Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 7/1 kur. 5-7
  • Je! Ibada ya Mama-Mungu-Mke I Hai Bado?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Ibada ya Mama-Mungu-Mke I Hai Bado?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Artemi wa Kiefeso
  • Kutoka Kuwa Mama Mungu-Mke Hadi Kuwa “Mama ya Mungu”
  • Ibada ya Mama Mungu-Mke I Hai Bado
  • Mahali Ambako Ibada ya Kweli na Upagani Ilitofautiana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Hadithi ya Tano ya Uwongo: Maria Ni Mama ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Je, Maria Ni Mama ya Mungu?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Kutoka Kuwa Mama Dunia Hadi Kuwa Miungu-Wake wa Uzazi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 7/1 kur. 5-7

Je! Ibada ya Mama-Mungu-Mke I Hai Bado?

IBADA ya mama-mungu-mke bado ilizoewa wakati wa siku za Wakristo wa mapema. Mtume Paulo alikutana nayo katika Efeso katika Esia Ndogo. Kama vile katika Athene, jiji jingine lenye ibada ya mungu-mke, alikuwa ametoa ushuhuda juu ya “Mungu aliyeufanya ulimwengu,” Muumba anayeishi, ambaye si “mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu.” Jambo hilo lilikuwa gumu sana kwa Waefeso kuvumilia, wengi ambao waliabudu mama-mungu-mke Artemi. Wale waliojiruzuku kwa kufanyiza vihekalu vya fedha vya mungu-mke huyo walichochea ghasia. Kwa muda wa saa mbili hivi, umati huo ulipaaza sauti hivi: “Artemi wa Waefeso ni mkuu”!—Matendo 17:24, 29; 19:26, 34.

Artemi wa Kiefeso

Wagiriki waliabudu Artemi pia, lakini Artemi aliyeabudiwa katika Efeso hawezi kutambulishwa naye moja kwa moja. Artemi wa Kigiriki alikuwa mungu-mke bikira wa uwindaji na uzalishaji watoto. Artemi wa Kiefeso alikuwa mungu-mke wa uzazi. Hekalu lake kubwa sana huko Efeso lilionwa kuwa mojawapo ya maajabu saba ya ulimwengu. Sanamu yake, ambayo ilidhaniwa kwamba ilianguka kutoka mbinguni, ilimwonyesha kuwa ufananisho wa uzazi, kifua chake kikiwa kimefunikwa kwa mistari ya matiti yenye umbo la mayai. Umbo hilo la matiti hayo lisilo la kawaida limetokeza maelezo mbalimbali, kama kuwa yanafananisha mashada ya mayai au hata makende ya mafahali. Elezo liwe ni nini, mfano wa uzazi uko wazi.

Kwa kupendeza, kulingana na The New Encyclopœdia Britannica, sanamu ya kwanza ya mungu-mke huyo “ilifanyizwa kwa dhahabu, mpingo, fedha, na jiwe jeusi.” Sanamu yenye kujulikana sana ya Artemi wa Kiefeso, yenye tarehe ya kuanzia karne ya pili W.K., inamwonyesha kuwa na uso, mikono na miguu, myeusi.

Sanamu ya Artemi ilionyeshwa katika barabara za jiji. Mwanachuo wa Biblia R. B. Rackham aandika hivi: “Ndani ya hekalu [la Artemi] mliwekwa . . . sanamu, madhabahu, na vyombo vyake vitakatifu vya dhahabu na fedha, vilivyopelekwa kwenye jiji na kurudi katika mwandamamo wa utukufu wakati wa sikukuu kubwa.” Sikukuu hizo zilivutia mamia ya maelfu ya wasafiri kutoka Esia Ndogo yote. Walinunua vihekalu vya mungu-mke huyo na kumpongeza kuwa mkuu, bibi yao, malkia, bikira, “mmoja asikizaye na kukubali sala.” Katika mazingira kama hayo, ilihitaji moyo mkuu sana kwa upande wa Paulo na Wakristo wa mapema ili kumsifu “Mungu aliyeufanya ulimwengu,” badala ya miungu na miungu-wake waliofanyizwa kwa “dhahabu au fedha au jiwe.”

Kutoka Kuwa Mama Mungu-Mke Hadi Kuwa “Mama ya Mungu”

Mtume Paulo alitabiri uasi-imani kwa wazee wa kundi la Kikristo la Efeso. Alionya kwamba waasi-imani wangeinuka na kusema “mapotovu.” (Matendo 20:17, 28-30) Miongoni mwa hatari zenye kujibanza daima katika Efeso kulikuwa ni kurudi kwenye ibada ya mama-mungu-mke. Je! hilo kwa kweli lilitokea?

Tunasoma hivi katika New Catholic Encyclopedia: “Pakiwa ni kitovu cha ziara za patakatifu, Efeso palionwa kuwa mahali ambapo Yohana alizikwa. . . . Pokeo jingine, lililoshuhudiwa na Baraza la Efeso (431), lalinganisha Bikira Mariamu Mbarikiwa na [Mtakatifu] Yohana. Basilika ambamo baraza hilo lilikutana iliitwa Kanisa la Mariamu.” Kitabu kingine cha Kikatoliki (Théo—Nouvelle encyclopédie catholique) chasema juu ya “pokeo la kupendeza” kwamba Mariamu aliandamana na Yohana kwenda Efeso, ambapo aliishi salio la maisha yake. Kwa nini huo ulinganifu wa kudhaniwa kati ya Efeso na Mariamu ni wenye umaana kwetu sisi leo?

Acha The New Encyclopœdia Britannica ijibu: “Kutukuzwa kwa mama ya Mungu kulitiwa nguvu wakati Kanisa la Kikristo lilipopata kuwa kanisa la kifalme chini ya Konstantino na umati wa wapagani ulipomiminika kanisani. . . . Utawa na ufahamu wao wa kidini ulikuwa umefanyizwa kwa muda wa mamileani kupitia kidhehebu cha mungu-mke aliye ‘mama mkuu’ na ‘bikira wa kimungu,’ maendeleo yaliyoanzia kutoka dini za zamani zilizopendwa na wengi za Kibabuloni na Kiashuri.” Ni mahali gani pengine pangeweza kufaa zaidi ya Efeso kwa “kufanya kuwa ya Kikristo” ibada ya mama-mungu-mke?

Hivyo, ilikuwa katika Efeso, katika 431 W.K., kwamba lililoitwa eti baraza la tatu la maaskofu wote lilitangaza Mariamu kuwa “Theotokos,” neno la Kigiriki linalomaanisha “mzaa-Mungu,” au “Mama ya Mungu.” New Catholic Encyclopedia inataarifu hivi: “Utumizi wa cheo hicho na Kanisa bila shaka ulikuwa jambo lenye kukata maneno kwa ukuzi wa fundisho na ujitoaji wa Kimariamu katika karne za baadaye.”

Magofu ya “Kanisa la Bikira Mariamu,” ambapo baraza hilo lilikutania, yaweza bado kuonekana leo kwenye mahali pa Efeso ya kale. Kikanisa chaweza kuzuriwa pia ambacho, kulingana na mapokeo, ndicho nyumba ambapo Mariamu aliishi na kufa. Papa Paul wa 6 alizuru mahali hapo patakatifu pa Kimariamu katika Efeso katika 1967.

Ndiyo, Efeso ilikuwa kitovu cha kubadilika kwa ibada ya kipagani ya mama-mungu-mke, kama ile ambayo Paulo alipata katika karne ya kwanza, kuwa ujitoaji wenye juhudi kwa Mariamu akiwa “Mama ya Mungu.” Ni hasa kupitia ujitoaji kwa Mariamu kwamba ibada ya mama-mungu-mke imedumu katika mabara ya Jumuiya ya Wakristo.

Ibada ya Mama Mungu-Mke I Hai Bado

Encyclopœdia of Religion and Ethics inataja mwanachuo wa Biblia W. M. Ramsay akisababu kwamba katika “karne ya 5 heshima iliyopewa Bikira Mariamu katika Efeso ilikuwa namna [mpya] ya ibada ya zamani ya kipagani ya Kianatolia ya Mama Bikira.” The New International Dictionary of New Testament Theology inataarifu hivi: “Mawazo ya Kikatoliki ya ‘mama ya Mungu’ na ya ‘malkia wa mbinguni,’ ingawa ni ya baada ya A[gano] J[ipya], huelekezea mashina ya mapema zaidi ya historia ya kidini katika Mashariki. . . . Katika kutukuzwa kwa baadaye kwa Mariamu kuna alama nyingi za kidhehebu cha kipagani cha mama wa kimungu.”

Alama hizo ni nyingi mno na zenye mambo madogo madogo mengi zisiweze kuwa zenye kufanana kiasili tu. Ufanano kati ya sanamu za mama na mtoto za Bikira Mariamu na sanamu za miungu-wake wa kipagani, kama vile Isisi, haukosi kuonwa. Mamia ya sanamu na picha za Madonna Mweusi katika makanisa ya Kikatoliki kotekote ulimwenguni hazikosi kukumbusha juu ya ile sanamu ya Artemi. Kitabu Théo—Nouvelle encyclopédie catholique kinasema hivi juu ya Mabikira Weusi hao: “Wanaonekana kuwa walikuwa njia ya kupishia Mariamu salio la ujitoaji ule uliopendwa na wengi kwa Diana [Artemi] . . . au Cybele.” Miandamano ya Siku ya Kuchukuliwa Mbinguni kwa Bikira Mariamu inapata pia kiolezo chayo katika miandamano ya kuheshimu Cybele na Artemi.

Vyeo vyenyewe vinavyopewa Mariamu vinatukumbusha mama miungu-wake wa kipagani. Ishtari alipongezwa kuwa “Bikira Mtakatifu,” “Bibi yangu,” na “mama mwenye rehema asikiaye sala.” Isisi na Astarte waliitwa “Malkia wa Mbinguni.” Cybele alipewa jina “Mama ya Wabarikiwa wote.” Vyeo vyote hivyo, vikiwa na tofauti ndogo ndogo, vyatumiwa kwa Mariamu.

Vatikani 2 ilitia moyo kidhehebu cha “Bikira Mbarikiwa.” Papa John Paul 2 anajulikana sana kwa ujitoaji wake wenye bidii kwa Mariamu. Wakati wa kusafiri kwake kwingi, hakosi nafasi ya kuzuru vihekalu vya Kimariamu, kutia ndani kile cha Madonna Mweusi wa Czestochowa, katika Polandi. Alimkabidhi Mariamu ulimwengu mzima. Kwa hiyo, haishangazi kwamba chini ya “Mama Mungu-Mke,” The New Encyclopœdia Britannica inaandika hivi: “Maneno hayo yametumika pia kwa sanamu za namna mbalimbali kama zile zinazoitwa eti Wavenusi wa zile Zamani za Vyombo vya Mawe na kwa Bikira Mariamu.”

Lakini utukuzo wa Katoliki Roma kwa Mariamu si njia ya pekee tu ambayo ibada ya mama-mungu-mke imedumu hadi siku yetu. Kwa ajabu, wenye kuunga mkono harakati ya kike wametokeza vichapo vingi juu ya ibada ya mama-miungu-wake. Wanaamini kwamba wanawake wameonewa vibaya katika ulimwengu huu ambapo wanaume hutawala wanawake kwa jeuri na kwamba ibada yenye mwongozo wa kike inaonyesha tamaa ya ainabinadamu ya ulimwengu usio na jeuri nyingi. Wanaonekana pia kuamini kwamba leo ulimwengu ungekuwa mahali pazuri zaidi na penye amani zaidi kama ungekuwa na mwongozo wa kike zaidi.

Hata hivyo, ibada ya mama-mungu-mke haikuleta amani katika ulimwengu wa kale, nayo haitaleta amani leo. Tena, watu zaidi na zaidi leo, kwa hakika mamilioni wanaoshiriki pamoja na Mashahidi wa Yehova, wanasadiki kwamba dunia hii haitaokolewa na Mariamu, hata wakiwa wanamheshimu na kumpenda kwa kadiri gani akiwa mwanamke mwaminifu wa karne ya kwanza aliyekuwa na pendeleo la ajabu la kumzaa na kumlea Yesu. Wala Mashahidi wa Yehova hawaamini kwamba Harakati ya Ukombozi wa Wanawake yaweza kuleta ulimwengu wenye amani, hata kama madai yayo mengine huenda yakawa ya haki. Kwa jambo hilo wanamtegemea Mungu ambaye Paulo alijulisha kwa Waathene na kwa Waefeso, “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo.” (Matendo 17:24; 19:11, 17, 20) Mwenyezi Mungu huyo, ambaye jina lake ni Yehova, ameahidi ulimwengu mpya mtukufu ambamo “haki yakaa ndani yake,” nasi twaweza kutegemea ahadi yake kwa uhakika.—2 Petro 3:13.

Kwa habari ya maoni ya Biblia juu ya mahali pa mwanamke mbele ya Mungu na mwanamume, habari hiyo itakuzwa zaidi katika gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 5]

ASHTORETHI

mungu-mke wa Kikanaani wa ngono na vita

[Picha katika ukurasa wa 6]

ARTEMI

mungu-mke wa uzazi wa Efeso

[Hisani]

Musei dei Conservatori, Roma

[Picha katika ukurasa wa 7]

“MAMA YA MUNGU” wa Jumuiya ya Wakristo

[Hisani]

Kathedro ya Chartres, Ufaransa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki