Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 5/15 kur. 21-23
  • Yehova Husikia Vilio Vyetu Vya Uharaka Vya Kuomba Msaada

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Husikia Vilio Vyetu Vya Uharaka Vya Kuomba Msaada
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ombi kwa Ajili ya Kukombolewa Upesi
  • Wale Wanaosema, “Ewe! Ewe!”
  • ‘Atukuzwe Mungu!’
  • Tumainia Mwandalizi wa Wokovu
  • Yehova Alikuwa “Mwokoaji” Katika Nyakati za Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Yehova Hadharau Moyo Uliovunjika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • “Tufundishe Sisi Kusali”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Je, Sala Zako ‘Hutayarishwa Kama Uvumba’?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 5/15 kur. 21-23

Yehova Husikia Vilio Vyetu Vya Uharaka Vya Kuomba Msaada

MSAADA ulihitajika kwa uharaka. Hilo lilikuwa wazi kutokana na uso wenye huzuni nyingi sana wa mnyweshaji wa mfalme. Alipoulizwa ni jambo gani lilikuwa baya, mnyweshaji alieleza huzuni yake juu ya hali ya kuharibika ya Yerusalemu na kuta zayo. Halafu kukaja swali hili: “Una haja gani unayotaka kuniomba?” “Basi [mara hiyo, NW] nikamwomba Mungu wa mbinguni,” mnyweshaji Nehemia akaandika baadaye. Hicho kilikuwa kilio cha upesi, cha kimya, na cha uharaka cha kuomba msaada wa Yehova. Na tokeo likawa nini? Mfalme Mwajemi Artashasta upesi alimruhusu Nehemia ajenge upya kuta za Yerusalemu!—Nehemia 2:1-6.

Ndiyo, Mungu husikia maombi ya uharaka ya wale wanaompenda. (Zaburi 65:2) Kwa hiyo ikiwa jaribu laonekana kuwa kubwa kupita kiasi unachoweza kuvumilia, ungeweza kusali kama vile mtunga zaburi Daudi alivyofanya katika Zaburi 70, alipokuwa anahitaji msaada wa kimungu wa wakati uo huo. Maandishi ya utangulizi [katika New World Translation] wa zaburi hiyo yanaonyesha kwamba kusudi yayo ni “kukumbusha.” Hurudia tena Zaburi 40:13-17, ikiwa na mabadilisho machache. Lakini Zaburi 70 yaweza kutusaidiaje tukiwa watu wa Yehova?

Ombi kwa Ajili ya Kukombolewa Upesi

Daudi aanza na ombi hili: “Ee Mungu, uniokoe, Ee BWANA [Yehova, NW], unisaidie hima.” (Zaburi 70:1) Tunapokuwa katika msononeko, tunaweza kusali kwamba Yehova atusaidie upesi. Yehova hatujaribu kwa mambo maovu, naye “ajua kuwaokoa watauwa [wenye ujitoaji kimungu, NW] na majaribu.” (2 Petro 2:9; Yakobo 1:13) Lakini vipi ikiwa anakubali jaribu liendelee, labda ili kutufunza jambo fulani? Basi tutamwomba hekima ili kushughulika nalo. Tukiomba kwa imani, anatupa hekima. (Yakobo 1:5-8) Mungu hutupa pia imara inayohitajiwa kuvumilia majaribu yetu. Kwa mfano, yeye ‘hututegemeza tulipo wagonjwa kitandani.’—Zaburi 41:1-3; Waebrania 10:36.

Hali yetu ya asili ya dhambi, na pia hali ya kuwekwa wazi daima kwa ushawishi na juhudi za Ibilisi za kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova, yapasa kutusukuma kusali kila siku ili kupata msaada wa Mungu. (Zaburi 51:1-5; Warumi 5:12; 12:12) Yanayostahili kuangaliwa sana ni maneno haya ya Yesu katika sala ya kiolezo: “Usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) Naam, tunaweza kumwomba Mungu kwamba asituruhusu tushindwe tunaposhawishwa kutomtii na kwamba azuie Shetani, “yule mwovu,” asitunase. Lakini acha tuunganishe vilio vyetu vya kuomba kukombolewa pamoja na hatua za kuepuka hali ambazo zingetuweka wazi isivyo lazima kwa ushawishi na mitego ya Shetani.—2 Wakorintho 2:11.

Wale Wanaosema, “Ewe! Ewe!”

