Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Mwenendo Unaopamba Huduma Yetu ya Kikristo
MTUME Petro aonya kwa upole Wakristo: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa.” (1 Petro 2:12) Mtume Paulo aonyesha kwamba kwa mwenendo wetu mzuri, ‘tunayapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’ (Tito 2:10) Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wana sifa ya mwenendo mzuri. Angalia mifano fulani.
Kuvutiwa kwa Mwalimu na Mwenendo Mwema
◻ Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Costa Rica inaripoti kwamba idadi kubwa ya vijana katika nchi hiyo hutoa mfano mzuri. Ndugu mmoja aeleza kilichomvutia kwenye kweli. Aeleza hivi: “Jambo lililonivutia zaidi lilikuwa ule mwenendo mzuri wa vijana na watu wazima pia lakini hasa vijana. Nilipokuwa nikifanya kazi nikiwa mwalimu, nilikuwa na nafasi ya kuchunguza kwa ukaribu Mashahidi kwenye shule yangu. Na kwa kuwa nilikaa na familia ya Mashahidi wa Yehova, nilichunguza mwenendo wa watoto huko pia.
“Sikuwa na budi ila kuona tofauti kati ya wanafunzi waliokuwa Mashahidi na wanafunzi wengineo katika shule yangu. Mashahidi sikuzote hawakuchelewa na walikuwa wenye tabia nzuri, hawakusema uwongo, na sikuzote walifanya migawo yao. Niliona pia kwamba walifuata haki walipokuwa wakifanya mitihani, hata ingawa wanafunzi wengine walidanganya kwa kawaida. Zaidi ya hayo, walikuwa na adabu na staha nyingi kwangu nikiwa mwalimu wao. Nikiwa nimevutwa na Mashahidi shuleni na katika nyumba nilipokuwa nikikaa, nilianza kuchunguza dini hiyo na hatimaye nikakubali kweli.”
Matokeo Mazuri Kutokana na Mwenendo wa Kikristo Kwenye Mkusanyiko
◻ Mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika kundi katika sehemu ya magharibi mwa El Salvador alitamani kushiriki habari njema za Ufalme pamoja na ndugu zake wa kimwili wawili. Mmoja alisikiliza akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Yule ndugu mwingine alikuwa wa kanisa la Evanjeliko lililoitwa Mwana-Mfalme wa Amani, akasema kwa ndugu yake: “Usiongee nami; unatumikia masilahi ya Ibilisi.”
Wakati ulipokuja wa mkusanyiko wa wilaya, yule aliyekuwa akijifunza alialika ndugu yake kwenda pamoja naye kwenye mkusanyiko. Ndugu huyo alisema hivi: “Haya basi, nitaenda; naenda tu ili nione ninavyoweza kuwanasa Mashahidi.” Hao ndugu wawili walihudhuria mkusanyiko pamoja. Hudhurio kubwa na utengemano mzuri kwenye mkusanyiko ulimvutia Mwevanjeliko huyo, ambaye alisema hakuwa ameona kamwe jambo kama hilo kabla ya wakati huo. Alipofika nyumbani, alisema kwa ndugu yake: “Nipe mkono wako.” “Haya ni mambo gani hasa?” ndugu yake akauliza. “Nipe tu mkono wako,” likawa jibu. Walishikana mikono, na ndugu aliyekuwa wa kanisa la Evanjeliko akataarifu hivi: “Toka sasa na kuendelea mimi nitajifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kweli, sikujua yale niliyokuwa nikikosa.” Sasa yeye pia ni mpiga mbiu mwenye utendaji na bidii wa habari njema za Ufalme wa Mungu.y