, na Biblia kotekote katika Bonde Amazon la Peru. Tokeo la moja kwa moja ni kwamba makundi mapya manne yameanzishwa, pamoja na vikundi vitano vilivyo peke yavyo vinavyoripoti utendaji na kufanya mikutano. Inatumainiwa kwamba karibuni vikundi hivi vitakuwa makundi.”
◻ Mji mmoja wa nyikani ulikua kwa kuzungukia kituo cha kupiga mafuta bomba kwa ajili ya mfereji-mafuta wa shirika la Trans-Andes, unaochukua mafuta kutoka nyika hiyo kuyapitisha juu ya milima Andes iliyoinuka na kuyafikisha kwenye pwani ya magharibi. Kwa sababu ya kuwapo kwa wafanya kazi wa mafuta ya mfereji huo, mji huu ulikuwa na karibu baa 20 na ukaja kujulikana kuwa mahali pa kunywa na kujifurahisha. Hata hivyo, baada ya mapainia wa pekee kutoa ushahidi wa bidii kweli kweli, wengi waliitikia ujumbe wa Ufalme, na sasa ni baa nne tu zimebaki mjini! Wakati wa ziara moja ya hivi majuzi ya mwangalizi wa mzunguko, watu 189 walikuja kwenye hotuba ya watu wote. Sasa kuna kikundi cha wahubiri 7 mjini, na watu zaidi ya 45 wanahudhuria mikutano yote. Karibuni, kwa baraka ya Yehova, bila shaka kitakuwa kundi.
◻ Katika moja la yale makundi 221 yaliyo katika jiji kuu la Peru, Lima, mwanamume wa miaka 29 anaeleza jinsi alivyopata ukweli. Akiisha kuacha shule akiwa na miaka 13, alijiunga na genge la wenye makelele na kuanza kazi-maisha ya kupigana, kutumia dawa za kulevya, na kuzoea ukosefu wa adili. Baada ya miaka miwili ya utumishi wa kuwa jeshini kwa lazima, alianza kuwa na matatizo ya akili. Halafu, katika 1983, dada mmoja mnyenyekevu, asiye kimbelembele akawasiliana naye katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Kwa mara ya kwanza, alipata habari juu ya ule ulimwengu mpya wenye upendo na amani. Funzo la Biblia lilianzwa, na kwa msaada wenye upendo kutoka kwenye kundi na kwa nguvu ya Yehova, akaweza kushinda maovu yake. Katika 1986 alibatizwa na sasa anatumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kundi.
Kwa kweli, maneno ya Yesu kwamba Ufalme utahubiriwa kwenye “sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia” yanatimizwa katika Peru kwa matokeo mazuri ajabu, kwa faida ya wengi katika bara hilo ambao wana njaa na kiu kwa ajili ya ukweli.