Endeleeni Kutembea Katika Nuru na Upendo
Mambo Makuu Kutoka Yohana ya Kwanza
YEHOVA ni chanzo cha nuru na upendo. Ni lazima tumtegemee Mungu kwa ajili ya nuru ya kiroho. (Zaburi 43:3) Na upendo ni mojapo matunda ya roho takatifu yake.—Wagalatia 5:22, 23.
Nuru, upendo, na mambo mengine yanazungumzwa katika barua ya kwanza ya Yohana iliyoongozwa na Mungu, ambayo huenda ikawa iliandikwa katika au karibu na Efeso yapata 98 W.K. Sababu kubwa ya kuiandika ilikuwa kulinda Wakristo dhidi ya uasi-imani na kuwasaidia kuendelea kutembea nuruni. Kwa kuwa sisi hukabili magumu kuhusiana na upendo, imani, na ukamilifu wetu kwa ukweli, ufikirio wa barua hii kwa uhakika utatufaidi.
‘Enendeni Nuruni’
Yohana alionyesha wazi kwamba ni lazima Wakristo waaminifu watembee katika nuru ya kiroho. (1:1–2:29) Alisema hivi: “Mungu ni nuru, wala giza lo lote [chochote kiovu, kisicho na maadili, kisicho kweli, au kisicho kitakatifu] hamna ndani yake.” Kwa sababu Wakristo wapakwa mafuta kwa roho ‘huenenda nuruni,’ wao ‘wanashirikiana’ pamoja na Mungu, Kristo, na wao kwa wao. Wao pia wamesafishwa dhambi kwa damu ya Yesu.
Tukiwa ama Wakristo wapakwa mafuta walio na tumaini la kimbingu ama tukitazamia mbele uhai wa milele duniani, tutaendelea kufaidika na dhabihu ya Yesu ikiwa tu tunapenda ndugu zetu na si ulimwengu. Ni lazima pia tuepuke kuvutwa na waasi-imani, kama yule “mpinga Kristo,” ambaye humkana Baba na Mwana pia. Na tusisahau kamwe kwamba uhai wa milele utaonewa shangwe na wale tu wanaoshikamana na ukweli na wanaozoea uadilifu.
Watoto wa Mungu Huonyesha Upendo
Yohana halafu alitambulisha watoto wa Mungu. (3:1–4:21) Jambo moja ni kwamba, wao hufanya yaliyo ya uadilifu. Wao pia hutii amri ya Yehova Mungu ‘kwamba waamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana wao kwa wao.’
Mtu ambaye ‘anamjua Mungu’ ajua juu ya makusudi ya Yehova na jinsi upendo Wake unavyoonyeshwa. Hilo linapaswa kumsaidia mtu huyo aonyeshe upendo. Kwa kweli, “yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.” Upendo wa kimungu ulionyeshwa wakati Mungu ‘alipomtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.’ Ikiwa Yehova alitupenda kwa kadiri hiyo, tunapaswa tupendane sisi kwa sisi. Ndiyo, mtu yeyote anayedai kumpenda Mungu ni lazima awe akimpenda ndugu yake wa kiroho pia.
Imani ‘Hushinda Ulimwengu’
Upendo husukuma watoto wa Mungu washike amri zake, lakini wao ‘hushinda ulimwengu’ kupitia imani. (5:1-21) Imani yetu katika Mungu, Neno lake, na Mwana wake hutuwezesha ‘kuushinda ulimwengu’ kwa kukataa kuwaza kwao na njia zao mbaya na kwa kushika amri za Yehova. Mungu amewapa ‘washinda ulimwengu’ tumaini la uhai wa milele na husikiliza sala zao zinazopatana na mapenzi yake. Kwa sababu mtu yeyote “aliyezaliwa na [kutoka kwa, NW] Mungu” hafanyi zoea la dhambi, Shetani hamshikilii sana mtu kama huyo. Lakini wapakwa-mafuta na watumishi wa Yehova walio na matumaini ya kidunia pia wanapaswa kukumbuka kwamba ‘dunia yote [ulimwengu mzima, NW] hukaa katika yule mwovu.’
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]
Dhabihu ya Upatanisho: Yesu “ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu [zile za wafuasi wake wapakwa-mafuta]; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote,” wale waliosalia wa ainabinadamu. (1 Yohana 2:2) Kifo chake kilikuwa “kipatanisho” (kwa Kigiriki, hi·la·smosʹ, kumaanisha “njia ya kutuliza,” “kifuniko”) lakini si kwa maana ya kutuliza kuchukizwa kwa Mungu. Bali, dhabihu ya Yesu ilituliza, au ilitosheleza, madai ya haki kamilifu ya kimungu. Kwa jinsi gani? Kwa kuandaa msingi wa uadilifu na haki kwa ajili ya msamaha wa dhambi, ili Mungu, “awe mwenye haki na mwenye kumhesabia haki yeye [mwanadamu aliye na dhambi ya kiasili] amwaminiye Yesu.” (Warumi 3:23-26; 5:12) Kwa kutoa njia ya kutosheleza kabisa dhambi za mwanadamu, dhabihu ya Yesu ilifanya iwezekane kwa mwanadamu kutafuta na kupokea urudisho kwenye uhusiano unaofaa pamoja na Yehova. (Waefeso 1:7; Waebrania 2:17) Sote twapaswa kuwa wenye shukrani kama nini kwa jambo hilo!