Ukweli Ni Nini Juu ya Bethlehemu na Krismasi?
“TUNAPOFIKIRIA Fumbo la Bethlehemu hatuwezi kuzuia maswali na shaka zisije kwenye akili yetu.”—Bethlehem, cha Maria Teresa Petrozzi.
‘Kwa nini maswali na shaka?’ huenda ukauliza. Ingawaje, imani mbalimbali zinazohusu Krismasi, na sehemu zinazohusiana na imani hizi, zina msingi wa uhakika. Je! ndivyo zilivyo?
Alizaliwa Wakati Gani?
Kuhusu tarehe ya kuzaliwa kwa Yesu, Maria Teresa Petrozzi anauliza hivi: “Ni wakati gani hasa Mfidiaji alipozaliwa? Tungependa kujua si mwaka tu bali pia mwezi, siku, saa. Hatupewi hesabu barabara.” New Catholic Encyclopedia inaunga mkono jambo hili: “Tarehe ya uzaliwa wa Yesu Kristo inaweza kuhesabiwa kwa kukadiria tu.” Inasema hivi juu ya tarehe inayohesabiwa kuwa ndiyo ya uzaliwa wa Kristo: “Tarehe ya Desemba 25 hailingani na uzaliwa wa Kristo bali na sikukuu ya Natalis Solis Invicti, sikukuu-jua ya Waroma wakati wa umbali wa jua.”
Hivyo basi huenda wewe ukauliza, ‘Ikiwa Yesu hakuzaliwa katika Desemba 25, alizaliwa wakati gani?’ Kutokana na Mathayo sura 26 na 27, tunaelewa kwamba Yesu alikufa wakati wa sikukuu Kupitwa ya Kiyahudi, iliyoanza Aprili 1, 33 W.K. Zaidi ya hilo, Luka 3:21-23 inatupasha habari kwamba Yesu alikuwa na umri wa miaka karibu 30 alipoanza huduma yake. Kwa kuwa huduma yake ya kidunia iliendelea kwa miaka mitatu na nusu, alikuwa na umri wa karibu miaka 33 1/2 wakati wa kifo chake. Kristo angalikuwa na umri wa miaka 34 kamili miezi sita baadaye, na hiyo ingekuwa karibu Oktoba 1. Tukihesabu kurudi nyuma tuone Yesu alipozaliwa, tunafika, si Desemba 25 au Januari 6, bali karibu Oktoba 1 ya mwaka 2 K.W.K.
Pia inastahili kuangaliwa kwamba wakati wa mwezi wa Desemba, Bethlehemu na mazingira yake inakuwa na hali ya hewa yenye baridi ya kipupwe, mvua zenye kuleta baridi nyingi, na nyakati fulani theluji. Mtu hakuti wachungaji wakiwa na makundi ya kondoo zao nje usiku wakati huo. Hii si hali ya hewa ya hivi majuzi. Maandiko yanaripoti kwamba mfalme Myudea Yehoyakimu “alikuwa ameketi katika nyumba iliyotumika wakati wa baridi, mwezi wa kenda [Kislevu, unaolingana na Novemba-Desemba]; na pale palikuwa na moto wa makaa mbele yake.” (Yeremia 36:22) Alihitaji joto lile ili aendelee kupashwa ujoto. Zaidi ya hilo, kwenye Ezra 10:9, 13 tunapata ushuhuda wa wazi kwamba mwezi wa Kislevu ulikuwa “wakati wa mvua nyingi, nasi hatuwezi kusimama nje.” Yote haya yanaonyesha kwamba hali za hewa katika Bethlehemu katika Desemba hazilingani na elezo la Biblia juu ya matukio yanayohusiana na kuzaliwa kwa Yesu Kristo.—Luka 2:8-11.
Mahali Gani?
Ni nini maoni yanayofaa juu ya mahali palipokuwa sehemu ya kichochezi cha ile vita ya Krimea (1853-56), ‘pambano la umwagaji wa damu’ ambalo ndilo peke yalo lililotoa uhai wa askari Wafaransa zaidi ya mia moja elfu? Je! kweli mahali hapo ndipo pa kuzaliwa kwa Yesu?
Kwanza, Biblia yenyewe haitaji mahali barabara pa uzaliwa wa Yesu. Mathayo na Luka wanahakikisha kwamba uzaliwa wa Yesu ulitimiza unabii wa Kimesiya kwenye Mika 5:2, uliokuwa umetabiri kwamba “mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake [asili yake, NW] yamekuwa tangu zamani za kale,” angetoka Bethlehemu. (Mathayo 2:1, 5; Luka 2:4) Masimulizi yote mawili ya Gospeli yanataja mambo yale yaliyo ya maana tu, yaani, kwamba Yesu alizaliwa katika Bethlehemu na, kulingana na Luka, kwamba mtoto mchanga huyo alipatikana amefungwa kwa vitambaa na kulazwa katika sanduku la chakula cha ng’ombe.—Luka 2:7.
Kwa nini waandikaji wa Gospeli hawakuongeza habari zaidi? Maria Teresa Petrozzi anaona hivi: “Waevanjeli wanaacha mambo haya madogo-madogo, inaonekana kwa sababu wanayaona kuwa yasiyo na maana.” Kwa uhakika, ni wazi kwamba Yesu mwenyewe hakuyaona maelezo madogo-madogo juu ya uzaliwa wake kuwa ya maana sana, kwa kuwa hanakiliwi hata mara moja kuwa akitaja ama tarehe ya uzaliwa wake ama mahali barabara pa uzaliwa wake. Hata ingawa alizaliwa katika Bethlehemu, Yesu hakupaona mahali hapo kuwa makao yake, bali eneo la Galilaya lilitajwa kuwa “eneo la nyumbani kwake.”—Marko 6:1, 3, 4; Mathayo 2:4, 5; 13:54, NW.
Usomaji wa Yohana 7:40-42 unaonyesha kwamba watu kwa ujumla hawakuwa na habari juu ya mahali pa uzaliwa wake, wakifikiri kwamba yeye alizaliwa katika Galilaya: “Wengine wakasema, Je! Kristo atoka Galilaya?” Kwa msingi wa yaliyoandikwa kwenye Yohana 7:41, The Church of the Nativity, Bethlehem kinakata shauri hivi: “Jambo la kwamba mazungumzo ya jinsi hiyo yalitokea halikanushi uhakika wa kwamba Kristo alizaliwa katika Bethlehemu; lakini angalau linaonyesha kwamba wengi wa washirika Wake hawakujua hilo.”
Ni wazi kwamba wakati wa muda wa maisha ya Yesu mwenyewe ya kidunia, yeye hakutangaza mambo yote madogo-madogo ya uzaliwa wake. Hakuna mkazo uliotiwa juu ya mahali pa uzaliwa wake. Basi, ni nini msingi wa imani ya kwamba lile Pango la Uzaliwa ndipo mahali ambapo Yusufu alimleta Mariamu ili azae?
Petrozzi anakubali wazi hivi: “Haiwezekani kujua kwa uhakika kama hilo pango lilikuwa moja la mapango ya kiasili yasiyohesabika yaliyokuwako katika ujirani wa Bethlehemu, au lilikuwa kipango kilichotumiwa kama kibanda cha wanyama wa kufugwa katika mkahawa mdogo. Hata hivyo, mapokeo yanayorudi nyuma mpaka nusu ya kwanza ya karne ya 2, yanasema wazi; hicho ni kibanda-pango.”—Italiki ni zetu.
Mapokeo Tu
Wote wawili Maria Teresa Petrozzi na R. W. Hamilton, pamoja na wanafunzi wengine mbalimbali wa historia ya Bethlehemu, wanaonyesha kwamba Justin Martyr, wa karne ya pili W.K., alikuwa wa kwanza kudai kwamba Yesu alizaliwa katika pango, bila kutaja wazi ni jipi. Hamilton anakata shauri hivi kuhusu maneno ya Justin Martyr: “Huu ni mtajo wa juujuu tu, na kudhania kwamba Mtakatifu Justin alikuwa akifikiria pango fulani hasa, na hata zaidi kwamba alikuwa akimaanisha Pango la Uzaliwa la sasa, kungekuwa ni kukazia mno ushuhuda wa neno moja tu.”
Katika elezo moja la chini Hamilton anaandika hivi: “Usimulizi wa Uzaliwa unaotukia katika ‘Kitabu cha Yakobo’ cha utungaji usiothibitishwa au ‘Evanjeliunabii’, ulioandikwa karibu na kipindi icho hicho, unajulisha juu ya pango pia, lakini unaeleza kwamba liko nusu-mwendo wa kufika Bethlehemu. Kwa kadiri lilivyo na thamani yoyote ya kihistoria hadithi hiyo inadokeza kwamba mapokeo hayo hayakuwa yamehusiana na mahali pamoja tu, hakika si na lile Pango la Uzaliwa.”
Waandikaji wa kidini wa karne ya tatu Origeni na Eusebio wanahusianisha mapokeo yaliyojulikana wakati huo na mahali fulani hasa. Hamilton anasababu hivi: “Mara hadithi hiyo ilipokwisha kushikamanishwa na pango fulani hususa haingeelekea kuacha kamwe kueleza hivyo; na ni salama kukata shauri kwamba pango lililoonyeshwa kwa wageni upesi baada ya A.D. 200 lilifanana na Pango la Uzaliwa la sasa.”
W. H. Bartlett, katika kitabu chake Walks About the City and Environs of Jerusalem (1842), alidhania hivi kuhusu hili pango: “Ingawa mapokeo ya kwamba hapa ndipo mahali pa uzaliwa wa Mwokozi wetu, yamekuwako kwa muda mwingi wa kadiri yenye kuheshimika, yakitajwa na Mt. Jerome, aliyeishi na kufa katika kijumba-gereza kilicho jirani, haielekei kwamba hapo ndipo mahali penyewe, kwa kuwa ingawa pindi kwa pindi huenda ikawa vipango vilitumiwa kama vibanda vya wanyama wa kufugwa katika Palestina, hiki ni kina kirefu sana chini ya ardhi kuliko kile ambacho kingefaa kwa kusudi hilo; na, kwa kuongezea, tunapofikiria elekeo la watawa-waume kukazia kwamba tamasha za kimaandiko zilizo za ajabu zilitukia katika mapango, labda kwa sababu ya uvutio wa mahali hapo, inaonekana ikikaribia kuwa hakika kabisa kwamba hapo ni mahali pa kudhaniwa tu.”
Tunaweza kukata shauri gani kutokana na ushuhuda wa kihistoria unaopatikana na, la maana zaidi, kutokana na uhakika wa Kimaandiko kwamba wala Yesu wala wanafunzi wake hawakupagawia umaana wowote mahali pa uzaliwa wake? Ni wazi kwamba wakati Malkia Helena, mama ya Konstantino Mkuu, alipotaja wazi mahali pa Kanisa la Uzaliwa katika 326 W.K., mwanamke huyo alifanya hivyo kwa msingi wa kile ambacho Hamilton anakitaja kuwa ‘ushirika wa mapokeo ya muda mrefu.’ Haikuwa kwa msingi wa uthibitisho wa kihistoria wala wa Kibiblia.
Hii inaongoza kwenye umalizio zaidi wa kwamba mahali hasa pa uzaliwa wa Kristo hapajulikani. Kwa hiyo, je! ni jambo la akili kwamba waaminifu wanapaswa kufunga safari za upiligrimu kwenda mahali kama Pango la Uzaliwa na kuzipa heshima ya ibada? Ikiwa, kwa kweli, kungekuwa na takwa la jinsi hiyo kwa Wakristo, je! Yesu mwenyewe asingaliwapasha habari wanafunzi wake juu ya wajibu huo au hata ataje kwamba alitaka iwe hivyo? Je! hilo lisingeandikwa katika Neno la Mungu, Biblia, ili ulimwengu wa ainabinadamu usome? Kwa kuwa shuhuda za jinsi hiyo zimekosekana wazi katika Maandiko Matakatifu, ingefaa tuulize ni kitu gani ambacho Yesu aliona kinastahili kukumbukwa.
Hata tutafute namna gani, pindi ya pekee tutakayopata ambayo wanafunzi wa Yesu walipaswa kukumbuka muda wa vizazi ni kifo chake cha dhabihu. Yeye alikufa katika masika, muda mfupi baada ya kuadhimisha mlo wake wa mwisho wa Kupitwa akiwa pamoja na wanafunzi wake. Katika pindi hiyo alielekeza wanafunzi wake waaminifu wale mlo wa mfano wakitumia mkate usiotiwa chachu, kama matzoh, na divai nyekundu. Kuhusu sherehe hii rahisi, ambayo kwanza ilitukia Aprili 1, 33 W.K., aliamuru hivi: “Endeleeni kufanya hivi katika kunikumbuka mimi.”—Luka 22:19, 20, NW.
Kwa kutii amri hii ya Kimaandiko kutoka kwa Yesu mwenyewe, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanaadhimisha kila mwaka Ukumbusho wa kifo cha dhabihu cha Kristo. Hawafanyi kusanyiko hili la Kikristo mahali fulani pa pekee katika chumba cha juu katika Yerusalemu, kwa maana Yesu hakutaja wazi hilo. Lakini katika sehemu zote za ulimwengu, wao wanakusanyika katika Majumba ya Ufalme yao na mahali pengine panapofaa kukutania katika eneo la kwao. Mwadhimisho ule unaofuata utakuwa katika Machi 30, 1991, baada ya jua kushuka. Wewe unaalikwa kuhudhuria kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lililo karibu zaidi na nyumbani kwako.
Ili kuhudhuria mwadhimisho huu wa maana kwa kutii amri ya Yesu, si lazima usafiri kwenda Yerusalemu wala Bethlehemu. Wala Yesu wala wanafunzi wake hawakuhesabia mahali mbalimbali umaana wa kuwa vitovu vikuu vya ibada ya Kikristo. Tofauti na hilo, Yesu aliambia hivi mwanamke mmoja Msamaria, aliyeona kitovu cha ibada yake kuwa huko Gerizimu, mlima mmoja katika Samaria, kaskazini ya Yerusalemu: “Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.”—Yohana 4:21, 23.
Wale wanaoabudu Baba kwa roho na ukweli hawategemei mahali pa pekee, kama Bethlehemu, wala vitu, kama mifano, katika ibada yao. Mtume Paulo alisema hivi: “Wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. (Maana twaenenda kwa imani, si kwa kuona).”—2 Wakorintho 5:6, 7.
Hata hivyo, huenda bado ukafikiria, mtu anawezaje kuabudu Mungu kwa njia inayokubalika naye? Wakati mwingine mmoja wa Mashahidi wa Yehova akija mlangoni kwako, tafadhali mwulize.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Katika kipupwe, huenda theluji ikafunika ardhi iliyo karibu na Bethlehemu. Je! wachungaji wangelala nje pamoja na kondoo zao?
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kanisa la Uzaliwa katika Bethlehemu na pango lake la chini ya ardhi
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.
[Hisani]
Garo Nalbandian