Huenda ikawa tunajaribiwa sana kwa sababu adui hutushutumu kwa ajili ya imani tuliyo nayo. Ikiwa jambo hilo lingetokea kwako, fikiria maneno ya Daudi haya: “Waaibike, wafedheheke, wanaoitafuta nafsi yangu. Warudishwe nyuma, watahayarishwe, wapendezwao na shari yangu. Warudi nyuma, na iwe aibu yao, wanaosema, Ewe! Ewe!” (Zaburi 70:2, 3) Adui wa Daudi walitaka kumwona amekufa; walikuwa ‘wanatafuta nafsi yake,’ au uhai wake. Hata hivyo, badala ya kujaribu kulipa kisasi, aliamini kwamba Mungu angewaaibisha. Daudi alisali kwamba adui zake ‘wangeaibika na kufedheheka’—wakiwa wamefadhaishwa, wamefumbwa, wameudhika, wametatanika katika kujaribu kutimiza makusudi yao maovu. Naam, acha wale wanaotafuta kumwumiza na wanaopata raha kwa pigo lake wawe wenye kuvurugika na wenye kuona aibu.

Kama tungekuwa na ile inayoweza kuitwa shangwe yenye uovu wakati pigo lingempata adui, tungepaswa kutoa hesabu kwa Yehova dhambi yetu. (Mithali 17:5; 24:17, 18) Hata hivyo, adui wanapomshutumu Mungu na watu wake, tunaweza kusali kwamba kwa ajili ya jina lake takatifu, Yehova ‘awarudishe nyuma, watahayarishwe’ machoni pa watu wale ambao mbele yao wao hutafuta utukufu. (Zaburi 106:8) Kisasi ni cha Mungu, naye aweza kuangamiza na kuaibisha adui zake na zetu. (Kumbukumbu 32:35) Kwa mfano, kiongozi Mnazi Adolf Hitler alitafuta kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani. Jinsi alivyoshindwa vibaya, kwa kuwa sasa maelfu mengi wao hutangaza wazi ujumbe wa ufalme huko!

Kwa mzaha wa kudharau, huenda adui zetu wakasema hivi: “Ewe! Ewe!” Kwa kuwa wanadhihaki Mungu na watu wake, acha wale watenda dhambi “warudi nyuma, na iwe aibu yao,” wakipatwa na fedheha. Tunaposali juu ya hiyo, acheni tudumishe ukamilifu wetu na kufanya moyo wa Yehova ushangilie, ili kwamba aweze kumpa Shetani jibu na mwingine yeyote anayemlaumu. (Mithali 27:11) Na tusiwaogope kamwe adui zetu wenye kiburi, kwa kuwa “amtumainiye BWANA [Yehova, NW] atakuwa salama.” (Mithali 29:25) Mfalme Mbabulonia Nebukadreza mwenye kiburi, ambaye alikuwa amewapeleka watu wa Mungu kuwa watekwa, aliona fedheha na alipaswa kukiri kwamba ‘Mfalme wa mbinguni aweza kuwadhili waendao kwa kutakabari.’—Danieli 4:37.

‘Atukuzwe Mungu!’

Ingawa adui wanaweza kutusababishia matatizo, acha sikuzote tumsifu Yehova pamoja na waabudu wenzetu. Badala ya kujiacha amezwe na usumbufu hivi kwamba ashindwe kumtukuza Mungu, Daudi alisema hivi: “Washangilie, wakufurahie, wote wakutafutao. Waupendao wokovu wako waseme daima, Atukuzwe Mungu.” (Zaburi 70:4) Watu wa Yehova huendelea kuwa wenye shangwe nyingi kwa sababu wao ‘hushangilia na kumfurahia’ yeye. Wakiwa Mashahidi wake walio wakfu, na kubatizwa, wana shangwe kubwa inayotokana na uhusiano wa kindani pamoja naye. (Zaburi 25:14) Hata hivyo, wanaweza kuonwa kama watafutaji wa Mungu wanyenyekevu. Wakiwa waamini wanaoshika amri za Mungu, wao huendelea kutafuta maarifa zaidi ya yeye na ya Neno lake.—Mhubiri 3:11; 12:13, 14; Isaya 54:13.

