Ni Nini Chasababisha Msononeko Wa Familia?
‘YEYE ni mvivu!’ Bob alipaaza sauti. ‘Yeye ni mtunzaji mbaya sana wa nyumba!’
‘Hiyo si kweli hata kidogo!’ Jean akajibu vikali. ‘Yeye hathamini chochote ninachojaribu kufanya. Yeye ni mwanamume mchambuzi zaidi niliyepata kukutana naye.’
Kasoro ilikuwa nini katika maisha ya Bob na Jean?a Ndoa yao changa ilikuwa ya miezi minne tu, lakini ilikuwa karibu kupatwa na msiba. Hata hivyo, hali yao si ya peke yake, kwa kuwa habari za takwimu zinaonyesha kwamba kutopatana katika ndoa ni kwa kawaida. Wenye ustadi husema kwamba nusu ya ndoa zote mpya katika United States zitaisha katika talaka. Vivyo hivyo habari za takwimu zenye huzuni huja kutoka kwa nchi nyinginezo nyingi. Hata hivyo, talaka ni sehemu tu ya mambo. Familia za idadi isiyo na kifani zina msononeko kwa sababu nyingi mbalimbali.
Sababu Nyinginezo za Msononeko wa Familia
Watoto wanaathiriwa sana wakati hali za msononeko zimo katika familia. Gazeti Newsweek linaripoti hivi: “Theluthi moja ya watoto wote waliozaliwa katika mwongo uliopita [katika United States] huenda wataishi katika familia ya kambo kabla hawajawa na miaka 18. Mtoto mmoja kati ya kila wanne leo analelewa na mzazi mmoja. Karibu asilimia 22 ya watoto leo walizaliwa nje ya ndoa; kati yao, karibu theluthi moja walizaliwa na mama aliye mtineja.”
J. Patrick Gannon mwenye ustadi katika kutendewa vibaya kwa watoto akitaja sababu inayohusika ya msononeko wa familia, asema hivi: “Uchunguzi wa karibuni unaonyesha kwamba makumi ya mamilioni ya watu walikua katika familia zisizo na utararibu mzuri, ambamo jeuri, kufanya ngono na watu wa ukoo, au kuumizwa hisia-moyo kunakosababishwa na ulevi yalikuwa mambo ya uhalisi ya kila siku.” Si jambo la kushangaza kwamba watoto wengi walioona mambo kama hayo huenda hawatajua jinsi ya kuepuka msononeko wa familia wakiwa watu wazima.
Wachunguzi wengine wangelaumu mabadiliko ya kiuchumi, ya kijamii, na ya kiadili ambayo yameenea kote katika mabara yenye viwanda kuwa visababishi vya msononeko wa familia. Kwa mfano, mwingio wa wanawake kazini kwa kadiri kubwa umeanzisha mpango mpya wenye kuchukiza wa madaraka na jukumu za kinyumbani. Kwa uwoga akina mama hujaribu kufanya kazi zenye ustadi ambazo wamesahau, huku akina baba waking’ang’ana kufanya kazi za nyumbani bila kutaka, na watoto wakijirekebisha kwa machozi kufuata maisha ya vitovu vya utunzi wa mchana.
Familia nyingi katika mabara kuzunguka tufe ziko chini ya mkazo mwingi sana. Mzazi mmoja anayefanya kazi alilinganisha hiyo na “kuishi katika hali ya dharura daima.” Haishangazi kwamba zaidi ya karibu nusu ya wale waliohojiwa wakati wa uchunguzi wa Gallup wa karibuni wa kuhoji watu walisema kwamba ‘familia ya Kiamerika imo katika hali mbaya zaidi leo kuliko ilivyokuwa miaka kumi iliyopita,’ na wachache waliamini kwamba hali ingekuwa afadhali.
Kwa hiyo msononeko wa familia ni kichwa cha mazungumzo cha sikuzote katika programu za maongezi katika televisheni na redio. Umma husoma kwa bidii vitabu vya kujisaidia juu ya familia, vinginevyo vikitoa kadiri ya shauri timamu na lenye kutumika. Ingawa himizo la ‘kuwasiliana kwa wazi zaidi’ au ‘kushirikiana maoni ya moyoni’ laweza kusaidia, linapungukiwa kushika kisababishi halisi cha matatizo ya kinyumbani. Makala inayofuata itafanya hivyo nayo itaonyesha jinsi ya kushughulika na msononeko wa familia.
[Maelezo ya Chini]
a Majina bandia yametumiwa ili kudumisha usiri.