Nikiwa Mjane, Nilipata Faraja Ya Kweli
Kama ilivyosimuliwa na Lily Arthur
MHUDUMU mchanga wa Mashahidi wa Yehova alikuwa akienda nyumba kwa nyumba katika sehemu moja ya Ootacamund, India. Kwa desturi wanawake hawakufungulia mtu mgeni wa jinsi hiyo mlango. Baada ya saa chache, akiwa amechoka na kuvunjika moyo kidogo, aligeuka aende nyumbani. Lakini akasimama, akihisi kidogo lazima ya kwenda mlango ule mwingine. Fikiria lililotukia, kama linavyoelezwa na mwanamke aliyemfungulia mlango.
MSICHANA wangu wa miezi miwili akiwa mikononi mwangu na mwana wangu wa miezi 22 akiwa kando yangu, nilifungua mlango nikaona mtu mgeni amesimama hapo. Usiku ule tu uliotangulia nilikuwa nimesononeka kupita kiasi. Nikitafuta faraja, nilikuwa nimesali hivi: “Baba wa kimbingu, tafadhali nifariji kupitia Neno lako.” Sasa, nikastaajabu kuelezwa hivi na mtu huyo mgeni: “Mimi nakuletea ujumbe wa faraja na tumaini kutokana na Neno la Mungu.” Nilihisi ni lazima yeye awe ni nabii aliyetumwa na Mungu. Lakini ni hali gani iliyokuwa imesukuma sala yangu ya kuomba msaada?
Kujifunza Kweli za Biblia
Nilizaliwa katika 1922 katika kijiji cha Gudalur katika Vilima Nilgiri vyenye uzuri kusini mwa India. Mama yangu alikufa nilipokuwa na miaka mitatu. Baadaye, Baba, aliyekuwa kasisi Mprotestanti, alifunga ndoa upya. Mara tu tulipoweza kusema, Baba alifundisha ndugu na dada zangu na mimi kusali. Nikiwa na miaka minne, Baba alipokuwa akiketi kila siku kwenye dawati lake akisoma Biblia, mimi ningekuwa sakafuni nikisoma Biblia yangu mwenyewe.
Nilipokua, nikawa mwalimu. Halafu, nilipo-fika umri wa 21, baba yangu alipanga ndoa yangu. Mume wangu na mimi tulibarikiwa kupata mwana, Sunder, na baadaye binti, Rathna. Hata hivyo, karibu na wakati ambapo Rathna alizaliwa mume wangu akawa mgonjwa sana, na upesi baadaye akafa. Kwenye umri wa 24, nikawa mjane kwa ghafula nikiwa na daraka la kutunza watoto wachanga wawili.
Baada ya hapo nilimsihi sana Mungu anifariji kutoka Neno lake, na siku iliyofuata ndipo mhudumu wa Mashahidi wa Yehova aliponitembelea. Nilimwalika aingie ndani nami nikakikubali kitabu “Let God Be True.” Usiku huo nilipokuwa nikikisoma, niliendelea kuona jina Yehova, ambalo kwangu lilikuwa jambo la ajabu sana. Baadaye mhudumu huyo alirudi akanionyesha katika Biblia kwamba hili ni jina la Mungu.
Upesi nilijifunza pia kwamba mafundisho kama Utatu na moto wa mateso hayana msingi wa Biblia. Faraja na tumaini vilinijia nilipojifunza kwamba chini ya Ufalme wa Mungu dunia itakuwa paradiso na wapendwa waliokufa watarudi katika ufufuo. La maana zaidi, nilianza kumjua na kumpenda Mungu wa kweli, Yehova, aliyesikia sala yangu na kuja kunisaidia.
Kushiriki Maarifa Yaliyopatikana Karibuni
Nilianza kushangaa ni jinsi gani nilikuwa nimekosa kusoma mistari hiyo ya Biblia yenye jina la Mungu. Na kwa nini sikuwa nimeona katika usomaji wangu mwenyewe wa Biblia lile tumaini la wazi la uhai wa milele katika dunia-paradiso? Nilikuwa nikifundisha katika shule yenye kuendeshwa na wamisionari wa Kiprotestanti, hivyo basi nikaonyesha mistari hiyo ya Biblia kwa msimamizi wa shule. (Kutoka 6:3; Zaburi 37:29; 83:18; Isaya 11:6-9; Ufunuo 21:3, 4) Nilitaja kwamba kwa njia fulani tulikuwa tumekosa kuiona. Lakini nilishangaa mwanamke huyo alipoonekana kutofurahishwa.
Ndipo nikaandikia mkuu wa shule aliyekuwa katika mji mwingine, nikinakili mistari hii ya Biblia. Niliomba nafasi ya kuongea na mkuu huyu wa kike. Akajibu kwamba baba yake, aliye kasisi mwenye kujulikana sana kutoka Uingereza, angezungumza jambo hilo na mimi. Ndugu ya mkuu huyo wa shule alikuwa askofu mashuhuri.
Nilitayarisha mawazo na maandiko yote nikaenda na kitabu changu “Let God Be True” na watoto wangu kwenye mji unaofuata. Kwa shauku nikaeleza Yehova ni nani, kwamba hakuna Utatu, na mambo mengine niliyokuwa nimejifunza. Walinisikiliza kwa muda lakini hawakusema neno. Halafu yule kasisi wa kutoka Uingereza akasema: “Mimi nitasali kwa ajili yako.” Halafu akasali juu yangu na kuniambia niende zangu.
Kutoa Ushahidi wa Barabarani
Siku moja yule mhudumu wa Mashahidi wa Yehova alinialika kutoa ushahidi wa barabarani nikiwa na magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Nikamwambia mhudumu huyo mwanamume kwamba hilo ni jambo ambalo singeweza kamwe kulifanya. Unaona, katika India watu wangefikiri mambo mabaya kabisa juu ya mwanamke ambaye angesimama barabarani au kwenda nyumba kwa nyumba. Hiyo ingeleta suto juu ya sifa ya mwanamke huyo na hata juu ya familia yake. Kwa kuwa nilimheshimu na kumstahi sana baba yangu, sikutaka kuleta suto juu yake.
Lakini mhudumu huyo alinionyesha mstari mmoja wa Biblia unaosema hivi: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wa-ngu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Alisema hivi: “Unafurahisha moyo wa Yehova kwa kuonyesha peupe kwamba wewe uko upande wake na wa Ufalme wake.” Nikitamani kufurahisha moyo wa Yehova zaidi ya jambo jingine lolote, nikachukua mfuko wa magazeti nikaenda naye katika kazi ya kutoa ushahidi barabarani. Hata sasa siwezi kuwazia niliwezaje. Hiyo ilikuwa katika 1946, karibu miezi minne baada ya mimi kufikiwa.
Katiwa Moyo Kushinda Hofu
Katika 1947, nilikubali kazi ya kufundisha katika sehemu za nje za Madras, katika pwani ya Mashariki ya India, nami nikahamia huko pamoja na watoto. Kikundi kidogo cha Mashahidi wa Yehova karibu wanane kilikutana kwa ukawaida mjini. Ili kuhudhuria mikutano hiyo, ilikuwa lazima tusafiri kilometa 26. Katika India nyuma huko, wanawake kwa kawaida hawakusafiri peke yao. Walitegemea wanaume wawapeleke. Sikujua jinsi ya kupanda basi, jinsi ya kuomba tiketi, jinsi ya kuondoka katika basi, na mambo kama hayo. Nilihisi kwamba napaswa kumtumikia Yehova, lakini jinsi gani? Hivyo basi nikasali hivi: “Yehova Mungu, siwezi kuishi bila kukutumikia. Lakini ni jambo lisilowezekana kabisa kabisa kwa mimi mwanamke Mhindi kwenda nyumba kwa nyumba.”
Nilitumaini Yehova angeniacha nife ili kuniondolea fikira hizi zenye kushindana. Hata hivyo, nikaamua kusoma jambo fulani kutoka Biblia. Ikatukia kwamba, niliifungua Yeremia, panaposema hivi: “Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao; maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe.”—Yeremia 1:7, 8.