Mashahidi wa Yehova wanapotangaza habari njema, kwa kweli wao husema daima: ‘Atukuzwe Mungu!’ Wanamsifu Yehova, wakimpa heshima ya juu zaidi. Kwa shangwe, wao husaidia watafutaji kweli kujifunza juu ya Mungu na pia kumtukuza. Tofauti na wapendao anasa wa kilimwengu, watu wa Yehova ‘hupenda wokovu wake.’ (2 Timotheo 3:1-5) Wakiwa wanafahamu udhambi wao wa kurithi, wana shukrani yenye kina kirefu kwa maandalizi yenye upendo ya Yehova Mungu kwa ajili ya wokovu wa uhai wa milele, ambao unawezekana kupita dhabihu ya kupatanisha ya Mwana wake mpenzi, Yesu Kristo. (Yohana 3:16; Warumi 5:8; 1 Yohana 2:1, 2) Je! wewe unamtukuza Mungu na kumwonyesha kwamba ‘unapenda wokovu wake’ kwa kuzoea ibada ya kweli kwa sifa yake?—Yohana 4:23, 24.

Tumainia Mwandalizi wa Wokovu

Daudi alipojieleza mwenyewe katika zaburi hii, aliona uhitaji wa kuhitajiwa sana hivi kwamba alisema: “Nami ni maskini na mhitaji, ee Mungu, unijilie kwa haraka. Ndiwe msaada wangu na mwokozi [Mwandalizi wa wokovu, NW] wangu, ee BWANA [Yehova, NW], usikawie.” (Zaburi 70:5) Tunapoumizwa na majaribu yanayowapata waamini—dhiki za namna ya mnyanyaso, vishawishi, na mashambulio ya Shetani—huenda tukaonekana kuwa “maskini.” Ingawa huenda tusiwe maskini, tunaonekana kuwa bila ulinzi dhidi ya adui wabaya. Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova aweza kutuponya na atafanya hivyo tukiwa watumishi wake waaminifu.—Zaburi 9:17-20.

Yehova ni “Mwandalizi wa wokovu” tunapouhitaji. Huenda ikawa makosa yetu wenyewe yalituingiza katika hali yenye majaribu. Lakini ikiwa ‘upumbavu ndio ulipotosha njia yetu,’ tusiache ‘moyo wetu unune juu ya Yehova.’ (Mithali 19:3) Yeye si mwenye kulaumiwa naye yuko tayari kutusaidia tukisali kwake katika imani. (Zaburi 37:5) Vipi ikiwa tunajitahidi kuepuka dhambi? Basi acheni tuwe hususa juu ya hiyo katika sala, tukiomba msaada wa kimungu ili kuendelea kufuatia mwendo wenye uadilifu. (Mathayo 5:6; Warumi 7:21-25) Mungu atajibu sala yetu yenye kutoka moyoni na tutafanikiwa kiroho tukijitiisha kwa mwongozo wa roho takatifu yake—Zaburi 51:17; Waefeso 4:30.

Tunapokuwa katika maumivu makubwa ya jaribu la imani, huenda tukaona kwamba hatuwezi kuvumilia zaidi. Kwa kuwa mwili wetu wenye dhambi uko dhaifu, huenda ukatamani sana kuponywa upesi. (Marko 14:38) Kwa hiyo tungeomba hivi: “Ee Bwana [Yehova, NW], usikie; Ee Bwana [Yehova, NW], usamehe; Ee Bwana [Yehova, NW], usikilize, ukatende, usikawie; kwa ajili yako wewe, Ee Mungu wangu; kwa sababu . . . watu wako wanaitwa kwa jina lako. (Danieli 9:19) Tuna imani kwamba Baba yetu wa kimbingu hatakawia, kwa kuwa mtume Paulo alitoa uhakikisho huu: “Na tukikaribie kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahilika tukiwa na uhuru wa kusema, tupate kupokea rehema na kuona fadhili zisizostahilika za kutusaidia wakati unaofaa.”—Waebrania 4:16, NW.

Usisahau kamwe kwamba Yehova ndiye Mwandalizi wa wokovu. Tukiwa watumishi wake, itatufaidi kukumbuka jambo hili na maoni ya sala ya Zaburi 70. Nyakati nyingine huenda tukahitaji kusali tena na tena juu ya jambo lenye kuhangaisha sana. (1 Wathesalonike 5:17) Huenda ikaonekana kwamba hakuna utatuzi wa tatizo fulani, hakuna suluhisho la mashaka yetu. Lakini Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo atatuimarisha naye hataturuhusu tujaribiwe kupita tuwezavyo. Kwa hiyo, usichoke kamwe kwenda mbele ya kiti cha ufalme cha Mfalme wa Milele katika sala ya moyoni. (1 Wakorintho 10:13; Wafilipi 4:6, 7, 13; Ufunuo 15:3) Sali kwa imani, na umtegemee kikamili, kwa kuwa Yehova husikia vilio vyetu vya uharaka vya kuomba msaada.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki