Tafuta Wenye Mwelekeo Unaofaa Kwa Ajili ya Uhai wa Milele
“Wote wale waliokuwa na mwelekeo wenye kufaa kwa ajili ya uhai wa milele wakawa waamini.”—MATENDO 13:48, NW.
1. Kwa habari ya moyo wa kibinadamu, Yehova ana uwezo gani?
YEHOVA MUNGU anaweza kuusoma moyo. Hilo lilionyeshwa wazi wakati nabii Samweli alipoenda kupaka mafuta mwana wa Yese kuwa mfalme wa Israeli. Alipomwona Eliabu, Samweli “akasema [mara hiyo, NW]: Yakini masihi wa BWANA [Yehova, NW] yupo hapa mbele zake. Lakini BWANA [Yehova, NW] akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. BWANA [Yehova, NW] haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA [Yehova, NW] huutazama moyo.” Kwa hiyo, Samweli alielekezwa kumpaka mafuta Daudi, ambaye alithibitika kuwa ‘mtu aupendezaye moyo wa Mungu.’—1 Samweli 13:13, 14; 16:4-13.
2. Ni nini kimetia mizizi katika moyo wa kitamathali wa mtu, na hivyo twasoma nini juu ya hili katika Maandiko?
2 Mtu huonyesha mwelekeo fulani mkuu. Yeye huwa na nia fulani hasa ambayo imetia mizizi katika moyo wake wa kitamathali. (Mathayo 12:34, 35; 15:18-20) Hivyo, twasoma juu ya mtu ambaye “moyo wake ni vita [una mwelekeo wa kupigana, NW].” (Zaburi 55:21) Twaambiwa kwamba “mtu mwenye ghadhabu huasi sana [ana makosa mengi, NW].” Na twasoma hivi: “Kuna marafiki wenye mwelekeo wa kuvunjana vipande vipande, lakini kuna rafiki anayeshikamana kwa ukaribu sana kuliko ndugu.” (Mithali 18:24, NW; 29:22, UV) Kwa furaha, wengi wanathibitika kuwa kama watu fulani wasio Wayahudi katika Antiokia ya kale katika Pisidia. Waliposikia juu ya uandalizi wa Yehova kwa ajili ya wokovu, “walianza kushangilia na kutukuza lile neno la Yehova, na wote wale waliokuwa na mwelekeo wenye kufaa kwa ajili ya uhai wa milele wakawa waamini.”—Matendo 13:44-48, NW.
Waamini Ni “Wenye Moyo Safi”
3, 4. (a) Wenye moyo safi ni nani? (b) Wale wenye moyo safi humwonaje Mungu?
3 Waamini hao katika Antiokia wakawa Wakristo waliobatizwa, na walio waaminifu kati yao wangeweza kutumia maneno haya ya Yesu yawahusu wao wenyewe: “Heri wenye moyo safi; maana hao watamwona Mungu.” (Mathayo 5:8) Lakini ni nani “wenye moyo safi”? Nao ‘wanamwonaje Mungu’?
4 Wenye moyo safi ni safi kwa ndani. Usafi wa uthamini, wa shauku, tamaa, na wa makusudio ni wao. (1 Timotheo 1:5) Wao wamwona Mungu sasa kwa njia ya kwamba wamwona akitenda kwa ajili ya washikao ukamilifu wa kimaadili. (Linganisha Kutoka 33:20; Ayubu 19:26; 42:5.) Neno la Kigiriki lililofasiriwa hapa ‘ona’ linamaanisha pia ‘kuona kwa akili, kuhisi, kujua.” Kwa kuwa Yesu alionyesha kikamilifu utu wa Mungu, kuwa na muono-ndani katika utu huo kunaonewa shangwe na “wenye moyo safi,” ambao hujizoeza imani katika Kristo na katika dhabihu yake yenye kulipia dhambi, hupata msamaha wa dhambi zao, na waweza kutolea Mungu ibada yenye kukubalika. (Yohana 14:7-9; Waefeso 1:7) Kwa wapakwa mafuta, kumwona Mungu hufikia kilele wafufuliwapo kwenda mbinguni, ambako kwa kweli wao huona Mungu na Kristo. (2 Wakorintho 1:21, 22; 1 Yohana 3:2) Lakini kuona Mungu kupitia maarifa sahihi na ibada ya kweli kwawezekana kwa wote wale wenye moyo safi. (Zaburi 24:3, 4; 1 Yohana 3:6; 3 Yohana 11) Wao wana mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele mbinguni au katika dunia-paradiso.—Luka 23:43; 1 Wakorintho 15:50-57; 1 Petro 1:3-5.