Nilihisi kwamba kwa kweli Yehova alikuwa akisema nami. Hivyo basi nilijipa moyo mkuu na mara hiyo nikaenda kwenye cherehani (mashine) yangu nikashona mfuko wa kutumia kubeba magazeti. Baada ya sala ya bidii, nilienda peke yangu nyumba kwa nyumba, nikaangusha vitabu vyangu vyote, na hata nikaanzisha funzo la Biblia siku hiyo. Niliazimia kumpa Yehova mahali pa kwanza katika maisha yangu, nami nikatia tumaini na uhakika wangu kamili katika yeye. Kazi ya kuhubiri peupe ikawa sehemu ya kawaida ya maisha yangu kujapokuwa na suto la maneno. Ijapokuwa upinzani ule, utendaji wangu ulivutia sana watu fulani.
Mfano wa jambo hili ulikuwa wakati binti yangu na mimi tulipoenda nyumba kwa nyumba katika Madras miaka mingi baadaye. Bwana mmoja mheshimiwa wa Kihindu, aliye hakimu wa Mahakama Kuu, kwa kukosea umri wangu, alisema hivi: “Mimi nimeyajua magazeti haya hata kabla wewe hujazaliwa! Miaka thelathini iliyopita bibi mmoja alikuwa akisimama kwa ukawaida kwenye Barabara ya Mount na kuyatoa.” Akataka andikisho.
Kwenye nyumba nyingine Brahman mmoja Mhindu, ambaye ni ofisa aliyeacha kazi sababu ya umri, alitualika ndani akasema: “Miaka mingi sana iliyopita bibi mmoja alikuwa akitoa Mnara wa Mlinzi katika Barabara ya Mount. Nitachukua unachonitolea kwa kumheshimu yeye.” Nililazimika kuwa na uso wa furaha kwa sababu nilijua kwamba mimi ndiye bibi ambaye wote wawili walimtaja.
Nikaimarishwa na Kubarikiwa
Katika Oktoba 1947 ndipo nilipofananisha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Wakati huo ni mimi tu niliyekuwa Shahidi wa kike mwenye kusema Kitamil katika mkoa mzima, lakini sasa mamia ya wanawake Watamil ni Mashahidi wa Yehova walio waaminifu na watendaji.
Nilipokwisha kubatizwa, upinzani ukaja kutoka pande zote. Ndugu yangu aliandika hivi: “Wewe umeruka mpaka wa mambo yote yanayofaa na adabu.” Pia nilipata upinzani katika shule nilimofanya kazi na kutoka kwa jumuiya. Lakini nilishikamana na Yehova kwa ukaribu hata zaidi kwa sala yenye uendelevu, ya bidii. Ikiwa niliamka katikati ya usiku, mara hiyo ningewasha taa ya mafuta na kujifunza.
Kwa kuwa niliimarishwa, nilikuwa katika hali bora ya kufariji na kusaidia wengine. Bibi mmoja mzee-mzee wa Kihindu ambaye nilijifunza naye alichukua msimamo thabiti upande wa ibada ya Yehova. Alipokufa, mwanamke mwingine katika nyumba yao alisema hivi: “Kilichotufurahisha kilikuwa uaminifu-mshikamanifu wake kwa Mungu ambaye yeye alichagua kumwabudu moja kwa moja mpaka mwisho.”
Bibi mwingine niliyejifunza naye hakuwa kamwe akionyesha uso wa furaha. Sikuzote uso wake ulionyesha wasiwasi na huzuni. Lakini baada ya kumfundisha juu ya Yehova, nilimtia moyo ampelekee sala, kwa kuwa yeye anajua taabu zetu na anatujali. Juma lililofuata uso wake uling’aa. Ilikuwa ndiyo mara ya kwanza kabisa mimi kumwona akiwa na uso wa furaha. “Nimekuwa nikisali kwa Yehova,” akaeleza, “nami nina amani ya akili na moyo.” Aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova na anabaki akiwa mwaminifu ajapokuwa na magumu mengi.
Kusawazisha Madaraka
Nikiwa na watoto wawili wa kutunza, nilihisi haikuelekea kwamba ningetimiza tamaa yangu ya kumtumikia Yehova wakati wote nikiwa painia. Lakini ndipo njia mpya ya utumishi ikafunguka wakati mtu fulani alipohitajiwa kutafsiri vitabu vya Biblia katika lugha ya Kitamil. Kwa msaada wa Yehova niliweza kutunza mgawo huo na, wakati uo huo, nikafanya kazi ya kimwili nikiwa mwalimu, kuwatunza watoto, kufanya kazi yangu ya nyumbani, kuhudhuria mikutano yote, na kujitia katika utumishi wa shambani. Mwishowe, watoto walipoongezeka umri, nikawa painia wa pekee, pendeleo ambalo nimelionea shangwe kwa miaka 33 iliyopita.
