Kwa Nini Kuchukua Dini Kwa Uzito?
“BINADAMU hawezi kuishi kwa kutegemea mkate tu.” (Mathayo 4:4, The New English Bible) Maneno haya ambayo yamenakiliwa mara nyingi yanagusia uhitaji wa kibinadamu ambao wengi leo wameacha kuuona. Yanaonyesha kwamba sisi tuna sehemu fulani ya kiroho katika umbo letu inayohitaji kuridhishwa. Ndiyo sababu mwenye kusema maneno hayo, Yesu Kristo, alisema hivi pia: “Ni wabarikiwa kama nini wale wanaojua uhitaji wao wa Mungu.”—Mathayo 5:3, NEB.
Ni dini pekee inayoweza kutimiza ‘uhitaji wetu wa Mungu.’ Ni dini pekee inayoweza kujibu maswali yetu ya msingi juu ya mwanzo, kusudi, na maana ya maisha. Na ni dini pekee inayoweza kuzipa maisha zetu maana na ubora halisi. Lakini si dini yoyote tu itafanya yote haya. Yesu aliambia mwanamke mmoja Msamaria hivi: “Waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli.” (Yohana 4:23) Kuabudu ‘katika kweli’ kunamaanisha zaidi ya kufuata mapokeo na desturi za ibada zinazoheshimiwa kwa sababu zimekuwako kwa muda mrefu. Mara nyingi hizi zinawapa wafuasi hisia ya hali njema kwa muda tu, huku zikiwaacha wakiwa wenye njaa kiroho.
Kwa mfano, Edwin O. Reischauer, balozi wa hapo zamani wa United States huko Japani, alisema hivi: “Kwa watu walio wengi Ushinto na Ubuddha sana-sana ni desturi na kawaida tu wala si imani zenye umaana.” Kwa wazi, Wajapani wengi wanaridhika mambo yawe hivyo. Lakini kutokea kwa “dini mpya-mpya” katika Japani kunaonyesha ongezeko la kutoridhishwa na dini ya kimapokeo.
Zile “dini mpya-mpya” zinaelekea kukaza fikira juu ya viongozi wenye vipawa vya roho—si juu ya Mungu. Wengi wa hawa viongozi wa kidini wanadai kuwa walipewa uongozi wa kimungu. Lakini mafundisho yao kwa ujumla ni kama tu chungu cha mchanganyiko wa imani za Kibuddha, Kishinto, na nyinginezo—humo ndani likiwa limetupwa tonge kubwa la falsafa ya mwanzishi wazo. Mara nyingi uvutio wao umo katika ahadi ya maisha bora na nguvu wanazodai kuwa nazo za kifumbo au za kuponya. Lakini je! dini hizo zinatoa ushuhuda wa kwamba zinafundisha wafuasi wazo kuabudu “katika roho na kweli”? Sivyo hasa. Kwa jambo moja, viibada vya kidini vinaelekea kuwapo leo na kutokomea kesho yake. Asili yavyo iliyo kama mitindo yenye kupita haitoi sababu ya kuvichukua kwa uzito.
Dini ya Kuchukuliwa kwa Uzito
Hata hivyo, kuna dini fulani ambayo imekuwako kwa muda mrefu kuliko namna nyingine yoyote ya ibada. Ni ile dini inayofundishwa katika Biblia Takatifu. Biblia ilianza kuandikwa kama karne 35 zilizopita, na baadhi ya zile ‘historia’ zilizohifadhiwa katika sura zayo za mapema ni za miaka inayopita elfu moja kurudi nyuma zaidi.a Ina maandishi ya zamani zaidi yaliyopo kuhusu vyanzo vya dini. Hiyo pekee ni sababu ya kuifikiria Biblia kwa uzito.
The Encyclopedia Americana inasema hivi kuhusu Biblia: “Nuru yayo ‘imeenda ikaingia ndani ya ulimwengu wote.’ Sasa inaonwa kuwa hazina ya kiadili na ya kidini ambayo fundisho layo lisilomalizika lina tazamio la kuwa lenye thamani hata zaidi kwa kadiri tumaini la kuwako maendeleo ya ulimwengu linavyoongezeka.” Lakini ikiwa kweli kitabu fulani ni kiongozi kinachoaminika cha kuleta kwenye dini ya kweli, je! wewe usingekitazamia kienezwe kwa kadiri kubwa kupita vyote, ili kipatikane na watafutaji wote wa ukweli?
Ndivyo Biblia ilivyo. Imetafsiriwa katika lugha 1,928, ikiwa nzima au kwa sehemu, na ndicho kitabu chenye kuenezwa kwa mapana zaidi katika historia. Zaidi ya hilo, imethibitika kuwa sawa kihistoria na kisayansi. Uchimbuzi wa vitu vya kale na historia inashuhudia utimizo sahihi wa unabii mbalimbali wa Biblia. Haina namna zozote za uwasiliani-roho na hadithi za kifumbo na mafumbo ya kimazingaombwe. Yote haya yanapatana na dai la Biblia yenyewe kwamba imeongozwa kimungu.b—2 Timotheo 3:16, ZSB.
“Matunda” ya Dini ya Kweli
Lakini je! si kweli kwamba dini nyingi zinadai kufuata Biblia? Na je! ugomvi, uadui, na unafiki hauonekani wazi miongoni mwa wengi wanaodai ni Wakristo? Ndiyo, lakini hii si sababu ya kupuuza Biblia. Yesu Kristo mwenyewe alionyesha kwamba walio wengi wa wale wanaodai kufuata Ukristo wangekosa kukubaliwa na Mungu. (Ona Mathayo 7:13, 14, 21-23.) Basi, mtu angewezaje kutambua wale wanaozoea dini ya kweli inayofundishwa katika Biblia? Yesu alijibu hivi: “Mtawatambua kwa matunda yao. Je! watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.”—Mathayo 7:16, 17, 20.
Ndiyo, dini ya kweli inapaswa kuwa nguvu yenye uwezo ya kuleta wema, ikitokeza matokeo yenye manufaa kati ya waabudu. Chukua, kwa mfano, Akinori, mwanamume mmoja Mjapani ambaye, kulingana na maneno yake mwenyewe, “akawa kielelezo halisi cha roho ya ushindani.” Alifanikiwa kufikia miradi yake ya kupata cheti kutoka chuo kikuu kimoja chenye sifa kubwa na kupata kazi kwenye shirika lenye kujulikana sana. Hakuona sababu ya kutia dini katika maisha yake. ‘Dini ni ya watu wanyonge wanaohitaji kiegemeo maishani,’ akafikiri.
Kila kitu kilikuwa kikiendelea kwa ulaini mpaka alipowekwa chini na ugonjwa mzito, kutokana na mkazo na uchovu. Shingo yake ikapindika, na kidevu chake ‘kikagandamana’ kwenye bega lake la kushoto. Wengi wa ‘marafiki’ kwenye shirika la Akinori walithibitika kuwa wenye faraja kidogo katika wakati wake wa msononeko. (Linganisha Mithali 17:17.) Hivyo alishuka ndani ya shimo refu la utumiaji vileo na hata akafikiria kujiua.
Ingawa hivyo, baada ya muda mke wa Akinori alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Siku moja maongezi yalipokuwa yakiendelea, mke alimwambia yeye juu ya andiko kwenye Wagalatia 6:7, linalosomeka hivi: “Cho chote apandacho mtu ndicho atakachovuna.” Kwa kugongwa na maneno haya, Akinori alijiunga naye katika funzo, na aliyojifunza yalibadili maoni yake juu ya maana ya maisha. Matazamio ya Akinori yalipopata uangavu, mateso yake yenye kuletwa na mkazo yalianza kutoweka! Kama vile mithali moja ya Biblia inavyoweka wazo hilo: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili.” (Mithali 14:30) Ndiyo, dini ya kweli inatokeza tunda zuri!
Toshiro ni mwanamume mwingine Mjapani aliyekuja kuona jinsi dini ya kweli ingeweza kuwa nguvu ya kuleta mema. Ingawa aliamini kwamba kuzoea dini kuna thamani, hakufanya lolote juu ya hilo. Upendezi wake ulikazwa juu ya kujipatia nyumba yake mwenyewe. Hata hivyo, kufikia mradi huo hakukuleta uradhi aliotazamia. Zaidi ya hilo, alipotazama kuzunguka mahali pake pa kazi, aliona kwamba mazoea ya kutofuata haki yalikuwa ya kawaida na kwamba mahusiano mabaya ya kibinafsi yalitokana nayo. Toshiro alichukizwa sana na aliyoona.
Siku moja mke wake alialika mzee mmoja kutoka kundi la kwao la Mashahidi wa Yehova amzuru. Mara hiyo Toshiro akafahamu kwamba mzee huyo alikuwa tofauti na wenzi wake. Sababu? Mzee alikuwa akitumia kanuni za Biblia kwa moyo mweupe katika maisha yake. Kwa kuvutiwa na hilo, Toshiro alikubali mwaliko wa kujifunza Biblia na kuanza kuifanya dini ya Biblia iwe njia yake ya maisha.
Tunakualika wewe pia uzoeane na Mashahidi wa Yehova. “Matunda” yao yanatoa ushuhuda wa kwamba wanaabudu “katika roho na kweli.” Wanajitaabisha kufuata mafundisho ya Biblia kwa matendo katika maisha zao. Na ingawa wakiwa watu mmoja mmoja wao si wakamilifu kamwe, wakiwa kikundi wanaonyesha jinsi dini ya kweli inavyoweza kuwa nguvu ya kuleta mema.
Maelfu miongoni mwa Mashahidi wakati mmoja walikosa furaha na njia yao ya maisha. Lakini kupitia kutumia kanuni za Biblia, wengi wao wameweza kufanya mabadiliko ya kuvutia. Kwa kusitawisha kile ambacho Biblia inakiita “tunda la roho,” yaani, sifa za upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti (kujiweza), wamepata ufunguo wa furaha ya kibinafsi.—Wagalatia 5:22, 23.
Manufaa za Milele Kutokana na Kuzoea Dini ya Kweli
Hata hivyo, ni lazima dini ya kweli ifanye mengi zaidi ya kugeuza umbo la nyutu za watu au kulegeza matatizo ya kibinafsi. Ma-tatizo ya duniani pote kama vile uchafuzi, tisho la vita ya nyukilia, na utumizi mbaya wa mazingira yanatisha kuangamiza sayari yetu nzuri. Matatizo ya kiuchumi yanakandamiza furaha na hali njema ya mamilioni. Hakuna dini inayoweza kuchukuliwa kwa uzito isipotoa tumaini fulani kwa ajili ya kutatua matatizo haya ya duniani pote.
Dini ya Biblia inatoa tumaini la jinsi hiyo. Mungu anaahidi kuleta upesi ulimwengu mpya wa uadilifu chini ya serikali au “ufalme” wa kimbingu. (Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Ufalme huu ndio dawa ya matatizo yote ya ainabinadamu. Na kuhusu udumifu wa manufaa hizo za duniani pote, Biblia inatuhakikishia hivi: “Dunia [ulimwengu, NW] inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” Ndiyo, uhai wa milele katika furaha ndilo tumaini la kila Mkristo wa kweli! (1 Yohana 2:17) Lakini ni wale tu ambao wamechukua kwa uzito zoea la dini ya kweli watanufaika na Ufalme huu unaokuja. Kwa hiyo sisi tunakuhimiza uanze funzo la Biblia lenye uzito.c (Yohana 17:3) Unapoanza kuacha nuru ya Neno la Mungu ing’ae katika maisha yako, utapata shangwe kubwa kwa kuwa ‘uhitaji wako wa Mungu’ utajazwa, hatua kwa hatua. Kwa kweli, baraka za milele zitakuwa zako kwa sababu ulichukua dini—ile dini ya kweli—kwa uzito.
[Maelezo ya Chini]
a Ona, kwa mfano, Mwanzo 2:4; 5:1; 6:9.
b Kwa habari zaidi, ona kitabu The Bible—God’s Word or Man’s?, kinachopatikana kutoka kwa wachapishaji wa gazeti hili.
c Mashahidi wa Yehova wangefurahi kukusaidia katika jambo hili. Funzo la Biblia la nyumbani lisilo la malipo linaweza kupangwa kwa kupashana habari ama na wachapishaji wa gazeti hili ama na kundi la kwenu la Mashahidi wa Yehova katika mtaa wenu.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kupatikana kwa Biblia katika lugha zaidi ya 1,900 kunapatana na dai layo la kuwa lina uongozi wa kimungu
[Picha katika ukurasa wa 7]
Dini ya Biblia inatoa tumaini la hali zenye amani ulimwenguni pote chini ya serikali ya kimbingu