5. Ni jinsi gani tu mtu aweza kuwa mwaminifu na mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo?
5 Wale wasio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele hawatakuwa waamini. Haiwezekani kwao kujizoeza imani. (2 Wathesalonike 3:2) Zaidi ya hilo, hakuna mtu awezaye kuwa mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo iwapo yeye si mwenye kufundishika, na Yehova ambaye huona moyo ulivyo humvuta mtu huyo. (Yohana 6:41-47) Bila shaka, katika kuhubiri kutoka nyumba kwa nyumba, Mashahidi wa Yehova hawatangulii kuhukumu mtu yeyote. Hawawezi kusoma mioyo bali wao huacha matokeo katika mikono ya Mungu yenye upendo.
6. (a) Ni nini limesemwa juu ya mfikio wa kibinafsi katika huduma ya nyumba kwa nyumba? (b) Ni maandalizi gani ambayo yamefanywa kusaidia Mashahidi wa Yehova wawapate wale walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele?
6 Kwa kufaa mwanachuo mmoja amesema hivi: “[Paulo] alifundisha ukweli peupe na kutoka nyumba kwa nyumba. Si kutoka jukwaani tu, bali katika kupashana habari kibinafsi na watu mmoja mmoja ambao aliwahubiri Kristo. Mara nyingi mfikio wa kibinafsi una matokeo sana kuliko namna au njia nyingine yoyote katika kufikia nafsi.” (August van Ryn) Vichapo kama vile Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, na Huduma ya Ufalme Yetu husaidia Mashahidi wa Yehova kutoa hotuba na kufanya kadiri wawezavyo katika kufikia watu kibinafsi katika utumishi wao wa shambani. Yenye msaada, pia, ni maonyesho ya Mkutano wa Utumishi na shauri la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wale wanaohudhuria shule wanapokea mazoezi yenye thamani katika sifa za usemi kama vile tangulizi nzuri, utumizi ufaao wa Maandiko, usemi wenye kufuatana vizuri, hoja inayosadikisha, utumizi wa mifano, na mimalizio yenye matokeo. Acheni tuone jinsi Biblia inavyoongezea agizo hili linaloweza kufanya watu wa Mungu wawe wenye matokeo zaidi watafutapo wale wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele.
Tangulizi Zenye Kuchochea Fikira
7. Maneno ya kufungua ya Mahubiri ya Yesu juu ya Mlima hufundisha nini juu ya tangulizi?
7 Kutokana na mfano wa Yesu, wale wanaojitayarisha kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba wanaweza kujifunza jambo fulani juu ya tangulizi zenye kuamsha upendezi. Katika kufungua Mahubiri yake juu ya Mlima, yeye alitumia neno “wenye furaha” mara tisa. Kwa mfano, alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao. . . . Wenye furaha ni wale wapole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:3-12, NW) Sentensi zake zilikuwa za moja kwa moja na za wazi. Na kwa uhakika utangulizi huo uliamsha kupendezwa na ukafanya wasikilizaji wake wahusike, kwa maana ni nani asiyetaka kuwa mwenye furaha?
8. Katika huduma ya nyumba kwa nyumba, kichwa cha mazungumzo chapasa kufanyiwaje utangulizi?
8 Kichwa chochote cha mazungumzo chenye kutumiwa katika huduma ya nyumba kwa nyumba chapasa kufanyiwa utangulizi kwa njia chanya, ya kupendeza. Lakini hakuna mtu apaswaye kutumia utangulizi wa kushtusha sana, kama vile, “Nina ujumbe wako kutoka anga za juu.” Habari njema zina chanzo cha kimbingu, lakini utangulizi wa jinsi hiyo ungeweza hata kufanya mwenye nyumba ashangae kama Shahidi huyo apaswa kuchukuliwa kwa uzito au afukuzwe upesi iwezekanavyo.
Kutumia Neno la Mungu kwa Halali
9. (a) Maandiko yapasa kufanyiwaje utangulizi, kusomwa, na kutumiwa katika huduma? (b) Ni mfano gani ambao watajwa ili kuonyesha jinsi Yesu alivyotumia maswali?