Hata kuanzia wakati Sunder na Rathna walipokuwa na umri mchanga, nilijaribu kukaza kikiki ndani yao upendo kwa Yehova na tamaa ya kutanguliza sikuzote mapendezi yake katika kila upande wa maisha zao. Walijua kwamba mtu wa kwanza waliyepaswa kuongea naye wakati wa kuamka ni Yehova, na kwamba Yeye ndiye wa mwisho wanayepaswa kuongea naye kabla ya kwenda kulala. Na walijua kwamba kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na utumishi wa shambani hakupasi kuachiliwa kwa sababu ya masomo ya kufanyiwa nyumbani. Ingawa niliwatia moyo wafanye yote wanayoweza katika masomo yao, sikusisitiza kwamba wapate kiwango cha juu katika mtihani, nikihofu kwamba wangefanya hilo liwe ndilo jambo la maana zaidi katika maisha zao.
Walipokwisha kubatizwa, walitumia malikizo yao ya shule kupainia. Nilimtia moyo Rathna awe mwenye moyo mkuu, si mwoga-mwoga wala mwenye haya kama mimi nilivyokuwa nimekuwa. Alipokwisha kumaliza shule ya masomo ya juu na mazoezi ya kibiashara, alianza kupainia, na baadaye akawa painia wa pekee. Baada ya muda, aliolewa na mwangalizi mmoja mwenye kusafiri, Richard Gabriel, ambaye sasa anatumikia akiwa kodineta wa Halmashauri ya Tawi kwa ajili ya Watch Tower Society katika India. Wao na binti yao, Abigail, wanafanya kazi ya wakati wote kwenye tawi la India, na mwana wao mdogo, Andrew, ni mhubiri wa habari njema.
Hata hivyo, Sunder akiwa na umri wa miaka 18 alivunja moyo wangu alipoacha kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Miaka iliyofuata ilikuwa ya maumivu makali kwangu. Niliendelea kumsihi sana Yehova ili anisamehe kwa mapungukio yoyote ambayo huenda nikawa nilikuwa nayo katika kumlea na ili nimrudishe Sunder kwenye fahamu zake aweze kurudi. Lakini, baada ya muda, nilipoteza tumaini lote. Halafu siku moja miaka 13 baadaye yeye akaja na kuniambia: “Mama, usijali, nitakuwa sawa.”
Upesi baada ya hapo, Sunder alifanya jitihada za pekee kuwa mkomavu kiroho. Alifanya maendeleo kufikia hatua ya kukabidhiwa uangalizi wa kundi moja la Mashahidi wa Yehova. Baadaye aliacha kazi yake yenye mshahara mkubwa ili awe painia. Sasa yeye na mke wake, Esther, wanatumikia pamoja katika kazi hii katika Bangalore katika sehemu ya kusini ya India.
Faraja ya Maisha Yote
Mara nyingi mimi namtolea Yehova asante kwa kuniruhusu nipite chini ya mateso na magumu muda wa miaka ile. Bila kupatwa na hayo nisingalikuwa na lile pendeleo lenye thamani kubwa la kuonja kwa kadiri kubwa hivyo wema wa Yehova, rehema yake, na maonyesho yake ya utunzaji mwororo na shauku. (Yakobo 5:11) Inachangamsha moyo kusoma katika Biblia juu ya utunzaji na hangaikio la Yehova kwa “yatima, na mjane.” (Kumbukumbu 24:19-21) Lakini hiyo si kitu ikilinganishwa na faraja na upendezo wa kujionea kikweli utunzaji na hangaikio lake.
Nimejifunza kuweka tumainio na uhakika kamili katika Yehova, si kutegemea uelewevu wangu mwenyewe, bali kumkiri katika njia zangu zote. (Zaburi 43:5; Mithali 3:5, 6) Nikiwa mjane kijana, nilisali kwa Mungu ili nipate faraja kutoka Neno lake. Sasa, nikiwa na umri wa 68, naweza kwa kweli kusema kwamba katika kuielewa Biblia na kutumia shauri layo, nimepata faraja isiyoweza kupimwa.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Lily Arthur akiwa na washiriki wa familia yake