9 Katika huduma ya shambani, kama vile jukwaani, maandiko yapasa kufanyiwa utangulizi ifaavyo, kusomwa kwa mkazo ufaao, na kutumiwa kwa njia ya wazi, iliyo sahihi. Maswali yafanyayo mwenye nyumba afikiri juu ya mawazo ya Kimaandiko huenda yakasaidia. Tena, njia za Yesu ni zenye mafundisho. Katika pindi moja, mwanamume mmoja mwenye ujuzi katika Sheria ya Kimusa alimwuliza hivi: “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?” Kwa kujibu Yesu aliuliza hivi: “Imeandikwa nini katika torati? Wasomaje?” Bila shaka, Yesu alijua kwamba hili lilikuwa swali ambalo mwanamume huyo angeweza kujibu. Alijibu kwa usahihi, akisema hivi: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako.” Hiyo iliongoza Yesu kutoa pongezi, na mazungumzo zaidi yakafuata.—Luka 10:25-37.
10. Ni nini lipasalo kuzingatiwa akilini kwa kadiri kichwa cha mazungumzo ya mtu kihusikavyo, na ni nini kipasacho kuepukwa wakati wa kuuliza wenye nyumba maswali?
10 Wale wanaotoa ushahidi kutoka nyumba kwa nyumba wapaswa kukazia mada ya kichwa cha mazungumzo na kuelewesha wazi sababu ya kusoma maandiko ya Biblia ambayo yakuza habari hiyo. Kwa kuwa Shahidi anajaribu kufikia moyo wa mwenye nyumba, apaswa kuepuka kuuliza maswali ya kuaibisha. Katika kutumia Neno la Mungu, ‘maneno yetu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu.’—Wakolosai 4:6.
11. Katika kutumia Maandiko ili kusahihisha maoni yenye makosa, tuna mfano gani kutokana na shawishi ambalo Yesu aliletewa na Shetani?
11 Hasa katika ziara za kurudia huenda kukawa na uhitaji wa kusahihisha maoni mabaya kwa kuonyesha yale ambayo hasa Maandiko husema au kumaanisha. Yesu alifanya jambo kama hilo katika kumkanusha Shetani, aliyesema hivi: “Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini [kutoka buruji ya hekalu, ni kama kuweza kujiua]; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; na mikononi mwao watakuchukua; usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.” Zaburi 91:11, 12, iliyonukuliwa na Shetani, haitetei kwamba ni haki kuhatarisha uhai, ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu. Akifahamu kwamba lilikuwa kosa kumjaribu Yehova kwa kujasiria kuhatarisha uhai wake, Yesu alimwambia Shetani hivi: “Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana [Yehova, NW] Mungu wako.” (Mathayo 4:5-7) Bila shaka, Shetani si mtafutaji wa ukweli. Lakini wakati watu wenye kusababu vizuri waonyeshapo maoni mabaya ambayo yangezuia maendeleo yao ya kiroho, mhudumu wa Neno la Mungu apaswa kuonyesha kwa busara Maandiko yasema na kumaanisha nini hasa. Hii yote ni sehemu ya ‘kutumia kwa halali neno la kweli.’—moja la masomo ya maana yafundishwayo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.—2 Timotheo 2:15.
Uvutio Wenye Kusadikisha Una Mahali Pao
12, 13. Kwa nini yafaa kutumia uvutio wenye kusadikisha katika huduma?
12 Uvutio wenye kusadikisha una nafasi yenye kufaa katika huduma ya Kikristo. Kwa mfano, Paulo alihimiza Timotheo mfanya kazi mwenzake aendelee katika mambo aliyokuwa amejifunza na “kuhakikishwa [kushawishwa kuamini, NW].” (2 Timotheo 3:14) Katika Korintho, Paulo “akatoa hoja zake katika sinagogi kila sabato, akajaribu kuwavuta Wayahudi na Wayunani.” (Matendo 18:1-4) Katika Efeso, kwa mafanikio ‘alitoa hotuba na kutumia uvutio wenye kusadikisha kuhusu ufalme wa Mungu.’ (Matendo 19:8, NW) Na alipokuwa amekamatwa katika Roma, mtume aliita watu waje alipo na kuwapa ushahidi, “akitumia uvutio wenye kusadikisha,” na wengine wao wakawa waamini.—Matendo 28:23, 24, NW.
13 Bila shaka, bila kujali huenda Mashahidi wakajaribu kuwa na uvutio wenye kusadikisha kadiri gani, ni wale tu wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele watakaokuwa waamini. Hoja zenye usadikishi na maelezo ya wazi, yenye kutolewa kwa busara, huenda zikawasadikisha kuamini. Lakini ni nini zaidi kinachoweza kuwa na msaada katika kuwavutia kwa usadikisho?
Fuatanisha Mawazo Yako Vizuri na Usadikishe
14. (a) Usemi wenye kufuatana vizuri, wenye kushikamana watia nini ndani? (b) Hoja inayosadikisha yahitaji kuwe na nini?
14 Moja ya sifa za usemi ambazo hukaziwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni usemi wenye kufuatana, wenye kushikamana. Hii inatia ndani kuweka mawazo makuu yote na mambo yanayohusu habari katika utaratibu mzuri. Iliyo ya maana pia ni hoja inayosadikisha, inayotaka kuweka msingi mzuri na kuandaa uthibitisho ufaao. Jambo lenye kuhusiana na hili ni kusaidia wasikilizaji wasababu kwa kudumisha msingi wa kuwa na ukubaliano katika jambo moja, kusitawisha mambo kwa utoshelevu, na kuyatumia kwa matokeo. Tena, Maandiko huandaa miongozo.
15. (a) Paulo alitekaje fikira na kuweka msingi wa kuwa na ukubaliano katika jambo moja alipohutubu juu ya Kilima cha Mars? (b) Katika hotuba ya Paulo, tuna ushuhuda gani juu ya usemi wenye kufuatana, wenye kushikamana?
15 Sifa hizi za usemi zaonekana wazi katika ule usemi maarufu wa mtume Paulo juu ya Kilima cha Mars katika Athene ya kale. (Matendo 17:22-31) Utangulizi wake uliteka fikira na kuweka msingi wa kuwa na ukubaliano katika jambo moja, kwa maana alisema hivi: “Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini [kuliko wengine walivyo, NW].” Kwao, bila shaka hili lilionekana kuwa pongezi. Baada ya kutaja madhabahu iliyowekwa wakfu ‘Kwa Mungu Asiyejulikana,’ Paulo aliendelea na usemi wake wenye kufuatana, wenye kushikamana na hoja yenye kusadikisha. Alionyesha wazi kwamba Mungu huyu ambaye hawakumjua ‘alifanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo.’ Tofauti na Athena au viabudiwa vingine vya Kigiriki, ‘hakai katika hekalu zilizojengwa kwa mikono, wala hahitaji kutumikiwa kwa mikono ya wanadamu.’ Halafu mtume akaonyesha kwamba Mungu huyu alitupa sisi uhai na hatufanyi tupapase tukimtafuta kiupofu. Ndipo Paulo akasababu kwamba Muumba wetu, ambaye ameacha kutazama nyakati za ujinga wa kuabudu sanamu, ‘anaagiza watu wote wa kila mahali watubu.’ Hii iliongoza kwa mfuatano mzuri kwenye jambo la kwamba ‘Mungu atahukumu walimwengu kwa uadilifu kupitia binadamu mwekwa ambaye yeye alimfufua kutoka kwa wafu.’ Kwa kuwa Paulo alikuwa amekuwa ‘akitangaza habari njema za Yesu na ufufuo,’ Waathene hao walijua kwamba Hakimu huyu angekuwa Yesu Kristo.—Matendo 17:18, NW.
16. Huduma ya mtu yaweza kuathiriwaje na hotuba ya Paulo juu ya Kilima cha Mars na kwa kufanya mazoezi katika Shule ya huduma ya Kitheokrasi?
16 Ni kweli, Paulo hakuwa akitoa ushahidi kutoka nyumba kwa nyumba juu ya Kilima cha Mars. Lakini kutokana na hotuba yake na mazoezi ambayo hutolewa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mashahidi wa Yehova waweza kujifunza mengi yawezayo kuongezea ubora wa huduma yao ya shambani. Ndiyo, yote haya husaidia kuwafanya wawe wahudumu wenye matokeo zaidi, hata kama vile usemi wenye kufuatana vizuri na utoaji hoja wenye kusadikisha wa Paulo ulivyowavutia kwa usadikisho wengine wa Waathene hao wawe waamini.—Matendo 17:32-34.
Tumia Vielezi Vyenye Kuagiza
17. Ni mifano ya aina gani ipasayo kutumiwa katika huduma?
17 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi husaidia pia wahudumu wa Mungu watumie vielezi vizuri katika kutoa ushahidi wa nyumba kwa nyumba na njia nyingine za huduma yao. Kukazia mambo ya maana, vielezi sahili (vyepesi) vinavyofaa vyapasa kutumiwa. Shahidi apaswa kuvichota kutokana na hali zenye kueleweka na kuwa mwangalifu kuelewesha wazi utumizi wavyo. Vielezi vya Yesu vilitimiza matakwa yote haya.
18. Mathayo 13:45, 46 ingewezaje kuthibitika kuwa yenye mafaa katika huduma?
18 Kwa mfano, fikiria maneno ya Yesu: “Ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri; naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akinunua.” (Mathayo 13:45, 46) Lulu ni vito vyenye thamani kubwa vipatikanavyo ndani ya maganda ya chaza na konokono wengine. Lakini ni lulu fulani tu zilizo “nzuri.” Mfanya-biashara huyo alikuwa na utambuzi uliohitajiwa ili kuthamini ubora unaozidi wa lulu moja hii na kuwa mwenye nia ya kuachana na vitu vingine vyote ili aipate. Labda wakati wa ziara ya kurudia au funzo la Biblia nyumbani, kielezi hiki kingeweza kutumiwa kuonyesha kwamba mtu mwenye kuuthamini kweli kweli Ufalme wa Mungu atatenda kama mfanya-biashara huyo. Mtu wa jinsi hiyo ataupa Ufalme nafasi ya kwanza maishani, akijua kwamba huo wastahili dhabihu yoyote.
Malizia kwa Kichocheo
19. Katika huduma ya nyumba kwa nyumba, mimalizio yapasa kumwonyesha nini mwenye nyumba?
19 Katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, watu wa Mungu pia hujifunza kwamba umalizio wa hotuba au mazungumzo wapasa kuwa na uhusiano wa moja kwa moja na mada (kichwa) na wapasa kuonyesha wasikiaji jambo la kufanya na kuwatia moyo kulifanya. Katika huduma ya nyumba kwa nyumba, mwenye nyumba ahitaji kuonyeshwa wazi ni mwendo gani ambao atazamiwa kuchukua, kama vile kukubali kichapo cha Biblia au kukubali ziara ya kurudia.
20. Tuna mfano gani mzuri sana wa umalizio wenye kuchochea kwenye Mathayo 7:24-27?
20 Umalizio wa Mahubiri ya Yesu juu ya Mlima huandaa kielelezo kizuri sana. Kwa njia ya kielezi chenye kueleweka kwa urahisi, Yesu alionyesha kwamba ungekuwa mwendo wa hekima kutii maneno yake. Alimalizia hivi: “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.” (Mathayo 7:24-27) Hii inaonyesha vizuri kama nini kwamba wahudumu wa Mungu wapaswa kujitahidi kuchochea wenye nyumba!
21. Mazungumzo yetu yameonyesha nini, lakini ni lazima jambo gani litambuliwe?
21 Mambo yaliyotangulia yatoa mfano wa jinsi Shule ya Huduma ya Kitheokrasi iwezavyo kusaidia wengi wawe wapiga mbiu ya Ufalme wenye kustahili. Bila shaka, kustahili kwa kadiri ya kutosha hutoka kwa Mungu hasa. (2 Wakorintho 3:4-6) Na hata mhudumu awe mwenye kustahili kadiri gani, hakuna mtu awezaye kuvutia watu kwa usadikisho ili wawe waamini wasipovutwa na Mungu kupitia Kristo. (Yohana 14:6) Hata hivyo, kwa uhakika watu wa Mungu hutumia kwa faida maandalizi yote ya kiroho yafanywayo na Yehova watafutapo wale wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai wa milele.
Majibu Yako Ni Nini?
◻ Ni nani “wenye moyo safi,” nao ‘wamwonaje Mungu’?
◻ Ni mambo gani yapasayo kufikiriwa wakati wa kufanya utangulizi wa ujumbe wa Ufalme katika kazi ya nyumba kwa nyumba?
◻ Neno la Mungu laweza kutumiwaje kwa halali katika huduma?
◻ Ni nini kitakachosaidia kufanya utoaji wenye kufuatana vizuri, wenye kusadikisha katika utumishi wa shambani?
◻ Ni nini lipasalo kukumbukwa juu ya mifano yenye kutumiwa katika huduma?
◻ Ni nini kipasacho kutimizwa na mimalizio yenye kutumiwa katika kazi ya kutoa ushahidi?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Yesu alisema kwamba “wenye moyo safi” ‘wangemwona Mungu.’ Hiyo ilimaanisha nini?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Maandiko yapasa kufanyiwa utangulizi ifaavyo, kusomwa kwa mkazo wenye kufaa, na kutumiwa kwa njia ya wazi, iliyo sahihi